Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wachungaji, Mwigeni Yule Mchungaji Mkuu

Wachungaji, Mwigeni Yule Mchungaji Mkuu

“Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.”1 PET. 2:21.

1, 2. (a) Kondoo wanapotunzwa vizuri wanakuwa katika hali gani? (b) Kwa nini watu wengi katika siku za Yesu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji?

KONDOO huwa na afya nzuri mchungaji anapowajali kikweli. Kitabu kimoja kinachohusu uchungaji wa kondoo kinasema kwamba “kondoo hudhoofika na kuwa wagonjwa baada ya miaka michache ikiwa mchungaji anawapeleka tu malishoni lakini hawatunzi au kuwajali.” Hata hivyo, kondoo wanapotunzwa ifaavyo, kundi lote linakuwa na afya nzuri.

2 Ikiwa wachungaji wa kundi la Mungu wanamtunza na kumjali ifaavyo kila kondoo waliyekabidhiwa, kutaniko lote litakuwa na afya nzuri ya kiroho. Huenda unakumbuka kwamba Yesu aliusikitikia umati kwa sababu “walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mt. 9:36) Kwa nini walikuwa katika hali hiyo yenye kusikitisha? Kwa sababu watu waliokuwa na daraka la kuwafundisha Sheria ya Mungu walikuwa wakali, waliwakandamiza watu, na walikuwa wanafiki. Badala ya kuwatunza na kuwasaidia washiriki wa kundi, viongozi wa kiroho wa Israeli waliweka “mizigo mizito” juu ya mabega yao.Mt. 23:4.

3. Wazee wa kutaniko wanapaswa kukumbuka nini wanapotimiza daraka lao wakiwa wachungaji wa kiroho?

3 Leo, wachungaji Wakristo, yaani, wazee waliowekwa rasmi, wana daraka zito. Kondoo wanaowatunza ni mali ya Yehova na Yesu. Na Yesu alisema kwamba yeye ni “mchungaji mwema.” (Yoh. 10:11) Kondoo hao ‘wamenunuliwa kwa bei’ ambayo Yesu alilipa kwa ‘damu yake mwenyewe yenye thamani.’ (1 Kor. 6:20; 1 Pet. 1:18, 19) Anawapenda sana kondoo hivi kwamba alidhabihu uhai wake kwa hiari  kwa ajili yao. Wazee wanapaswa kukumbuka sikuzote kwamba wanatumikia wakiwa wachungaji chini ya uangalizi wa “mchungaji mkuu wa kondoo,” Yesu Kristo, Mwana mpendwa wa Mungu.Ebr. 13:20.

4. Makala hii itazungumzia nini?

4 Basi, wachungaji Wakristo wanatazamiwa kuwatendea namna gani kondoo? Washiriki wa kutaniko wanahimizwa ‘wawatii wale wanaoongoza’ katikati yao. Nao wazee Wakristo wanahimizwa waepuke “kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu.” (Ebr. 13:17; soma 1 Petro 5:2, 3.) Basi, wazee wataliongozaje kundi bila kupiga ubwana? Yaani, wazee watawatunzaje kondoo bila kutumia vibaya mamlaka waliyopewa na Mungu ya kuwa waangalizi?

“ATAWABEBA KATIKA KIFUA CHAKE”

5. Mfano ulio katika Isaya 40:11 unatuonyesha nini kumhusu Yehova?

5 Nabii Isaya alisema hivi kumhusu Yehova: “Atalichunga kundi lake mwenyewe kama mchungaji. Atawakusanya pamoja wana-kondoo kwa mkono wake; naye atawabeba katika kifua chake. Wale wanaonyonya atawaongoza kwa uangalifu.” (Isa. 40:11) Mfano huo unaonyesha kwamba Yehova anawajali washiriki wa kutaniko walio dhaifu na wanaohitaji kulindwa. Sawa na mchungaji anayejua mahitaji ya kila kondoo katika kundi lake na kutoa msaada unaohitajiwa, Yehova anajua mahitaji ya kila mtu kutanikoni, naye hufurahia kutoa msaada. Yehova, “Baba ya rehema nyororo,” atatubeba na kutusaidia nyakati za taabu kama vile mchungaji anavyombeba mwana-kondoo kifuani pake. Atatufariji tunapokabili jaribu kali au tunapohitaji msaada wa pekee.2 Kor. 1:3, 4.

6. Mzee anaweza kuiga jinsi gani mfano wa Yehova?

6 Mchungaji wa kiroho anaweza kujifunza jambo muhimu sana kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni. Ni lazima akazie uangalifu mahitaji ya kondoo kama Yehova anavyofanya. Mzee anaweza kuwatia moyo na kuwasaidia kondoo ikiwa anajua matatizo wanayokabili na mahitaji hususa yanayohitaji kushughulikiwa haraka. (Met. 27:23) Ni wazi kwamba ni lazima mzee awe na mawasiliano mazuri na waamini wenzake. Anatilia maanani mambo anayoona na kusikia kutanikoni na kwa upendo anajitolea ‘kuwasaidia wale walio dhaifu,’ bila kuingilia faragha yao.—Mdo. 20:35; 1 The. 4:11.

7. (a) Kondoo wa Mungu walitendewa namna gani katika siku za Ezekieli na Yeremia? (b) Tunajifunza nini kutokana na jinsi Yehova alivyowashutumu wachungaji wa kiroho wasio waaminifu?

7 Fikiria mtazamo wa wachungaji walioshutumiwa na Mungu. Katika siku za Ezekieli na Yeremia, Yehova aliwashutumu wachungaji ambao hawakuwatunza ifaavyo kondoo wake. Kondoo walishambuliwa na kutawanyika kwa sababu ya kukosa mchungaji. Badala ya kuwalisha kondoo, wachungaji hao waliwanyanyasa na “kujilisha wenyewe.” (Eze. 34:7-10; Yer. 23:1) Mungu anawashutumu pia viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo kwa sababu hiyohiyo. Jambo hilo linaonyesha kwamba ni muhimu sana kwa wazee Wakristo kuwatunza kwa upendo kondoo wa Yehova.

“NILIWEKA KIELELEZO KWA AJILI YENU”

8. Yesu anawawekea wazee mfano gani bora inapohusu kutoa shauri?

8 Kwa kuwa wanadamu si wakamilifu, huenda baadhi ya kondoo wa Mungu wakakosa kuelewa matakwa yake. Huenda wakafanya maamuzi yasiyopatana  na Maandiko, au kutenda kwa njia inayoonyesha kwamba hawajakomaa kiroho. Wazee wanapaswa kutendaje? Wanapaswa kuiga subira aliyoonyesha Yesu aliposhughulika na wanafunzi wake walipobishana mara nyingi kuhusu ni nani angekuwa mkuu zaidi katika Ufalme. Badala ya kukosa subira, Yesu aliendelea kuwafundisha wanafunzi wake na kuwashauri kwa upendo kuhusu kuonyesha unyenyekevu. (Luka 9:46-48; 22:24-27) Yesu aliwafundisha unyenyekevu kwa kuwaosha miguu, na hiyo ndiyo sifa ambayo waangalizi Wakristo wanahitaji kuonyesha.Soma Yohana 13:12-15; 1 Pet. 2:21.

9. Yesu aliwashauri wanafunzi wake wawe na mtazamo gani?

9 Maoni ya Yesu kuhusu daraka la mchungaji wa kiroho yalikuwa tofauti na maoni ya Yakobo na Yohana. Mitume hao wawili walitaka cheo kikubwa katika Ufalme. Lakini Yesu alirekebisha maoni yao aliposema hivi: “Mnajua kwamba watawala wa kigeni huwaamuru-amuru watu. Na viongozi wao wakuu wana mamlaka kamili juu ya watu wanaowatawala. Lakini msitende kama wao. Ikiwa unataka kuwa mkuu, ni lazima uwe mtumishi wa wengine wote.” (Mt. 20:25, 26, Contemporary English Version) Mitume walihitaji kushinda mwelekeo wa ‘kupiga ubwana juu ya’ wenzao au ‘kuwaamuru-amuru watu.’

10. Yesu anataka wazee wawatendee kondoo jinsi gani? Paulo aliweka mfano gani katika jambo hilo?

10 Yesu anatarajia wazee Wakristo walitendee kundi kama alivyolitendea. Ni lazima wawe tayari kuwa watumishi badala ya kuwa mabwana juu ya kundi. Mtume Paulo alikuwa mnyenyekevu. Aliwaambia hivi wanaume wazee wa kutaniko la Efeso: “Ninyi mnajua vema jinsi tangu siku ya kwanza niliyokanyaga wilaya ya Asia nilivyokuwa pamoja nanyi wakati wote, nikimtumikia Bwana nikiwa na unyenyekevu mkubwa zaidi wa akili.” Mtume Paulo alitaka wazee hao wawasaidie wengine kwa bidii na unyenyekevu. Alisema hivi: “Nimewaonyesha ninyi wazi katika mambo yote kwamba kwa kufanya kazi kwa bidii hivyo ni lazima mwasaidie wale walio dhaifu.” (Mdo. 20:18, 19, 35) Paulo aliwaambia Wakorintho kwamba hakuwa bwana juu ya imani yao. Badala yake, alikuwa mfanyakazi mwenzao mnyenyekevu kwa shangwe yao. (2 Kor. 1:24) Paulo aliwawekea wazee leo mfano mzuri katika kuwa wanyenyekevu na kufanya kazi kwa bidii.

‘LISHIKE IMARA NENO LA UAMINIFU’

11, 12. Mzee anaweza kumsaidiaje mwamini mwenzake kufanya uamuzi?

11 Ni lazima mzee wa kutaniko ‘alishike imara neno la uaminifu kuhusiana na ufundi wake wa kufundisha.’ (Tito 1:9) Lakini anapaswa kufanya hivyo “katika roho ya upole.” (Gal. 6:1) Badala ya kujaribu kuwalazimisha waamini wenzake watende kwa njia fulani, mchungaji mzuri wa kiroho atajitahidi kuwasaidia wajifanyie uamuzi wakichochewa na upendo wao kwa Yehova. Mzee anaweza kumwonyesha ndugu kanuni za Kimaandiko anazopaswa kufikiria anapofanya uamuzi muhimu. Wanaweza kuchunguza pamoja makala zinazozungumzia jambo hilo. Anaweza pia kumhimiza ndugu huyo afikirie jinsi maamuzi yake yatakavyoathiri uhusiano wake na Yehova. Kisha, atamsaidia ndugu huyo kuona umuhimu wa kumwomba Mungu mwongozo kupitia sala kabla ya kufanya uamuzi. (Met. 3:5, 6) Baada ya kuzungumzia mambo hayo na mwamini mwenzake, mzee atamwacha ajifanyie uamuzi.—Rom. 14:1-4.

 12 Mamlaka ya waangalizi Wakristo yanategemea Maandiko. Kwa hiyo, ni muhimu sana kwamba watumie Biblia kwa ustadi na kufuata kabisa mashauri yake. Wazee wanapofanya hivyo wanaepuka kutumia vibaya mamlaka yao. Kwa kweli, wamewekwa kuwa wachungaji na kondoo si mali yao. Kila mshiriki wa kutaniko atawajibika mbele za Yehova na Yesu kwa sababu ya maamuzi anayofanya.Gal. 6:5, 7, 8.

“VIELELEZO KWA KUNDI”

13, 14. Ni lazima mzee aliwekee kundi mfano mzuri katika mambo gani?

13 Baada ya kuwashauri wanaume wazee wa kutaniko ‘wasipige ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu,’ mtume Petro aliwahimiza ‘wawe vielelezo kwa kundi.’ (1 Pet. 5:3) Mzee anawezaje kuwa kielelezo kwa kundi? Fikiria sifa mbili ambazo mwanamume ‘anayejitahidi kufikia cheo cha mwangalizi’ anapaswa kutimiza. Anahitaji kuwa “mwenye utimamu wa akili” na ni lazima awe ‘anaisimamia nyumba yake mwenyewe kwa njia nzuri.’ Ikiwa mzee ana familia, ni lazima aisimamie kwa njia nzuri, “kwa kweli ikiwa mtu yeyote hajui jinsi ya kuisimamia nyumba yake mwenyewe, atalitunzaje kutaniko la Mungu?” (1 Tim. 3:1, 2, 4, 5) Ili mwanamume astahili kupata cheo cha mwangalizi, ni lazima awe na utimamu wa akili, yaani, awe anaelewa vizuri kanuni za Biblia na anajua kuzitumia maishani mwake. Ni mtulivu na hafanyi maamuzi haraka-haraka. Wazee wanapoonyesha sifa hizo, washiriki wa kutaniko watawaona kuwa wanategemeka.

Wazee huzisaidia familia zao kujitayarisha kwa ajili ya huduma (Tazama fungu la 13)

14 Wazee huwawekea Wakristo wenzao kielelezo kizuri wanapoongoza pia katika kazi ya kuhubiri. Yesu aliwawekea wazee kielelezo katika kazi hiyo. Kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme ilikuwa sehemu muhimu ya utendaji wa Yesu alipokuwa duniani. Aliwaonyesha wanafunzi wake jinsi ya kufanya kazi hiyo. (Marko 1:38; Luka 8:1) Leo, wahubiri wanatiwa moyo sana wanapohubiri na wazee, wanapoona bidii yao katika kazi hiyo inayookoa uhai, na wanapojifunza mbinu zao za kufundisha. Wazee wanapotumia wakati wao kuhubiri kwa bidii habari njema licha ya kuwa na shughuli nyingi, kutaniko lote linachochewa pia kuwa na bidii. Wazee wanaweza pia kuwawekea mfano mzuri ndugu zao kwa kutayarisha na kushiriki katika mikutano na utendaji mwingine kama vile kusafisha na kutunza Jumba la Ufalme.Efe. 5:15, 16; soma Waebrania 13:7.

Wazee huweka mfano katika kazi ya kuhubiri (Tazama fungu la 14)

“TEGEMEZENI WALIO DHAIFU”

15. Wazee hufanya ziara za uchungaji kwa sababu gani?

15 Mchungaji mzuri humsaidia haraka kondoo aliye mgonjwa au aliyeumia. Vivyo hivyo, wazee wanahitaji kumsaidia  haraka mshiriki yeyote wa kutaniko anayeteseka au anayehitaji msaada wa kiroho. Huenda washiriki wa kutaniko waliozeeka na wagonjwa wakahitaji msaada wa kimwili, lakini wanahitaji hasa kusaidiwa kiroho na kutiwa moyo. (1 The. 5:14) Huenda vijana walio kutanikoni wanakabili matatizo yanayotokana na “tamaa zinazotukia ujanani.” (2 Tim. 2:22) Kwa hiyo, uchungaji unatia ndani kuwatembelea mara kwa mara washiriki wa kutaniko na kujitahidi kuelewa hali wanazokabili, kisha kuwatia moyo kwa kuwapa mashauri ya Kimaandiko yanayofaa. Wazee wakiwasaidia ndugu na dada haraka iwezekanavyo, wanaweza kutatua matatizo mengi kabla hayajawa mazito.

16. Wazee wanaweza kumsaidiaje ndugu au dada anayehitaji msaada wa kiroho?

16 Namna gani ikiwa ndugu ana matatizo mazito yanayohatarisha uhusiano wake na Yehova? Yakobo, mwandikaji wa Biblia, aliuliza hivi: “Je, kuna yeyote mgonjwa kati yenu?” Kisha akasema: “Na awaite kwake wanaume wazee wa kutaniko, nao wasali juu yake, wakimpaka mafuta katika jina la Yehova. Na sala ya imani itamponya huyo asiyejisikia vizuri, na Yehova atamwinua. Pia, ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.” (Yak. 5:14, 15) Wazee wanapaswa kumsaidia haraka iwezekanavyo ndugu au dada aliye mgonjwa kiroho, hata ‘asipowaita wanaume wazee.’ Wazee wanaposali pamoja na ndugu zao na kwa ajili yao na kuwategemeza wakati wa shida, wanawaburudisha kiroho na kuwatia moyo wote walio chini ya utunzaji wao.Soma Isaya 32:1, 2.

17. Kutaniko litanufaika jinsi gani wazee wanapomwiga yule “mchungaji mkuu”?

17 Wachungaji Wakristo hujitahidi kumwiga “mchungaji mkuu,” Yesu Kristo, wanapotimiza majukumu yao yote katika tengenezo la Yehova. Wanaume hao wanaochukua majukumu yao kwa uzito hulisaidia kundi kuendelea kuimarika na kumtumikia Mungu kwa uaminifu. Tunashukuru sana kwa ajili ya wachungaji hao wenye upendo nasi tunamsifu Mchungaji wetu asiye na kifani, Yehova.