Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwatunza Waliozeeka

Kuwatunza Waliozeeka

Watoto wadogo, acheni tupendane, si kwa neno wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.”1 YOH. 3:18.

1, 2. (a) Familia nyingi zinakabili matatizo gani, na ni maswali gani yanayozuka? (b) Wazazi na watoto wanawezaje kukabiliana na hali zinapobadilika?

UNAWEZA kuvunjika moyo sana ukiwaona wazazi wako waliokuwa na nguvu na uwezo wa kujitunza wakishindwa kufanya hivyo. Baadhi ya wazazi wameanguka na kuvunjika nyonga, kuvurugika akili na kupotea njia, au wamegunduliwa kuwa na ugonjwa mbaya sana. Na huenda waliozeeka wasikubali kwamba hawawezi kufanya mambo fulani sasa kwa sababu wamedhoofika kimwili au hali zao zimebadilika. (Ayu. 14:1) Mnaweza kufanya nini? Wanaweza kutunzwaje?

2 Makala fulani inayohusu kuwatunza waliozeeka inasema hivi: “Ingawa ni vigumu kuzungumzia matatizo ya waliozeeka, familia inayozungumzia hatua za kuchukua na kufanya mipango inayofaa itakabiliana na hali yoyote itakayotokea.” Tukikumbuka kwamba matatizo ya uzeeni hayaepukiki, tutaona umuhimu wa kuyazungumzia. Hata hivyo, tunaweza kufanya matayarisho na mipango fulani mapema. Acheni tuchunguze jinsi familia zinavyoweza kushirikiana kwa upendo ili kushughulikia baadhi ya matatizo hayo.

 KUPANGA KWA AJILI YA “SIKU ZENYE MSIBA”

3. Familia zinaweza kufanya nini ikiwa wazazi waliozeeka wanahitaji msaada zaidi? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

3 Wakati hufika ambapo watu wengi waliozeeka hushindwa kujitunza ifaavyo. Hivyo, wanahitaji msaada. (Soma Mhubiri 12:1-7.) Wazazi waliozeeka wanaposhindwa kujitunza, wanapaswa kuamua pamoja na watoto wao msaada bora wanaohitaji na kufanya mipango inayofaa. Kwa kawaida ni jambo la hekima kufanya mkutano wa familia ili kuzungumzia mahitaji, njia bora za kuwasaidia, na jinsi wote watakavyoshirikiana. Familia yote, hasa wazazi, wanapaswa kueleza waziwazi wanavyohisi na jinsi wanavyotaka hali hiyo ishughulikiwe. Familia inaweza kuzungumzia ikiwa itafaa wazazi kusaidiwa wakiwa nyumbani. * Au inaweza kuzungumzia jinsi kila mmoja anavyoweza kusaidia. (Met. 24:6) Kwa mfano, baadhi yao wanaweza kuwatunza wazazi hao kila siku huku wengine wakiwasaidia kifedha. Wote wanapaswa kutambua kwamba kila mtu ana jukumu la kutimiza; hata hivyo, huenda majukumu hayo yakabadilika kadiri wakati unavyopita na huenda wakafikiria kubadilishana majukumu.

4. Washiriki wa familia wanaweza kupata wapi msaada?

4 Unapoanza kuwatunza wazazi wako, jitahidi kujifunza mengi iwezekanavyo kuhusu hali yao. Ikiwa ana ugonjwa unaomdhoofisha hatua kwa hatua, fanya utafiti kuhusu athari za ugonjwa huo. (Met. 1:5) Wasiliana na mashirika ya serikali yanayowasaidia waliozeeka. Chunguza ikiwa kuna mipango ya kuwatunza waliozeeka inayoweza kuwasaidia kuwatunza wazazi wenu kwa njia bora na rahisi zaidi. Hali za familia zinapobadilika huenda ukashtuka, ukahuzunika, au kuvurugika. Mwambie rafiki unayemwamini jinsi unavyohisi. Zaidi ya yote, mmiminie Yehova hisia zako. Atakupa amani ya akili unayohitaji ili ukabiliane na hali yoyote.Zab. 55:22; Met. 24:10; Flp. 4:6, 7.

5. Kwa nini ni jambo la hekima kukusanya habari kabla ya kuamua jinsi ya kuwatunza waliozeeka?

5 Kwa hekima, baadhi ya waliozeeka na familia zao hukusanya habari mapema kabla ya kuamua ikiwa mzazi huyo anaweza kuishi na mwana au binti yake, kuishi katika makao ya waliozeeka, au kunufaika na mipango mingine. Wao huona “taabu na mambo yenye kuumiza” yanayoweza kutokea baadaye na kujitayarisha kukabiliana nayo. (Zab. 90:10) Familia nyingi hazifanyi mipango yoyote, hivyo tatizo linapotokea wanalazimika kufanya maamuzi mazito haraka-haraka. Mtaalamu mmoja anasema kwamba huo “ndio wakati mbaya zaidi wa kufanya maamuzi kama hayo.” Washiriki wa familia wanapolazimika kufanya maamuzi haraka-haraka wakiwa na wasiwasi, huenda wasikubaliane. Hata hivyo, familia inaweza kukabiliana kwa urahisi zaidi na mabadiliko ikijitayarisha mapema.Met. 20:18.

Familia inaweza kukutana ili kuzungumzia jinsi ya kumsaidia mzazi aliyezeeka(Tazama fungu la 6-8)

6. Wazazi na watoto watanufaika jinsi gani wakizungumza kuhusu mipango ya makao?

6 Huenda ikawa vigumu kuzungumza na wazazi wenu kuhusu makao na uhitaji wa kuhama. Hata hivyo, wengi wamesema kwamba mazungumzo hayo yaliwanufaisha baadaye. Kwa nini? Kwa sababu walipanga mambo kwa njia ya upendo na kwa uelewaji. Waligundua kwamba ilikuwa rahisi zaidi kufanya maamuzi baadaye kwa sababu walizungumzia masuala hayo mapema kwa upendo na fadhili. Hata ikiwa waliozeeka wanataka kuishi peke yao na kujitunza, bila shaka watanufaika wakiwaambia watoto wao msaada ambao wangependa uhitaji unapotokea.

7, 8. Ni mambo gani ambayo familia zinapaswa kuzungumzia, na kwa nini?

7 Wazazi, julisheni familia yenu kuhusu  hali yenu ya kifedha na mambo ambayo mngependelea. Kufanya hivyo kutaisaidia familia kufanya maamuzi yanayofaa mnapohitaji msaada. Inaelekea kwamba wataheshimu maamuzi yenu na hawataingilia uhuru wenu. (Efe. 6:2-4) Kwa mfano, je, unatarajia kwenda kuishi na mtoto wako mwenye familia, au unatarajia jambo tofauti? Tazama mambo kihalisi na utambue kwamba huenda washiriki wengine wa familia wana maoni tofauti kuhusu jinsi ya kukutunza. Hivyo, mtahitaji wakati ili kuzungumza na kufikia uamuzi.

8 Wote wanapaswa kutambua kwamba matatizo yanaweza kuepukwa wakizungumza na kufanya mipango. (Met. 15:22) Hilo linatia ndani kuzungumza kuhusu matibabu mnayopenda. Bila shaka, mnapaswa kuzungumzia mambo yaliyo katika kadi ya Uwakilishi wa Kitiba au Hati ya Kitiba ambayo Mashahidi wa Yehova hubeba. Kila mtu ana haki ya kujulishwa kuhusu matibabu atakayopewa, na kisha kuamua kuyakubali au kuyakataa. Kadi hiyo ya kitiba inaonyesha matibabu ambayo mtu angependa. Kumchagua mwakilishi wa kitiba (ikiwa sheria ya nchi inaruhusu) kunaweza kuhakikisha kwamba mtu anayetegemeka atafanya maamuzi yanayofaa inapohitajika. Wale wanaohusika wanapaswa kuwa na nakala za hati zinazofaa ili wazitumie zinapohitajika. Baadhi ya watu huweka nakala hizo pamoja na wosia wao, hati nyingine muhimu za bima, fedha, nambari za kuwasiliana na ofisi za serikali, na hati nyinginezo.

KUKABILIANA NA HALI ZINAZOBADILIKA

9, 10. Ni mabadiliko gani yanayoweza kuwasaidia kujua msaada ambao mtu aliyezeeka anahitaji?

9 Katika visa vingi, washiriki wa familia huwapa waliozeeka uhuru mwingi iwezekanavyo ikitegemea hali yao. Labda wanaweza kupika, kufanya usafi, kutumia dawa kulingana na maagizo ya daktari, na kuwasiliana bila matatizo. Hivyo, watoto hawahitaji kujihusisha sana na maisha yao ya kila siku. Hata hivyo, kadiri wakati unavyopita, wazazi hushindwa kutembea, kwenda dukani, au huanza kusahau-sahau mambo, hivyo huenda watoto wakahitaji kuwasaidia.

10 Huenda mtu aliyezeeka akavurugika kiakili, akashuka moyo, akashindwa kuzuia mkojo, akapoteza uwezo wa kusikia, kuona, na kukumbuka mambo; hata hivyo, baadhi ya magonjwa hayo yanaweza kutibiwa. Mnapoona dalili za tatizo lolote, tafuteni matibabu haraka. Watoto wanaweza kuchukua hatua ya kutafuta matibabu. Baada ya muda, huenda wakaanza kuwasaidia wazazi katika shughuli zao za kibinafsi. Ili kuwatunza wazazi ifaavyo, huenda watoto wakalazimika kuzungumza kwa niaba yao, kuwasaidia kuandika barua, kuwapeleka wanakohitaji kwenda, na kufanya mambo mengine.Met. 3:27.

11. Mnaweza kufanya nini ili kuwasaidia wazazi kukabiliana na mabadiliko?

 11 Ikiwa matatizo ya wazazi wenu hayawezi kusuluhishwa, huenda mkahitaji kubadili mipango ya kuwatunza au ya makao yao. Inaelekea kwamba ni rahisi zaidi kufanya marekebisho ikiwa matatizo si makubwa. Ikiwa mnaishi mbali na wazazi wenu, je, Shahidi mwenzenu au jirani anaweza kuwatembelea wazazi wenu mara kwa mara na kuwajulisha hali yao? Je, wazazi wanahitaji kusaidiwa kufanya usafi na kupika? Je, mnaweza kubadili mpangilio wa nyumba ili wasiumie wanapotembea nyumbani, wanapooga, na kufanya mambo mengine? Huenda wazazi waliozeeka wanahitaji tu mtu wa kuwasaidia nyumbani ili wawe na kiasi fulani cha uhuru. Hata hivyo, ikiwa si salama kwao kuishi peke yao, huenda wakahitaji msaada wa kudumu. Kwa vyovyote vile, tafuteni huduma kwa ajili ya waliozeeka zinazopatikana kwenu. *Soma Methali 21:5.

JINSI WENGINE WANAVYOKABILIANA NA CHANGAMOTO

12, 13. Watu wanaoishi mbali na wazazi wao wameendeleaje kuwaheshimu na kuwatunza?

12 Watoto wenye upendo watahakikisha kwamba wazazi wao wanaishi vizuri. Watakuwa na amani ya akili wakijua kwamba wazazi wao wanatunzwa. Hata hivyo, watu wengi hawaishi karibu na wazazi wao kwa sababu wana majukumu mengine. Chini ya hali hizo, wengine hutumia likizo yao kuwatembelea wazazi wao na kuwasaidia kazi ambazo hawawezi kufanya. Kuwapigia wazazi simu kwa ukawaida, na hata kila siku ikiwezekana, kuwaandikia—barua au barua-pepe huwahakikishia kwamba wanapendwa.Met. 23:24, 25.

13 Hata hali iweje, unapaswa kuchunguza jinsi wazazi wako wanavyotunzwa kila siku. Ikiwa unaishi mbali na wazazi wako ambao ni Mashahidi, unaweza kuzungumza na wazee wa kutaniko lao na kuwaomba mashauri. Na usikose kusali kuhusu jambo hilo. (Soma Methali 11:14.) Hata ikiwa wazazi wako si Mashahidi, unapaswa ‘kumheshimu baba yako na mama yako.’ (Kut. 20:12; Met. 23:22) Bila shaka, familia zote hazitafanya maamuzi yanayofanana. Baadhi ya familia hupanga ili mzazi aliyezeeka aje kuishi nao au karibu nao. Hata hivyo, nyakati nyingine jambo hilo haliwezekani. Wazazi fulani hawapendi kuishi na familia za watoto wao ambao ni watu wazima; wanathamini uhuru wao na hawataki kuwa mzigo kwao. Huenda wengine wakamlipa mtu fulani ili awatunze wazazi wanaoishi peke yao.Mhu. 7:12.

14. Wale wanaotumia wakati mwingi kuwatunza waliozeeka wanaweza kukabili matatizo gani?

14 Katika familia nyingi, inaonekana kwamba yule anayeachiwa jukumu la kuwatunza wazazi ni mwana au binti anayeishi karibu nao. Hata hivyo, wale walio na daraka kuu la kuwatunza wazazi wanapaswa kuwa na usawaziko wanapotosheleza mahitaji ya wazazi na ya familia zao wenyewe. Huwezi kupata wakati na nguvu za kutimiza kila jambo. Huenda maisha ya anayewatunza wazazi yakabadilika, na hivyo familia ikalazimika kufanya mipango mingine. Je, labda mshiriki mmoja wa familia ameachiwa majukumu mengi mno? Je, wengine katika familia wanaweza kufanya mengi zaidi, kama vile kuwatunza wazazi kwa zamu?

15. Wanaowatunza waliozeeka wanawezaje kusaidiwa ili wasichoke?

15 Mzazi aliyezeeka anapohitaji kutunzwa  daima, yule anayemtunza anaweza kuchoka. (Mhu. 4:6) Watoto wenye upendo wanahitaji kujitahidi kadiri wawezavyo kuwatunza wazazi wao, lakini huenda wakalemewa na majukumu hayo. Wale wanaokabili hali hizo wanahitaji kuona mambo kihalisi na labda kuomba msaada. Huenda wakahitaji kusaidiwa mara kwa mara na hilo litawazuia kufanya uamuzi wa haraka wa kuwapeleka wazazi wao katika makao ya kuwatunzia waliozeeka.

16, 17. Ni matatizo gani ambayo huenda watoto wakakabili wanapowatunza wazazi waliozeeka? Wanawezaje kukabiliana nayo? (Tazama pia sanduku lenye kichwa “Watunze na Kuwathamini.”)

16 Inavunja moyo kuwaona wazazi wapendwa wakiteseka kwa sababu ya uzee. Pindi fulani, watu wengi wanaowatunza waliozeeka wanahuzunika, wanahangaika, wanakata tamaa, wanakasirika, wanajilaumu, na hata kuwa na uchungu moyoni. Nyakati nyingine, huenda mzazi aliyezeeka akasema maneno yenye kuumiza au akakosa uthamini. Ukitendewa hivyo, usiwe mwepesi kukasirika. Mtaalamu mmoja wa magonjwa ya akili anasema hivi: “Njia bora ya kukabiliana na hisia, hasa zisizofaa, ni kukubali ukweli wa mambo. Usipuuze hisia hizo au kujilaumu kupita kiasi kwa sababu ya kuhisi hivyo.” Zungumza na mwenzi wako wa ndoa, mshiriki mwingine wa familia, au rafiki unayemwamini kuhusu unavyohisi. Mazungumzo kama hayo yanaweza kukusaidia kuelewa hisia zako na kuwa na usawaziko.

17 Huenda familia ikakosa fedha au uwezo wa kuendelea kumtunza mpendwa wao akiwa nyumbani. Huenda ikahitaji kumpeleka katika makao ya kuwatunzia waliozeeka. Dada mmoja Mkristo alimtembelea mama yake katika makao hayo karibu kila siku. Anasema hivi kuhusu familia yake: “Hatungeweza kamwe kumtunza Mama kwa saa 24. Haikuwa rahisi kufikia uamuzi wa kumpeleka katika makao ya kuwatunzia waliozeeka. Tuliumia sana kihisia. Hata hivyo, ulikuwa uamuzi bora zaidi katika miezi ya mwisho ya maisha yake, na alikubali uamuzi huo.”

18. Wale wanaowatunza waliozeeka wanaweza kuwa na uhakika gani?

18 Wajibu wa kuwatunza wazazi wako wanapozeeka unaweza kuwa mgumu na kukulemea kihisia. Hakuna njia hususa ya kuwatunza waliozeeka. Hata hivyo, mkifanya mipango kwa hekima, mkishirikiana kwa upendo, mkiwasiliana vizuri, na zaidi ya yote, mkisali kutoka moyoni, mnaweza kutimiza wajibu wa kuwaheshimu wapendwa wenu. Mkifanya hivyo, mtakuwa na uradhi kwa sababu mnajua kwamba mnawapa msaada na uangalifu wanaohitaji. (Soma 1 Wakorintho 13:4-8.) Na zaidi ya yote, mnaweza kuwa na uhakika kwamba mtafurahia amani ya akili ambayo Yehova huwapa wale wanaowaheshimu wazazi wao.Flp. 4:7.

^ fu. 3 Wazazi na watoto wanaweza kuamua jambo la kufanya ikitegemea hali za kwao. Katika nchi nyingine, ni kawaida kwa washiriki wa familia wa vizazi mbalimbali kuishi pamoja au kuwasiliana kwa ukawaida.

^ fu. 11 Ikiwa wazazi waliozeeka wanaishi peke yao, hakikisheni kwamba watunzaji wanaotegemeka wana funguo zitakazowawezesha kuingia katika nyumba yao hali ya dharura ikitokea.