Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Yehova Anatutimizia Mahitaji Yetu na Kutulinda

Yehova Anatutimizia Mahitaji Yetu na Kutulinda

‘Kwa sababu ameweka upendo wake juu yangu, Mimi nitamuokoa pia. Nitamulinda kwa sababu amelijua jina langu.’​—ZAB. 91:14.

1, 2. Tulikomaa katika hali gani tofauti, na namna gani tulijifunza kweli kwa njia tofauti?

 YEHOVA ndiye aliyeanzisha familia. (Efe. 3:14, 15) Hata ikiwa tumezaliwa katika familia moja, tuna sifa tofauti na tulikomaa katika hali tofauti. Pengine uliishi na wazazi wako kuanzia utoto mupaka wakati ulipokuwa mutu muzima. Wengine wamefiwa na wazazi wao kwa sababu ya magonjwa, aksidenti, ao misiba mingine. Wengine hata hawajue wazazi wao.

2 Vilevile, sisi waabudu wa Yehova tulijifunza kweli kwa njia tofauti. Pengine ‘ulikomalia katika kweli,’ kama vile wengine wanavyosema, na wazazi wako walikufundisha kanuni za Mungu. (Kum. 6:6, 7) Ao pengine wewe ni mumoja kati ya wengi ambao walihubiriwa na watumishi wengine wa Yehova.​—Rom. 10:13-15; 1 Tim. 2:3, 4.

3. Sisi wote tuko katika hali gani zinazofanana?

3 Hata ikiwa hali zetu zinatofautiana na hata ikiwa tumejifunza kweli kwa njia tofauti, sisi wote tuko katika hali fulani zinazofanana. Tunapatwa na matokeo ya kutokutii kwa Adamu na tumeriti hali ya kutokamilika, zambi, na kifo. (Rom. 5:12) Hata hivyo, sisi waabudu wa kweli wa Yehova tuna haki ya kumuita “Baba yetu.” Katika andiko la Isaya 64:8, Waisraeli walimuambia Mungu hivi: “Ee Yehova, wewe ni Baba yetu.” Zaidi ya hilo, Yesu alianza sala yake ya mufano kwa maneno haya: ‘Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.’​—Mt. 6:9.

4, 5. Ili kutusaidia tumupende zaidi Baba yetu wa mbinguni, Yehova, tutazungumuzia nini?

4 Baba yetu wa mbinguni analinda waabudu wake na kuwatolea mambo wanayohitaji. Mutunga​-zaburi anamuzungumuzia Mungu akisema hivi: ‘Kwa sababu [muabudu wa kweli] ameweka upendo wake juu yangu, Mimi nitamuokoa pia. Nitamulinda kwa sababu amelijua jina langu.’ (Zab. 91:14) Kwa upendo, Yehova Mungu anatuokoa kutokana na maadui wetu na kutulinda sisi watumishi wake ili tusiangamizwe kabisa.

5 Ili kutusaidia tumupende zaidi Baba yetu wa mbinguni, acheni tuzungumuzie mambo matatu ya maana: (1) Baba yetu anatutimizia mahitaji yetu. (2) Yehova anatulinda. (3) Na Yehova ndiye Rafiki yetu muzuri zaidi. Tunapozungumuzia mambo hayo, itakuwa jambo la lazima tutafakari kuhusu uhusiano wetu na Mungu na kuona namna gani tunaweza kumuheshimu Baba yetu wa mbinguni. Ni vizuri pia tufikirie baraka ambazo Yehova amewawekea wale wanaomukaribia.​—Yak. 4:8.

YEHOVA NDIYE MUTIMIZAJI MUKUBWA WA MAHITAJI YETU

6. Ni katika njia gani Yehova anaonekana kuwa Mutoaji wa “kila zawadi njema”?

6 Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: ‘Kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu inatoka juu, kwa maana inashuka kutoka kwa Baba wa mianga ya mbinguni.’ (Yak. 1:17) Uzima ni zawadi nzuri ambayo Yehova ametupatia. (Zab. 36:9) Tunapotumia maisha yetu ili kufanya mapenzi ya Mungu, tunabarikiwa sana na tuna tumaini la kuishi milele katika ulimwengu mupya. (Met. 10:22; 2 Pet. 3:13) Lakini namna gani hilo linawezekana kwa kuwa sisi wote tumeriti zambi na kifo kutoka kwa Adamu?

7. Mungu alifanya nini ili tuwe na uhusiano wa karibu pamoja naye?

7 Yehova ndiye Mutimizaji Mukubwa wa Mahitaji yetu, na anafanya hivyo kwa njia mbalimbali. Kwa mufano, anatuokoa kwa sababu ya fazili zake zisizostahiliwa. Bila shaka, sisi wote ni watenda​-zambi na tumeriti kutokamilika kutokana na baba yetu wa kwanza, Adamu. (Rom. 3:23) Lakini, kwa sababu Yehova anatupenda, alifanya mipango ili tuwe na uhusiano wa karibu pamoja naye. Mutume Yohana aliandika hivi: ‘Kwa hili upendo wa Mungu ulifunuliwa kwa habari yetu, kwa sababu Mungu alimutuma Mwana wake muzaliwa-pekee kuja ulimwenguni ili tupate uzima kupitia yeye. Hivi ndivyo upendo ulivyo, si kwamba sisi tumemupenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda akamutuma Mwana wake kuwa zabihu ya upatanisho kwa ajili ya zambi zetu.’​—1 Yoh. 4:9, 10.

8, 9. Namna gani Yehova alionyesha kwamba yeye ni Mutimizaji Mukubwa wa Mahitaji yetu katika siku za Abrahamu na Isaka? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.)

8 Katika mwaka wa 1893 hivi, mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, tukio moja la kiunabii lilionyesha ni kwa kiasi gani Yehova angejitoa kabisa ili kuwasaidia wanadamu wanaomutii wapate uzima wa milele. Andiko la Waebrania 11:17-19 linaeleza hivi: “Kwa imani Abrahamu, alipojaribiwa, ni kana kwamba alimutoa Isaka, na huyo mutu aliyekuwa amezipokea ahadi kwa furaha alijaribu kumutoa mwana wake muzaliwa​-pekee, ijapokuwa alikuwa ameambiwa: ‘Ule utakaoitwa uzao wako utakuwa kupitia Isaka.’ Lakini alifikia uamuzi kwamba Mungu alikuwa na uwezo wa kumufufua hata kutoka kwa wafu; na kutoka huko alimupokea pia kwa njia ya mufano.” Ni rahisi kuona ulinganifu huu: Kama vile Abrahamu alivyokuwa tayari kumutoa mwana wake Isaka, Yehova pia alimutoa Mwana wake, Yesu Kristo, ili kuwaokoa wanadamu.​—Soma Yohana 3:16, 36.

9 Tunaweza kuwazia namna Isaka alivyofurahi sana alipojua kwamba hatatolewa tena kuwa zabihu! Bila shaka alimushukuru Mungu kwa kutayarisha zabihu nyingine ambayo ingetolewa, ni kusema, kondoo​-dume aliyekuwa katika kichaka ao miti midogo iliyokuwa hapo karibu. (Mwa. 22:10-13) Ndio sababu Abrahamu aliita mahali hapo “Yehova-yire,” maana yake “Yehova Ataandaa.”​—Mwa. 22:14.

MIPANGO YA UPATANISHO

10, 11. Ni nani ambao wamesimamia “huduma ya upatanisho,” na namna gani wamefanya kazi hiyo?

10 Tunapofikiria namna Yehova ameonyesha kuwa yeye ndiye Mutimizaji Mukubwa wa Mahitaji yetu, tunatambua kazi ya maana sana ambayo Yesu ametufanyia. Hata mutume Paulo aliandika hivi: ‘Hili ndilo tumehukumu, kwamba mutu mumoja alikufa kwa ajili ya wote; kwa hiyo, basi, wote walikuwa wamekufa; naye alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yao na kufufuliwa.’​—2 Kor. 5:14, 15.

11 Kwa sababu walimupenda Mungu na walifurahia sana pendeleo lao la kumutumikia, Wakristo wa kwanza-kwanza walikubali kwa furaha “huduma ya upatanisho.” Kazi yao ya kuhubiri na kufanya wanafunzi iliwafungulia njia watu waliopenda haki ili wawe na amani pamoja na Mungu, wafurahie urafiki pamoja naye, na mwishowe wawe wana wake wa kiroho. Leo pia, watumishi watiwa-mafuta wa Yehova wanaendelea kufanya kazi hiyohiyo. Kazi wanayofanya wakiwa mabalozi ao waambasadere wa Mungu na Kristo inawasaidia watu wamukaribie Yehova na kuwa watumishi wake.​—Soma 2 Wakorintho 5:18-20; Yoh. 6:44; Mdo. 13:48.

12, 13. Namna gani tunaweza kuonyesha shukrani yetu kuhusu mambo yote ambayo Yehova ametutolea?

12 Kwa kuwa wanamupenda Yehova, Mutimizaji Mukubwa wa Mahitaji yao, Wakristo wote walio na tumaini la kuishi duniani wanawasaidia watiwa-mafuta katika kazi ya kuhubiri Ufalme. Katika kazi hiyo, tunatumia Biblia ambayo ni moja kati ya mambo mazuri ambayo Yehova ametutolea. (2 Tim. 3:16, 17) Tunapotumia Neno la Mungu lilioongozwa na roho yake kwa ufundi katika mahubiri, tunawatolea wengine nafasi ya kupata uzima wa milele. Ili kutusaidia katika kazi hiyo, Yehova ametutolea jambo lingine, ni kusema, roho yake takatifu. (Zek. 4:6; Lu. 11:13) Tunapata matokeo yenye kushangaza sana katika kazi hiyo, kama inavyoonyeshwa kila mwaka katika Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova. Ni pendeleo kabisa kushiriki katika kazi hiyo ya kumusifu Baba yetu na Mutimizaji Mukubwa wa Mahitaji yetu!

13 Tunapofikiria mambo yote ambayo Mungu wetu ametutolea, tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, ninafanya yangu yote katika kazi ya kuhubiri ili kuonyesha kwamba ninasamini sana mambo yote ambayo Yehova ametutolea? Ni katika sehemu gani ninaweza kufanya maendeleo ili niwe muhubiri muzuri zaidi wa habari njema?’ Tunaweza kuonyesha shukrani yetu kwa mambo yote ambayo Mungu ametutolea kwa kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu. Ikiwa tunafanya hivyo, Yehova atatutimizia mahitaji yetu. (Mt. 6:25-33) Kwa kuwa Mungu anatupenda, acheni tufanye yote tunayoweza ili kumupendeza na kufurahisha moyo wake.​—Met. 27:11.

14. Namna gani Yehova amekuwa Muokoaji wa watu wake?

14 Mutunga​-zaburi Daudi aliimba hivi: ‘Mimi ninateseka nami ni maskini. Yehova mwenyewe ananijali. Wewe ni musaidizi wangu na Muokoaji wangu.’ (Zab. 40:17) Mara nyingi Yehova amekuwa akiwaokoa watu wake kwa ujumla, zaidi sana wanapoendelea kuteswa sana na kusumbuliwa na maadui wao. Tunamushukuru sana Mungu kwa mipango anayofanya kila siku ili kutusaidia tubaki waaminifu kwake katika nyakati hizo ngumu!

YEHOVA ANATULINDA

15. Eleza namna baba mwenye upendo alivyomuokoa mutoto wake.

15 Zaidi ya kuwatolea mahitaji yao ya kimwili, baba mwenye upendo analinda pia watoto wake. Kwa kawaida anafanya yote anayoweza ili kuwakomboa katika hatari. Ndugu mumoja anakumbuka namna baba yake alivyomuokoa alipokuwa kijana mudogo. Yeye na baba yake walipokuwa wakirudi nyumbani kutoka katika mahubiri walipaswa kuvuka muto mudogo. Mvua kubwa iliyonyesha asubuhi hiyo ilikuwa imefanya muto huo ujae sana. Ili kuvuka iliomba tu kuruka kutoka kwenye jiwe moja mupaka lingine. Kijana huyo aliruka wa kwanza, kisha alitereza, na akaanguka katika maji, na kuzama mara mbili. Kijana huyo alifurahi sana wakati baba yake alimushika mara moja kwenye bega na kumuokoa! Vivyo hivyo, Baba yetu wa mbinguni anatuokoa ili tusizame katika matatizo yanayofanana na muto wenye kujaa sana wa ulimwengu huu muovu na anatuokoa mikononi mwa mutawala wake Shetani. Bila shaka, Yehova ndiye Mulinzi wetu muzuri zaidi.​—Mt. 6:13; 1 Yoh. 5:19.

16, 17. Namna gani Yehova aliwasaidia na kuwalinda Waisraeli walipokuwa wakipigana na Waamaleki?

16 Yehova aliwalinda kwa upendo watu wake katika mwaka wa 1513. Alikuwa amewaokoa Waisraeli katika utumwa wa Misri na alikuwa amewalinda kimuujiza walipokuwa wakivuka Bahari Nyekundu. Kisha kutembea katika jangwa mupaka kwenye Mulima Sinai, walifika Refidimu.

17 Kulingana na unabii ulio katika Mwanzo 3:15, tunaweza kuwazia namna Shetani alitafuta juu chini kuwashambulia Waisraeli, walioonekana kuwa hawana mutu wa kuwapigania. Alitumia Waamaleki, ambao walikuwa maadui wa watu wa Mungu. (Hes. 24:20) Fikiria yale ambayo Yehova alifanya kupitia wanaume wane waaminifu, ni kusema, Yoshua, Musa, Haruni, na Huru. Yoshua na wanaume wake walipokuwa wakipigana na Waamaleki, Musa, Haruni na Huru walikuwa kwenye mulima mudogo uliokuwa karibu na mahali hapo. Waisraeli walishinda vita wakati Musa aliinua mikono yake. Mikono yake ilipochoka, Haruni na Huru waliitegemeza. Ni kwa musaada na ulinzi wa Yehova tu ndipo ‘Yoshua aliwashinda kabisa Amaleki na watu wake.’ (Kut. 17:8-13) Musa alijenga mazabahu hapo, na kuyaita “Yehova-nisi,” maana yake “Yehova Ni Nguzo Yangu ya Ishara.”​—Soma Kutoka 17:14, 15.

YEHOVA ANATUOKOA KATIKA MAKUCHA YA SHETANI

18, 19. Mungu ametulinda namna gani siku hizi?

18 Yehova anawalinda wale wanaomupenda na kumutii. Kama Waisraeli hapo Refidimu, tunamutegemea Yehova tunaposhambuliwa na maadui. Yehova ametulinda mara nyingi kwa ujumla, na anatuokoa katika makucha ya Ibilisi. Fikiria namna Mungu amelinda mara nyingi ndugu na dada zetu ambao wamejikaza ili wasiunge mukono upande wowote katika siasa. Alifanya hivyo katika kipindi cha Wanazi huko Ujerumani na katika inchi zingine katika miaka ya 1930 na mwanzoni mwa miaka ya 1940. Kusoma na kutafakari masimulizi ya maisha na habari mbalimbali katika Kitabu cha Mwaka zinazoonyesha namna Mungu alivyowalinda ndugu na dada wakati wa upinzani kutatufanya tumutumainie zaidi Yehova, Kimbilio letu.​—Zab. 91:2.

Yehova anaweza kutumia waamini wenzetu ili kutusaidia tuendelee kuwa waaminifu katika nyakati za matatizo (Ona mafungu ya 18-20)

19 Yehova anatulinda kwa kututolea vikumbusho kupitia tengenezo lake na vichapo vinavyotegemea Biblia. Fikiria namna vikumbusho hivyo vimetulinda katika miaka ya hivi karibuni. Ulimwengu huu unapoendelea kuzama kabisa katika matope ya uasherati na ponografia, Yehova ametutolea vikumbusho kwa wakati unaofaa ili kutusaidia tulinde hali yetu ya kiroho. Kwa mufano, hivi karibuni, Baba yetu, Yehova, ametushauri tuepuke kupashana habari na marafiki wabaya kwenye Internete. *​—1 Kor. 15:33.

20. Ni ulinzi na muongozo gani ambao tunapata katika makutaniko yetu?

20 Namna gani tunaweza kuonyesha kabisa kwamba sisi ni “watu waliofundishwa na Yehova”? Kwa kushika kwa uangalifu amri zake. (Isa. 54:13) Makutaniko yetu, ni mahali salama ambapo tunapata ulinzi na muongozo, kwa sababu ni mahali hapo ndipo wanaume waaminifu, ni kusema, wazee wanatutolea musaada wa kiroho na mashauri. (Gal. 6:1) Yehova anatumia wazee hao ambao ni “zawadi zikiwa wanadamu” ili kututunza kwa upendo. (Efe. 4:7, 8) Tunapaswa kuitikia namna gani tunaposhauriwa? Tukitii kwa unyenyekevu mashauri yao, tutabarikiwa.​—Ebr. 13:17.

21. (a) Tunapaswa kuazimia kufanya nini? (b) Habari inayofuata itazungumuzia nini?

21 Acheni tuazimie kuongozwa na roho takatifu na kufuata uongozi wa Baba yetu wa mbinguni. Tunapaswa pia kutafakari kuhusu maisha ya Mwana wake, Yesu Kristo, na kujikaza kufuata mufano wake muzuri. Kwa sababu alitii mupaka kifo, Yesu alipokea zawadi kubwa. (Flp. 2:5-11) Kama yeye, tutabarikiwa ikiwa tunamutumainia Yehova kwa moyo wetu wote. (Met. 3:5, 6) Kwa hiyo, acheni tuendelee kumutegemea Yehova, Mutimizaji Mukubwa wa Mahitaji yetu na Mulinzi wetu mukubwa zaidi. Ni jambo lenye kufurahisha na ni pendeleo kubwa kumutumikia! Lakini, namna gani Yehova ni Rafiki yetu muzuri zaidi? Tutamupenda tena zaidi tunapozungumuzia ulizo hilo katika habari inayofuata.

^ Unaweza kupata vikumbusho vingine kama hivyo katika habari “Intaneti Kutumia kwa Hekima Kifaa cha Ulimwenguni Pote” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15/08/2011, ukurasa wa 3-5 na “Fanya Angalisho na Mitego ya Shetani!” na “Simama Imara na Epuka Mitego ya Shetani!” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15/08/2012, ukurasa wa 20-29.