Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Msifuni Kristo—Mfalme Mtukufu!

Msifuni Kristo—Mfalme Mtukufu!

Katika fahari yako endelea mpaka ufanikiwe.”—ZAB. 45:4.

1, 2. Kwa nini tunapendezwa na Zaburi ya 45?

MFALME mtukufu anapanda ili kutetea kweli na uadilifu na kuwashinda adui zake. Baada ya kuwashinda katika vita vya mwisho, anafunga ndoa na bibi-arusi mrembo. Mfalme huyo anakumbukwa na kusifiwa katika vizazi vyote. Hiyo ndiyo habari kuu katika Zaburi ya 45.

2 Hata hivyo, Zaburi ya 45 si hadithi tu yenye kusisimua na yenye kufurahisha. Matukio yanayotajwa katika zaburi hiyo yana maana kwetu. Yanahusu maisha yetu ya sasa na ya wakati ujao. Basi, acheni tuchunguze kwa makini zaburi hiyo.

“MOYO WANGU UMESISIMUKA KWA SABABU YA JAMBO JEMA”

3, 4. (a) Ni ‘jambo gani jema’ linalotuhusu, na linaweza kuwa na matokeo gani kwa moyo wetu? (b) ‘Kazi zetu zinamhusuje mfalme,’ na ulimi wetu ni kama kalamu jinsi gani?

3 Soma Zaburi 45:1. “Jambo jema” linalogusa moyo wa mtunga-zaburi na kuufanya ‘usisimuke’ linamhusu mfalme. Kitenzi cha Kiebrania kilichotafsiriwa “umesisimuka,” kiasili kilimaanisha “umebubujika,” au “umechemka.” Jambo hilo liliufanya moyo wa mtunga-zaburi uchemke kwa msisimuko na ulimi wake uwe kama “kalamu ya mwandikaji stadi.”

 4 Namna gani sisi? Habari njema ya Ufalme wa Kimasihi ni jambo jema linalogusa moyo wetu. Ujumbe wa Ufalme ulikuwa hasa jambo “jema” katika mwaka wa 1914. Tangu wakati huo, ujumbe huo hauhusu tena Ufalme utakaotawala wakati ujao, bali unahusu serikali halisi inayotawala mbinguni sasa. Hiyo ndiyo “habari njema ya ufalme” tunayohubiri “katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14) Je, moyo wetu ‘unasisimuliwa’ na ujumbe wa Ufalme? Je, tunahubiri habari njema ya Ufalme kwa bidii? Sawa na mtunga-zaburi, ‘kazi zetu zinamhusu mfalme’—Mfalme wetu Yesu Kristo. Tunamtangaza kuwa Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi aliyetawazwa mbinguni. Isitoshe, tunawaalika watu wote, yaani, watawala na wale wanaotawaliwa, wajinyenyekeze chini ya ufalme wake. (Zab. 2:1, 2, 4-12) Na ulimi wetu ni kama “kalamu ya mwandikaji stadi” kwa kuwa tunapohubiri, tunatumia kikamili Neno lililoandikwa, Biblia.

Tunahubiri kwa shangwe habari njema kumhusu Mfalme wetu Yesu Kristo

‘UVUTIO HUMIMINIKA KUTOKA KWENYE MIDOMO YA MFALME’

5. (a) Yesu alikuwa na “sura nzuri” katika njia zipi? (b) ‘Uvutio ulimiminika jinsi gani kutoka kwenye midomo ya Mfalme,’ na tunawezaje kujitahidi kuiga mfano wake?

5 Soma Zaburi 45:2. Maandiko hayasemi mengi kuhusu sura au umbo la Yesu. Bila shaka, Yesu alikuwa na “sura nzuri” kwa sababu alikuwa mtu mkamilifu. Hata hivyo, Yesu alivutia kwa njia ya pekee sana kwa sababu ya uaminifu na utimilifu wake usioyumba-yumba kwa Yehova. Isitoshe, Yesu alihubiri ujumbe wa Ufalme ‘kwa njia yenye kuvutia.’ (Luka 4:22; Yoh. 7:46) Je, tunajitahidi kibinafsi kuiga mfano wake tunapohubiri na kujitahidi kutumia maneno yanayogusa mioyo ya watu?—Kol. 4:6.

6 Yehova alimbariki Yesu katika huduma yake duniani na kumpa thawabu baada ya kifo chake cha kidhabihu kwa sababu Yesu alimtumikia kwa moyo wote. Mtume Paulo aliandika hivi: “Zaidi ya hayo, [Yesu] alipojikuta katika umbo la mwanadamu, alijinyenyekeza naye akawa mtiifu mpaka kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso. Kwa sababu hii pia Mungu alimpandisha kwenye cheo cha juu zaidi na kumpa kwa fadhili jina lililo juu ya kila jina lingine, ili katika jina la Yesu kila goti lipigwe la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya nchi, na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.” (Flp. 2:8-11) Yehova ‘alimbariki Yesu mpaka wakati usio na kipimo,’ yaani, milele, kwa kumfufua na kumpa uhai usioweza kufa.—Rom. 6:9.

MFALME AKWEZWA KULIKO ‘WENZAKE’

7. Mungu alimtiaje Yesu mafuta ‘kuliko wenzake’?

7 Soma Zaburi 45:6, 7Yehova alimtia mafuta Yesu kuwa Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi kwa sababu Yesu alipenda sana uadilifu na kuchukia kitu chochote kinachoweza kumvunjia heshima Baba yake, Yehova. Yesu alitiwa “mafuta ya kushangilia” kuliko ‘wenzake,’ yaani, wafalme wa Yuda wa ukoo wa Daudi. Jinsi gani? Kwanza, Yesu alitiwa mafuta na Yehova mwenyewe. Isitoshe, Yehova alimtia mafuta ili awe Mfalme na Kuhani Mkuu. (Zab. 2:2; Ebr. 5:5, 6) Zaidi ya hayo, Yesu alitiwa mafuta  kwa roho takatifu, na ufalme wake ni wa mbinguni si wa duniani.

8. ‘Mungu ni kiti cha ufalme cha Yesu’ jinsi gani, na kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba ufalme wake ni wa uadilifu?

8 Yehova alimweka Mwana wake kuwa Mfalme wa Kimasihi mbinguni katika mwaka wa 1914. ‘Fimbo ya enzi ya ufalme wake ni fimbo ya unyoofu,’ na hilo linatuhakikishia kwamba anatawala kwa uadilifu na haki. Mamlaka yake ni halali kwa kuwa ‘Mungu ni kiti chake cha ufalme.’ Yaani, Yehova ndiye msingi wa ufalme wake. Zaidi ya hayo, kiti cha ufalme cha Yesu kitadumu “mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.” Je, hujivunii kumtumikia Yehova chini ya Mfalme huyo mwenye nguvu aliyemchagua?

MFALME ‘AJIFUNGA UPANGA WAKE’

9, 10. (a) Kristo alijifunga upanga wake wakati gani, naye aliutumiaje bila kukawia? (b) Kristo atautumiaje upanga wake wakati ujao?

9 Soma Zaburi 45:3. Yehova anamwagiza Mfalme wake ‘ajifunge upanga wake kwenye paja lake,’ na hivyo anampa Yesu mamlaka ya kupigana vita na wote wanaopinga enzi kuu ya Mungu na pia kutekeleza hukumu Zake. (Zab. 110:2) Kristo anaitwa “mwenye nguvu” kwa sababu yeye ni Mfalme na Shujaa asiyeshindwa. Alijifunga upanga wake mwaka wa 1914 alipomshinda Shetani na roho wake waovu na kuwatupa kutoka mbinguni hadi kwenye ujirani wa dunia.—Ufu. 12:7-9.

10 Huo ulikuwa mwanzo tu wa ushindi wa Mfalme huyo. Ni lazima ‘akamilishe ushindi wake.’ (Ufu. 6:2) Ni lazima hukumu za Yehova zitekelezwe juu ya sehemu zote za mfumo wa Shetani duniani na ni lazima Shetani na roho wake waovu waangamizwe. Kwanza, Babiloni Mkubwa, yaani, milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo itaharibiwa. Yehova anakusudia kuwatumia watawala wa kisiasa kumharibu “kahaba” huyo mwovu. (Ufu. 17:16, 17) Kisha, Mfalme huyo Shujaa atageukia mfumo wa kisiasa wa Shetani na kuuharibu kabisa. Halafu, Kristo, anayeitwa pia “malaika wa abiso,” atakamilisha ushindi wake kwa kumtupa Shetani na roho wake waovu ndani ya abiso. (Ufu. 9:1, 11; 20:1-3) Acheni tuone jinsi Zaburi ya 45 ilivyotabiri matukio hayo yenye kusisimua.

MFALME APANDA “KWA KUTETEA KWELI”

11. Kristo anapanda “kwa kutetea kweli” jinsi gani?

11 Soma Zaburi 45:4. Mfalme huyo Shujaa hapigani vita vya ushindi ili kumiliki nchi mbalimbali na kuwatiisha watu. Anapigana vita vya uadilifu kwa makusudi yafaayo. Anapanda “kwa kutetea kweli na unyenyekevu na uadilifu.” Kweli muhimu zaidi ambayo ni lazima itetewe inahusu enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu mzima. Shetani alipomwasi Yehova, alitilia shaka haki ya Yehova ya kutawala. Tangu wakati huo, kweli hiyo ya msingi imepingwa na roho waovu na wanadamu pia. Sasa, wakati umefika wa Mfalme aliyetiwa mafuta na Yehova kupanda ili kutetea kweli kuhusu enzi kuu ya Yehova kwa umilele wote.

12. Mfalme anapandaje ‘kwa kutetea unyenyekevu’?

12 Mfalme huyo anapanda pia ‘kwa kutetea unyenyekevu.’ Akiwa Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, ameweka mfano bora sana kwa kuwa mnyenyekevu na kujitiisha kwa ushikamanifu chini ya enzi kuu ya Baba yake. (Isa. 50:4, 5; Yoh. 5:19) Raia wote washikamanifu wa Mfalme huyo ni lazima waige mfano wake, na kujitiisha kwa unyenyekevu chini ya enzi kuu ya Yehova katika mambo yote. Ni wale tu wanaofanya hivyo watakaoruhusiwa  kuishi katika ulimwengu mpya alioahidi Mungu.—Zek. 14:16, 17.

13. Kristo anapandaje ‘kwa kutetea uadilifu’?

13 Kristo pia anapanda ‘kwa kutetea uadilifu.’ Uadilifu anaotetea Mfalme huyo ni “uadilifu wa Mungu,” yaani, viwango vya Yehova vya mambo yanayofaa na yasiyofaa. (Rom. 3:21; Kum. 32:4) Isaya alitabiri hivi kumhusu Mfalme Yesu Kristo: “Mfalme atatawala kwa ajili ya uadilifu.” (Isa. 32:1) Utawala wa Yesu utaleta “mbingu mpya” na “dunia mpya” zilizoahidiwa, ambamo “uadilifu utakaa.” (2 Pet. 3:13) Kila mkaaji wa ulimwengu huo mpya atahitaji kutii viwango vya Yehova.—Isa. 11:1-5.

MFALME ANATIMIZA “MAMBO YENYE KUOGOPESHA”

14. Mkono wa kuume wa Kristo utatimizaje “mambo yenye kuogopesha”? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 3.)

14 Mfalme huyo anayepanda amejifunga upanga kwenye paja lake. (Zab. 45:3) Lakini, wakati utafika wa kuchukua upanga huo na kuushika kwa mkono wake wa kuume. Mtunga-zaburi alitabiri hivi: “Mkono wako wa kuume utakufundisha mambo yenye kuogopesha.” (Zab. 45:4) Yesu Kristo atakapopanda ili kutekeleza hukumu za Yehova katika Har–Magedoni, atatimiza “mambo yenye kuogopesha” dhidi ya adui zake. Hatujui atatumia njia gani kuuharibu mfumo wa Shetani. Lakini, hatua hiyo itawatia woga wakaaji wa dunia ambao hawajatii onyo la Mungu la kujitiisha chini ya utawala wa Mfalme huyo. (Soma Zaburi 2:11, 12.) Katika unabii wake kuhusu siku za mwisho, Yesu alisema kwamba watu ‘wangezimia kwa woga na tarajio la mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa; kwa maana nguvu za mbingu zitatikiswa.’ Kisha akasema hivi: “Na ndipo watakapomwona Mwana wa binadamu akija katika wingu akiwa na nguvu na utukufu mwingi.”—Luka 21:26, 27.

15, 16. “Majeshi” yanayomfuata Kristo vitani yatatia ndani nani?

15 Kitabu cha Ufunuo kinatangaza kuja kwa Mfalme “akiwa na nguvu na utukufu mwingi” kwa kusema hivi: “Nikaona mbingu imefunguliwa, na, tazama! farasi mweupe. Na yeye aliyeketi juu yake anaitwa Mwaminifu na wa Kweli, naye anahukumu na kufanya vita kwa uadilifu. Pia, majeshi yaliyokuwa mbinguni yalikuwa yakimfuata juu ya farasi weupe, nayo yalikuwa yamevikwa kitani bora cheupe, safi. Na upanga mrefu mkali unachomoza kutoka kinywani mwake, ili ayapige mataifa nao, naye atawachunga kwa fimbo ya chuma. Yeye anakanyaga pia shinikizo la divai ya hasira ya ghadhabu ya Mungu Mweza-Yote.”—Ufu. 19:11, 14, 15.

16 “Majeshi” ya mbinguni yanayomfuata Kristo vitani yanatia ndani nani? Yesu aliandamana na “malaika zake” alipojifunga upanga kwa mara ya kwanza ili kumfukuza Shetani na roho wake waovu kutoka mbinguni. (Ufu. 12:7-9) Ni jambo linalopatana na akili kufikia mkataa wa kwamba katika vita vya Har–Magedoni, majeshi ya Kristo yatatia ndani malaika watakatifu. Ni nani wengine walio katika majeshi hayo? Yesu aliwaahidi hivi ndugu zake watiwa-mafuta: “Yeye atakayeshinda na kushika matendo yangu mpaka mwisho nitampa mamlaka juu ya mataifa, naye atawachunga watu kwa fimbo ya chuma hivi kwamba watavunjwa vipande-vipande kama vyombo vya udongo, kama vile nilivyopokea kutoka kwa Baba yangu.” (Ufu. 2:26, 27) Hivyo, majeshi ya Kristo ya mbinguni yatatia ndani pia ndugu zake watiwa-mafuta, na watakuwa wamepata thawabu yao mbinguni wakati huo. Watawala hao watiwa-mafuta watakuwa pamoja na Kristo atakapotimiza “mambo  yenye kuogopesha” huku akiwachunga mataifa kwa fimbo ya chuma.

MFALME AKAMILISHA USHINDI WAKE

17. (a) Farasi mweupe anayepandwa na Kristo anafananisha nini? (b) Upanga na upinde vinafananisha nini?

17 Soma Zaburi 45:5. Mfalme huyo amepanda farasi mweupe anayefananisha vita safi na vya uadilifu machoni pa Yehova. (Ufu. 6:2; 19:11) Ana upanga na vilevile upinde. Tunasoma hivi: “Nami nikaona, na, tazama! farasi mweupe; na yule anayeketi juu yake alikuwa na upinde; naye akapewa taji, naye akaenda akishinda na kukamilisha ushindi wake.” Upanga na upinde vinafananisha njia atakayotumia Kristo kutekeleza hukumu dhidi ya adui zake.

Ndege wataitwa ili waisafishe dunia(Tazama fungu la  18)

18. “Mishale” ya Kristo itakuwa “mikali” katika maana gani?

18 Mtunga-zaburi anatumia lugha ya kishairi kutabiri kwamba ‘mishale ya Mfalme huyo ni mikali, inaichoma mioyo ya adui zake’ na ‘kuwaangusha watu mbele yake.’ Atawaangamiza adui zake duniani pote. Unabii wa Yeremia unatabiri hivi: “Wale waliouawa na Yehova siku hiyo hakika watakuwa kutoka mwisho mmoja wa dunia mpaka mwisho wa pili wa dunia.” (Yer. 25:33) Unabii mwingine kama huo unasema hivi: “Nikaona pia malaika amesimama katika jua, naye akapaaza kilio kwa sauti kubwa na kuwaambia ndege wote wanaoruka katikati ya mbingu: ‘Njooni hapa, mkusanyike pamoja kwenye mlo mkubwa wa jioni wa Mungu, ili mpate kula sehemu zenye nyama za wafalme na sehemu zenye nyama za viongozi wa kijeshi na sehemu zenye nyama za watu wenye nguvu na sehemu zenye nyama za farasi na za wale wanaoketi juu yao, na sehemu zenye nyama za wote, za watu huru na vilevile za watumwa na za wadogo na wakubwa.’”—Ufu. 19:17, 18.

19. Kristo ‘ataendelea mpaka afanikiwe’ na kukamilisha ushindi wake jinsi gani?

19 Baada ya kuuharibu mfumo mwovu wa Shetani duniani, Kristo ‘ataendelea mpaka afanikiwe katika fahari yake.’ (Zab. 45:4) Atakamilisha ushindi wake kwa kumtupa Shetani na roho wake waovu ndani ya abiso kwa Miaka Elfu Moja. (Ufu. 20:2, 3) Ibilisi na malaika zake wakiwa katika hali ya kutotenda kama ya wafu, wakaaji wa dunia hawatakuwa tena chini ya uvutano wa kishetani nao watajitiisha kikamili chini ya Mfalme wao mshindi na mwenye utukufu. Hata hivyo, kabla ya kuona dunia nzima ikigeuzwa hatua kwa hatua kuwa paradiso, watakuwa na sababu nyingine ya kushangilia pamoja na Mfalme wao na watawala wenzake. Makala inayofuata itazungumzia tukio hilo lenye shangwe.