Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MKARIBIE MUNGU

“Mthawabishaji wa Wale Wanaomtafuta kwa Bidii”

“Mthawabishaji wa Wale Wanaomtafuta kwa Bidii”

Je, Yehova anawathamini waabudu wake wanapojitahidi kumpendeza? Huenda watu fulani wakasema hapana, wakidai kwamba Mungu hapendezwi nasi. Lakini madai hayo yanaendeleza uwongo kumhusu Mungu. Neno lake Biblia, linatuambia ukweli. Linatuhakikishia kwamba Yehova anathamini jitihada za waabudu wake waaminifu. Hebu tuchunguze maneno ya mtume Paulo kwenye Waebrania 11:6.

Tunawezaje kumpendeza Yehova? “Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza [Mungu] vema,” akaandika Paulo. Ona kwamba Paulo hasemi ni vigumu kumpendeza Mungu bila imani. Badala yake mtume huyo anasema haiwezekani. Yaani, ili mtu ampendeze Mungu ni lazima awe na imani.

Yehova hupendezwa na imani ya aina gani? Ni lazima imani yetu katika Mungu iwe na mambo mawili. Kwanza, ni ‘lazima tuamini kwamba yeye yuko.’ Tafsiri nyingine husema “tuamini yeye ni halisi.” Tunawezaje kumpendeza Mungu ikiwa tunashuku kwamba yuko? Hata hivyo, imani ya kweli inatia ndani mengi zaidi kwa kuwa hata roho waovu wanaamini Yehova yuko. (Yakobo 2:19) Tukiamini kwamba Mungu ni halisi, tutachochewa kutenda, yaani, kuonyesha imani yetu kwa kuishi kwa njia inayompendeza.Yakobo 2:20, 26.

Pili, ni ‘lazima tuamini kwamba’ Mungu ni “mthawabishaji.” Mtu mwenye imani ya kweli anasadiki kwamba jitihada zake za kumpendeza Mungu si za bure. (1 Wakorintho 15:58) Tunawezaje kumpendeza Yehova ikiwa tunashuku kwamba anaweza na anataka kututhawabisha? (Yakobo 1:17; 1 Petro 5:7) Mtu anayefikiri kwamba Mungu hajali, hana shukrani, na si mkarimu hamjui Mungu wa kweli.

Yehova huthawabisha watu wa aina gani? “Wale wanaomtafuta kwa bidii,” anasema Paulo. Kitabu kimoja cha marejeo ya watafsiri wa Biblia kinasema kwamba neno la Kigiriki lililotafsiriwa “wanaomtafuta kwa bidii” halimaanishi “kwenda kutafuta,” badala yake, linamaanisha “kumwabudu” Mungu. Kitabu kingine cha marejeo kinaeleza kwamba kitenzi hiki cha Kigiriki kinaonyesha bidii na jitihada nyingi. Naam, Yehova huwathawabisha watu wanaochochewa na imani kumwabudu kwa moyo wote na kwa bidii.Mathayo 22:37.

Tunawezaje kumpendeza Yehova ikiwa tunashuku kwamba anaweza na anataka kututhawabisha?

Yehova huwathawabishaje waabudu wake waaminifu? Amewaahidi zawadi inayoonyesha jinsi alivyo mwenye upendo na ukarimu mwingi, yaani, uzima wa milele katika Paradiso duniani. (Ufunuo 21:3, 4) Hata sasa, wale wanaomtafuta Yehova kwa bidii wanapata baraka nyingi. Kupitia msaada wa roho yake takatifu na hekima iliyo katika Neno lake, wanafurahia maisha yenye kuridhisha.Zaburi 144:15; Mathayo 5:3.

Kwa kweli, Yehova ni Mungu mwenye shukrani anayethamini jitihada za waabudu wake waaminifu. Je, kujua jambo hilo kunakuchochea utake kumkaribia zaidi? Ikiwa ndivyo, basi jifunze mengi kuhusu jinsi unavyoweza kusitawisha na kuonyesha imani ambayo itathawabishwa na Yehova.

Usomaji wa Biblia Unaopendekezwa Mwezi wa Novemba

Tito 1-3; Filemoni 1-25; Waebrania 1-13 hadi Yakobo 1-5