Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tuwaheshimu Ndugu na Dada Zetu Wenye Kuzeeka

Tuwaheshimu Ndugu na Dada Zetu Wenye Kuzeeka

‘Umuheshimu mutu aliye muzee.’​—LAW. 19:32. (Verbum Bible)

1. Wanadamu wako katika hali gani yenye kuhuzunisha?

 YEHOVA hakukusudia hata kidogo wanadamu wapatwe na matatizo ya uzee ambayo yanafanya mwili uwe zaifu. Tofauti na hilo, kusudi lake lilikuwa kwamba wanaume na wanawake wafurahie afya nzuri katika Paradiso. Lakini sasa “uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu.” (Rom. 8:22) Unafikiri Mungu anajisikia namna gani wakati anaona matokeo mabaya ya zambi? Zaidi ya hilo, watu wengi wenye kuzeeka wanaachiliwa na kuzarauliwa wakati wanahitaji musaada zaidi.​—Zab. 39:5; 2 Tim. 3:3.

2. Sababu gani tunafurahia sana kuwa na ndugu na dada wenye kuzeeka?

2 Sisi watumishi wa Yehova tunafurahia sana kuwa na ndugu na dada wenye kuzeeka katika makutaniko. Tunafaidika na hekima yao na tunachochewa na imani yao. Wengine kati ya ndugu na dada hao ni watu wa jamaa yetu. Hata hivyo, iwe wao ni wa jamaa yetu ao hapana, tunapaswa kuwahangaikia. (Gal. 6:10; 1 Pet. 1:22) Tutafaidika sisi wote kwa kuchunguza namna gani Mungu anawaona ndugu na dada hao wenye kuzeeka. Tutazungumuzia pia daraka la familia na la kutaniko kuelekea ndugu na dada zetu wapendwa ambao wamezeeka.

“USINITUPE”

3, 4. (a) Ni ombi gani la maana ambalo mwandikaji wa Zaburi ya 71 alifanya kwa Yehova? (b) Ndugu na dada zetu wenye kuzeeka wanaweza kumuomba Mungu nini?

3 Akiongozwa na roho ya Mungu, mwandikaji wa Zaburi 71:9 alimulilia Mungu hivi: “Usinitupe wakati wa uzee; wakati tu nguvu zangu zinapungua, usiniache.” Inaonekana kwamba Zaburi hiyo inaendeleza mawazo ya Zaburi ya 70 iliyo na maneno ya utangulizi “Ya Daudi.” Kwa hiyo, inaonekana kwamba Daudi ndiye alifanya ombi tunalosoma kwenye Zaburi 71:9. Alimutumikia Mungu tangu ujana wake mupaka wakati wa uzee, na Yehova alimutumia kufanya mambo mengi ya ajabu. (1 Sam. 17:33-37, 50; 1 Fal. 2:1-3, 10) Hata hivyo, Daudi aliona kwamba anahitaji kumuomba Yehova aendelee kumutegemeza.​—Soma Zaburi 71:17, 18.

4 Leo, ndugu na dada wengi wenye kuzeeka wako kama Daudi. Ijapokuwa wamezeeka na wanapambana na ‘siku zenye musiba,’ wanaendelea kumusifu Mungu na kufanya yote wanayoweza. (Mhu. 12:1-7) Wengi kati yao hawana tena uwezo wa kufanya yote waliyokuwa wakifanya katika maisha, na vilevile katika utumishi. Lakini wao pia wanaweza kuendelea kumuomba Yehova aendelee kupendezwa nao na kuwatunza. Ndugu na dada hao waaminifu wanapaswa kuwa hakika kwamba Mungu atajibu sala zao. Bila shaka, sala zao zinafanana na sala ambayo Daudi alifanya alipoongozwa na roho ya Mungu.

5. Namna gani Yehova anawaona ndugu na dada waaminifu wenye kuzeeka?

5 Maandiko yanaonyesha waziwazi kwamba Yehova anapendezwa sana na uaminifu wa ndugu na dada wenye kuzeeka na anataka watumishi wake wawaheshimu. (Zab. 22:24-26; Met. 16:31; 20:29) Andiko la Walawi 19:32 linasema hivi: ‘Unapaswa kusimama mbele ya mutu mwenye imvi, nawe umwonyeshe ufikirio [umuheshimu] mutu muzee, nawe umuogope Mungu wako. Mimi ni Yehova.’ Bila shaka, maneno hayo yalipoandikwa, kuwaheshimu watu waliozeeka ilikuwa daraka kubwa sana katika Israeli, kama ilivyo pia leo. Lakini, namna gani wanapaswa kutunzwa? Na ni daraka la nani?

DARAKA LA FAMILIA

6. Yesu alituachia mufano gani kuhusiana na kuwatunza wazazi?

6 Neno la Mungu linatuambia hivi: ‘Muheshimu baba yako na mama yako.’ (Kut. 20:12; Efe. 6:2) Yesu alikazia amri hiyo alipowalaumu waandishi na Mafarisayo waliokataa kutimiza mahitaji ya wazazi wao. (Mk. 7:5, 10-13) Yesu mwenyewe alituachia mufano muzuri. Alipokaribia kufa kwenye muti wa mateso, alifanya mipango ili mwanafunzi ambaye alimupenda sana, ni kusema, Yohana, amutunze Maria mama yake, ambaye pengine alikuwa mujane wakati huo.​—Yoh. 19:26, 27.

7. (a) Mutume Paulo alitoa kanuni gani kuhusu kuwatunza wazazi? (b) Paulo alikuwa akizungumuzia nini alipotoa kanuni hiyo?

7 Mutume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika kwamba watumishi wa Yehova wanapaswa kuwatunza watu wa jamaa zao wenyewe. (Soma 1 Timotheo 5:4, 8, 16.) Tuchunguze maneno ambayo Paulo alimuandikia Timotheo. Paulo alikuwa akizungumuzia yule ambaye kutaniko linaweza kumutolea musaada wa feza na yule ambaye hastahili kupokea musaada huo. Paulo alionyesha waziwazi kwamba watoto wanaoamini, wajukuu, na watu wengine wa jamaa ya wajane wenye kuzeeka ndio walipaswa kwanza kuwatimizia mahitaji yao. Kwa hiyo, kutaniko halingebeba muzigo huo. Vivyo hivyo leo, Wakristo wanaonyesha kwamba “wamejitoa kwa Mungu” kwa kuwatimizia watu wa jamaa zao mahitaji yao ya kimwili.

8. Kwa kuwa Biblia haizungumuzie kila jambo kuhusu kuwatunza wazazi wenye kuzeeka, tunapaswa kuepuka nini?

8 Kwa kifupi, watoto walio Wakristo ambao ni watu wazima wanapaswa kuwatimizia wazazi wao mahitaji yao ya kimwili. Hata ikiwa Paulo alikuwa akizungumuzia watu wa jamaa ambao ni waamini, hatupaswe kuwaachilia wazazi wetu wasiokuwa Mashahidi. Ni kweli kwamba watoto wanatumia njia mbalimbali ili kuwatunza wazazi wao. Hakuna hali zinazofanana. Mahitaji, tabia, na afya ya wale wanaotunzwa inatofautiana. Watu fulani wenye kuzeeka wana watoto wengi, lakini wengine wana mutoto mumoja tu. Watu fulani wenye kuzeeka wanasaidiwa na serikali, lakini wengine hapana. Na kila mutu ana mapendezi yake. Kwa hiyo, si vizuri na ni kukosa upendo kuchambua-chambua namna mutu anavyojikaza kuwatunza watu wa jamaa yake wenye kuzeeka. Yehova anaweza kubariki uamuzi wowote unaopatana na Maandiko ili uwe na matokeo mazuri, kama amekuwa akifanya tangu siku za Musa.​—Hes. 11:23.

9-11. (a) Watumishi fulani wa wakati wote wanaweza kujikuta mbele ya uamuzi gani? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.) (b) Sababu gani mutu hapaswe kuamua haraka-haraka kuacha utumishi wa wakati wote? Toa mufano.

9 Ikiwa wazazi wenye kuzeeka wanaishi mbali na watoto wao, inaweza kuwa vigumu kwa watoto kuwatolea musaada unaohitajiwa. Muzazi mwenye kuzeeka anaweza kuhitaji kutembelewa haraka ikiwa amepatwa na hali mbaya ya gafula, pengine kwa sababu ya kuanguka, kuvunjika mufupa, ao tatizo lingine. Kwa hiyo, anaweza kuhitaji musaada wa muda mufupi ao murefu. *

10 Watumishi wa wakati wote wanaotumikia mbali na kwao wanaweza kujikuta mbele ya uamuzi ulio muzito kabisa. Wanabeteli, wamisionere, na waangalizi wanaosafiri wanaona migawo yao kuwa ya maana sana, wanaiona kuwa baraka kutoka kwa Yehova. Hata hivyo, ikiwa wazazi wao wanagonjwa, wazo la kwanza linaweza kuwa kuacha migawo yao na kurudi nyumbani ili kuwatunza wazazi. Lakini, ni jambo la hekima kusali na kufikiri kwa uzito ili kujua ikiwa hilo ndilo jambo ambalo wazazi wanapenda ao kuhitaji kabisa. Mutu hapaswe kuamua haraka-haraka kuacha mapendeleo yake ya utumishi, na pengine si lazima tu kufanya hivyo. Pengine ugonjwa wa wazazi wetu ni wa muda mufupi unaoweza kuhangaikiwa na ndugu na dada fulani walio katika kutaniko lao.​—Met. 21:5.

11 Kwa mufano, fikiria ndugu wawili wa kimwili waliokuwa wakitumikia mbali na nyumbani. Mumoja alikuwa misionere huko Amerika Kusini, na mwengine alitumika kwenye makao makubwa, huko Brooklyn, New York. Wazazi wenye kuzeeka wa ndugu hao walihitaji musaada. Ndugu hao wawili na bibi zao walitembelea wazazi wao huko Asia Mashariki ili kuona ni musaada gani ambao wazazi wao walihitaji kabisa na namna gani wangewasaidia. Kisha, yule aliyekuwa akitumikia huko Amerika Kusini na bibi yake walianza kufikiria kuacha mugawo wao na kurudi nyumbani. Kisha, muratibu wa baraza la wazee wa kutaniko la wazazi wake alimuita kupitia telefone. Wazee walikuwa wamezungumuzia jambo hilo na walitaka wamisionere hao waendelee na mugawo wao. Wazee hao walipendezwa sana na kazi ya ndugu huyo na bibi yake na walikuwa tayari kufanya yote wanayoweza ili kuwasaidia kutunza wazazi wao. Wote katika jamaa walifurahia sana tendo hilo lenye upendo.

12. Tunapaswa kuhangaikia nini kwanza tunapochukua uamuzi kuhusu kuwatunza wazazi wenye kuzeeka?

12 Iwe tunachukua uamuzi gani ili kutunza wazazi wetu wenye kuzeeka, sisi wote tunapaswa kuhakikisha kwamba jina la Mungu halitalaumiwa. Hatupaswe hata kidogo kuwa kama viongozi wa dini wa wakati wa Yesu. (Mt. 15:3-6) Tunataka kuchukua uamuzi ambao utaletea Mungu na kutaniko sifa.​—2 Kor. 6:3.

DARAKA LA KUTANIKO

13, 14. Namna gani Maandiko yanatuonyesha kwamba makutaniko yanapaswa kuwatunza ndugu na dada wenye kuzeeka?

13 Si wote wanaoweza kusaidia watumishi wa wakati wote kama tulivyoona hapo juu. Lakini, hali fulani iliyotokea wakati wa mitume inaonyesha kwamba makutaniko yalihangaikia mahitaji ya ndugu na dada wenye kuzeeka waliokuwa mifano mizuri. Biblia inasema kwamba katika kutaniko la Yerusalemu ‘hapakuwa hata mumoja aliyekuwa na uhitaji kati yao.’ Hilo halimaanishe kwamba wote walikuwa matajiri. Wengine kati yao hawakuwa na vitu vingi, lakini ‘kila mumoja wao alikuwa akigawiwa kulingana na uhitaji wake.’ (Mdo. 4:34, 35) Baadaye hali fulani ilitokea. Iliripotiwa kwamba ‘wajane [fulani] walikuwa hawaangaliwe katika ugawaji wa kila siku’ wa chakula. Kwa hiyo, mitume walichagua wanaume fulani wenye kustahili, ambao wangefanya mipango ili mahitaji ya wajane hao yatimizwe sawasawa. (Mdo. 6:1-5) Bila shaka ugawaji huo wa kila siku ulikuwa mupango wa muda mufupi uliofanywa ili kutimiza mahitaji ya wale waliogeuka kuwa Wakristo kwenye Pentekoste ya mwaka wa 33 na ambao walibaki Yerusalemu kwa muda kidogo ili kujengwa kiroho. Hata hivyo, jambo ambalo mitume walifanya linaonyesha kwamba kutaniko linaweza kusaidia ndugu na dada walio katika uhitaji.

14 Kama tulivyoona, mutume Paulo alimutolea Timotheo maagizo yaliyoonyesha hali za wajane Wakristo ambao walistahili kusaidiwa na kutaniko. (1 Tim. 5:3-16) Yakobo, mwandikaji wa Biblia, alionyesha vilevile kwamba Mukristo ana daraka la kuwatunza mayatima, wajane, na wengine katika ziki zao. (Yak. 1:27; 2:15-17) Mutume Yohana pia alisema hivi: ‘Yeyote aliye na riziki ya ulimwengu huu naye amuone ndugu yake akiwa na uhitaji na bado amufungie mulango wa huruma zake nyororo, ni katika njia gani kumupenda Mungu kunakaa ndani yake?’ (1 Yoh. 3:17) Ikiwa kila Mukristo ana daraka la kusaidia wale walio katika uhitaji, je, kutaniko lote haliwezi pia kuwasaidia?

Ikiwa kunatokea aksidenti, kutaniko linaweza kusaidia namna gani? (Ona fungu la 15, 16)

15. Ni mambo gani tunayopaswa kufikiria tunapowasaidia ndugu na dada wenye kuzeeka?

15 Katika inchi fulani, serikali inatoa malipo ya uzee, inawatolea watu wenye kuzeeka dawa na matunzo, na inajenga nyumba za kuwatunzia watu wenye kuzeeka. (Rom. 13:6) Lakini, mambo hayako hivyo katika inchi zingine. Kwa hiyo, musaada ambao watu wa jamaa na kutaniko wanaweza kutoa kwa ajili ya ndugu na dada wenye kuzeeka unategemea hali. Ikiwa watoto ambao ni Wakristo wanaishi mbali na wazazi wao, hilo linaweza kuwa na matokeo fulani juu ya musaada ambao watoto hao wanaweza kutoa. Ni vizuri watoto wazungumuze waziwazi na wazee wa kutaniko la wazazi wao ili kila mutu aelewe hali za familia. Kwa mufano, wazee wa kutaniko wanaweza kuwaonyesha wazazi namna ya kufaidika na mipango ambayo serikali imefanya kwa ajili yao. Wazee wanaweza kutambua mambo fulani ambayo watoto hao wanapaswa kujulishwa, kama vile barua nyingi ambazo hazijafunguliwa ao dawa ambazo wazazi wamesahau kutumia. Kupashana habari vizuri kwa njia hiyo kunaweza kusaidia hali fulani ihangaikiwe mbele mambo yaharibike zaidi. Kwa kweli, ikiwa kuna mutu wa karibu anayesaidia na kuwatolea mashauri watu wa jamaa wanaoishi mbali na wazazi wao wenye kuzeeka, hilo linaweza kupunguzia familia wasiwasi.

16. Namna gani ndugu na dada fulani wanasaidia washiriki wa kutaniko wenye kuzeeka?

16 Kwa sababu wanawapenda ndugu na dada wenye kuzeeka, washiriki fulani katika makutaniko wametoa wakati na uwezo wao ili kuwatunza kadiri wanavyoweza. Wanajikaza kupendezwa sana na washiriki wa kutaniko wenye kuzeeka. Ndugu na dada wengine wa kutaniko wanajitolea kwa kupenda ili kufanya kazi mbalimbali katika kuwatunza ndugu na dada wenye kuzeeka, na wanafanya hivyo kwa kugomboana. Kwa kuwa wanatambua kwamba hali zao haziwaruhusu kufanya utumishi wa wakati wote, wanafurahia kuwasaidia watoto hao wabaki katika utumishi ambao wamechagua kadiri inavyowezekana. Ndugu na dada hao wanaonyesha roho nzuri kabisa. Lakini, ukarimu wao hauwaondolee watoto daraka la kufanya yote wanayoweza ili kusaidia wazazi wao.

TUWAHESHIMU KUPITIA MANENO YENYE KUTIA MOYO

17, 18. Tunapaswa kuwa watu wa namna gani tunapowatunza watu wenye kuzeeka?

17 Wote wanaowatunza ndugu na dada wenye kuzeeka wanapaswa kujikaza kufurahia kazi hiyo. Ikiwa una daraka hilo, fanya yako yote ili uendelee kufurahia daraka hilo. Wakati fulani, ndugu na dada wenye kuzeeka wanaweza kukata tamaa, na hata kuvunjika moyo. Kwa hiyo unahitaji kujikaza sana ili kuwaonyesha heshima na kuwatia moyo kwa kuendelea kuzungumuza nao mambo yenye kujenga. Ndugu na dada wenye kuzeeka ambao wamemutumikia Yehova kwa uaminifu wanastahili kupongezwa. Yehova hajasahau yale waliyofanya katika kazi yake, na sisi pia hatupaswe kusayahau.​—Soma Malaki 3:16; Waebrania 6:10.

18 Zaidi ya hayo, ili kazi ngumu ya kuwatunza kila siku isiwe yenye kuchokesha, ndugu na dada wenye kuzeeka na wale wanaowatunza wanapaswa kuwa wenye kuchekesha wakati fulani. (Mhu. 3:1, 4) Watu wengi wenye kuzeeka hawaombe mambo mengi. Wanajua kwamba hali yao inaweza kutufanya tufurahie kuwahangaikia na kuwatembelea. Kila mara tunasikia wale waliowatembelea wakisema hivi: “Nilienda kumutia moyo ndugu ao dada mwenye kuzeeka, lakini ni yeye aliyenitia moyo.”​—Met. 15:13; 17:22.

19. Sisi wote, vijana na wazee, tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu wakati ujao?

19 Tunangojea kwa hamu wakati mateso na matokeo ya kutokamilika yatakwisha. Kwa sasa, watumishi wa Mungu wanapaswa kuendelea kukaza akili zao juu ya uzima wa milele. Tunajua kwamba imani katika ahadi za Mungu ni nanga katika nyakati za taabu ao ziki. Kwa sababu ya imani hiyo, ‘hatufi moyo, lakini hata ikiwa mutu tuliye kwa inje anachakaa, hakika mutu tuliye kwa ndani anafanywa upya siku baada ya siku.’ (2 Kor. 4:16-18; Ebr. 6:18, 19) Lakini, zaidi ya kuendelea kuwa na imani yenye nguvu katika ahadi za Mungu, ni nini inaweza kutusaidia kutimiza vizuri daraka la kuwatunza wazazi wetu wenye kuzeeka? Habari inayofuata itatutolea mashauri mazuri kuhusu jambo hilo.

^ Habari inayofuata itazungumuzia njia mbalimbali za kuwatunza watu wenye kuzeeka.