Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Miaka 100 ya Utawala wa Ufalme​—⁠Inakuhusuje?

Miaka 100 ya Utawala wa Ufalme​—⁠Inakuhusuje?

 

Matendo yako ni makuu na ya ajabu, Yehova Mungu, . . . Mfalme wa umilele.”UFU. 15:3.

1, 2. Ufalme wa Mungu utatimiza nini? Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Ufalme huo utakuja?

ALIPOKUWA mlimani karibu na Kapernaumu wakati wa majira ya kuchipua ya mwaka wa 31 W.K., Yesu Kristo aliwafundisha wafuasi wake kusali hivi: “Ufalme wako na uje.” (Mt. 6:10) Watu wengi leo wana shaka ikiwa Ufalme huo utakuja. Hata hivyo, tuna hakika kwamba sala zetu za kutoka moyoni za kuomba Ufalme wa Mungu uje zitajibiwa.

2 Yehova atatumia Ufalme huo kuunganisha familia yake ya mbinguni na duniani. Kusudi hilo la Mungu litatimia. (Isa. 55:10, 11) Kwa kweli, Yehova tayari amekuwa Mfalme katika siku zetu! Mambo yenye kusisimua yaliyotukia katika miaka 100 iliyopita yanathibitisha hilo. Mungu anatenda mambo makuu na ya ajabu kwa ajili ya mamilioni ya raia wake washikamanifu. (Zek. 14:9; Ufu. 15:3) Hata hivyo, kuna tofauti kati ya Yehova kuwa Mfalme na kuja kwa Ufalme wa Mungu ambao Yesu alitufundisha kusali kuuhusu. Matukio hayo yanatofautianaje na yanatuhusuje?

MFALME ALIYEWEKWA RASMI NA YEHOVA ACHUKUA HATUA

3. (a) Yesu aliwekwa rasmi kuwa Mfalme wakati gani na wapi? (b) Unaweza kuthibitishaje kwamba Ufalme ulianza kutawala katika mwaka wa 1914? (Tazama maelezo ya chini.)

3 Mwishoni mwa karne ya 19, unabii huu wa Danieli ulioandikwa miaka 2,500 iliyopita ulianza kueleweka: “Katika siku za wafalme  hao, Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe.” (Dan. 2:44) Kwa makumi ya miaka Wanafunzi wa Biblia waliendelea kusema kwamba mwaka wa 1914 ungekuwa wa muhimu. Watu wengi walitarajia hali nzuri. Mwandishi mmoja anasema hivi: “Ulimwengu wa mwaka wa 1914 ulikuwa na tumaini na matarajio mengi mazuri.” Hata hivyo, unabii wa Biblia ulitimia baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu kuanza mwaka huo. Kutokea kwa njaa, matetemeko ya nchi, tauni, na kutimia kwa unabii mwingine wa Biblia kulionyesha wazi kwamba Yesu Kristo alianza kutawala mbinguni akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu katika mwaka wa 1914. * Alipomweka rasmi Mwana wake kuwa Mfalme wa Kimasihi, Yehova alianza kuwa Mfalme kwa njia mpya!

4. Mfalme mpya aliyewekwa rasmi alichukua hatua gani mara moja? Kisha aliwaelekezea nani fikira?

4 Mfalme mpya aliyewekwa rasmi na Mungu alianza kwa kupigana vita na Shetani, Adui mkuu wa Baba yake. Yesu na malaika zake waliwatupa Ibilisi na roho wake waovu kutoka mbinguni. Hilo lilileta shangwe kubwa mbinguni lakini msiba ambao haukuwa umewahi kutokea duniani. (Soma Ufunuo 12:7-9, 12.) Kisha, Mfalme akawaelekezea fikira raia wake walio duniani ili awasafishe, awafundishe, na kuwapanga kufanya mapenzi ya Mungu. Acheni tuone jinsi walivyotuwekea mfano mzuri kwa kutii utawala wa Ufalme katika mambo hayo matatu.

MFALME WA KIMASIHI AWASAFISHA RAIA WAKE WASHIKAMANIFU

5 Baada ya Yesu kusafisha mbingu kwa kuondoa uvutano wote wenye kudhuru wa Shetani na roho waovu, Yehova alimwagiza Mfalme huyo akague na kuwasafisha kiroho wafuasi wake duniani. Nabii Malaki alisema kwamba walitakaswa kiroho. (Mal. 3:1-3) Historia inaonyesha kwamba jambo hilo lilitokea kati ya mwaka wa 1914 na mwanzoni mwa 1919. * Ili tuwe sehemu ya familia ya ulimwenguni pote ya Yehova ni lazima tuwe safi, au watakatifu. (1 Pet. 1:15, 16) Ni lazima tuepuke kuchafuliwa kwa njia yoyote ile na dini ya uwongo au siasa za ulimwengu huu.

6 Kisha, Yesu alitumia mamlaka yake ya kifalme kumweka rasmi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Mtumwa huyo angeandaa kwa ukawaida chakula cha kiroho cha kutosha kilicho bora kwa ajili ya wote walio sehemu ya “kundi moja” lililo chini ya uangalizi wa Yesu. (Mt. 24:45-47; Yoh. 10:16) Kuanzia mwaka wa 1919, kikundi kidogo cha ndugu watiwa-mafuta kimetimiza kwa ushikamanifu jukumu hilo zito la kulisha “watumishi wa nyumbani.” Chakula kingi cha kiroho kinachoandaliwa na kikundi hicho hutusaidia kukua katika imani. Kinaimarisha azimio letu la kuendelea kuwa safi kiroho, kiadili, kiakili, na kimwili. Pia, chakula hicho cha kiroho kinatufundisha na kutuwezesha kuwa na ustadi wa kushiriki kikamili katika kazi muhimu zaidi ya kuhubiri. Je, unatumia kikamili maandalizi hayo?

MFALME AWAFUNDISHA RAIA WAKE KUHUBIRI ULIMWENGUNI POTE

7 Yesu alisema hivi alipoanza huduma yake duniani: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu kwenye majiji mengine pia, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Kwa miaka mitatu  na nusu, kazi hiyo ilikuwa muhimu sana maishani mwa Yesu. Aliwaagiza hivi wanafunzi wake: “Mnapoenda, hubirini, mkisema, ‘Ufalme wa mbinguni umekaribia.’” (Mt. 10:7) Baada ya kufufuliwa, Yesu alitabiri kwamba wafuasi wake wangeeneza ujumbe huo “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Aliahidi kwamba angeitegemeza kazi hiyo muhimu sana mpaka mwisho.—Mt. 28:19, 20.

8 Kufikia mwaka wa 1919, “habari njema ya ufalme” ilikuwa muhimu hata zaidi. (Mt. 24:14) Mfalme alikuwa anatawala mbinguni, na tayari alikuwa amekusanya duniani kikundi kidogo cha raia waliotakaswa. Raia hao walitii kwa haraka agizo hili la Yesu: Hubiri duniani pote habari njema ya Ufalme wa Mungu unaotawala! (Mdo. 10:42) Kwa mfano, mnamo Septemba 1922, wahubiri 20,000 hivi wa Ufalme walihudhuria kusanyiko la kimataifa huko Cedar Point, Ohio, nchini Marekani. Hebu wazia jinsi walivyosisimka Ndugu Rutherford alipotoa hotuba yenye kichwa “Ufalme,” na kisha akatangaza hivi: “Tazameni, Mfalme anatawala! Ninyi ndio mawakili wa kumtangaza. Kwa hiyo, mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.” Wajumbe elfu mbili waliitikia mwito huo kwa kushiriki katika ‘Siku ya pekee ya Utumishi.’ Walihubiri kufikia umbali wa kilomita 72 kutoka katika eneo la kusanyiko. Mjumbe mmoja aliyechochewa na himizo hilo alisema hivi: “Siwezi kamwe kusahau mwito huo wa kutangaza Ufalme na bidii ya umati uliokusanyika!” Wahudhuriaji wengi walikuwa na maoni kama yake.

9, 10. (a) Ni mipango gani ambayo imefanywa ili kuwazoeza watangazaji wa Ufalme? (b) Wewe binafsi umefaidikaje na mazoezi hayo?

9 Kufikia mwaka wa 1922, kulikuwa na watangazaji wa Ufalme zaidi ya 17,000 wenye bidii katika nchi 58 duniani pote. Hata hivyo, walihitaji kuzoezwa. Katika karne ya kwanza, Mfalme Aliyechaguliwa aliwaeleza waziwazi wanafunzi wake ujumbe wa kuhubiri, eneo la kuhubiri, na jinsi ya kuhubiri. (Mt. 10:5-7; Luka 9:1-6; 10:1-11) Vivyo hivyo leo, Yesu anahakikisha kwamba wote wanaoshiriki katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme wanapewa maagizo na vifaa wanavyohitaji ili wahubiri kwa ustadi. (2 Tim. 3:17) Kupitia Kutaniko la Kikristo, Yesu anawazoeza raia wake kwa ajili ya huduma. Anatumia Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ili kuwazoeza raia wake. Shule hiyo inafanywa katika makutaniko zaidi ya 111,000 ulimwenguni pote. Kupitia shule hiyo, wahubiri zaidi ya milioni saba wamezoezwa kikamili kuhubiri na kufundisha kwa njia inayovutia “watu wa namna zote.”—Soma 1 Wakorintho 9:20-23.

10 Zaidi ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, shule nyingine za Biblia zimeanzishwa  ili kuzoeza wazee wa kutaniko, mapainia, ndugu waseja, wenzi wa ndoa Wakristo, washiriki wa Halmashauri za Tawi na wake zao, waangalizi wanaosafiri na wake zao, na wamishonari. * Wanafunzi wa darasa moja la Shule ya Biblia ya Wenzi wa Ndoa Wakristo walisema hivi kwa uthamini kuhusu shule hiyo: “Mazoezi ya pekee tuliyopokea yametusaidia kumpenda zaidi Yehova na kutuzoeza kikamili kuwasaidia wengine.”

11. Wahubiri wa Ufalme wamewezaje kuendelea na kazi ya kuhubiri licha ya upinzani?

11 Adui yetu Shetani anapinga jitihada hizo kubwa za kuhubiri na kufundisha kuhusu Ufalme. Anajaribu kukomesha kazi hiyo kwa kuwashambulia wahubiri wa Ufalme na ujumbe wao. Anafanya hivyo kwa njia ya moja kwa moja au kwa hila. Hata hivyo, jitihada za adui huyo hazitafanikiwa. Yehova amemweka Mwana wake “juu zaidi kuliko kila serikali na mamlaka na nguvu na utawala.” (Efe. 1:20-22) Akiwa Mfalme, Yesu anatumia mamlaka yake kulinda na kuwaongoza wafuasi wake ili kuhakikisha kwamba mapenzi ya Baba yake yanatimizwa. * Habari njema inahubiriwa na mamilioni ya watu wenye mioyo minyoofu wanafundishwa njia za Yehova. Tuna pendeleo kubwa la kushiriki katika kazi hiyo muhimu sana.

MFALME AWAPANGA RAIA WAKE KWA AJILI YA UTENDAJI ZAIDI

12. Ni baadhi ya marekebisho gani yaliyofanywa katika tengenezo tangu Ufalme ulipoanza kutawala?

12 Tangu Ufalme ulipoanza kutawala mwaka wa 1914, Mfalme ameboresha utaratibu wa kitengenezo unaofuatwa na watumishi wa Mungu ili kutimiza mapenzi ya Baba yake. (Soma Isaya 60:17.) Mwaka wa 1919, mkurugenzi wa utumishi aliwekwa rasmi katika kila kutaniko ili kuongoza katika kazi ya kuhubiri. Kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba kila Jumapili ilianzishwa mwaka wa 1927. Wahubiri wa Ufalme walichochewa kuhubiri kwa bidii zaidi mwaka wa 1931 walipoanza kutumia jina la Kimaandiko, Mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:10-12) Mwaka wa 1938, waangalizi katika makutaniko walianza kuwekwa rasmi kitheokrasi badala ya kuchaguliwa kidemokrasia. Mnamo 1972, usimamizi wa kutaniko uliwekwa chini ya baraza la wazee badala ya mwangalizi mmoja wa kutaniko. Wanaume wote waliostahili walihimizwa wafanye maendeleo ili washiriki katika kazi ya ‘kulichunga kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wao.’ (1 Pet. 5:2) Mwaka wa 1976, Baraza Linaloongoza lilipangwa katika halmashauri sita ili kusimamia kazi ya Ufalme  ulimwenguni pote. Kwa kufaa, Mfalme aliyewekwa rasmi na Yehova ameendelea kuwapanga raia wa Ufalme kitheokrasi, yaani, kulingana na utawala wa Mungu.

13. Umenufaikaje na mambo ambayo yametimizwa na utawala wa Ufalme katika muda wa miaka 100?

13 Fikiria mambo ambayo Mfalme wa Kimasihi ametimiza katika miaka 100 ya kwanza ya utawala wake. Amewasafisha watu kwa ajili ya jina la Yehova. Ameongoza kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme katika nchi 239 na kuwafundisha mamilioni ya watu njia za Yehova. Amewakusanya raia zaidi ya milioni saba walio washikamanifu, na kila mmoja wao amejitoa kwa hiari kufanya mapenzi ya Baba yake. (Zab. 110:3) Kwa kweli, Yehova anatimiza kazi kubwa na za ajabu kupitia Ufalme wa Kimasihi. Tunatazamia matukio yenye kusisimua hata zaidi wakati ujao!

BARAKA ZITAKAZOLETWA NA UFALME WA KIMASIHI

14. (a) Tunamwomba Mungu nini tunaposali: “Ufalme wako na uje”? (b) Andiko letu la mwaka wa 2014 ni andiko gani, na kwa nini linafaa?

14 Ingawa Yehova alimvisha taji Mwana wake Yesu Kristo kuwa Mfalme wa Kimasihi mwaka wa 1914, sala ya “Ufalme wako na uje” haikujibiwa kikamili. (Mt. 6:10) Biblia ilitabiri kwamba Yesu ‘angeenda akitiisha katikati ya adui zake.’ (Zab. 110:2) Hata hivyo, bado Ufalme wa Mungu unapingwa na serikali za kibinadamu zinazoongozwa na Shetani. Tunaposali Ufalme wa Mungu uje, tunamwomba Mungu atumie Mfalme wa Kimasihi na watawala wenzake kukomesha utawala wa wanadamu na kuondoa adui za Ufalme walio duniani. Hilo litatimiza maneno ya Danieli 2:44 kwamba Ufalme wa Mungu “utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote.” Utaondoa serikali zinazopinga Ufalme huo. (Ufu. 6:1, 2; 13:1-18; 19:11-21) Hilo litatukia hivi karibuni. Miaka 100 imepita tangu Ufalme wa Mungu ulipoanza kutawala mbinguni. Na inafaa kwamba andiko letu la mwaka wa 2014 ni Mathayo 6:10 linalosema hivi: “Ufalme wako na uje!”

Andiko letu la mwaka wa 2014 ni:“Ufalme wako na uje.”—Mathayo 6:10

15, 16. (a) Ni mambo gani yenye kusisimua yatakayotukia wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja? (b) Mwishowe Yesu, yule Mfalme wa Kimasihi, atafanya nini? Hilo litamaanisha nini kuhusiana na kutimizwa kwa kusudi la Yehova?

15 Baada ya Mfalme wa Kimasihi kuangamiza adui za Mungu, atamtupa Shetani na roho wake waovu ndani ya abiso kwa miaka elfu moja. (Ufu. 20:1-3) Baada ya uvutano mwovu wa Shetani kuondolewa, Ufalme utaanza kuwasaidia watu kunufaika na faida za dhabihu ya fidia ya Yesu, nao utaondoa kabisa madhara ya dhambi ya Adamu. Mfalme huyo atafufua mamilioni ya wafu na kupanga programu kubwa ya elimu ili wafundishwe kumhusu Yehova. (Ufu. 20:12, 13) Dunia nzima itakuwa paradiso kama bustani ya Edeni. Wanadamu wote waaminifu watakuwa wakamilifu.

16 Mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo, Ufalme wa Kimasihi utakuwa umetimiza kusudi lake. Kisha Yesu atamkabidhi Baba yake Ufalme. (Soma 1 Wakorintho 15:24-28.) Hakutakuwa tena na uhitaji wa kuwa na mpatanishi kati ya Yehova na watoto wake walio duniani. Wana wote wa Mungu walio mbinguni na watoto wake walio duniani wataungana na Baba yao wa mbinguni na kuwa washiriki wa familia yake ya ulimwenguni pote.

17. Umeazimia kufanya nini kuhusu Ufalme?

17 Matukio yenye kusisimua katika miaka 100 ya utawala wa Ufalme yanatuhakikishia kwamba Yehova hajapoteza mamlaka yake na atatimiza kusudi lake kwa ajili ya dunia. Acheni tuendelee kuwa raia wake washikamanifu na kumtangaza Mfalme na Ufalme wake. Tunafanya hivyo tukiwa na uhakika kabisa kwamba hivi karibuni Yehova atajibu sala hii tunayotoa kwa bidii: “Ufalme wako na uje”!

^ fu. 10 Tazama Mnara wa Mlinzi, Septemba 15, 2012, ukurasa wa 13-17, chini ya kichwa “Shule za Kitheokrasi Zinathibitisha Upendo wa Yehova.”

^ fu. 11 Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1998, ukurasa wa 19-22, linaonyesha ushindi wa kisheria tuliopata katika nchi kadhaa.