Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Namna ya Kuwatunza Watu Wenye Kuzeeka

Namna ya Kuwatunza Watu Wenye Kuzeeka

“Watoto wadogo, acheni tupendane, si kwa neno wala ulimi, bali kwa tendo na kweli.”​—1 YOH 3:18.

1, 2. (a) Familia nyingi zinapambana na matatizo gani na hilo linatokeza maulizo gani? (b) Wazazi na watoto wanaweza kufanya nini ili kupambana na mabadiliko ya uzee?

 NI JAMBO lenye kuumiza kutambua kwamba wazazi wetu, ambao zamani walikuwa wenye nguvu na wenye kujitunza, hawawezi tena kufanya hivyo. Pengine Mama ao Baba ameanguka na kuvunjika kiuno, amevurugika akili na kupotea, ao amepatikana na ugonjwa hatari. Kwa upande mwengine, watu wenye kuzeeka wanaweza kushindwa kuelewa mabadiliko ya afya yao ao hali zingine zinazowafanya washindwe kujifanyia mengi. (Ayu. 14:1) Tunaweza kufanya nini? Wanapaswa kutunzwa namna gani?

2 Gazeti moja linalozungumuzia namna ya kuwatunza watu wenye kuzeeka linasema hivi: “Hata ikiwa ni vigumu kuzungumuzia matatizo ya uzee, familia ambayo imezungumuza na kukubaliana kuhusu mipango itakayofanywa, itahangaikia vizuri hali yoyote inayoweza kutokea.” Ni vizuri sana kuzungumuzia mambo hayo mbele ya wakati kwa sababu matatizo ya uzee hayawezi kuepukwa. Lakini, tunaweza kufanya mipango na kuchukua maamuzi fulani mbele ya wakati. Tuzungumuzie basi namna familia zinaweza kuchukua mipango pamoja ili kupambana na matatizo ya kuwatunza watu wenye kuzeeka.

TUFANYE MIPANGO KWA AJILI YA SIKU ZA TAABU

3. Washiriki wa familia wanaweza kufanya nini wakati wazazi wao wenye kuzeeka wanahitaji musaada zaidi? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.)

3 Kuna wakati ambao watu wengi wenye kuzeeka hawawezi tena kujitunza kabisa. Wakati huo, wanahitaji kusaidiwa. (Soma Mhubiri 12:1-7.) Wakati wazazi wenye kuzeeka hawawezi tena kujitunza, wao na watoto wao wanapaswa kuangalia ni musaada gani utakaohitajiwa kabisa na mambo ambayo wanaweza kufanya. Kwa kawaida, ni jambo la hekima kufanya mukutano wa jamaa ili kuzungumuzia ni musaada gani unaohitajiwa, utatolewa namna gani, na kila mutu anaweza kusaidia namna gani. Wote, zaidi sana wazazi, wanapaswa kujieleza na kuzungumuzia mambo waziwazi. Wanaweza kuangalia ikiwa wazazi wanaweza kupewa musaada kidogo ili waendelee kuishi nyumbani kwao. * Ao wanaweza kuzungumuzia jambo ambalo kila mutu anaweza kufanya ili wazazi wapate mahitaji yao. (Met. 24:6) Kwa mufano, wamoja wanaweza kuwatunza kila siku na wengine wanaweza kuwasaidia kulipa garama zao. Kila mutu anapaswa kujua daraka lake, lakini kadiri wakati unavyopita, daraka hilo linaweza kubadilika na washiriki wa familia wanaweza kugomboana ili kusaidiana kuwatunza.

4. Washiriki wa familia wanaweza kutafuta musaada wapi?

4 Unapoanza kumutunza muzazi wako, jikaze kadiri inavyowezekana kujua hali yake. Ikiwa anasumbuliwa na ugonjwa utakaofanya afya yake iendelee kuwa mbaya zaidi, tafuta kujua kutatokea nini baadaye. (Met. 1:5) Zungumuza na mashirika ya serikali yanayowatunza wazee. Tafuta misaada ya kijamii inayopatikana katika eneo lako ili kurahisisha kazi yako ya kusaidia atunzwe vizuri. Unapofikiria mabadiliko yatakayotokea katika familia, unaweza kuanza kuwa na huzuni, maumivu ya moyoni, ao hata kuchanganyikiwa akili. Muelezee rafiki unayetumainia namna unavyojisikia. Zaidi sana, muelezee Yehova mambo yaliyo katika moyo wako. Anaweza kukusaidia upate amani ya akili unayohitaji ili kupambana na hali yoyote.​—Zab. 55:22; Met. 24:10; Flp. 4:6, 7.

5. Sababu gani ni jambo la hekima kujifunza mbele ya wakati kuhusu namna mbalimbali za kuwatunza watu wenye kuzeeka?

5 Ni jambo la hekima watu wenye kuzeeka na jamaa zao wajifunze mbele ya wakati kuhusu namna mbalimbali za kuwatunza wazazi wao wenye kuzeeka. Kwa mufano, wanaweza kuona ikiwa itawezekana muzazi aende kuishi kwa mutoto wake mwanaume ao mwanamuke, ao kufaidika na mipango mingine inayofanywa katika eneo lenu. Kwa kufanya hivyo, watakuwa wameona ‘taabu na mambo yenye kuumiza’ mbele ya wakati na kujitayarisha ili kupambana nayo. (Zab. 90:10) Lakini, familia nyingi hazifanye mipango fulani, na hivyo zinalazimika kuchukua maamuzi mazito haraka-haraka wakati mambo yanaharibika. Mushauri mumoja alisema kwamba huo “ndio wakati mubaya zaidi wa kuchukua uamuzi huo.” Katika hali hiyo inayoomba kutenda haraka, washiriki wa familia wanakuwa katika wasiwasi, na mabishano yanaweza kutokea. Lakini, ikiwa tunapanga mambo mbele ya wakati, tutapambana vizuri na mabadiliko ya wakati ujao.​—Met. 20:18.

Jamaa inaweza kukutana pamoja ili kuzungumuzia namna ya kumutunza muzazi mwenye kuzeeka (Ona fungu la 6-8)

6. Kuzungumuza mbele ya wakati kuhusu mahali na namna wazazi wataishi watakapozeeka kuna faida gani?

6 Inaweza kuwa vigumu kuzungumuza na wazazi wako kuhusu mahali ambapo wataishi na namna gani wataishi watakapozeeka. Lakini, wengi wamesema kwamba mazungumuzo hayo yaliwasaidia sana baadaye. Sababu gani? Kwa sababu yaliwatolea nafasi ya kufanya mipango mbele ya wakati, kuzungumuzia matatizo, na kusikiliza maoni ya wengine katika hali ya kirafiki. Walitambua kwamba, mazungumuzo hayo yanayofanywa mbele ya wakati, katika roho ya upendo na utulivu, yalifanya iwe rahisi kuchukua maamuzi. Hata wakati ambapo watu wenye kuzeeka wanapenda waendelee kuishi pekee yao na kujitunza, ni jambo lenye faida wazungumuze pamoja na watoto kuhusu namna ambavyo wangependa kutunzwa wakati hawataweza tena kujitunza.

7, 8. Ni mambo gani ambayo familia zinapaswa kuzungumuzia, na sababu gani?

7 Wakati wa mazungumuzo hayo, wazazi, munapaswa kujulisha watu wa jamaa mahitaji yenu, feza mulizo nazo, na namna munapenda mutunzwe. Hilo litasaidia watu wa jamaa kufanya maamuzi ambayo mutafurahia siku ambayo hamutakuwa na uwezo wa kujifanyia maamuzi. Watapenda kuheshimu mipango yenu na kufanya yote wanayoweza ili muendelee kujitunza kadiri inavyowezekana. (Efe. 6:2-4) Kwa mufano, je, unapenda uende kuishi kwa mutoto wako, ao unataka jambo lingine? Ona mambo kwa njia inayofaa na ujue kwamba washiriki wengine wa jamaa wana maoni tofauti na yako, na inaomba wakati ili muzazi ao mutoto abadili maoni yake.

8 Ni vizuri wote wajue kwamba inawezekana kuepuka matatizo mengi ikiwa watu wanazungumuza na kupanga mambo mbele ya wakati. (Met. 15:22) Elezea watu wa jamaa yako kuhusu matunzo ya kiganga ambayo unafurahia. Munapaswa kuzungumuzia pia habari zilizo kwenye kadi ya kiganga ya DPA (Instructions Médicales, Pas de Sang) ambayo Mashahidi wa Yehova wanatumia. Kila mutu anapaswa kujua aina ya matunzo yanayopatikana, na ana haki ya kuikubali ao kuikataa. Kuna kikaratasi cha kiganga kinachoonyesha namna unavyotaka utunzwe. Kuchagua mutu atakayekutetea kuhusiana na matunzo (ikiwa serikali ya kwenu inaruhusu) kutafanya mutu unayetumainia achukue maamuzi yanayofaa kwa ajili yako wakati itahitajiwa. Wale wanaokutunza na wale watakaokutetea wanapaswa kuwa na kopi ya vikaratasi hivyo ili wavitumie vinapohitajiwa. Wengine wanaweka kopi za vikaratasi hivyo pamoja na testama zao na vikaratasi vyao vya maana kama vile vinavyohusu bima ao asiranse, akaunti zao za benki, feza, vikaratasi vya serikali, na mambo mengine.

NAMNA YA KUPAMBANA NA MABADILIKO

9, 10. Ni mabadiliko gani yanayoweza kutusaidia tujue musaada ambao muzazi mwenye kuzeeka anahitaji?

9 Mara nyingi, wote katika familia wanapenda wazazi wao wenye kuzeeka wasitegemee jamaa katika kila jambo. Pengine wangali na uwezo wa kujipikia chakula, kujifulia na kusafisha nyumba, kutumia dawa, na kuzungumuza bila matatizo. Kwa hiyo, wanaweza kuwaambia watoto wao wawaache wajifanyie mambo mengine. Lakini, ikiwa wakati fulani wazazi wanaanza kushindwa kutembea, kujinunulia vitu, ao wanaanza kusahau​-sahau, ni lazima watoto waone namna gani watawasaidia.

10 Watu wenye kuzeeka wanaweza kuchanganyikiwa akili, kushuka moyo, kushindwa kuzuia mukojo, kutosikia vizuri, kutoona vizuri, na kuwa wenye kusahau​-sahau. Ikiwa matatizo hayo ya afya yanatokea, waganga wanaweza kusaidia. Muonane na muganga wakati tu matatizo kama hayo yanatokea. Watoto wanapaswa kuchukua mipango ili wazazi wao waonane na muganga. Wakati fulani, wanaweza pia kuanza kuchukua maamuzi kuhusu mambo ambayo wazazi walisimamia hapo zamani. Ili kuhakikisha kwamba wazazi wao wanatunzwa vizuri, watoto wanaweza kuwatetea, kuwasaidia kuandika mambo yao, kuwapeleka kwa muganga, na mambo mengine.​—Met. 3:27.

11. Ni lazima kufanya nini ili iwe rahisi kwa wazazi kuzoea mabadiliko?

11 Ikiwa wazazi wana matatizo ya afya yenye kuendelea, munaweza kujaribu matunzo mengine ao kutengeneza mahali wanapoishi. Ikiwa mabadiliko ni machache, basi watayazoea kwa urahisi. Ikiwa unaishi mbali na wazazi wako, je, inatosha ndugu ao jirani mumoja aliye karibu nao awatembelee kwa ukawaida na kukujulisha ikiwa wako katika hali gani? Je, wanahitaji tu mutu wa kuwasaidia kupika chakula na kufanya usafi? Je, unahitaji kufanya mabadiliko madogo katika nyumba yao ili waweze kutembea ndani, kuoga, na kufanya mambo mengine kwa urahisi na bila kujiumiza? Pengine wanahitaji tu mufanyakazi wa kuwasaidia ili waendelee kuishi katika nyumba yao. Hata hivyo, ikiwa kuna hatari kama wanaishi pekee yao, musaada mwingine wa kawaida utahitajiwa. Iwe hali iko namna gani, tafuta kujua mipango ya kusaidia watu wenye kuzeeka inayopatikana kwenu. *​—Soma Methali 21:5.

WENGINE WANAFANYA NAMNA GANI?

12, 13. Namna gani watoto wanaoishi mbali na wazazi wao wameendelea kuwaheshimu wazazi wao?

12 Watoto wenye upendo wanataka wazazi wao waishi vizuri. Kujua kwamba wazazi wao wanatunzwa vizuri kunawasaidia wawe na amani ya akili. Lakini, kwa sababu ya madaraka mbalimbali, watoto wengi hawaishi karibu na wazazi wao. Katika hali hizo, wengine wametumia mapumziko yao ili kuwatembelea wazazi wao na kuwasaidia katika kazi fulani ambazo hawana tena uwezo wa kufanya. Watoto wanaweza kuonyesha kwamba wanawapenda wazazi wao kwa kuzungumuza nao kwenye telefone, kila siku ikiwezekana, ao kwa kuwaandikia barua.​—Met. 23:24, 25.

13 Hata ikiwa unaishi mbali ao karibu na wazazi wako, lazima uamue namna wazazi wako watatunzwa kila siku. Ikiwa hauko karibu na wazazi wako na ikiwa wao ni Mashahidi, unaweza kuomba mashauri kwa wazee walio katika kutaniko lao. Na usikose kusali kuhusu jambo hilo. (Soma Methali 11:14.) Unapaswa ‘kuheshimu baba yako na mama yako’ hata ikiwa wao si Mashahidi. (Kut. 20:12; Met. 23:22) Bila shaka, kila familia inaamua namna itakavyowatunza wazazi wao. Wengine wanafanya mipango ili muzazi aende kuishi kwao ao karibu nao. Lakini, kila mara hilo haliwezekane. Wazazi fulani hawapendelee kuishi pamoja na watoto wao na jamaa zao; wanapenda wajitegemee na hawataki kuwa muzigo. Wengine wana uwezo, na wanapendelea kulipa mutu wa kuwatunza wakiwa nyumbani kwao.​—Mhu. 7:12.

14. Wale wanaotunza wazazi wanaweza kupambana na matatizo gani?

14 Katika familia nyingi, ni mutoto mumoja ndiye anayewatunza wazazi, zaidi sana yule anayeishi karibu nao. Hata hivyo, wale wanaotunza wazazi wao wanapaswa kuwa na usawaziko, wanapaswa kuhangaikia mahitaji ya wazazi bila kuzarau mahitaji ya familia zao wenyewe. Mutu hana uwezo wa kutimiza mambo yote. Na ikiwa hali ya yule anayewatunza wazazi inabadilika, familia inaweza kufanya mabadiliko fulani. Je, kuna mushiriki wa familia ambaye tumeachia mambo mengi sana? Je, watoto wengine wanaweza kufanya mengi zaidi, kama vile kugomboana katika kuwatunza wazazi?

15. Ni jambo gani linaloweza kusaidia mutu anayetunza watu wenye kuzeeka, asichoke?

15 Wakati muzazi mwenye kuzeeka anahitaji kusaidiwa kila wakati, hilo linaweza kumuchokesha yule anayemutunza. (Mhu. 4:6) Watoto wenye upendo wanataka kufanya yote wanayoweza ili kuwatunza wazazi wao, lakini hilo linaweza kuwalemea. Wale wanaojikuta katika hali kama hiyo wanapaswa kuielewa vizuri, na wanaweza kuomba musaada. Ikiwa tu wengine wanasaidia mara kwa mara, hilo linaweza kufanya iwe rahisi kwa yule anayemuchunga aendelee kumutunzia nyumbani.

16, 17. Watoto wanaweza kujisikia namna gani wanapowatunza wazazi wao wenye kuzeeka, na wanaweza kufanya nini katika hali hiyo? (Ona pia kisanduku “Wanafurahia Kuwatunza Wazazi Wao.”)

16 Inahuzunisha sana kuona muzazi mupendwa akiteseka kwa sababu ya matatizo ya uzee. Wengi wanaotunza watu wenye kuzeeka wanakuwa wenye huzuni, wasiwasi, hasira, kinyongo, wanavunjika moyo, na kufikiri kwamba kosa ni lao. Wakati fulani, muzazi mwenye kuzeeka anaweza kusema maneno yenye kuumiza ao anaweza kukosa shukrani. Ikiwa hali hiyo inatokea, usikasirike haraka. Muganga mumoja wa magonjwa ya akili alisema hivi: “Njia nzuri zaidi ya kupambana na jambo fulani, zaidi sana lile linalokuumiza, ni kulikubali. Usifanye kama hakuna jambo linalokuumiza ao kujilaumu vikali kwa sababu unajisikia hivyo.” Muelezee bwana ao bibi yako, mutu mwingine wa jamaa, ao rafiki unayemutumainia kuhusu namna unavyojisikia. Mazungumuzo hayo yanaweza kukusaidia utulizane.

17 Kuna wakati familia inaweza kushindwa kuendelea kumuchungia muzazi wao nyumbani. Familia inaweza kuamua kumupeleka kwenye nyumba ya kuwatunzia wazee. Dada mumoja alimutembelea karibu kila siku mama yake aliyekuwa katika nyumba ya kuwatunzia wazee. Anasema hivi kuhusu familia yake: “Hatungeweza kabisa kumutolea Mama matunzo aliyohitaji kila siku. Haikuwa rahisi kwake kukubali kuenda kuishi katika nyumba ya kuwatunzia wazee. Huo ulikuwa uamuzi muzito kabisa. Lakini, uamuzi huo ulimusaidia sana katika miezi ya mwisho​-mwisho ya maisha yake, na alifikia kuelewa hivyo.”

18. Wale wanaowatunza wazazi wao wanaweza kuwa hakika na jambo gani?

18 Kuwatunza wazazi wenye kuzeeka ni daraka ngumu na lenye kuchokesha akili. Hakuna maagizo kamili kuhusu kuwatunza wazazi wenye kuzeeka yanayopatana na kila hali. Lakini, kufanya mipango mbele ya wakati, kusaidiana, kuzungumuza waziwazi, na zaidi sana sala, yote hayo yanaweza kukusaidia utimize vizuri madaraka ya kuwaheshimu wazazi wako wapendwa. Kwa kufanya hivyo, unaweza kuwa mwenye furaha kwa sababu unajua kwamba wazazi wako wanatunzwa na kuhangaikiwa vizuri. (Soma 1 Wakorintho 13:4-8.) Zaidi ya yote, uwe hakika kwamba utakuwa na amani ya akili ambayo Yehova anatolea wale wanaoheshimu wazazi wao.​—Flp. 4:7.

^ Mapendezi ya wazazi na watoto yanategemea hali za kwao. Katika maeneo fulani, washiriki mbalimbali wa jamaa wanapendelea kuishi pamoja, na wana uhusiano wa karibu sana.

^ Ikiwa muzazi wako angali anaishi nyumbani, hakikisha kwamba wale wanaomutunza wana funguo ili waweze kumusaidia ikiwa kunatokea tatizo linaloomba kutenda haraka.