Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Thomas Emlyn—Aliasi ao Alitetea Kweli?

Thomas Emlyn—Aliasi ao Alitetea Kweli?

THOMAS Emlyn alikuwa nani, na ni nini iliyomuchochea atetee kweli? Mufano wake unaweza kutufundisha mambo gani yanayoweza kutusaidia leo?

Ili kujibu maulizo hayo, ni lazima tukumbuke mambo yaliyotokea kati ya mwaka wa 1701 na 1900 katika inchi ya Uingereza na Irlande. Kanisa la Irlande lilikuwa na mamlaka kubwa wakati huo. Watu fulani pamoja na vikundi mbalimbali vya Kiprotestanti walikuwa wanapinga kanisa.

THOMAS EMLYN ALIKUWA NANI?

Thomas Emlyn alizaliwa tarehe 27 Mwezi wa 5, 1663 katika muji wa Stamford, Lincolnshire, inchi ya Uingereza, wakati watu walikuwa wanapinga kanisa. Alipokuwa na miaka 19, alifanya mahubiri yake ya kwanza. Kisha, alikuwa muchungaji katika kanisa la mwanamuke mumoja mwenye cheo aliyeishi Londres; na baadaye, alihamia katika muji wa Belfast, Irlande.

Kisha siku kupita, Emlyn alisoma misa katika kanisa la parokia la muji wa Belfast. Kisha, alitumika akiwa muchungaji mahali mbalimbali, na pia Dublin.

SABABU GANI ALISHITAKIWA KUWA ALIASI?

Wakati huo, Emlyn alikuwa anajifunza Biblia kwa uangalifu. Mambo aliyojifunza yalimufanya awe na mashaka juu ya fundisho la Utatu, hata ikiwa mbele ya hapo alikuwa analiamini. Wakati alitafuta habari katika vitabu vya Injili alipata uhakika kwamba vitabu hivyo viliunga mukono mambo mapya aliyokuwa ameelewa.

Emlyn hakueleza mara moja mambo aliyopata. Hata hivyo, watu fulani katika kanisa lake lililokuwa katika muji wa Dublin walitambua kwamba hakuzungumuzia tena Utatu katika mahubiri yake. Kwa sababu alijua kwamba watu wengine hawangekubali mambo aliyovumbua, aliandika hivi: “Sitazamie kuendelea hapa katika cheo changu cha sasa, kama nilivyosema hapo mbele.” Katika Mwezi wa 6, 1702, wenzake wawili walibishana naye kwamba ameondoa Utatu katika mahubiri yake. Emlyn alieleza waziwazi kwamba haamini tena Utatu na akaamua kuacha cheo chake katika kanisa.

Kitabu cha Emlyn kilichohakikisha kupitia Maandiko sababu gani Yesu hawezi kuwa Mungu Mukubwa Zaidi

Kisha siku chache, alitoka katika muji wa Dublin, Irlande, na kuhamia katika inchi ya Uingereza. Hata hivyo, kisha majuma kumi alirudi tena Dublin ili kushugulikia mambo fulani, akiwa na kusudi la kuhamia Londres na kubakia huko maisha yake yote. Akiwa huko, alichapisha kitabu kimoja (An Humble Inquiry Into the Scripture-Account of Jesus Christ), akitumaini kwamba atatetea mawazo yake ili yakubaliwe. Katika kitabu hicho, alihakikisha kupitia Maandiko sababu gani Yesu hawezi kuwa ndiye Mungu Mukubwa Zaidi. Hilo liliwakasirisha washiriki wa dini yake ya zamani katika muji wa Dublin. Kwa hiyo, walimushitaki waziwazi.

Emlyn alifungwa na akapelekwa kwenye Mahakama ao Tribinali ya Malkia katika muji wa Dublin tarehe 14 Mwezi wa 6, 1703. Katika kitabu chake kimoja, Emlyn anasema kwamba alishitakiwa kwa “kuandika na kuchapisha kitabu kinachosema, nilitumia maneno ya uasi na maovu, na mambo mengine. Kwamba Yesu Kristo hakuwa sawa na Mungu Baba.” (True Narrative of the Proceedings) Masambo yalifanyika kama muchezo. Maaskofu saba wa kanisa la Irlande walikaa pamoja na waamuzi ili kumusambisha Emlyn. Lakini Emlyn hakuruhusiwa kusema ili kujitetea. Richard Levins, mwanasheria mwenye kuheshimiwa, alimuambia Emlyn kwamba atawindwa kabisa “kama imbwa wa pori bila sheria wala muchezo.” Wakati walimaliza kusamba, Richard Pyne, Musimamizi Mukubwa wa Mahakama ya Irlande, aliambia baraza la mahakama hiyo kwamba ikiwa hawangekuja kusikiliza hukumu yenye walikuwa wanangojea, “mabwana zao maaskofu walikuwa hapo,” pengine alisema hivyo ili kuonyesha kuwa baraza hilo la mahakama lingeazibiwa vikali.

“Ninateseka kwa sababu ya mambo ninayoona kuwa kweli na utukufu wake [Mungu].”​—Thomas Emlyn

Wakati Emlyn alihukumiwa kuwa mwenye kosa, mwanasheria mukubwa wa serikali alimuambia kwamba akatae uamuzi huo. Emlyn hakukubali wazo hilo. Aliombwa kiasi fulani cha feza na akahukumiwa kifungo cha mwaka mumoja. Kwa sababu hakuweza kulipa feza hizo, alibaki katika gereza miaka miwili mupaka wakati rafiki yake mumoja aliwafanya wakubwa wa serikali wakubali kupunguza feza hizo. Emlyn alifunguliwa tarehe 21 Mwezi wa 7, 1705. Kushushiwa heshima hivyo kulimufanya aseme maneno haya yaliyoonyeshwa kwenye mwanzo wa habari hii: “Ninateseka kwa sababu ya mambo ninayoona kuwa kweli na utukufu wake [Mungu].”

Emlyn alihamia katika muji wa Londres, ambako alijiunga na musomi mwengine wa Biblia, William Whiston, aliyechukiwa pia na watu kwa sababu alichapisha mambo aliyoona kuwa kweli ya Biblia. Whiston alimuheshimu Emlyn, na alikuwa anamuita “‘padri mukubwa na wa kwanza wa kuungamisha zambi’ za ‘ukristo wa zamani.’”

SABABU GANI ALIKATAA FUNDISHO LA UTATU?

Kama William Whiston na musomi mwengine mwenye kuheshimika anayeitwa Isaac Newton, Emlyn alitambua kwamba Biblia haiunge mukono fundisho la Utatu. Alieleza hivi: “Kisha kufikiri kwa uzito sana, na kujifunza Maandiko matakatifu, . . . Nilipata sababu kubwa . . . ya kubadilisha mawazo yangu, kuhusiana na mambo niliyoamini juu ya Utatu.” Alifikia uamuzi wa kwamba “Mungu na Baba wa Yesu Kristo ndiye peke yake Mutu Mukubwa Zaidi Kuliko Wote.”

Ni nini iliyomufanya Emlyn afikie uamuzi huo? Alipata maandiko mengi yanayoonyesha tofauti kati ya Yesu na Baba Yake. Ona maandiko machache tu (maelezo ya Emlyn juu ya maandiko hayo yako katika italiki):

  •   Yohana 17:3: “Kristo hajasemwa hata siku moja kuwa Mungu Mweza​-Yote ao Mungu wa kweli, ao kuwa ndiye Mungu wa pekee.” Ni Baba tu ndiye anaitwa “Mungu wa pekee wa kweli.”

  •   Yohana 5:30: “Mwana hafanye mapenzi yake mwenyewe, lakini anafanya mapenzi ya Baba.”

  •   Yohana 5:26: “Baba ndiye alimupatia uzima.”

  •   Waefeso 1:3: “Hata ikiwa mara nyingi Yesu Kristo anaitwa Mwana wa Mungu, hakuna nafasi Baba anaitwa Baba wa Mungu, ijapokuwa anaitwa mara nyingi Baba wa Bwana wetu Yesu.”

Kisha Emlyn kuchunguza mambo yote yanayohakikisha kuwa Mungu haiko Utatu, alisema hivi kwa mukazo: “Hakuna hata mustari mumoja katika Maandiko matakatifu, unaoonyesha kwamba Baba, Mwana, na Roho Mutakatifu ni mutu yuleyule mumoja, kama watu wanavyowazia.”

TUNAJIFUNZA NINI?

Watu wengi leo wanaogopa kutetea mambo ambayo Maandiko yanafundisha. Lakini Emlyn alikuwa tayari kutetea kweli ya Biblia. Aliuliza, “Ikiwa mutu hatetee mafundisho ya maana zaidi yenye anaona kuwa wazi na bila makosa katika Maandiko matakatifu, sababu gani asome na kutafuta mambo hayo?” Emlyn hakulegeza musimamo wake.

Mufano wa Emlyn na watu wengine unaweza kutuchochea tuchunguze ikiwa tuko tayari kutetea kweli hata wakati tunazarauliwa. Tunaweza kujiuliza, ‘Jambo la maana zaidi ni gani, ni kusifiwa na kukubaliwa na watu ao kutetea kweli ya Neno la Mungu?’