Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU | UWONGO UNAOFANYA WATU WASIMPENDE MUNGU

Ukweli Unaweza Kukuweka Huru

Ukweli Unaweza Kukuweka Huru

Siku moja, huko Yerusalemu, Yesu alikuwa akizungumza kuhusu Baba yake, Yehova, na alifichua mafundisho ya uwongo ya viongozi wa kidini wa wakati huo. (Yohana 8:12-30) Maneno ya Yesu yanatufundisha jinsi ya kuchunguza mafundisho yanayofanya watu wasimpende Mungu. Yesu alisema hivi: “Mkikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, nanyi mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.”Yohana 8:31, 32.

Yesu aliposema, “mkikaa katika neno langu,” aliweka kiwango cha kupima mafundisho ya viongozi wa kidini. Unaposikia mafundisho kumhusu Mungu, kwanza jiulize, ‘Je, yanapatana na maneno ya Yesu na Biblia kwa ujumla?’ Fuata mfano wa wale waliomsikia mtume Paulo akizungumza na ambao walikuwa “wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo [waliyokuwa wakijifunza] ndivyo yalivyo.”Matendo 17:11.

Marco, Rosa, na Raymonde, waliotajwa katika makala ya kwanza, walichunguza kwa makini imani yao kwa kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Waligundua nini?

Marco: “Mwalimu wetu wa Biblia alitumia Maandiko kujibu maswali yote ambayo mimi na mke wangu tulimwuliza. Upendo wetu kwa Yehova ulianza kukua, na pia uhusiano wangu na mke wangu ukaimarika!”

Rosa: “Mwanzoni nilifikiri kwamba Biblia ilikuwa kitabu chenye mawazo ya wanadamu. Hatua kwa hatua, nilipata majibu ya maswali yangu katika Biblia. Sasa, Yehova ni halisi kwangu na ninaweza kumtumaini.”

Raymonde: “Nilisali kwa Mungu ili anisaidie kumjua. Punde si punde, mimi na mume wangu tulianza kujifunza Biblia. Hatimaye, tulijifunza ukweli kumhusu Yehova! Tulifurahi sana kumjua Mungu.”

Biblia haifunui tu mafundisho ya uwongo kumhusu Mungu, badala yake inaeleza pia kuhusu sifa zake zenye kupendeza. Biblia iliandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu, na inatusaidia ‘kuyajua mambo ambayo Mungu ametupa sisi kwa fadhili.’ (1 Wakorintho 2:12) Tafadhali chunguza jinsi Biblia inavyojibu maswali muhimu kuhusu Mungu, kusudi lake, na wakati wetu ujao. Soma majibu ya baadhi ya maswali hayo chini ya kichwa “Mafundisho ya Biblia > Majibu ya Maswali ya Biblia” kwenye www.pr418.com/sw. Pia, kwenye Tovuti hiyo unaweza kuomba ufundishwe Biblia na Shahidi wa Yehova. Bila shaka, ukifanya hivyo utaona kwamba inawezekana kuwa na uhusiano mzuri na Mungu kuliko ulivyodhani.