Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU | JE KIFO NI MWISHO WA MAMBO YOTE?

Jitihada za Mwanadamu za Kupambana na Kifo

Jitihada za Mwanadamu za Kupambana na Kifo

MALIKI QIN SHI HUANG

MVUMBUZI PONCE DE LEÓN

Kifo ni adui mwenye kuogopesha. Sisi hupigana naye kwa hali na mali. Huenda tusikubali ukweli wa mambo tunapofiwa na mpendwa wetu. Au, kwa kuwa tuna nguvu za ujana, huenda tukadhani kwamba hatutawahi kufa—wazo ambalo sisi hushikilia kwa muda mrefu kadiri tuwezavyo.

Hata hivyo, Mafarao wa kale walijitahidi sana kuepuka kifo. Walitumia muda mwingi wa maisha yao, na pia maisha ya maelfu ya wafanyakazi wao, kujaribu kushinda kifo. Mapiramidi waliyojenga yanathibitisha jitihada hizo ambazo ziliambulia patupu.

Maliki wa China walijitahidi vivyo hivyo ingawa walitumia njia tofauti, yaani, walitafuta dawa za kurefusha maisha kimuujiza. Maliki Qin Shi Huang aliwaamuru wataalamu wa madawa watafute dawa ya kimuujiza ambayo ingemzuia kufa. Lakini mchanganyiko wa madawa waliotengeneza ulikuwa na zebaki, na huenda mchanganyiko huo ndio uliomuua.

Katika karne ya 16 W.K., mvumbuzi Mhispania, Juan Ponce de León, alifunga safari kwenda visiwa vya Karibea ili kutafuta chemchemi ya ujana. Katika safari hiyo, alivumbua jimbo la Florida, Marekani, lakini alikufa miaka michache baadaye katika mapigano na Wenyeji wa Asili wa Amerika. Hakuna chemchemi ya ujana ambayo imewahi kugunduliwa.

Watu hao wote—Mafarao, maliki, na wavumbuzi—walijaribu kushinda kifo. Hatuwezi kupuuza jitihada zao ingawa hatukubaliani na mbinu walizotumia. Sisi sote tuna tamaa ya kuishi milele.

JE, KIFO KINAWEZA KUSHINDWA?

Kwa nini hatutaki kufa? Biblia inaeleza sababu. Inasema hivi kumhusu Muumba wetu, Yehova Mungu *: “Amefanya kila kitu kiwe chenye kupendeza kwa wakati wake. Tena wakati usio na  kipimo ameuweka ndani ya moyo wao [wanadamu].” (Mhubiri 3:11) Tungependa kufurahia uzuri wa dunia milele, si kwa miaka 80 hivi tu. (Zaburi 90:10) Hiyo ndiyo tamaa ya moyo wetu.

Kwa nini Mungu aliweka “wakati usio na kipimo” ndani ya mioyo yetu? Je, ni ili kutukatisha tamaa? Hawezi kufanya hivyo. Badala yake, Mungu anaahidi kwamba kifo kitaondolewa. Biblia inataja tena na tena kuhusu kuondolewa kwa kifo na ahadi ya Mungu ya uzima wa milele.—Ona sanduku,  “Ushindi Dhidi ya kifo.”

Yesu Kristo mwenyewe alisema hivi waziwazi: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Kwa hiyo, kifo kitashindwa. Lakini kama Yesu alivyothibitisha, ni Mungu peke yake anayeweza kushinda vita hivyo kwa ajili yetu.

^ fu. 9 Yehova ni jina la Mungu kama linavyofunuliwa kwenye Biblia.