Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Ona Uzuri wa Yehova’

‘Ona Uzuri wa Yehova’

Hali ngumu zinaweza kutuathiri sana. Zinaweza kuathiri mawazo yetu, mtazamo wetu kuhusu maisha na kutuvunja moyo. Mfalme Daudi wa taifa la kale la Israeli alikabili hali nyingi ngumu. Alikabilianaje na hali hizo? Daudi anajibu hivi katika zaburi moja inayogusa moyo: “Kwa sauti yangu, nilimwomba Yehova msaada; kwa sauti yangu, nilianza kumlilia Yehova anionyeshe kibali. Mbele zake niliendelea kumwaga hangaiko langu; mbele zake niliendelea kutangaza juu ya taabu yangu mwenyewe, roho yangu ilipozimia ndani yangu. Ndipo wewe mwenyewe ulipoijua barabara yangu.” Kwa kweli, Daudi alisali kwa Mungu kwa unyenyekevu ili amsaidie.—Zab. 142:1-3.

Katika nyakati za taabu, Daudi alisali kwa unyenyekevu ili Yehova amsaidie

Katika zaburi nyingine, Daudi aliimba hivi: “Nimemwomba Yehova jambo moja—ndilo nitakalolitafuta, kwamba nipate kukaa katika nyumba ya Yehova siku zote za maisha yangu, ili kuuona uzuri wa Yehova na kulitazama kwa uthamini hekalu lake.” (Zab. 27:4) Daudi hakuwa Mlawi, lakini wazia akiwa amesimama nje ya ua mtakatifu karibu kabisa na kitovu cha ibada ya kweli. Moyo wa Daudi umejaa shukrani hivi kwamba anataka kutumia siku zote za maisha yake katika nyumba hiyo ili “kuuona uzuri wa Yehova.”

Neno “uzuri” linahusianishwa na sifa au hali “inayokubalika au kutuliza akili, hisia au hisi.” Sikuzote Daudi aliutazama kwa uthamini mpango wa Mungu wa ibada. Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je ninahisi kama Daudi?

‘TAZAMA KWA UTHAMINI’ MPANGO WA MUNGU

Leo, mpango wa kumfikia Yehova hautegemei jengo fulani. Badala yake, unahusisha hekalu kuu la kiroho la Mungu, yaani, mpango mtakatifu wa ibada ya kweli. * ‘Tukitazama kwa uthamini’ mpango huo, sisi pia tunaweza “kuuona uzuri wa Yehova.”

Fikiria madhabahu ya shaba ya matoleo ya kuteketezwa iliyokuwa mbele ya mwingilio wa maskani ya hema la mkutano. (Kut. 38:1, 2; 40:6) Madhabahu hiyo ilionyesha kwamba Mungu alikuwa tayari kukubali uhai wa Yesu wa kibinadamu ukiwa dhabihu. (Ebr. 10:5-10) Wazia jambo hilo linavyomaanisha kwetu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kupitia kifo cha Mwana wake.” (Rom. 5:10) Tunapodhihirisha imani katika damu ya Yesu iliyomwagwa, tunaweza kufurahia kibali na utegemezo unaotokana na kuwa marafiki wa Mungu. Kwa hiyo, tunakuwa na “urafiki wa karibu pamoja na Yehova”—Zab. 25:14.

Kwa kuwa ‘dhambi zetu zinapata kufutwa,’ tunafurahia ‘majira ya kuburudisha kutoka kwa Yehova.’ (Mdo. 3:19) Hali yetu ni kama ya mfungwa anayejutia makosa yake ya zamani na anayeamua kufanya mabadiliko makubwa huku akisubiri kutekelezwa kwa hukumu yake ya kifo. Anapoona hilo, hakimu mwenye fadhili anachochewa kufuta makosa yake na kumwondolea hukumu ya kifo. Mfungwa huyo anafarijika na kufurahi sana. Kama hakimu huyo, Yehova huwaonyesha kibali na kuwaondolea hukumu ya kifo wanadamu wanaotubu.

UWE NA SHANGWE KATIKA IBADA YA KWELI

Mambo aliyoona Daudi katika nyumba ya Yehova yaliyohusu ibada ya kweli yalitia ndani kukusanyika pamoja na Waisraeli wenzake, kusomwa na kufafanuliwa kwa Sheria mbele ya watu, kufukizwa kwa uvumba, na utumishi mtakatifu  uliofanywa na makuhani na Walawi. (Kut. 30:34-38; Hes. 3:5-8; Kum. 31:9-12) Sehemu hizo za ibada ya kweli katika Israeli la kale zina ulinganifu katika siku zetu.

Leo, tunaona “jinsi ilivyo vyema na jinsi inavyopendeza ndugu kukaa pamoja kwa umoja!” kama tu ilivyokuwa zamani. (Zab. 133:1) Ulimwenguni pote kumekuwa na ongezeko kubwa katika “ushirika mzima wa akina ndugu.” (1 Pet. 2:17) Neno la Mungu linasomwa na kufafanuliwa mbele ya watu katika mikutano yetu. Yehova anatufundisha kupitia tengenezo lake. Vilevile, kuna chakula kingi cha kiroho kinachopatikana katika machapisho tunachoweza kutumia tunapojifunza kibinafsi na tukiwa familia. Mshiriki mmoja wa Baraza Linaloongoza alisema hivi: “Kutafakari Neno la Yehova, kufikiria maana yake, na kutafuta ufahamu na uelewaji kumenifanya kila asubuhi niamke nikiwa nimeridhika na kuhisi nikiwa tajiri kiroho.” Naam, ‘ujuzi na upendeze nafsi yetu.’—Met. 2:10.

Leo, sala zinazokubalika za watumishi wa Mungu humfikia Yehova kila siku. Yehova anaziona sala hizo kuwa kama uvumba wenye harufu tamu. (Zab. 141:2) Tunashukuru kama nini kujua kwamba Yehova Mungu anafurahi sana tunaposali kwake tukiwa na unyenyekevu!

Musa alisali hivi: “Nao uzuri wa Yehova Mungu wetu na uwe juu yetu, na kazi ya mikono yetu uifanye imara juu yetu.” (Zab. 90:17) Yehova hutubariki tunapoendelea kuhubiri kwa bidii. (Met. 10:22) Labda tumesaidia baadhi ya watu kujifunza kweli. Huenda tumehubiri kwa miaka mingi licha ya watu kutopendezwa na ujumbe wetu, afya mbaya, maumivu ya kihisia, au mateso. (1 The. 2:2) Hata hivyo, je, si kweli kwamba tumeona uzuri wa Yehova na kutambua kwamba Baba yetu wa kimbingu anapendezwa sana na jitihada zetu?

Daudi aliimba hivi: “Yehova ndiye sehemu ya fungu langu nililogawiwa na ya kikombe changu. Wewe unaishika sana kura yangu. Kamba za kupimia zimeniangukia mahali panapopendeza.” (Zab. 16:5, 6) Daudi alithamini “sehemu” yake, yaani, kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova na pendeleo la kumtumikia. Huenda tukakabili hali ngumu kama Daudi, lakini tuna baraka nyingi sana za kiroho. Na tuendelee kupata shangwe katika ibada ya kweli na ‘kulitazama sikuzote kwa uthamini’ hekalu la kiroho la Yehova.

^ fu. 6 Tazama Mnara wa Mlinzi, Julai 1, 1996, ukurasa 14-24.