Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwabudu Yehova, Mfalme wa Umilele

Mwabudu Yehova, Mfalme wa Umilele

Kwa Mfalme wa umilele . . . kuwe na heshima na utukufu milele.1 TIM. 1:17.

1, 2. (a) Ni nani aliye “Mfalme wa umilele,” na kwa nini anastahili cheo hicho? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.) (b) Kwa nini tunavutiwa na utawala wa Yehova?

MFALME SOBHUZA WA PILI wa Swaziland alitawala kwa miaka 61 hivi. Hakuna mfalme mwingine yeyote katika siku zetu aliyewahi kutawala kwa kipindi kirefu hivyo. Hata ingawa tunavutiwa na urefu wa utawala wa Mfalme Sobhuza, kuna mfalme asiyeweza kufa. Kwa kweli, Biblia inasema kwamba yeye ni “Mfalme wa umilele.” (1 Tim. 1:17) Mtunga-zaburi mmoja alitaja jina la huyo Mwenye Enzi Kuu kwa kusema hivi: “Yehova ni Mfalme mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.”—Zab. 10:16.

2 Hakuna mwanadamu yeyote anayeweza kutawala kwa umilele kama Mungu. Hata hivyo, tunavutiwa hasa na njia ya Yehova ya kutawala. Mfalme aliyetawala taifa la kale la Israeli kwa miaka 40 alimsifu Mungu hivi: “Yehova ni mwenye rehema na mwenye neema, si mwepesi wa hasira na ni mwingi wa fadhili zenye upendo. Yehova amekifanya imara kiti chake cha ufalme mbinguni; nao ufalme wake mwenyewe umetawala juu ya kila kitu.” (Zab. 103:8, 19) Yehova si Mfalme wetu tu bali pia ni Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo. Hilo linatokeza maswali haya mawili: Yehova ni Baba katika njia gani? Yehova ametumiaje mamlaka yake akiwa Mfalme tangu uasi ulipotokea katika Edeni? Majibu ya maswali hayo yatatuchochea  kumkaribia zaidi Yehova na kumwabudu kwa moyo wetu wote.

MFALME WA UMILELE AANZISHA FAMILIA YA ULIMWENGUNI POTE

3. Ni nani aliyekuwa mshiriki wa kwanza wa familia ya Yehova ya ulimwenguni pote? Ni nani wengine walioumbwa wakiwa “wana” wa Mungu?

3 Bila shaka, Yehova alifurahi sana alipomuumba Mwana wake mzaliwa-pekee! Mungu hakumtendea mzaliwa wake wa kwanza kana kwamba ni mtu wa hali ya chini. Badala yake, alimpenda kama Mwana na kushiriki naye shangwe ya kuumba viumbe wengine wakamilifu. (Kol. 1:15-17) Viumbe hao walitia ndani makumi ya maelfu ya malaika. Malaika hao wanaomtumikia Mungu kwa shangwe wanaitwa ‘wahudumu wake, wanaofanya mapenzi yake,’ naye anawaheshimu kwa kuwaita “wana.” Wao ni sehemu ya familia ya Yehova ya ulimwenguni pote.—Zab. 103:20-22; Ayu. 38:7.

4. Wanadamu walikujaje kuwa sehemu ya familia ya Mungu ya ulimwenguni pote?

4 Baada tu ya kuumba mbingu na dunia, Yehova alipanua familia yake ya ulimwenguni pote. Baada ya kuifanya dunia kuwa makao maridadi yanayodumu, Yehova alifikia upeo wa kazi zake duniani kwa kumuumba mwanadamu wa kwanza, Adamu, kwa mfano Wake mwenyewe. (Mwa. 1:26-28) Akiwa Muumba, Yehova alikuwa na haki ya kutarajia Adamu amtii. Akiwa Baba, Yehova alitoa maagizo yake yote kwa upendo na fadhili. Maagizo hayo hayakuwanyima uhuru isivyo lazima.—Soma Mwanzo 2:15-17.

5. Mungu alifanya mpango gani ili dunia ijae watoto wake wa kibinadamu?

5 Tofauti na wafalme wengi wanadamu, Yehova hufurahia kuwakabidhi raia wake mapendeleo akiwaona kuwa washiriki wa familia yake wanaotegemeka. Kwa mfano, alimpa Adamu mamlaka ya kutawala viumbe wengine na mgawo wenye kufurahisha usio rahisi wa kuwapa wanyama majina. (Mwa. 1:26; 2:19, 20) Mungu hakuumba mamilioni ya wanadamu wakamilifu ili kuijaza dunia. Badala yake, aliamua kumuumba Hawa, mwanamke mkamilifu ili awe kikamilisho cha Adamu. (Mwa. 2:21, 22) Kisha, akawapa wenzi hao pendeleo la kuzaa watoto na kuijaza dunia. Chini ya hali nzuri kabisa, wanadamu wangepanua mipaka ya Paradiso hatua kwa hatua ili ienee duniani pote. Wakiwa sehemu ya familia ya Yehova ya ulimwenguni pote, wangemwabudu milele kama malaika wanavyofanya mbinguni. Hilo lilikuwa tumaini zuri ajabu! Kwa kweli, Yehova aliwaonyesha upendo kama wa baba.

WANA WAASI WAKATAA UTAWALA WA MUNGU

6. (a) Uasi ulianzaje katika familia ya Mungu? (b) Tunajuaje kwamba Yehova hakupoteza mamlaka yake baada ya uasi kutokea?

6 Inasikitisha kwamba Adamu na Hawa hawakumkubali Yehova kuwa Mwenye Enzi Kuu wao. Badala yake, walichagua kumfuata Shetani, mwana wa roho aliyemwasi Mungu. (Mwa. 3:1-6) Kuishi bila utawala wa Mungu kuliwaletea wao na watoto wao huzuni, kuteseka, na kifo. (Mwa. 3:16-19; Rom. 5:12) Mungu hakuwa tena na raia waliomtii duniani. Je, hilo lilimaanisha kwamba alipoteza mamlaka yake juu ya dunia na wanadamu akiwa Mwenye Enzi Kuu? La hasha! Alitumia mamlaka yake kumfukuza Adamu na Hawa kutoka katika bustani ya Edeni, na ili kuwazuia wasirudi, aliweka makerubi kuilinda njia ya kuingia kwenye bustani. (Mwa. 3:23, 24) Wakati huohuo, Mungu alionyesha upendo wake akiwa Baba kwa kuahidi kwamba bado angetimiza kusudi lake la kuwa na familia ya ulimwenguni pote ya malaika na wanadamu waaminifu. Aliahidi kutokeza ‘mzao’ atakayemwangamiza Shetani na kuondoa madhara ya dhambi ya Adamu.—Soma Mwanzo 3:15.

7, 8. (a) Hali zilikuwa mbaya kadiri gani kufikia siku za Noa? (b) Yehova alichukua hatua gani ili kuisafisha dunia na kuilinda familia ya wanadamu?

 7 Katika karne zilizofuata, kuna watu waliochagua kuwa washikamanifu kwa Yehova, kama vile Abeli na Enoko. Hata hivyo, wanadamu wengi walimkataa Yehova aliyekuwa Mfalme na Baba yao. Kufikia siku za Noa, dunia ilikuwa ‘imejaa jeuri.’ (Mwa. 6:11) Je, hilo lilimaanisha kwamba Yehova alipoteza mamlaka yake juu ya dunia? Historia inaonyesha nini?

8 Fikiria simulizi linalomhusu Noa. Yehova alimpa maagizo hususa ya kujenga safina kubwa sana ambayo ingemwokoa Noa na familia yake. Pia, Mungu alionyesha kwamba anaipenda sana familia yake yote ya wanadamu alipomwagiza Noa awe “mhubiri wa uadilifu.” (2 Pet. 2:5) Bila shaka, Noa aliwasihi pia watu watubu na aliwaonya kuhusu uharibifu uliokuwa karibu, lakini hawakumsikiliza. Kwa miaka mingi, Noa na familia yake waliishi katika ulimwengu uliojaa jeuri na wenye maadili mapotovu sana. Akiwa Baba anayejali, Yehova aliwalinda na kuwabariki wanadamu hao wanane waliokuwa washikamanifu. Yehova alitumia mamlaka yake kuwahukumu wanadamu waasi na malaika waovu kwa kuleta Gharika juu ya dunia yote. Bila shaka, Yehova hakupoteza kamwe mamlaka yake.—Mwa. 7:17-24.

Sikuzote Yehova ametumia mamlaka yake akiwa mfalme (Tazama fungu la 6, 8, 10, 12, 17)

UTAWALA WA YEHOVA BAADA YA GHARIKA

9 Noa na familia yake walipotoka ndani ya safina na kupumua hewa safi katika dunia iliyosafishwa, bila shaka walimshukuru sana Yehova kutoka moyoni kwa kuwatunza na kuwalinda. Mara moja, Noa alijenga madhabahu na kumwabudu Yehova kwa kumtolea dhabihu. Mungu alimbariki Noa na familia yake na kuwaagiza ‘wazae, wawe wengi na kuijaza dunia.’ (Mwa. 8:20–9:1) Kwa mara nyingine tena, wanadamu walikuwa na fursa ya kuungana katika ibada na kuijaza dunia.

10. (a) Uasi dhidi ya Yehova ulitokea wapi na wakati gani baada ya Gharika? (b) Yehova alichukua hatua gani ili kuhakikisha kwamba kusudi lake linatimia?

10 Hata hivyo, Gharika haikuondoa hali ya kutokamilika, na wanadamu walihitaji kuendelea kupambana na uvutano usioonekana wa Shetani na malaika wengine waasi. Baada ya muda mfupi, uasi ulitokea dhidi ya utawala wa Yehova wenye upendo. Kwa mfano, Nimrodi, mwana wa mjukuu wa Noa, aliupinga vikali utawala wa Yehova. Nimrodi anaitwa “mwindaji mwenye nguvu kwa kumpinga Yehova.” Alijenga majiji makubwa kama vile Babeli, na kujiweka mwenyewe kuwa mfalme “katika nchi ya Shinari.” (Mwa. 10:8-12) Akiwa Mfalme wa umilele, Mungu alichukua hatua gani ya kumkomesha mfalme huyo mwasi na jitihada zake za kuzuia kusudi la Mungu la ‘kuijaza dunia’? Mungu alivuruga lugha yao, na kuwafanya wafuasi wa Nimrodi wasioelewana watawanyike “juu ya uso wote wa dunia.” Waliendelea kufuata ibada yao ya uwongo na mifumo ya wanadamu ya kutawala.—Mwa. 11:1-9.

11. Yehova alionyeshaje ushikamanifu kwa Abrahamu rafiki yake?

11 Hata ingawa wengi waliabudu miungu ya uwongo baada ya Gharika, wanadamu fulani waaminifu waliendelea kumheshimu Yehova. Kwa mfano, Abrahamu alimtii Yehova kwa kuacha maisha ya starehe katika jiji la Uru na kuishi katika mahema kwa miaka mingi. (Mwa. 11:31; Ebr. 11:8, 9) Abrahamu aliyekuwa akihama-hama, alizungukwa mara nyingi na wafalme walioishi katika majiji yaliyozingirwa na kuta. Hata hivyo, Yehova alimlinda Abrahamu na familia yake. Mtunga-zaburi alisema hivi kuhusu jinsi Yehova alivyowalinda akiwa Baba yao: “[Mungu] hakuruhusu binadamu  yeyote awapunje, bali aliwakaripia wafalme kwa sababu yao.” (Zab. 105:13, 14) Yehova alionyesha ushikamanifu kwa Abrahamu rafiki yake kwa kumwahidi hivi: “Wafalme watatoka ndani yako.”—Mwa. 17:6; Yak. 2:23.

12. Yehova alitumiaje mamlaka yake juu ya Misri? Na hilo lilikuwa na matokeo gani kwa watu wake?

12 Mungu alimwahidi pia Isaka, mwana wa Abrahamu, na Yakobo mjukuu wake, kwamba angewabariki na wazao wao wangekuwa wafalme. (Mwa. 26:3-5; 35:11) Hata hivyo, kabla ya wazao wa Yakobo kutokeza wafalme, walikuwa watumwa huko Misri. Je, hilo lilimaanisha kwamba Yehova hangetimiza ahadi yake au alikuwa amepoteza mamlaka yake juu ya dunia akiwa Mwenye Enzi Kuu? Hapana! Kwa wakati unaofaa, Yehova alimwonyesha Farao aliyekuwa mkaidi kwamba Yeye ni Mungu mwenye nguvu na Mwenye Enzi Kuu. Waisraeli waliokuwa utumwani walimtegemea Yehova, naye akawakomboa kwa njia ya pekee sana kwa kuwapitisha katikati ya Bahari Nyekundu. Bila shaka, Yehova bado alikuwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, na akiwa Baba anayejali, alitumia nguvu zake nyingi kuwalinda watu wake.—Soma Kutoka 14:13, 14.

YEHOVA AWA MFALME WA ISRAELI

13, 14. (a) Waisraeli walitangaza nini kuhusu ufalme wa Yehova walipoimba? (b) Mungu alimwahidi nini Daudi kuhusu ufalme wake?

13 Baada tu ya kukombolewa kimuujiza kutoka Misri, Waisraeli walimsifu Yehova kwa kumwimbia wimbo wa ushindi. Wimbo huo ulio katika Kutoka sura ya 15, unatia ndani maneno haya yaliyo katika mstari wa 18: “Yehova atatawala akiwa mfalme mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.” Kwa kweli, Yehova alikuwa Mfalme wa taifa hilo jipya. (Kum. 33:5) Hata hivyo, Waisraeli hawakuridhika kutawaliwa na Yehova, Mfalme wao asiyeonekana. Miaka 400 hivi baada ya kuondoka Misri, walimwomba Mungu awachagulie mfalme mwanadamu ili wawe kama jirani zao wapagani. (1 Sam. 8:5) Hata hivyo, bado Yehova alikuwa Mfalme na alionyesha hivyo waziwazi wakati wa utawala wa Daudi, mfalme wa pili wa Israeli.

14 Daudi alilileta sanduku takatifu la agano Yerusalemu. Wakati huo wa shangwe, Walawi waliimba wimbo wa sifa uliokuwa  na maneno ya pekee yaliyo katika 1 Mambo ya Nyakati 16:31: ‘Semeni kati ya mataifa: “Yehova amekuwa Mfalme!”’ Huenda mtu akajiuliza hivi: ‘Kwa kuwa Yehova ni Mfalme wa umilele, inawezekanaje kwamba alikuwa Mfalme wakati huo?’ Yehova huwa Mfalme anapotumia mamlaka yake au anapomweka mtu ili amwakilishe kwa kipindi fulani au ashughulikie hali fulani hususa. Ni muhimu sana kuelewa jambo hilo. Kabla Daudi hajafa, Yehova alimwahidi kwamba ufalme wake haungekuwa na mwisho. Alisema hivi: ‘Nitainua uzao wako baada yako, ambao utatoka ndani ya viuno vyako; nami kwa kweli nitaufanya imara ufalme wake.’ (2 Sam. 7:12, 13) Hatimaye, “uzao” huo wa Daudi ulitokea zaidi ya miaka 1,000 baadaye. Mzao huyo alikuwa nani, na angekuwa Mfalme wakati gani?

YEHOVA AMWEKA RASMI MFALME MPYA

15, 16. Yesu alitiwa mafuta wakati gani ili awe Mfalme? Yesu alipokuwa duniani alifanya mipango gani kwa ajili ya utawala wake?

15 Katika mwaka wa 29 W.K., Yohana Mbatizaji alianza kuhubiri kwamba “ufalme wa mbinguni umekaribia.” (Mt. 3:2) Yohana alipombatiza Yesu, Yehova alimtia mafuta Yesu kuwa Masihi aliyeahidiwa na Mfalme ambaye angetawala katika Ufalme wa Mungu. Akiwa Baba, Yehova alionyesha kwamba anampenda Yesu aliposema hivi: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.”—Mt. 3:17.

16 Katika huduma yake yote, Yesu alimtukuza Baba yake. (Yoh. 17:4) Alifanya hivyo kwa kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu. (Luka 4:43) Hata aliwafundisha wafuasi wake wasali Ufalme huo uje. (Mt. 6:10) Yesu aliwaambia hivi watu waliompinga kwa sababu alikuwa Mfalme Aliyechaguliwa: “Ufalme wa Mungu umo katikati yenu.” (Luka 17:21) Baadaye, jioni ya mwisho kabla ya kifo chake, Yesu alifanya ‘agano kwa ajili ya ufalme’ pamoja na wafuasi wake. Hivyo, akawapa baadhi ya wanafunzi wake waaminifu tumaini la kuwa wafalme pamoja naye katika Ufalme wa Mungu.—Soma Luka 22:28-30.

17. Yesu alianzaje kutumia kwa kadiri fulani mamlaka yake ya kifalme katika karne ya kwanza, lakini alihitaji kusubiri nini?

17 Yesu angeanza wakati gani kutawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu? Hangeanza kutawala mara moja. Siku iliyofuata wakati wa mchana, Yesu aliuawa na wafuasi wake wakatawanyika. (Yoh. 16:32) Hata hivyo, sawa na ilivyokuwa zamani, Yehova hakupoteza mamlaka yake. Mungu alimfufua Mwana wake siku ya tatu, na katika siku ya Pentekoste ya 33 W.K., Yesu alianzisha ufalme wa kiroho juu ya kutaniko la Kikristo la ndugu zake watiwa-mafuta. (Kol. 1:13) Hata hivyo, Yesu alihitaji kusubiri ili apewe mamlaka kamili ya kifalme juu ya dunia akiwa “uzao” ulioahidiwa. Yehova alimwambia hivi Mwana wake: “Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka niwaweke adui zako kuwa kiti cha miguu yako.”—Zab. 110:1.

MWABUDU MFALME WA UMILELE

18, 19. Tunachochewa kufanya nini? Tutajifunza nini katika makala inayofuata??

18 Kwa maelfu ya miaka, utawala wa Yehova ulipingwa mbinguni na duniani. Yehova hakupoteza kamwe mamlaka yake akiwa Mwenye Enzi Kuu; aliendelea kutawala. Akiwa Baba mwenye upendo, aliwalinda na kuwatunza raia wake washikamanifu kama vile Noa, Abrahamu, na Daudi. Je, hilo halituchochei kujinyenyekeza kwa Mfalme wetu na kumkaribia zaidi?

19 Lakini huenda tukauliza: Yehova amekuwaje Mfalme leo? Tutaonyeshaje kwamba sisi ni raia washikamanifu wa Ufalme wa Yehova ili wakati ujao tuwe watoto wakamilifu katika familia yake ya ulimwenguni pote? Tunaposali Ufalme wa Mungu uje, tunamaanisha nini? Maswali hayo yatajibiwa katika makala inayofuata.