Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Ufalme wa Masiya Umetimiza Nini Katika Miaka Hii 100?

Ufalme wa Masiya Umetimiza Nini Katika Miaka Hii 100?

‘Matendo yako ni makubwa na ya ajabu, Yehova Mungu, . . . Mufalme wa umilele.’​—UFU. 15:3.

1, 2. Ufalme wa Mungu utafanya nini, na sababu gani tunaweza kuwa hakika kwamba Ufalme huo utakuja?

 KATIKA mwaka wa 31, kwenye mulima ulio karibu na muji wa Kapernaumu, Yesu alifundisha wafuasi wake kusali hivi: ‘Ufalme wako uje.’ (Mt. 6:10) Leo, wengi wanafikiri kwamba Ufalme huo hautakuja hata kidogo. Lakini, sisi tuko hakika kwamba Mungu atajibu sala zetu za kuomba Ufalme wake uje.

2 Yehova atatumia Ufalme huo ili kuunganisha familia yake mbinguni na duniani. Kusudi hilo la Mungu litatimia. (Isa. 55:10, 11) Bila shaka, tayari Yehova amekuwa Mufalme katika siku zetu! Mambo yenye kupendeza ambayo yametokea katika miaka 100 ambayo imepita yanahakikisha jambo hilo. Mungu anatimiza mambo makubwa na mazuri kwa ajili ya mamilioni ya raia wake waaminifu. (Zek. 14:9; Ufu. 15:3) Lakini, Yehova kuwa Mufalme ni tofauti na kuja kwa Ufalme wa Mungu, ambao Yesu alitufundisha tusali kwa ajili yake. Mambo hayo mawili yanatofautiana namna gani, na yanatuhusu namna gani?

MUFALME YESU ANAANZA KUFANYA KAZI

3. (a) Yesu aliwekwa kuwa Mufalme wakati gani na wapi? (b) Namna gani unaweza kuonyesha mutu kwamba Ufalme wa Mungu ulianza kutawala katika mwaka wa 1914? (Soma maelezo yaliyo chini.)

3 Miaka 20 hivi mbele ya mwaka wa 1900, watumishi wa Mungu walianza kuelewa unabii ambao Danieli aliandika zaidi ya miaka 2 500 iliyopita. Unabii huo unasema hivi: “Katika siku za wafalme hao, Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe.” (Dan. 2:44) Kwa miaka mingi Wanafunzi wa Biblia walitangaza jambo la maana sana lingetokea katika mwaka wa 1914. Watu wengi wa wakati huo walitazamia mambo mazuri. Kwa mufano, muandikaji mumoja alisema: “Ulimwengu wa 1914 ulijaa tumaini na ahadi.” Lakini, Vita ya Kwanza ya Ulimwengu iliyotokea baadaye katika mwaka huo, ilitimiza unabii wa Biblia. Njaa, matetemeko ya inchi, na magonjwa ya kuambukiza yaliyotokea kisha vita hiyo na vilevile mambo mengine yaliyotimiza unabii wa Biblia yalionyesha kwamba Yesu Kristo alikuwa ameanza kutawala akiwa Mufalme wa Ufalme wa Mungu katika mwaka wa 1914. * Kwa kumuweka Mwana wake kuwa Mufalme wa Kimasiya, Yehova alikuwa kabisa Mufalme katika maana ingine!

4. Ni jambo gani ambalo Mufalme mupya alifanya mara moja kisha tu kuwekwa kuwa Mufalme, na kisha alikazia uangalifu wake wapi?

4 Jambo la kwanza ambalo Mufalme wa Ufalme wa Mungu alipaswa kufanya lilikuwa kupigana vita na Shetani, Adui mukubwa wa Baba yake. Yesu na malaika wake walifukuza Shetani na mashetani wake mbinguni. Jambo hilo lilitokeza shangwe mbinguni lakini lilitokeza taabu ambayo ilikuwa haijatokea duniani. (Soma Ufunuo 12:7-9, 12.) Kisha, Mufalme alikazia uangalifu wake kuelekea raia wake walio duniani ili awasafishe, awafundishe, na kuwapanga vizuri ili wafanye mapenzi ya Mungu. Acheni tuone namna walivyotuachia mufano muzuri kwa kukubali Mufalme awasaidie katika njia hizo tatu.

MUFALME WA KIMASIYA ANASAFISHA RAIA WAKE WAAMINIFU

5. Ni usafishaji gani uliofanywa kati ya mwaka wa 1914 mupaka mwanzoni mwa mwaka wa 1919?

5 Kisha Mufalme kusafisha mbingu kwa kuondoa Shetani na mashetani wake, Yehova alimuomba achunguze na kusafisha hali ya kiroho ya wafuasi wake walio duniani. Nabii Malaki alizungumuzia jambo hilo kuwa kutakaswa kiroho. (Mal. 3:1-3) Historia inaonyesha kwamba jambo hilo lilitokea kati ya mwaka wa 1914 mupaka mwanzoni mwa mwaka wa 1919. * Ili tuwe katika familia ya Yehova ya ulimwenguni pote, tunapaswa kuwa safi, ao watakatifu. (1 Pet. 1:15, 16) Tunapaswa kujiepusha na uchafu wowote wa dini za uongo na siasa za ulimwengu huu.

6. Ni nani anayetutolea chakula cha kiroho, na kwa nini ni cha lazima sana?

6 Kisha Yesu alitumia mamlaka yake ya kifalme ili kumuweka ‘mutumwa mwaminifu na mwenye busara.’ Mutumwa huyo alipaswa kutoa chakula cha kiroho kinachofaa kwa ukawaida kwa wote walio katika “kundi moja” linaloongozwa na Yesu. (Mt. 24:45-47; Yoh. 10:16) Kuanzia mwaka wa 1919, mutumwa mwaminifu na mwenye busara ametimiza kwa uaminifu daraka nzito la kukulisha “watumishi wa nyumbani.” Chakula cha kiroho ambacho tunapata kwa uwingi kupitia mutumwa huyo kinatusaidia tukomae kiroho, kinatuchochea tuazimie kuwa na mwenendo safi, tubaki safi kiroho, kiakili, na kimwili. Pia, kupitia chakula hicho tunapata mafundisho na vifaa tunavyohitaji ili tufanye kazi ya maana sana inayofanywa duniani leo, ni kusema, kuhubiri habari njema. Je, unafaidika kabisa na chakula hicho?

MUFALME ANAFUNDISHA RAIA WAKE KUHUBIRI DUNIANI POTE

7. Ni kazi gani ya maana ambayo Yesu alianzisha alipokuwa duniani, na kazi hiyo ingeendelea mupaka wakati gani?

7 Yesu alipoanza kazi yake ya kuhubiri duniani, alisema hivi: “Ni lazima nitangaze habari njema ya Ufalme wa Mungu kwenye majiji mengine pia, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Lu. 4:43) Kwa miaka mitatu na nusu, Yesu alitia kazi hiyo pa nafasi ya kwanza katika maisha yake. Aliagiza wanafunzi wake hivi: “Munapoenda, muhubiri, mukisema: ‘Ufalme wa mbinguni umekaribia.’” (Mt. 10:7) Kisha kufufuliwa, Yesu alitabiri kwamba wafuasi wake wangefikisha ujumbe huo ‘mupaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.’ (Mdo. 1:8) Aliwaahidi kwamba yeye mwenyewe angewategemeza katika kazi hiyo kuanzia wakati huo mupaka leo.​—Mt. 28:19, 20.

8. Namna gani Mufalme alichochea raia wake wa dunia ili watende?

8 Katika mwaka wa 1919, kazi ya kuhubiri “habari njema ya Ufalme” ilitiliwa mukazo sana. (Mt. 24:14) Mufalme alikuwa akitawala mbinguni, na alikuwa amekusanya duniani kikundi kidogo cha raia wake wenye kusafishwa. Walikubali kwa furaha maagizo ya Yesu ya kuhubiri duniani pote habari njema ya Ufalme ambao ulikuwa umeanza kutawala! (Mdo. 10:42) Kwa mufano, katika Mwezi wa 9, 1922, wategemezaji wa Ufalme karibu 20000 walikusanyika kwenye mukusanyiko wa kimataifa katika Cedar Point, Ohio, Amerika. Wazia namna walivyosisimuka wakati Ndugu Rutherford alitoa hotuba yenye kichwa “Ufalme” na aliposema hivi: “Tazameni, Mufalme anatawala! Ninyi ndio mawakili wake. Kwa hiyo tangazeni, tangazeni, tangazeni, Mufalme na ufalme wake.” Ndugu na dada elfu mbili walikubali mualiko huo kwa kushiriki katika “Siku ya Pekee ya mahubiri.” Walienda kuhubiri umbali wa kilometre 72 kutoka mahali pa mukusanyiko. Kwa sababu ya kuchochewa na maneno hayo, ndugu mumoja alisema hivi: “Siwezi kusahau hata kidogo tangazo hilo na bidii ya watu wengi waliokusanyika siku hiyo.” Wengi walikuwa na maoni hayo.

9, 10. (a) Ni mipango gani ambayo imefanywa ili kuzoeza watangazaji wa Ufalme? (b) Namna gani unafaidika na mazoezi hayo?

9 Katika mwaka wa 1922, watangazaji wa Ufalme zaidi ya 17 000 walikuwa wakihubiri katika inchi 58. Lakini, walihitaji mazoezi. Wakati wa mitume, Mufalme Aliyechaguliwa alitolea wanafunzi wake maagizo yaliyokuwa wazi kuhusu kazi ya kuhubiri, ni kusema, wangehubiri ujumbe gani, wapi, na namna gani. (Mt. 10:5-7; Lu. 9:1-6; 10:1-11) Leo pia, Yesu anafanya mipango ili wale wote wanaohubiri wapate maagizo na anawatolea vyombo vya kutumia ili wafanye kazi yao ya kuhubiri vizuri. (2 Tim. 3:17) Kupitia kutaniko la Kikristo, Yesu anazoeza raia wake kwa ajili ya kazi ya kuhubiri. Njia moja anayotumia ili kuwazoeza ni Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi, ambayo inaongozwa katika makutaniko zaidi ya 111 000 duniani pote. Masomo hayo yanawazoeza wahubiri zaidi ya milioni saba ili wahubiri na kufundisha kwa njia yenye kuvutia “watu wa namna zote.”​—Soma 1 Wakorintho 9:20-23.

10 Zaidi ya Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi, kuna masomo mengine ambayo yameanzishwa ili kuzoeza wazee wa makutaniko, mapainia, ndugu wasio na bibi, ndugu na bibi zao, washiriki wa halmashauri ya Biro ya Tawi na bibi zao, waangalizi wenye kusafiri na bibi zao, na wamisionere. * Ili kuonyesha shukrani yao, wanafunzi fulani wa Masomo kwa Ajili ya Ndugu na Bibi Zao walisema hivi: “Mazoezi ya pekee ambayo tumepata yametufanya tumupende Yehova sana na tumezoezwa vizuri zaidi ili kuwasaidia wengine.”

11. Namna gani watangazaji wa Ufalme wameendelea kuhubiri ijapokuwa wanashambuliwa na Shetani?

11 Shetani anaona jitihada hizo zinazofanywa ili kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Ili kujaribu kusimamisha kazi ya kuhubiri, Shetani anashambulia ujumbe wa Ufalme na wahubiri kwa njia ya waziwazi na ile isiyo ya waziwazi. Lakini ameshindwa. Yehova amemuweka Mwana wake “juu zaidi kuliko kila serikali na mamlaka na nguvu na utawala.” (Efe. 1:20-22) Mufalme Yesu anatumia mamlaka yake ili kulinda na kuongoza wanafunzi wake ili mapenzi ya Baba yake yafanywe. * Habari njema inahubiriwa, na mamilioni ya watu wanaopenda haki wanajifunza njia za Yehova. Ni pendeleo kushiriki katika kazi hiyo ya maana!

MUFALME ANAWAPANGA VIZURI RAIA WAKE ILI WAFANYE KAZI KUBWA ZAIDI

12. Eleza mabadiliko fulani ambayo yamefanywa tangu Ufalme wa Mungu uanze kutawala.

12 Tangu Ufalme wa Mungu uanze kutawala katika mwaka wa 1914, Mufalme amepanga vizuri watumishi wa Mungu ili wafanye mapenzi ya Baba yake. (Soma Isaya 60:17.) Katika mwaka wa 1919, musimamizi wa utumishi aliwekwa katika kila kutaniko ili kuongoza kazi ya kuhubiri. Katika mwaka wa 1927, kila kutaniko lilianza kuhubiri nyumba kwa nyumba kila Siku ya Yenga. Wategemezaji wa Ufalme walichochewa kuhubiri kwa bidii katika mwaka 1931 walipokubali jina lililo katika Biblia la Mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:10-12) Katika mwaka wa 1938, ndugu wenye madaraka katika kutaniko hawakuchaguliwa tena kidemokrasia, lakini walianza kuchaguliwa kwa njia ya kiteokrasi. Katika mwaka wa 1972, makutaniko yalianza kusimamiwa na mabaraza ya wazee kuliko kusimamiwa na muzee mumoja tu. Wanaume wote wenye kustahili kutumikia kama wazee na watumishi wa huduma walitiwa moyo wawe tayari ‘kulichunga kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wao.’ (1 Pet. 5:2) Katika mwaka wa 1976, Baraza Linaloongoza lilipangwa katika halmashauri sita ili kusimamia kazi ya Ufalme duniani pote. Kwa hiyo, Mufalme ambaye amewekwa na Yehova ameendelea kupanga raia wake hatua kwa hatua kwa njia ya kiteokrasi, ao yenye kuongozwa na Mungu.

13. Ni mambo gani ambayo Ufalme wa Masiya umetimiza katika miaka hii 100?

13 Fikiria yale ambayo Mufalme wa Kimasiya ametimiza katika miaka hii 100 ya kwanza ya utawala wake. Amesafisha kikundi fulani cha watu ili watetee jina la Yehova. Ameongoza kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme katika inchi 239 na amefundisha mamilioni ya watu njia za Yehova. Ameunganisha raia waaminifu zaidi ya milioni saba, na kila mumoja wao anajitoa kwa kujipendea ili kufanya mapenzi ya Baba yake. (Zab. 110:3) Bila shaka, chini ya utawala wa Ufalme wa Masiya kazi kubwa na yenye kupendeza imefanywa. Mambo mengine yenye kupendeza yangali mbele!

BARAKA ZA WAKATI UJAO

14. (a) Tunaposali: ‘Ufalme wako uje,’ tunamuomba Mungu afanye nini? (b) Andiko la mwaka wa 2014 ni andiko gani, na sababu gani linafaa?

14 Hata ikiwa Yesu alianza kutawala katika mwaka wa 1914, tukio hilo halikuwa jibu kamili kwa sala tunayotoa ili ‘Ufalme uje.’ (Mt. 6:10) Ilitabiriwa katika Biblia kwamba Yesu angepaswa ‘kuenda kutiisha katikati ya adui zake.’ (Zab. 110:2) Serikali za wanadamu zinazoongozwa na Shetani zingali zinapinga Ufalme wa Mungu. Tunaposali, Ufalme wa Mungu uje, tunamuomba Mungu kwamba Mufalme wa Kimasiya na wale watakaotawala pamoja naye waje kumaliza utawala wa wanadamu na kuondoa maadui wote wa Ufalme wa Mungu. Tukio hilo litatimiza maneno ya Danieli 2:44 yanayoonyesha kwamba Ufalme wa Mungu “utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote.” Utaondoa viongozi wa serikali wanaopinga Ufalme wa Mungu. (Ufu. 6:1, 2; 13:1-18; 19:11-21) Jambo hilo liko karibu sana kutokea. Wakati huu ambao Ufalme wa Mungu unatimiza miaka 100, andiko letu la mwaka linafaa kabisa, andiko hilo ni Mathayo 6:10: ‘Ufalme wako uje’!

15, 16. (a) Ni mambo gani yenye kupendeza yatakayofanyika katika Utawala wa Miaka Elfu Moja? (b) Ni jambo gani la mwisho ambalo Mufalme wa Kimasiya atafanya, na hilo litakuwa na matokeo gani juu ya kusudi la Yehova?

15 Kisha Mufalme wa Kimasiya kuharibu maadui wa Mungu, atatupa Shetani na mashetani wake katika abiso kwa miaka elfu moja. (Ufu. 20:1-3) Watakapokuwa katika kifungo hicho, Ufalme wa Mungu utaendelea kutolea watu baraka zinazotokana na zabihu ya Yesu na utamaliza matokeo yote ya zambi ya Adamu. Mufalme atafufua mamilioni ya wale wanaolala katika makaburi na ataanzisha programe kubwa ya kuwafundisha mapenzi ya Yehova. (Ufu. 20:12, 13) Dunia nzima itakuwa paradiso kama bustani ya Edeni. Wanadamu wote waaminifu watafanywa kuwa wakamilifu.

16 Mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo, Ufalme wa Masiya utakuwa umetimiza kusudi lake. Kisha Yesu atamurudishia Baba yake Ufalme. (Soma 1 Wakorintho 15:24-28.) Hakutakuwa tena uhitaji wa kuwa na mupatanishi kati ya Yehova na watoto wake wa duniani. Wana wote wa Mungu mbinguni na duniani wataungana na Baba yao wa Mbinguni na kufanyiza familia moja ya Mungu ya ulimwenguni pote.

17. Unaazimia kufanya nini kuhusiana na Ufalme?

17 Mambo yenye kupendeza ambayo Ufalme wa Masiya umetimiza katika miaka hii 100 yanatuhakikishia kwamba Yehova anaongoza mambo na kwamba kusudi lake kuelekea dunia litatimia. Acheni tuendelee kuwa raia wake waaminifu na kutangaza Mufalme na Ufalme wake. Tunaazimia hivyo tukiwa hakika kwamba hivi karibuni Yehova atajibu sala tunayotoa kwa bidii ili ‘Ufalme wake uje’!

^ Soma habari “Masomo Mbalimbali Yanayoongozwa na Tengenezo la Mungu Yanaonyesha Upendo wa Yehova” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15/09/2012, ukurasa wa 13-17.

^ Soma Munara wa Mulinzi wa tarehe 01/12/1998, ukurasa wa 19-22, ili upate mifano fulani ya ushindi ambao tumepata kwenye mahakama ya inchi mbalimbali.

Andiko letu la mwaka wa 2014: ‘Ufalme wako uje.’​—Mathayo 6:10