Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Tunavyoweza Kudumisha Maoni Yanayofaa

Jinsi Tunavyoweza Kudumisha Maoni Yanayofaa

Mwanadamu akiishi miaka mingi, na aishangilie hiyo yote.MHU. 11:8.

1. Ni baraka gani kutoka kwa Yehova zinazoweza kutuletea furaha?

YEHOVA anataka tuwe na furaha, naye hutubariki kwa njia nyingi zinazopaswa kutufanya tuwe na furaha. Kwanza, ametupa uhai. Hivyo, tunaweza kutumia uhai wetu kumsifu Mungu kwa kuwa ametuvuta kwenye ibada ya kweli. (Zab. 144:15; Yoh. 6:44) Yehova anatuhakikishia kwamba anatupenda, naye hutusaidia kuendelea kumtumikia. (Yer. 31:3; 2 Kor. 4:16) Tunafurahia paradiso ya kiroho ambamo tunapata chakula kingi cha kiroho na undugu wenye upendo. Isitoshe, tuna tumaini la wakati ujao lenye thamani.

2. Baadhi ya watumishi waaminifu wa Mungu wanapambana na nini?

2 Baadhi ya watumishi waaminifu wa Mungu wanajiona hawafai licha ya kwamba tuna baraka hizo. Huenda wakahisi kwamba Yehova hawathamini na pia hathamini utumishi wanaomtolea. Wale wanaoendelea kupambana na hisia hizo zisizofaa wanaona kufurahia “miaka mingi” kuwa ndoto tu. Huenda wakaona kwamba maisha ni mfululizo wa siku za giza.Mhu. 11:8.

3. Ni nini kinachoweza kumfanya mtu ahisi kwamba hafai?

3 Huenda ndugu au dada hao wakaanza kuhisi kwamba hawafai kwa sababu ya hali zenye kuvunja moyo, ugonjwa, au matatizo ya uzeeni. (Zab. 71:9; Met. 13:12; Mhu. 7:7) Isitoshe, ni lazima kila Mkristo akubali ukweli wa kwamba moyo ni wenye  hila na unaweza kutuhukumu hata ikiwa Mungu anapendezwa nasi. (Yer. 17:9; 1 Yoh. 3:20) Ibilisi huwashtaki kwa uwongo watumishi wa Mungu. Na watu wenye mawazo kama ya Shetani wanaweza kujaribu kutuchochea tuwe na maoni kama ya Elifazi aliyekosa imani na kusema kwamba—hatuna thamani machoni pa Mungu. Huo ulikuwa uwongo katika siku za Ayubu na bado ni uwongo leo.Ayu. 4:18, 19.

4. Tutachunguza nini katika makala hii?

4 Yehova anasema waziwazi katika Maandiko kwamba atakuwa pamoja na wale ‘wanaotembea katika bonde lenye kivuli kizito.’ (Zab. 23:4) Njia moja ambayo Yehova yupo pamoja nasi ni kupitia Neno lake. Biblia ‘ina nguvu kutoka kwa Mungu kwa ajili ya kupindua ngome zenye nguvu,’ kutia ndani maoni na mawazo yasiyofaa. (2 Kor. 10:4, 5) Acheni tuone jinsi tunavyoweza kutumia Biblia ili itusaidie kusitawisha na kudumisha maoni yanayofaa. Ukifanya hivyo, unaweza kufaidika kibinafsi na kuwatia moyo wengine.

TUMIA BIBLIA KUSITAWISHA MAONI YANAYOFAA

5. Tunaweza kujijaribu kwa njia gani ili tudumishe maoni yanayofaa?

5 Mtume Paulo alitaja mambo fulani yanayoweza kutusaidia kusitawisha maoni yanayofaa. Aliwahimiza hivi washiriki wa kutaniko la Korintho: “Endeleeni kujijaribu kama ninyi mko katika imani.” (2 Kor. 13:5) “Imani” hiyo ni mafundisho yote ya Kikristo yanayofunuliwa katika Biblia. Ikiwa maneno na matendo yetu yanapatana na mafundisho hayo, basi yanathibitisha kwamba tuko “katika imani.” Bila shaka, ni lazima maisha yetu yapatane pia na mafundisho yote ya Kikristo. Hatupaswi kuchagua mafundisho tutakayofuata.Yak. 2:10, 11.

6. Kwa nini tunapaswa kujijaribu ili tuone ‘kama tuko katika imani’? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 12.)

6 Huenda ukasita kujijaribu kwa njia hiyo, hasa ikiwa unahisi kwamba huwezi kufaulu. Hata hivyo, maoni ya Yehova kutuhusu ni muhimu kuliko maoni yetu, na mawazo yake yako juu kuliko mawazo yetu. (Isa. 55:8, 9) Hawachunguzi waabudu wake ili awashutumu, badala yake anatafuta sifa zao nzuri na kuwasaidia. Ukitumia Neno la Mungu kujijaribu ili uone ‘kama uko katika imani,’ utaanza kuelewa jinsi Mungu anavyokuona. Hilo linaweza kukusaidia kutohisi kamwe kwamba huna thamani machoni pa Mungu na kukumbuka uhakikisho huu unaotegemea Biblia: Una thamani machoni pa Yehova. Kutambua hilo ni kama kufungua dirisha ili mwangaza wa jua uingie katika chumba chenye giza.

7. Tunaweza kufaidikaje kutokana na mifano ya watu waaminifu katika Biblia?

7 Njia nzuri ya kujichunguza ni kutafakari mifano ya watu waaminifu wanaotajwa katika Biblia. Linganisha hisia au hali zao na zako, na ufikirie jinsi ambavyo ungetenda katika hali hizo. Acheni tuchunguze mifano mitatu inayoonyesha jinsi unavyoweza kutumia Biblia kuthibitisha ikiwa uko “katika imani” na hivyo kusitawisha maoni yanayofaa.

MJANE MWENYE UHITAJI

8, 9. (a) Mjane mwenye uhitaji alikuwa katika hali gani? (b) Huenda mjane huyo alikuwa na hisia gani zisizofaa?

8 Yesu alimtazama mjane fulani mwenye uhitaji katika hekalu la Yerusalemu. Mfano wa mjane huyo unaweza kutusaidia kudumisha maoni yanayofaa licha ya udhaifu wetu. (Soma Luka 21:1-4.) Fikiria hali za mjane huyo. Alivumilia huzuni ya kufiwa na mume wake na pia alivumilia hali mbaya iliyosababishwa na viongozi wa kidini ‘waliomeza nyumba za wajane’ badala ya kuwasaidia watu hao wanyonge. (Luka 20:47) Alikuwa maskini sana hivi kwamba mchango aliotoa hekaluni ulikuwa sawa na mshahara ambao mfanyakazi angelipwa kwa kufanya kazi kwa dakika chache tu.

 9 Hebu wazia jinsi mjane huyo alivyohisi alipoingia kwenye ua wa hekalu akiwa na sarafu zake mbili zenye thamani ndogo. Je, huenda alifikiri kwamba angetoa mchango mkubwa ikiwa mume wake angekuwa hai? Je, aliaibika alipoona wengine waliokuwa mbele yake wakitoa michango mikubwa, pengine akihisi kwamba mchango wake haukuwa na thamani yoyote? Hata ikiwa alihisi hivyo, bado alifanya yote aliyoweza kwa ajili ya ibada ya kweli.

10. Yesu alionyeshaje kwamba mjane huyo alikuwa mwenye thamani machoni pa Mungu?

10 Yesu alionyesha kwamba Yehova alimthamini mjane huyo na mchango wake. Hata alisema kwamba mjane huyo ‘alitumbukiza ndani zaidi kuliko matajiri hao wote.’ Mchango wake ulichanganyika na michango ya watu wengine, lakini Yesu alimsifu mjane huyo. Watunzaji wa masanduku ya hazina ambao baadaye waliona sarafu hizo mbili zenye thamani ndogo hawangeweza kujua jinsi Yehova alivyothamini sana sarafu hizo na aliyezitoa. Hata hivyo, maoni ya Mungu ndiyo yaliyokuwa muhimu zaidi kuliko jinsi alivyojiona au jinsi wengine walivyomwona. Je, unaweza kutumia simulizi hilo kujijaribu ikiwa uko katika imani?

Tunajifunza nini kutokana na mfano wa mjane mwenye uhitaji?(Tazama fungu la 8-10)

11. Unaweza kujifunza nini kutokana na simulizi la mjane?

11 Hali zako zinaweza kuathiri moja kwa moja yale unayoweza kutimiza katika utumishi wa Yehova. Kwa sababu ya umri mkubwa au matatizo ya kiafya, wahubiri fulani hawawezi kuhubiri habari njema kwa saa nyingi. Je, wanapaswa kuhisi kwamba hawastahili kutoa ripoti ya utumishi wao? Hata ikiwa huna matatizo mengi, unaweza kuhisi kwamba jitihada zako hazina thamani zikilinganishwa na jumla ya saa ambazo watu wa Mungu hutumia kila mwaka kumwabudu. Hata hivyo, tunajifunza kutokana na simulizi la mjane maskini kwamba Yehova huona na kuthamini kila jambo tunalofanya katika ibada yake, hasa tunapokabili hali ngumu. Fikiria mambo uliyotimiza katika ibada ya Yehova mwaka  uliopita. Je, kuna pindi yoyote ulipohitaji kujidhabihu kwa njia ya pekee ili umtumikie Mungu? Ikiwa ndivyo, uwe na hakika kwamba Yehova anathamini utumishi uliomtolea katika pindi hiyo. Ikiwa unafanya yote unayoweza katika utumishi wa Yehova kama yule mjane mwenye uhitaji, hilo linathibitisha kwamba uko “katika imani.”

“IONDOE NAFSI YANGU”

12-14. (a) Hisia zisizofaa zilimwathirije Eliya? (b) Kwa nini huenda Eliya alihisi hivyo?

12 Nabii Eliya alikuwa mshikamanifu kwa Yehova na alikuwa na imani yenye nguvu. Hata hivyo, pindi moja alivunjika moyo sana hivi kwamba akamwambia Yehova amuue. Alisema hivi: “Inatosha! Sasa, Ee Yehova, iondoe nafsi yangu.” (1 Fal. 19:4) Wale ambao hawajawahi kukata tamaa kwa njia hiyo wanaweza kufikiri kwamba sala ya Eliya ni “mazungumzo ya ovyoovyo” tu. (Ayu. 6:3) Lakini, hivyo ndivyo alivyohisi. Hata hivyo, kumbuka kwamba badala ya kumshutumu Eliya kwa kuomba afe, Yehova alimsaidia.

13 Kwa nini Eliya alihisi hivyo? Muda mfupi kabla ya wakati huo, alisimamia jaribu la kukata maneno katika Israeli lililothibitisha kwamba Yehova ni Mungu wa kweli. Pindi hiyo, manabii 450 wa Baali waliuawa. (1 Fal. 18:37-40) Inaelekea Eliya alitarajia kwamba baada ya tukio hilo, watu wa Mungu wangerudia ibada safi, lakini hawakufanya hivyo. Malkia Yezebeli aliyekuwa mwovu alimtuma mjumbe amwambie Eliya kwamba anakusudia kumuua. Akihofia uhai wake, Eliya alikimbilia upande wa kusini akipitia Yuda na kuingia nyikani, eneo kame lisilo na chochote.1 Fal. 19:2-4.

14 Akiwa peke yake, huenda Eliya alifikiri kwamba mgawo wake akiwa nabii ulikuwa wa bure. Alimwambia Yehova hivi: “Mimi si bora kuliko mababu zangu.” Alimaanisha kwamba alihisi hana thamani yoyote, sawa na mavumbi na mifupa ya mababu zake. Ni kana kwamba alijijaribu kwa kutumia viwango vyake mwenyewe na kuamua kwamba yeye ni mtu asiyefaa kitu na asiyethaminiwa na Yehova wala na mtu yeyote.

15. Mungu alimhakikishiaje Eliya kwamba bado Alimthamini?

15 Hata hivyo, Mweza-Yote alikuwa na maoni tofauti kumhusu Eliya. Bado Eliya alikuwa mwenye thamani machoni pa Mungu, na Yehova alichukua hatua ili kumhakikishia hilo. Mungu alimtuma malaika kumwimarisha Eliya. Pia, Yehova alimwandalia Eliya chakula na maji ambayo yangemtegemeza katika safari yake ya siku 40 kuelekea kusini kwenye Mlima Horebu. Isitoshe, Mungu alisahihisha kwa fadhili maoni ya Eliya yasiyofaa ya kwamba hakukuwa na Mwisraeli mwingine mwaminifu kwa Yehova. Pia, Mungu alimpa Eliya migawo mipya, naye akaikubali. Eliya alinufaika kutokana na msaada wa Yehova, akarudia kazi yake ya kutoa unabii akiwa na nguvu mpya.—1 Fal. 19:5-8, 15-19.

16. Mungu amekutegemeza katika njia zipi?

16 Kisa cha Eliya kinaweza kukusaidia kujithibitishia kwamba uko katika imani na kukuchochea ili uwe na maoni yanayofaa. Kwanza, fikiria njia ambazo Yehova amekutegemeza. Je, huenda mmoja wa watumishi wake, pengine mzee wa kutaniko au Mkristo mwingine mkomavu, alikusaidia ulipokuwa na uhitaji? (Gal. 6:2) Je, umejengwa kiroho kwa kusoma Biblia, machapisho yetu ya Kikristo, na kuhudhuria mikutano ya kutaniko? Wakati ujao utakaponufaika kupitia mojawapo ya njia hizo, mkumbuke Yehova ambaye ndiye Chanzo halisi cha msaada huo na umshukuru kupitia sala.Zab. 121:1, 2.

17. Yehova huthamini sifa gani za watumishi wake?

17 Pili, tambua kwamba maoni yasiyofaa  yanaweza kukupotosha. Jambo muhimu zaidi ni jinsi Mungu anavyotuona. (Soma Waroma 14:4.) Yehova huthamini ujitoaji na uaminifu wetu; hapimi thamani yetu kwa mambo tunayotimiza. Na inawezekana kwamba kama Eliya, umefanya mambo mengi katika utumishi wa Yehova kuliko unavyofikiri. Inaelekea kwamba watu fulani kutanikoni wamechochewa na mfano wako mzuri na huenda jitihada zako zimewasaidia wengine katika eneo kupata kweli.

18. Mgawo uliopewa na Yehova unathibitisha nini?

18 Hatimaye, uone kila mgawo kutoka kwa Yehova kuwa uthibitisho wa kwamba yupo pamoja nawe. (Yer. 20:11) Sawa na Eliya, huenda ukavunjika moyo kwa sababu unafikiri kwamba hupati matokeo katika utumishi wako au kwa sababu unafikiri huwezi kutimiza miradi fulani ya kiroho. Hata hivyo, bado unafurahia pendeleo kubwa zaidi ambalo sote tunaweza kuwa nalo, yaani, pendeleo la kuhubiri habari njema na kuitwa kwa jina la Mungu. Endelea kuwa mwaminifu. Kisha, ‘utaingia katika shangwe ya bwana wako’ kama Yesu alivyosema katika mfano mmoja.Mt. 25:23.

“SALA YA MWENYE KUTESEKA”

19. Ni hali gani aliyokabili mwandikaji wa Zaburi ya 102?

19 Mwandikaji wa Zaburi ya 102 alikuwa amekata tamaa. ‘Aliteseka’ sana kimwili au kihisia, naye hakuwa na nguvu za kupambana na matatizo aliyokabili. (Zab. 102, maelezo ya utangulizi) Maneno aliyosema yanaonyesha kwamba alihangaishwa sana na maumivu, upweke, na hisia zake mwenyewe. (Zab. 102:3, 4, 6, 11) Aliamini kwamba Yehova alitaka kumtupilia mbali.—Zab. 102:10.

20. Sala inawezaje kumsaidia mtu anayepambana na maoni yasiyofaa?

20 Hata hivyo, mtunga-zaburi huyo aliendelea kutumia uhai wake kumsifu Yehova. (Soma Zaburi 102:19-21.) Kama tunavyoona katika Zaburi ya 102, hata watu walio katika imani wanaweza kuwa na maumivu na kushindwa kukazia fikira mambo mengine. Mtunga-zaburi alijiona kuwa “kama ndege aliye peke yake juu ya dari,” kana kwamba alizungukwa tu na taabu zake. (Zab. 102:7) Ukihisi hivyo, mmiminie Yehova moyo wako kama alivyofanya mtunga-zaburi. Sala za mwenye kuteseka, yaani,—sala zako,—zitakusaidia kupambana na maoni yasiyofaa. Yehova anaahidi kwamba “ataielekea sala ya wale waliovuliwa kila kitu, naye hataidharau sala yao.” (Zab. 102:17) Amini ahadi hiyo.

21. Mtu anayepambana na hisia zisizofaa atafanya nini ili awe na maoni yanayofaa zaidi?

21 Zaburi ya 102 inaonyesha pia jambo unaloweza kufanya ili uwe na maoni yanayofaa zaidi. Mtunga-zaburi alifanya hivyo kwa kukazia fikiria uhusiano wake na Yehova. (Zab. 102:12, 27) Alitiwa moyo alipojua kwamba Yehova atakuwa sikuzote pamoja na watu wake ili awasaidie kukabiliana na majaribu. Kwa hiyo, ikiwa hisia zisizofaa zinakuzuia kwa muda kufanya yote ambayo ungependa kufanya katika utumishi wa Mungu, sali kuhusu jambo hilo. Mwombe Mungu asikilize sala yako ili maumivu yako yapungue na “ili jina la Yehova litangazwe.”—Zab.—102:20, 21.

22.  Kila mmoja wetu anawezaje kumpendeza Yehova?

22 Naam, tunaweza kutumia Biblia kujithibitishia wenyewe kwamba tuko katika imani na kwamba sisi ni wenye thamani machoni pa Yehova. Ukweli ni kwamba katika mfumo huu wa mambo, huenda tusiweze kuondoa kabisa hisia zisizofaa au mambo yote yenye kuvunja moyo. Hata hivyo, kila mmoja wetu anaweza kumpendeza Yehova na kupata wokovu kwa kuendelea kuvumilia kwa uaminifu katika utumishi wake.—Mt. 24:13.