Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kichwa

Sababu Gani Ulizo Hilo Linaulizwa?

Sababu Gani Ulizo Hilo Linaulizwa?

“Je, unafikiri hauna lazima ya Mungu? Mamilioni ya watu wanafikiri hivyo.” Huo ni ujumbe ulioandikwa kwenye ubao na kikundi cha watu ambao hawaamini kuna Mungu. Bila shaka, watu hao wanaona kwamba hawana lazima ya Mungu.

Kwa upande mwengine, watu wengi ambao wanasema kwamba wanamuamini Mungu wanafanya maamuzi ambayo yanaonyesha kama vile hakuna Mungu. Salvatore Fisichella, askofu Mukatoliki, alisema hivi juu ya washiriki wa kanisa lake mwenyewe: “Mutu anapotuangalia labda hawezi kutambua kwamba sisi ni Wakristo kwa sababu namna yetu ya kuishi ni kama tu ya watu ambao hawamuamini Mungu.”

Watu fulani wanaona kwamba hawana wakati wa kuhangaikia mambo ya Mungu. Wanawaza kwamba hawezi kufanya jambo lolote la maana katika maisha yao kwa sababu wanamuona kuwa mbali sana ao asiyeweza kukaribiwa. Jambo la kushangaza ni kwamba, watu kama hao wanafikiri juu ya Mungu wakati wana shida ao wakati wanahitaji jambo fulani, ni kama vile Mungu ni mutumishi wao.

Wengine hawaone mafundisho ya kidini kuwa ya maana, ao kwa njia nyingine, hawafuate mambo ambayo makanisa yao yanawafundisha. Tutaje mufano mumoja tu: Wakatoliki wa Ujerumani 76 juu ya 100 wanaamini kwamba inakubalika mwanaume na mwanamuke kuishi pamoja mbele ya kufunga ndoa, wazo ambalo ni tofauti na mambo ambayo Biblia na kanisa lao linafundisha. (1 Wakorintho 6:18; Waebrania 13:4) Bila shaka, si Wakatoliki peke yao ndio ambao wanaishi tofauti na mambo wanayofundishwa. Viongozi wa dini nyingi wanalalamika kwamba washiriki wa dini zao wanajiendesha kama vile “watu ambao hawaamini kuna Mungu.”

Mifano hiyo inatokeza ulizo hili: Tuna lazima kabisa ya Mungu? Si mara ya kwanza ulizo hilo linaulizwa. Liliulizwa mara ya kwanza katika kurasa za kwanza​-kwanza za Biblia. Ili tupate jibu la ulizo hilo, acheni basi tufikirie zaidi maulizo mbalimbali ambayo yaliulizwa katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo.