Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini Wayahudi wa karne ya kwanza walikuwa ‘wakimtarajia’ Masihi?

Katika siku za Yohana Mbatizaji, “watu walikuwa wakitarajia na wote walikuwa wakiwaza mioyoni mwao juu ya Yohana: ‘Je, labda yeye ndiye Kristo? ’ ” (Luka 3:15) Kwa nini huenda Wayahudi walitarajia kwamba Masihi angetokea wakati huo? Kuna sababu kadhaa.

Baada ya Yesu kuzaliwa, malaika wa Yehova aliwatokea wachungaji waliokuwa wakichunga makundi yao karibu na Bethlehemu. Malaika huyo alitangaza hivi: “Leo katika jiji la Daudi, Mwokozi ambaye ni Kristo Bwana amezaliwa kwenu.” (Luka 2:8-11) Kisha, “umati wa jeshi la mbingu ukawa pamoja na yule malaika, ukimsifu Mungu na kusema: * ‘Utukufu katika vilele vilivyo juu kwa Mungu, na juu ya dunia amani kati ya watu wa nia njema.’ ”Luka 2:13, 14.

Bila shaka, tangazo hilo liliwachochea sana wachungaji hao wa kawaida. Mara moja wakaanza kwenda Bethlehemu, na walipompata Yosefu na Maria pamoja na mtoto wao mchanga Yesu, “wakasema mambo yaliyokuwa yamesemwa kuhusu mtoto huyo mchanga.” Matokeo ni kwamba “wote waliosikia wakastaajabu juu ya mambo waliyoambiwa na wachungaji.” (Luka 2:17, 18) Maneno, “wote waliosikia,” yanaonyesha kwamba wachungaji hao waliongea na watu wengine mbali na Yosefu na Maria. Kisha, wachungaji waliporudi nyumbani, waliendelea “kumsifu Mungu kwa ajili ya mambo yote waliyoyasikia na kuyaona, sawa na walivyokuwa wameambiwa.” (Luka 2:20) Bila shaka, wachungaji hao waliendelea kutangaza mambo mazuri waliyosikia kumhusu Kristo!

Maria alipomleta mwana wake mzaliwa wa kwanza Yerusalemu ili kumtoa kwa Yehova, kama Sheria ya Musa ilivyosema, nabii wa kike aliyeitwa Ana “akaanza kumshukuru Mungu akisema juu ya mtoto huyo kwa wale wote waliokuwa wakiungojea ukombozi wa Yerusalemu.” (Luka 2:36-38; Kut. 13:12) Hivyo, habari kuhusu kutokea kwa Masihi zikaendelea kuenea.

Baadaye, “wanajimu kutoka sehemu za Mashariki walikuja Yerusalemu, wakisema: ‘Yuko wapi yule mfalme wa Wayahudi aliyezaliwa? Kwa maana tuliiona nyota yake wakati tulipokuwa mashariki, nasi tumekuja kumsujudia.’ ” (Mt. 2:1, 2) Aliposikia hilo, “Mfalme Herode akafadhaika, na ­Yerusalemu yote pamoja naye; na alipowakusanya pamoja wakuu wa makuhani na waandishi wote wa watu akaanza kuuliza habari kutoka kwao juu ya ni wapi Kristo alipaswa  kuzaliwa.” (Mt. 2:3, 4) Kwa hiyo, watu wengi sana walikuwa wakijulishwa jambo hili: Yule ambaye angekuwa Masihi alikuwa amezaliwa! *

Andiko la Luka 3:15 lililonukuliwa mwanzoni linaonyesha kuwa Wayahudi fulani walifikiri kwamba Yohana Mbatizaji ndiye Kristo. Hata hivyo, Yohana alisema hivi: “Yule anayekuja nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, ambaye viatu vyake mimi sistahili kuvivua. Huyo atawabatiza ninyi kwa roho takatifu na kwa moto.” (Mt. 3:11) Bila shaka, maneno hayo ya unyenyekevu aliyosema Yohana yalifanya watu watarajie kwa hamu kutokea kwa Masihi.

Je, inawezekana kwamba Wayahudi wa karne ya kwanza walikadiria majira ya kutokea kwa Masihi kwa msingi wa ule unabii wa majuma 70 katika Danieli 9:24-27? Ingawa hilo linawezekana, hakuna uthibitisho. Ukweli ni kwamba Yesu alipokuwa duniani kulikuwa na ufafanuzi mbalimbali kuhusu majuma 70, na ufafanuzi huo haufanani na uelewaji wetu wa sasa. *

Waesene waliodhaniwa kuwa watawa wa dhehebu la Kiyahudi, walifundisha kwamba Masihi wawili wangetokea mwishoni mwa miaka 490, lakini hatuna uhakika ikiwa Waesene walitumia unabii wa Danieli kukadiria kipindi hicho. Hata ikiwa walifanya hivyo, huenda Wayahudi hawangeamini maoni ya kikundi hicho kilichojitenga.

Katika karne ya pili W.K., Wayahudi fulani waliamini kwamba majuma 70 yalianza hekalu la kwanza lilipoharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. hadi hekalu la pili lilipoharibiwa mwaka wa 70 W.K., lakini wengine walisema kwamba unabii huo ulitimia wakati wa Wamakabayo katika karne ya pili K.W.K. Kwa hiyo, watu walihesabu majuma hayo 70 kwa njia tofauti-tofauti.

Ikiwa kipindi hicho cha majuma 70 kilieleweka kwa usahihi katika karne ya kwanza W.K., basi mitume na Wakristo wengine katika karne ya kwanza wangekitumia kuthibitisha kwamba Yesu Kristo ndiye Masihi aliyeahidiwa na alitokea kwa wakati unaofaa. Hata hivyo, hakuna uthibitisho wa kwamba Wakristo wa mapema walifanya hivyo.

Tunapaswa pia kukumbuka jambo lingine. Mara nyingi, waandishi wa vitabu vya Injili walionyesha kwamba Yesu Kristo alitimiza unabii fulani katika Maandiko ya Kiebrania. (Mt. 1:22, 23; 2:13-15; 4:13-16) Hata hivyo, hakuna hata mmoja wao aliyehusianisha kutokea kwa Yesu na unabii wa majuma 70.

Kwa muhtasari: Hatujui kwa uhakika ikiwa watu katika siku za Yesu walielewa kwa usahihi ule unabii wa majuma 70. Hata hivyo, vitabu vya Injili vinataja sababu nyingine nzuri zinazoonyesha kwa nini watu walikuwa “wakimtarajia” Masihi.

^ fu. 4 Biblia haisemi kwamba malaika hao “waliimba” Yesu alipozaliwa.

^ fu. 7 Huenda tukauliza hivi: Kwa nini wanajimu walihusianisha “nyota” waliyoona wakiwa Mashariki na kuzaliwa kwa “mfalme wa Wayahudi”? Je, inawezekana kwamba walisikia kuhusu kuzaliwa kwa Yesu walipokuwa wakisafiri kupitia Israeli?

^ fu. 9 Sura ya 11 ya kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli! inaonyesha uelewaji wetu wa sasa kuhusu unabii huo wa majuma 70.