Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni Mwandalizi na Mlinzi Wetu

Yehova Ni Mwandalizi na Mlinzi Wetu

Kwa sababu ameweka upendo wake juu yangu, mimi nitamwokoa pia. Nitamlinda kwa sababu amelijua jina langu.”ZAB. 91:14.

1, 2. Tunatofautiana namna gani inapohusu hali za familia na jinsi tulivyopata kweli?

YEHOVA ndiye aliyeanzisha familia. (Efe. 3:14, 15) Hata watu wa familia moja wana tabia na hali zinazotofautiana. Huenda umeishi na wazazi wako tangu ulipokuwa mtoto. Kuna watu ambao wamepoteza wazazi wao katika kifo kwa sababu ya ugonjwa, aksidenti, au msiba mwingine. Na kuna wengine ambao hawawajui wazazi wao.

2 Washiriki wa familia ya waabudu wa Yehova walipata kweli kwa njia tofauti-tofauti. Huenda wazazi wako ‘walikulea katika kweli,’ kama wengine wanavyosema, yaani, walikufundisha kanuni za Mungu. (Kum. 6:6, 7) Au huenda wewe ni miongoni mwa maelfu waliojifunza kweli walipohubiriwa na watumishi wa Yehova.—Rom. 10:13-15; 1 Tim. 2:3, 4.

3. Sote tuna hali gani zinazofanana?

3 Licha ya tofauti hizo zilizotajwa, sote tuna hali fulani zinazofanana. Tunateseka kwa sababu ya kutotii kwa Adamu na tumerithi hali ya kutokamilika, dhambi, na kifo. (Rom. 5:12) Hata hivyo, tukiwa waabudu wa kweli, kwa kufaa tunaweza kumwita Yehova kuwa “Baba yetu.” Andiko la Isaya 64:8 linasema hivi kuhusu watu waliochaguliwa na Mungu katika nyakati za kale: “Ee Yehova, wewe ni Baba yetu.” Pia, Yesu alianza sala yake ya kielelezo  kwa kusema hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.”—Mt. 6:9.

4, 5. Itakuwa vizuri kufikiria nini tunapochunguza jinsi tunavyomthamini Baba yetu, Yehova?

4 Tukiwa watu wanaoliitia jina lake kwa imani, Baba yetu wa mbinguni anatutunza na kutulinda. Mtunga-zaburi anamnukuu kwa kusema hivi: “Kwa sababu [mwabudu wa kweli] ameweka upendo wake juu yangu, mimi nitamwokoa pia. Nitamlinda kwa sababu amelijua jina langu.” (Zab. 91:14) Naam, Yehova Mungu hutuokoa kwa upendo kutokana na maadui wetu na kutulinda tukiwa watu wake ili tusiangamizwe.

5 Ili tumthamini zaidi Baba yetu wa mbinguni, acheni tuchunguze mambo matatu muhimu: (1) Baba yetu ni Mwandalizi wetu. (2) Yehova ni Mlinzi wetu. (3) Na Mungu ni Rafiki yetu mkubwa zaidi. Tunapochunguza mambo hayo, ni vizuri tutafakari kuhusu uhusiano wetu na Mungu na kutambua jinsi tunavyoweza kumheshimu akiwa Baba yetu. Tutafaidika pia tukifikiria jinsi Yehova anavyowabariki wale wanaomkaribia.—Yak. 4:8.

YEHOVA NI MWANDALIZI MKUU

6 Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu hutoka juu, kwa maana hushuka kutoka kwa Baba wa mianga ya mbinguni.” (Yak. 1:17) Uhai ni zawadi nzuri ajabu kutoka kwa Yehova. (Zab. 36:9) Tunapotumia maisha yetu kufanya mapenzi ya Mungu, tunapata baraka nyingi sasa na tumaini la kuishi milele katika ulimwengu mpya. (Met. 10:22; 2 Pet. 3:13) Hata hivyo, inawezekanaje na bado tunapatwa na madhara ya kutotii kwa Adamu?

7. Mungu alifanya nini ili tuwe na uhusiano wa karibu pamoja naye?

7 Kwa kweli, Yehova ni Mwandalizi Mkuu kwa njia nyingi zisizohesabika. Kwa mfano, tunapata wokovu kwa sababu ya fadhili zake zisizostahiliwa. Sisi sote tuna dhambi na tumerithi hali ya kutokamilika kutoka kwa Adamu, baba yetu wa kwanza duniani. (Rom. 3:23) Hata hivyo, kwa upendo Yehova alichukua hatua ya kwanza kwa kutuwezesha kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. Mtume Yohana aliandika hivi: “Kwa hili upendo wa Mungu ulifunuliwa kwa habari yetu, kwa sababu Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee kuja ulimwenguni ili tupate uzima kupitia yeye. Hivi ndivyo upendo ulivyo, si kwamba sisi tumempenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda akamtuma Mwana wake kuwa dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu.”—1 Yoh. 4:9, 10.

8, 9. Yehova alithibitikaje kuwa Mwandalizi Mkuu wakati wa Abrahamu na Isaka? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 16.)

8 Katika karne ya 19 K.W.K., tukio fulani la kinabii lilionyesha jinsi Yehova alivyojidhabihu sana kwa upendo ili wanadamu waishi milele. Andiko la Waebrania 11:17-19 linasema hivi: “Kwa imani Abrahamu, alipojaribiwa, ni kana kwamba alimtoa Isaka—mtu aliyekuwa amezipokea ahadi kwa furaha alijaribu kumtoa mwana wake mzaliwa-pekee—ijapokuwa alikuwa ameambiwa: ‘Ule utakaoitwa “uzao wako” utakuwa kupitia Isaka.’ Lakini alifikia mkataa kwamba Mungu alikuwa na uwezo wa kumfufua hata kutoka kwa wafu; na kutoka huko alimpokea pia kwa njia ya mfano.” Si vigumu kuona ulinganifu uliopo. Yehova alimtoa Mwana wake, Yesu Kristo, kwa ajili ya ulimwengu wa wanadamu.—Soma Yohana 3:16, 36.

9 Ni wazi kwamba Isaka alifurahi sana alipookolewa kutokana na kifo cha kidhabihu. Bila shaka, alithamini sana Mungu alipoandaa dhabihu nyingine, yaani, kondoo-dume aliyenaswa kwa pembe zake katika kichaka kilichokuwa karibu.  (Mwa. 22:10-13) Si ajabu kwamba eneo hilo liliitwa “Yehova-yire,” kumaanisha “Yehova Ataandaa.”—Mwa. 22:14.

UANDALIZI KWA AJILI YA UPATANISHO

10, 11. Ni nani wanaoongoza katika “huduma ya upatanisho,” nao wameitimizaje?

10 Tunapotafakari jinsi Yehova anavyothibitisha kwamba yeye ni Mwandalizi Mkuu, tunashukuru na kuthamini daraka muhimu la Yesu Kristo, sawa na Paulo aliyeandika hivi: “Hili ndilo tumehukumu, kwamba mtu mmoja alikufa kwa ajili ya wote; kwa hiyo, basi, wote walikuwa wamekufa; naye alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yao na kufufuliwa.”—2 Kor. 5:14, 15.

11 Wakristo wa karne ya kwanza walikubali kwa shangwe “huduma ya upatanisho” kwa kuwa walimpenda Mungu na kumshukuru kwa sababu ya pendeleo lisilo na kifani la kumtumikia. Kazi yao ya kuhubiri na kufanya wanafunzi iliwapa watu wenye mioyo minyoofu nafasi ya kuwa na amani pamoja na Mungu, kuwa rafiki zake, na hatimaye kuwa watoto wake wa kiroho. Leo, watumishi wa Yehova waliotiwa mafuta wanatimiza pia huduma hiyo. Wakiwa mabalozi wa Mungu na Kristo, wanawasaidia watu wenye mwelekeo unaofaa kuvutwa na Yehova ili wamwabudu.—Soma 2 Wakorintho 5:18-20; Yoh. 6:44; Mdo. 13:48.

12, 13. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunathamini maandalizi mengi anayotoa Yehova?

12 Wakristo wote wenye tumaini la kuishi milele duniani wanashirikiana na watiwa-mafuta katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme kwa sababu wanamthamini Yehova akiwa Mwandalizi Mkuu. Tunatumia Biblia, uandalizi bora kutoka kwa Mungu, tunapofanya kazi hiyo. (2 Tim. 3:16, 17) Tunapotumia kwa ustadi Neno la Mungu lililoongozwa na roho takatifu katika huduma yetu, tunawapa wengine nafasi ya kupata uzima wa milele. Ili tutimize kazi hiyo, kila mmoja wetu anategemea uandalizi mwingine kutoka kwa Yehova, yaani, roho yake takatifu. (Zek. 4:6; Luka 11:13) Tunapofanya hivyo, tunapata matokeo mazuri sana kama kila Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova kinavyoonyesha. Ni heshima kubwa kama nini kushiriki katika kazi hii na hivyo kumsifu Baba na Mwandalizi wetu!

13 Tunapofikiria yote ambayo Mungu ametuandalia, tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, ninajitahidi kadiri niwezavyo katika huduma yangu na kumwonyesha Yehova kwamba ninathamini sana maandalizi yake? Ninawezaje kuboresha ustadi wangu wa kuhubiri habari njema?’ Tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini maandalizi mazuri ajabu ya Mungu kwa kutanguliza mambo ya Ufalme maishani mwetu. Tukifanya hivyo, Yehova atahakikisha kwamba tunapata mahitaji yetu. (Mt. 6:25-33) Bila shaka, tunataka kufanya yote tuwezayo ili kumpendeza Mungu na kuufanya moyo wake ushangilie kwa sababu anatupenda.—Met. 27:11.

14. Yehova amekuwa Mwokozi wa watu wake jinsi gani?

14 Mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Mimi ninateseka nami ni maskini. Yehova mwenyewe ananijali. Wewe ni msaidizi wangu na Mwokoaji wangu.” (Zab. 40:17) Yehova amewaokoa tena na tena watu wake wakiwa kikundi, hasa wanapoteswa vikali na kufuatwa na maadui wao. Tunathamini kama nini msaada wa Mungu katika pindi hizo na maandalizi mengi ya kiroho anayotupatia kwa ukawaida!

YEHOVA ANATULINDA

15. Toa mfano unaoonyesha jinsi baba mwenye upendo anavyojitahidi kumlinda mtoto wake.

15 Baba mwenye upendo hawaandalii tu  watoto wake mahitaji yao bali pia hujitahidi kuwalinda. Kwa kawaida, anajitahidi kuwaokoa wanapokabili hatari. Ndugu mmoja anakumbuka jambo fulani lililotukia alipokuwa mvulana mdogo. Alipokuwa akirudi nyumbani na baba yake baada ya kuhubiri, walifika mahali penye kijito. Kijito hicho kilikuwa kimefurika baada ya mvua kubwa kunyesha asubuhi. Ili kuvuka kijito hicho walihitaji kuruka kutoka jiwe moja kubwa hadi lingine. Akiwa mbele ya baba yake, mvulana huyo mdogo aliteleza na kutumbukia mara mbili ndani ya maji. Alishukuru sana wakati baba yake alipomshika kwa nguvu begani na kumwokoa asizame! Baba yetu wa mbinguni anatuokoa kutoka katika ulimwengu huu mwovu ulio kama mafuriko yenye nguvu na kutoka kwa mtawala wake, Shetani. Kwa kweli, Yehova ni Mlinzi bora zaidi unayeweza kupata.—Mt. 6:13; 1 Yoh. 5:19.

16, 17. Yehova aliwasaidia na kuwalinda Waisraeli jinsi gani walipopigana na Waamaleki?

16 Mambo yaliyotukia baada ya Yehova kuwaokoa Waisraeli kutoka utumwani huko Misri na kuwalinda kimuujiza walipovuka Bahari Nyekundu katika mwaka wa 1513 K.W.K., yanathibitisha kwamba yeye huwalinda watumishi wake kwa upendo. Baada ya kusafiri jangwani kuelekea Mlima Sinai, taifa hilo lilifika Refidimu.

17 Kwa sababu ya unabii uliotolewa na Mungu katika Mwanzo 3:15, huenda Shetani alikuwa akitafuta sana nafasi ya kuwashambulia Waisraeli walioonekana hawana ulinzi. Aliwashambulia kwa kuwatumia Waamaleki, waliokuwa maadui wa watu wa Mungu. (Hes. 24:20) Fikiria alichotimiza Yehova akitumia wanaume wanne waaminifu, yaani, Yoshua, Musa, Haruni, na Huru. Musa, Haruni, na Huru walisimama  juu ya kilima wakati Yoshua alipokuwa akipigana na Waamaleki. Wakati wa pambano hilo, Waisraeli walikuwa na nguvu zaidi Musa alipoinua mikono yake. Haruni na Huru waliitegemeza mikono ya Musa ilipokuwa mizito. Hivyo, kwa msaada na ulinzi wa Yehova, “Yoshua akawashinda kabisa Amaleki na watu wake.” (Kut. 17:8-13) Musa akajenga madhabahu na kuiita “Yehova-nisi,” jina linalomaanisha “Yehova Ni Nguzo Yangu ya Ishara.”—Soma Kutoka 17:14, 15.

KULINDWA DHIDI YA UTUMWA WA SHETANI

18, 19. Mungu amewalindaje watumishi wake katika siku zetu?

18 Yehova huwalinda wale wanaompenda na kumtii. Sisi pia tunamtegemea Mungu atulinde tunapokabili maadui kama Waisraeli walivyofanya huko Refidimu. Mara nyingi Yehova ametulinda tukiwa kikundi, na anaendelea kutulinda dhidi ya utumwa wa Ibilisi. Fikiria pindi nyingi ambazo Mungu amewalinda ndugu zetu wanaodumisha msimamo wao wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote. Kwa mfano, ilikuwa hivyo wakati wa Wanazi huko Ujerumani na katika nchi nyingine miaka ya 1930 na mwanzoni mwa 1940. Imani yetu katika Yehova, Kimbilio letu, itaimarika tukisoma na kutafakari masimulizi ya maisha na masimulizi yaliyo katika Kitabu cha Mwaka yanayoonyesha jinsi Mungu alivyowalinda watu wake wakati wa mateso.—Zab. 91:2.

Yehova anaweza kuwatumia waamini wenzetu kutusaidia kubaki waaminifu tunapokabili hali ngumu (Tazama fungu la 18-20)

19 Kwa upendo, tunapokea vikumbusho vinavyotulinda kupitia tengenezo la Yehova na machapisho yake. Fikiria jinsi ambavyo vikumbusho hivyo vimetunufaisha hivi karibuni. Ulimwengu huu unapoendelea kuzama katika dimbwi la upotovu na ponografia, Yehova ametupatia kwa wakati unaofaa msaada na vikumbusho vinavyotuonya kuhusu hatari za kimaadili. Kwa mfano, tunashauriwa kwa upendo kuepuka mashirika mabaya kwa kutotumia vibaya vituo vya mawasiliano. *1 Kor. 15:33.

20. Ni ulinzi namwongozo gani tunaopata katika kutaniko la Kikristo?

20 Tutaonyeshaje kwamba kwa kweli ‘tunafundishwa na Yehova’? Kwa kutii kabisa amri zake. (Isa. 54:13) Tunalindwa na kupata mwongozo tunaohitaji katika makutaniko yetu kwa sababu yana wanaume waaminifu wanaotumikia wakiwa wazee wanaotupatia msaada na mashauri ya Kimaandiko. (Gal. 6:1) Yehova anatutunza kwa upendo kupitia ‘zawadi hizo katika wanadamu.’ (Efe. 4:7, 8) Tuitikiaje mashauri yao? Mungu hutubariki tunaponyenyekea na kutii.—Ebr. 13:17.

21. (a) Tunapaswa kuazimia kufanya nini? (b) Makala inayofuata itazungumzia nini?

21 Tuazimie kuongozwa na roho takatifu na kutii mwongozo wa Baba yetu wa mbinguni. Tunahitaji pia kutafakari kuhusu maisha ya Mwana wake, Yesu Kristo, na kujitahidi kufuata kielelezo chake cha pekee sana. Yesu alipata thawabu kubwa kwa sababu alitii mpaka kifo chake. (Flp. 2:5-11) Sisi pia tutabarikiwa tukimtegemea Yehova kwa moyo wetu wote. (Met. 3:5, 6) Na tuendelee kumtegemea Yehova ambaye ni Mwandalizi na Mlinzi asiye na kifani. Ni pendeleo na shangwe kubwa kama nini kumtumikia Yehova! Upendo wetu kumwelekea utaongezeka tunapochunguza jambo la tatu linaloonyesha kwamba Yehova anatujali, yaani, urafiki wake. Makala inayofuata itaonyesha jinsi Yehova alivyo Rafiki yetu mkubwa zaidi.

^ fu. 19 Baadhi ya vikumbusho hivyo vinapatikana katika makala yenye kichwa “Intaneti—Kutumia kwa Hekima Kifaa cha Ulimwenguni Pote” katika Mnara wa Mlinzi, Agosti 15, 2011, ukurasa wa 3-5 na makala “Jihadhari na Mitego ya Ibilisi!” na “Simama Imara na Uepuke Mitego ya Shetani!” katika Mnara wa Mlinzi, Agosti 15, 2012, ukurasa wa 20-29.