Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ibada ya Familia—Je, Mnaweza Kuifanya Ifurahishe Zaidi?

Ibada ya Familia—Je, Mnaweza Kuifanya Ifurahishe Zaidi?

Baba mmoja nchini Brazili anasema hivi: “Sisi hufurahia sana mazungumzo yetu wakati wa jioni ya Ibada ya Familia hivi kwamba nisipoyakatiza yanaweza kuendelea mpaka usiku.” Ndugu mmoja nchini Japani anasema kwamba mwana wake mwenye umri wa miaka kumi hupenda Ibada ya Familia iendelee hivi kwamba hatambui wakati unapopita. Kwa nini? “Yeye hufurahia kujifunza, na hilo huongeza shangwe yake,” asema baba yake.

Bila shaka, si watoto wote wanaofurahia kujifunza, na ukweli ni kwamba watoto wengine hawafurahii ibada ya familia. Kwa nini? Baba mmoja nchini Togo alitaja jambo hili muhimu: “Ibada ya Yehova haipaswi kuchosha.” Je, labda inachosha kwa kuwa haiongozwi kwa njia inayofaa? Familia nyingi zimegundua kwamba ibada ya familia inaweza kuleta “furaha tele,” kama alivyosema Isaya kuhusu Sabato.Isa. 58: 13, 14.

Baba Wakristo wanatambua kwamba mazingira yanayofaa ni muhimu ili familia ifurahie ibada ya familia. Ralf, ambaye ana binti watatu na mvulana mmoja anasema kwamba wanapofanya ibada yao ya familia wanakuwa na mazungumzo ya kawaida yasiyo rasmi; kila mtu hushiriki. Ni kweli kwamba nyakati nyingine si rahisi kuhakikisha kwamba kila mtu anashiriki na kufurahia funzo. Mama mmoja anakiri hivi: “Nyakati nyingine mimi hushindwa kufanya ibada ya familia ifurahishe kama vile ambavyo ningependa.” Unaweza kufanya nini ili ibada yenu ifurahishe?

BADILIKA KULINGANA NA HALI NA UFANYE MAMBO TOFAUTI-TOFAUTI

“Ni lazima tubadilike kulingana na hali,” asema baba mwenye watoto wawili nchini Ujerumani. “Jambo lililo muhimu zaidi kwa familia yetu ni kufanya mambo tofauti-tofauti,”  asema Natalia, mama mwenye watoto wawili. Familia nyingi hufanya mambo kadhaa katika ibada yao ya familia. “Hilo hufanya funzo liwe lenye kuchangamsha zaidi na wote katika familia hushiriki,” anaeleza Cleiton, baba mwenye matineja wawili nchini Brazili. Wazazi wanaweza kugawanya wakati wa funzo ili kushughulikia mahitaji ya kila mtoto, hasa ikiwa umri wa watoto unatofautiana sana. Wanaweza kushughulikia mahitaji ya kila mshiriki wa familia na kuchagua habari na mbinu za kujifunza habari hiyo ikitegemea hali ya familia.

Familia nyingine zinafanya nini ili kuboresha ibada yao? Wengine huanza ibada yao ya familia kwa kuimba nyimbo za kumsifu Yehova. Juan anayeishi Mexico anasema hivi: “Kuimba huboresha ibada na kututayarisha kiakili.” Familia yake huchagua nyimbo zinazohusiana na habari watakazojifunza jioni hiyo.

Sri Lanka

Familia nyingi husoma sehemu fulani ya Biblia pamoja. Ili ibada ifurahishe, kila mshiriki wa familia husoma maneno ya mhusika fulani katika sehemu hiyo ya Biblia. Baba mmoja nchini Japani anakiri kwamba “mwanzoni lilionekana kuwa jambo lisilo la kawaida.” Hata hivyo, wavulana wake wawili walifurahi kuwaona wazazi wao wakisoma kwa njia hiyo pamoja nao. Familia nyingine huigiza masimulizi ya Biblia. Watoto “mara nyingi huona mambo ambayo sisi wazazi hatukuyaona katika simulizi la Biblia,” asema Roger, baba wa wavulana wawili nchini Afrika Kusini.

Afrika Kusini

Familia zinaweza pia kuwa na mradi fulani, kama vile kujenga safina ya Noa ya mfano au hekalu la Sulemani. Ili kutimiza miradi hiyo ni lazima mfanye utafiti, na hilo ni jambo linalosisimua. Kwa mfano, msichana mmoja mwenye umri wa miaka mitano kutoka Asia pamoja na wazazi wake na nyanya yake, walitengeneza mchezo ulioonyesha safari za umishonari za mtume Paulo. Familia nyingine zimetengeneza michezo inayotegemea masimulizi yaliyo katika kitabu cha Kutoka. Kufanya mambo tofauti-tofauti “kumeboresha ibada yetu ya familia na maisha yetu ya familia,” asema Donald mwenye umri wa miaka 19 anayeishi nchini Togo. Je, mnaweza kufikiria mradi ambao utafanya ibada yenu ya familia ifurahishe zaidi?

Marekani

KUJITAYARISHA NI MUHIMU

Kufanya mambo tofauti-tofauti na kubadili ibada ya familia kulingana na hali huifanya ipendeze. Hata hivyo, wote wanahitaji kujitayarisha ili iwe yenye kuelimisha. Nyakati nyingine watoto huchoka, hivyo akina baba wanahitaji kufikiria mapema habari iliyochaguliwa na kujitayarisha vizuri. Baba mmoja anasema hivi: “Ninapojitayarisha, kila mtu hunufaika zaidi wakati wa funzo.” Baba mwingine nchini Ujerumani huijulisha mapema familia yake mambo watakayojifunza katika majuma yanayofuata. Nchini Benin, baba mmoja mwenye watoto sita, huwapa mapema maswali atakayowauliza katika ibada ya familia baada ya kutazama DVD inayotegemea Biblia. Kwa kweli, kujitayarisha huboresha ibada yetu ya familia.

Familia inapojua mapema mambo watakayojifunza, inaweza kuyazungumzia kabla ya funzo na hivyo kuwa na hamu ya kujifunza. Na ikiwa kila mtu ana mgawo, atahisi kwamba ibada ya familia inamhusu yeye binafsi.

JITAHIDINI KUIFANYA KWA UKAWAIDA

Familia nyingi hukabili changamoto ya kufanya ibada yao ya familia kwa ukawaida.

Baba wengi hulazimika kufanya kazi saa nyingi ili kupata mahitaji ya lazima. Kwa mfano, baba mmoja nchini Mexico huondoka nyumbani saa kumi na mbili asubuhi na kurudi saa mbili usiku. Mara nyingine huenda mkahitaji kubadili wakati wa Ibada ya Familia kwa sababu ya utendaji mwingine wa kiroho.

Hata hivyo, tunahitaji kuazimia kufanya ibada ya familia kwa ukawaida. Loïs, mwenye umri wa miaka 11 anayeishi nchini Togo, anasema hivi kuhusu azimio la familia yao: “Ijapokuwa pindi nyingine tunaanza ibada yetu ya familia tukiwa tumechelewa kwa sababu ya jambo fulani lililotokea mchana, hatukosi kamwe kuifanya.” Basi unaweza kuelewa ni kwa nini familia nyingine hupanga kufanya ibada ya familia mwanzoni mwa juma. Ikiwa jambo lisilotazamiwa litatokea, wanaweza kufanya ibada ya familia siku nyingine katika juma hilo.

Maneno “ibada ya familia” yanaonyesha kwamba ni sehemu ya ibada yako kwa Yehova. Washiriki wote wa familia na wamletee Yehova ‘ng’ombe-dume wachanga wa midomo yao’ kila juma. (Hos. 14:2) Kila mmoja katika familia na afurahie pindi hiyo, “kwa maana shangwe ya Yehova ndiyo ngome yenu.”Neh. 8:9, 10.