Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Maulizo ya Wasomaji Wetu

Maulizo ya Wasomaji Wetu

Wayahudi wa siku za Yesu walikuwa na sababu gani za kungojea Masiya wakati huo?

Katika siku za Yohana Mubatizaji, “watu walikuwa wakitarajia [ao kungojea] na wote walikuwa wakiwaza mioyoni mwao juu ya Yohana: ‘Je, labda yeye ndiye Kristo?’” (Lu. 3:15) Sababu gani Wayahudi walikuwa wakingojea Masiya atokee wakati huo? Kuna sababu fulani.

Kisha kuzaliwa kwa Yesu, malaika wa Yehova aliwatokea wachungaji waliokuwa wakichunga makundi yao katika mashamba karibu na Bethlehemu. Malaika aliwatangazia hivi: “Leo katika jiji la Daudi, Mwokozi ambaye ni Kristo Bwana, amezaliwa kwenu.” (Lu. 2:8-11) Kisha, “umati wa jeshi la mbingu ukawa pamoja na yule malaika, ukimusifu Mungu na kusema: * ‘Utukufu katika vilele vilivyo juu kwa Mungu, na juu ya dunia amani kati ya watu wa nia njema.’”​—Lu. 2:13, 14.

Tangazo hilo liliwachochea kabisa wachungaji hao wanyenyekevu. Mara moja walienda huko Bethlehemu, na walipomuona Yosefu na Maria na mutoto Yesu, ‘walisema mambo yaliyokuwa yamesemwa kuhusu mutoto huyo muchanga.’ Kisha, ‘wote waliosikia walistaajabu [ao walishangaa] juu ya mambo waliyoambiwa na wachungaji.’ (Lu. 2:17, 18) Maneno “wote waliosikia” yanaonyesha kwamba wachungaji hao hawakuwaambia Yosefu na Maria tu, lakini walielezea wengine pia. Baadaye, wachungaji walirudi nyumbani ‘wakimutukuza na kumusifu Mungu kwa ajili ya mambo yote waliyoyasikia na kuyaona, sawa na walivyokuwa wameambiwa.’ (Lu. 2:20) Wachungaji hao hawakuficha mambo mazuri waliyosikia kuhusu kuzaliwa kwa Kristo, lakini waliyaelezea wengine!

Maria alipomupeleka muzaliwa wake wa kwanza Yerusalemu ili kumuonyesha mbele za Yehova, kama Sheria ya Musa ilivyosema, Ana, nabii mwanamuke, ‘alianza kumushukuru Mungu akisema juu ya mutoto huyo kwa wale wote waliokuwa wakiungojea ukombozi wa Yerusalemu. (Lu. 2:36-38; Kut. 13:12) Hivyo ndivyo habari za kutokea kwa Masiya ziliendelea kuenea.

Baadaye, “wanajimu kutoka sehemu za mashariki walikuja Yerusalemu, wakisema: ‘Yuko wapi yule mufalme wa Wayahudi aliyezaliwa? Kwa maana tuliiona nyota yake wakati tulipokuwa mashariki, nasi tumekuja kumusujudia.’” (Mt. 2:1, 2) Aliposikia hivyo, ‘Mufalme Herode alifazaika, na Yerusalemu yote pamoja naye; na alipowakusanya pamoja wakuu wa makuhani na waandishi wote wa watu alianza kuuliza habari kutoka kwao juu ya ni wapi Kristo alipaswa kuzaliwa.’ (Mt. 2:3, 4) Kwa hiyo, watu wengi walianza kutambua kwamba: Masiya aliyeahidiwa amefika! *

Maneno ya Luka 3:15, yaliyo mwanzoni mwa habari hii, yanaonyesha kwamba Wayahudi fulani walifikiri kwamba pengine Yohana Mubatizaji ndiye Kristo. Lakini, Yohana alionyesha kwamba mawazo yao si kweli kwa kusema hivi: “yule anayekuja nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, ambaye viatu vyake mimi sistahili kuvivua. Huyo atawabatiza ninyi kwa roho takatifu na kwa moto.” (Mt. 3:11) Maneno ya unyenyekevu ya Yohana yaliwafanya wamungojee Masiya kwa hamu zaidi.

Je, Wayahudi wa siku za Yesu walihesabu wakati wa kuja kwa Masiya kwa kutumia unabii wa majuma 70 unaopatikana katika Danieli 9:24-27? Hatuwezi kuhakikisha jambo hilo, lakini pengine walifanya hivyo. Ukweli ni kwamba kulikuwa mafasirio mengi yenye kupingana kuhusu yale majuma 70 katika siku za Yesu, lakini hakuna hata mafasirio fulani yanayokabiriana na namna tunavyoelewa unabii huo leo. *

Waesene ambao watu wengi walifikiri kwamba walikuwa kikundi kilichojitenga cha watawa ao mapadri wanaume wa dini ya Kiyahudi, walifundisha kwamba Masiya wawili wangetokea mwishoni mwa kipindi cha miaka 490, lakini hatuko hakika kwamba walitumia unabii wa Danieli ili kufanya hesabu zao. Hata ikiwa walifanya hivyo, ni vigumu kukubali kwamba Wayahudi wote wangeamini hesabu za kikundi hicho kilichojitenga.

Katika miaka kati ya 101 na 200, kisha kuzaliwa kwa Yesu, Wayahudi fulani waliamini kwamba majuma 70 yalianza na kuharibiwa kwa hekalu la kwanza katika mwaka wa 607 mbele ya Yesu kuzaliwa mupaka kuharibiwa kwa hekalu la pili katika mwaka wa 70 kisha Yesu kuzaliwa. Wengine waliamini kwamba unabii huo ulitimizwa katika kipindi cha utawala wa Wamakabayo kati ya mwaka wa 101 na 200 mbele ya Yesu kuzaliwa. Kwa hiyo, hakukuwa makubaliano yaliyo wazi kuhusu namna majuma 70 yalipaswa kuhesabiwa.

Ikiwa namna ya kuhesabu majuma 70 ilikuja kueleweka vizuri wakati wa mitume, mutu angeweza kufikiri kwamba mitume na Wakristo wengine wa kwanza​-kwanza walioishi kati ya mwaka wa 1 na 100 wangetumia unabii wa majuma 70 ili kuonyesha kwamba Yesu Kristo ndiye Masiya aliyeahidiwa na kwamba alikuwa amefika kwa wakati unaofaa. Hata hivyo, hakuna ushuhuda unaoonyesha kwamba Wakristo wa kwanza​-kwanza walifanya hivyo.

Lakini, kuna jambo lingine la maana. Waandikaji wa vitabu vya Injili walitaja mara nyingi unabii mbalimbali unaopatikana katika Maandiko ya Kiebrania uliotimia katika Yesu Kristo. (Mt. 1:22, 23; 2:13-15; 4:13-16) Lakini, hakuna hata mumoja wa waandikaji hao aliyehusianisha kutokea kwa Yesu duniani na unabii wa majuma 70.

Kwa kifupi: Hatuwezi kuhakikisha kwamba watu walielewa vizuri unabii wa majuma 70 katika siku za Yesu. Hata hiyo, vitabu vya Injili vinatutolea sababu nzuri ambazo zingewachochea watu ‘watarajie’ ao wangojee Masiya wakati huo.

^ Biblia haiseme kwamba malaika ‘waliimba’ wakati Yesu alizaliwa.

^ Tunaweza kujiuliza hivi: Namna gani wanajimu walihusianisha kuonekana kwa “nyota” katika mashariki na kuzaliwa kwa ‘mufalme wa Wayahudi’? Je, walisikia kwamba Yesu amezaliwa walipokuwa wanasafiri katika Israeli?

^ Ili kujua namna tunavyoelewa unabii wa majuma 70 leo, soma kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli! sura ya 11.