Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU

Vita Vilivyoubadili Ulimwengu

Vita Vilivyoubadili Ulimwengu

Miaka mia moja iliyopita, mamilioni ya vijana waliondoka makwao kwenda vitani. Walikuwa na msisimuko mwingi uliochochewa na uzalendo. Mjitoleaji mmoja kutoka Marekani aliandika hivi katika mwaka wa 1914: “Nina furaha na msisimuko kuhusu siku nzuri zijazo.”

Hata hivyo, punde si punde msisimuko wao uligeuka ukawa huzuni. Hakuna mtu aliyewazia kwamba wanajeshi hao wengi wangekabiliana na hali ngumu kwa miaka mingi huko Ubelgiji na Ufaransa. Wakati huo, vita hivyo viliitwa, “Vita Vikuu.” Leo vinajulikana kama Vita vya Kwanza vya Ulimwengu.

Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilikuwa vikuu kwa sababu ya idadi ya watu walioathiriwa. Makadirio fulani yanaonyesha kwamba watu milioni 10 hivi walikufa na milioni 20 wakalemazwa. Pia, vilikuwa vikuu kwa sababu vilisababishwa na makosa makubwa. Wanasiasa wa Ulaya walishindwa kuzuia mizozo ya kimataifa kulipuka na kuwa vita vya ulimwenguni pote. Jambo muhimu hata zaidi ni kwamba “Vita Vikuu” viliuharibu kabisa ulimwengu. Viliubadili ulimwengu katika njia ambayo bado inatuathiri hata sasa.

 MAKOSA YALIYOSABABISHA KUTOKUAMINIANA

Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilisababishwa na maamuzi mabaya. Viongozi barani Ulaya walitenda kama “kizazi cha watu wanaotembea wakiwa usingizini ambao walijikwaa na kuanguka kwenye msiba wakati wa kipindi kitulivu katika majira ya kiangazi ya 1914,” kinasema kitabu kimoja cha kihistoria (The Fall of the Dynasties—The Collapse of the Old Order 1905-1922).

Majuma machache tu baada ya kuuawa kwa mwana mfalme wa Austria, serikali zote kuu za Ulaya zilijiingiza katika vita ambavyo havikutazamiwa. “Vita hivyo vilianzaje?” akauliza kiongozi wa Ujerumani siku chache baada ya vita hivyo kuanza. “Hakuna ajuaye,” akajibu kwa huzuni.

Viongozi waliofanya maamuzi hayo mabaya ambayo yaliongoza kwenye vita hivyo hawakujua hata kidogo matokeo yangekuwaje. Lakini wanajeshi waliokuwa wakipigana kwenye mahandaki walianza kuona ukweli wa mambo. Wanasiasa wao walikuwa wamewakatisha tamaa, viongozi wao wa kidini walikuwa wamewadanganya, na majenerali wao walikuwa wamewasaliti. Jinsi gani?

Wanasiasa wao walikuwa wamewakatisha tamaa, viongozi wao wa kidini walikuwa wamewadanganya, na majenerali wao walikuwa wamewasaliti

Wanasiasa waliahidi kwamba vita hivyo vingeleta ulimwengu mpya ulio bora. Kiongozi wa Ujerumani alitangaza hivi: “Tunapigana ili kulinda matunda ya kazi yetu ya jasho tuliyofanya wakati wa amani, kulinda desturi na tamaduni tulizorithi na wakati wetu ujao.” Rais Woodrow Wilson wa Marekani alishiriki kutunga msemo huu unaojulikana sana ili kuwatuliza watu: Vita hivyo “vitaleta demokrasia ulimwenguni.” Huko Uingereza watu walidhani kwamba vingekuwa “vita vya kukomesha vita.” Lakini wote walikuwa wamekosea.

Viongozi wa kidini waliunga mkono vita hivyo kwa moyo wote. “Viongozi wa kidini walipaswa kuwafundisha watu Biblia badala ya kuwatia moyo waende vitani. Vita hivyo viliwachochea watu wachukiane,” kinasema kitabu kimoja cha kihistoria (The Columbia History of the World). Viongozi wa kidini walichochea chuki badala ya kuikomesha. Kitabu kimoja (A History of Christianity) kinasema hivi: “Makasisi hawakuweza, na kwa sehemu kubwa hawakutaka, kutanguliza imani ya Kikristo badala ya utaifa. Wengi wao walichagua njia ya mkato kwa kuuhusianisha Ukristo na uzalendo. Wanajeshi Wakristo wa dini zote walihimizwa wauane katika jina la Mwokozi wao.”

Majenerali waliahidi kwamba wanajeshi wangepata ushindi haraka na kwa urahisi, lakini haikuwa hivyo. Muda si muda, majeshi yaliyokuwa yakipigana yalishindwa kuafikiana na kufanya hali iwe ngumu. Mwanahistoria fulani alisema kwamba mamilioni ya wanajeshi walikabili kile walichokiita “ukatili mbaya sana wa kimwili na kihisia ambao mwanadamu anaweza kukabili.” Licha ya kuuawa kwa wanajeshi wengi, majenerali waliendelea kuwatuma wanajeshi kwenye mstari wa mbele vitani ambapo walifyatuliana risasi. Si ajabu kwamba wanajeshi wengi waliasi.

Vita vya Kwanza vya Ulimwengu viliathirije watu? Kitabu kimoja cha kihistoria kilimnukuu mwanajeshi mstaafu aliyesema hivi: “Vita hivyo . . . viliathiri fikira na tabia ya kizazi kizima.” Kwa sababu ya vita hivyo, miliki nzimanzima zilitoweka. Vita hivyo vilivyosababisha maafa makubwa vilikuwa mwanzo tu wa karne yenye umwagaji mwingi sana wa damu katika historia ya mwanadamu. Mapinduzi na maandamano yakawa mambo ya kawaida.

Kwa nini vita hivyo vilivuruga sana ulimwengu? Je, vita hivyo vilitukia tu bila kutazamiwa? Je, majibu ya maswali hayo yanafunua lolote kuhusu wakati wetu ujao?