Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Majibu ya Maswali ya Biblia

Majibu ya Maswali ya Biblia

Je, kweli Biblia ni Neno la Mungu?

Mtu angetazamia Neno la Mungu liwe la pekee, na ndivyo Biblia ilivyo. Nakala nyingi sana za Biblia zimechapishwa katika lugha nyingi. Hekima inayopatikana katika Biblia inaweza kubadili watu wawe na mwenendo mzuri.Soma 1 Wathesalonike 2:13; 2 Timotheo 3:16.

Tunajua kwamba Biblia ni Neno la Mungu kwa sababu inatabiri kwa usahihi wakati ujao. Hakuna mwanadamu anayeweza kufanya hivyo kwa uwezo wake mwenyewe. Kwa mfano, hebu fikiria unabii wa kitabu cha Isaya. Nakala ya kitabu hicho iliyoandikwa zaidi ya miaka mia moja kabla ya Yesu kuzaliwa ilipatikana kwenye pango lililo karibu na Bahari ya Chumvi. Unabii huo ulitabiri kwamba jiji la Babiloni lingeachwa ukiwa. Hilo lilitimia kwa mara ya kwanza miaka mingi baada ya Yesu kurudi mbinguni.Soma Isaya 13:19, 20; 2 Petro 1:20, 21.

Biblia iliandikwaje?

Biblia iliandikwa kwa kipindi cha karibu miaka 1,600. Iliandikwa na watu 40 hivi, na walifuata kichwa kimoja kikuu bila kupingana. Hilo liliwezekanaje? Mungu aliwaongoza.Soma 2 Samweli 23:2.

Nyakati nyingine Mungu alizungumza na waandikaji wa Biblia kupitia malaika, maono, au ndoto. Kwa kawaida, Mungu aliweka mawazo yake katika fikira za mwandikaji na kumruhusu achague maneno ambayo angetumia kutangaza ujumbe wa Mungu.Soma Ufunuo 1:1; 21:3-5.