Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Iga Imani ya Musa

Iga Imani ya Musa

“Kwa imani Musa, alipokuwa mtu mzima, alikataa kuitwa mwana wa binti ya Farao.”EBR. 11:24.

1, 2. (a) Musa alifanya uamuzi gani alipokuwa na umri wa miaka 40? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.) (b) Kwa nini Musa alichagua kutendewa vibaya pamoja na watu wa Mungu?

MUSA alijua ufanisi ambao angepata nchini Misri. Aliona nyumba za kifahari za matajiri. Aliishi na familia ya kifalme. ‘Alifundishwa hekima yote ya Wamisri,’ ambayo huenda ilitia ndani sanaa, elimu ya nyota, hesabu, na mambo mengine ya kisayansi. (Mdo. 7:22) Angepata mali, mamlaka, na pendeleo ambalo Mmisri wa kawaida hangeweza kupata.

2 Hata hivyo, Musa alipokuwa na umri wa miaka 40 alifanya uamuzi ambao bila shaka ulimshangaza Farao na familia ya kifalme iliyomlea. Hakuchagua tu maisha ya Wamisri wa kawaida, badala yake alichagua kuishi na watumwa. Kwa nini? Musa alikuwa na imani. (Soma Waebrania 11:24-26.) Kwa imani, Musa hakuona tu ufanisi ambao angepata ulimwenguni. Kwa kuwa Musa alithamini mambo ya kiroho, alikuwa na imani katika Yehova, ‘Yule asiyeonekana,’ na katika utimizo wa ahadi Zake.Ebr. 11:27.

3. Ni maswali gani matatu yatakayojibiwa katika makala hii?

3 Sisi pia hatupaswi kukazia fikira mambo tunayoona kwa macho halisi. Ni lazima tuwe “namna ya watu walio na imani.” (Ebr. 10:38, 39) Ili kuimarisha imani yetu, acheni tuchunguze mambo yaliyoandikwa kumhusu Musa katika  Waebrania 11:24-26. Tunapofanya hivyo, tafuta majibu ya maswali haya: Imani ilimchocheaje Musa kukataa tamaa za kimwili? Imani yake ilimsaidiaje kuthamini mapendeleo yake ya utumishi aliposhutumiwa? Na kwa nini Musa “alikaza macho kwenye malipo ya thawabu”?

ALIKATAA TAMAA ZA KIMWILI

4. Musa alitambua nini kuhusu “kufurahia dhambi”?

4 Musa aliona kwa macho ya imani kwamba “kufurahia dhambi” ni jambo la muda mfupi tu. Huenda wengine wangesema kwamba Misri ilikuwa serikali kuu ya ulimwengu licha ya kwamba ibada ya sanamu na uchawi ulikuwa umeenea sana nchini humo na wakati huo watu wa Yehova walikuwa watumwa. Hata hivyo, Musa alijua kwamba Mungu angeweza kubadili mambo. Ingawa waovu walionekana wanafanikiwa, Musa alikuwa na imani kwamba wangeangamia. Kwa hiyo, hakushawishika “kufurahia dhambi kwa muda.”

5. Ni nini kitakachotusaidia kukataa “kufurahia dhambi kwa muda”?

5 Unawezaje kupinga kishawishi cha “kufurahia dhambi kwa muda”? Usisahau kamwe kwamba mtu hawezi kufurahia dhambi kwa muda mrefu. Kwa macho ya imani, ona kwamba “ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake.” (1 Yoh. 2:15-17) Tafakari kuhusu wakati ujao wa watenda-dhambi wasiotubu. Wako ‘kwenye udongo unaoteleza, watamalizwa kwa matisho!’ (Zab. 73:18, 19) Unaposhawishiwa kutenda dhambi, jiulize hivi: ‘Jambo hili litaathirije wakati wangu ujao?’

6. (a) Kwa nini Musa alikataa “kuitwa mwana wa binti ya Farao”? (b) Kwa nini unafikiri kwamba Musa alifanya uamuzi unaofaa?

6 Imani ya Musa ilimsaidia pia kuamua jinsi atakavyotumia maisha yake. “Kwa imani Musa, alipokuwa mtu mzima, alikataa kuitwa mwana wa binti ya Farao.” (Ebr. 11:24) Musa hakujitetea kwamba angemtumikia Mungu akiwa katika makao ya mfalme na kutumia mali na mapendeleo yake kuwasaidia ndugu zake Waisraeli. Badala yake, Musa aliazimia kumpenda Yehova kwa moyo wake wote, nafsi yake yote, na nguvu zake zote. (Kum. 6:5) Uamuzi wa Musa ulimlinda kutokana na maumivu mengi ya moyo. Mwishowe, Waisraeli ndio waliochukua hazina nyingi za Misri alizoacha. (Kut. 12:35, 36) Farao aliaibishwa na kuuawa. (Zab. 136:15) Lakini Musa alitumiwa na Mungu kuliongoza taifa zima la Israeli mahali salama. Maisha yake yalikuwa na kusudi kwelikweli.

7. (a) Kulingana na Mathayo 6:19-21, kwa nini tunapaswa kukazia fikira wakati ujao? (b) Kuna tofauti gani kati ya hazina za kimwili na hazina za kiroho? Toa mfano.

7 Ikiwa unamtumikia Yehova ukiwa kijana, imani itakusaidiaje kuamua jinsi utakavyotumia maisha yako? Ni jambo la hekima kufikiria wakati wako ujao. Je, imani katika ahadi za Mungu itakuchochea kujiwekea hazina kwa ajili ya wakati ujao wa milele au wakati ujao usiodumu? (Soma Mathayo 6:19-21.) Mchezaji stadi wa dansi anayeitwa Sophie alikabili uamuzi kama huo. Kampuni nyingi za dansi nchini Marekani zilijitolea kumlipia masomo na kumwajiri. Anakiri hivi: “Ilisisimua sana kuwa mashuhuri. Kwa kweli, nilijiona kuwa bora kuliko vijana wenzangu. Lakini sikuwa na furaha.” Kisha Sophie akatazama video Young People Ask—What Will I Do With My Life? Anasema hivi: “Niligundua kwamba ingawa nilifanikiwa na kuwa maarufu katika ulimwengu, sikumwabudu Yehova kwa moyo wangu wote. Nikasali kwa bidii na kuacha kucheza dansi.” Anahisije kuhusu uamuzi wake? Anasema hivi: “Sitamani maisha yangu ya zamani. Nina furaha kwelikweli. Mimi na mume wangu ni mapainia. Sisi si maarufu, na hatuna vitu vingi vya kimwili. Lakini Yehova yupo pamoja nasi, tunaongoza  mafunzo ya Biblia, na tuna miradi ya kiroho. Sina majuto yoyote.”

8. Ni shauri gani la Biblia linaloweza kumsaidia kijana kuamua jinsi atakavyotumia maisha yake?

8 Yehova anajua unahitaji nini ili uwe na maisha bora. Musa alisema hivi: “Yehova Mungu wako anataka nini kutoka kwako ila kumwogopa Yehova Mungu wako, ili kutembea katika njia zake zote na kumpenda yeye na kumtumikia Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote; kuzishika amri za Yehova na sheria zake ninazokuamuru wewe leo, kwa faida yako?” (Kum. 10:12, 13) Ukiwa kijana, chagua kazi itakayokusaidia kumpenda Yehova na kumtumikia “kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote.” Unaweza kuwa na hakika kwamba uamuzi huo ‘utakufaidi.’

ALITHAMINI MAPENDELEO YAKE YA UTUMISHI

9. Eleza kwa nini huenda ilikuwa vigumu kwa Musa kutimiza mgawo wake.

9 Musa “aliona shutuma ya Kristo kuwa ni utajiri mkubwa kuliko hazina za Misri.” (Ebr. 11:26) Musa alitumwa kama “Kristo,” au “Mtiwa-mafuta,” katika maana ya kwamba alichaguliwa na Yehova kuwaongoza Waisraeli kutoka Misri. Musa alijua kwamba mgawo wake ungekuwa mgumu, hata ‘angeshutumiwa.’ Awali, Mwisraeli fulani alimdhihaki hivi: “Ni nani aliyekuweka wewe rasmi kuwa mkuu na mwamuzi juu yetu?” (Kut. 2:13, 14) Baadaye, Musa alimuuliza Yehova hivi: “Farao atawezaje kunisikiliza?” (Kut. 6:12) Ili kukabiliana na shutuma, Musa alimweleza Yehova mambo yaliyomwogopesha na kumhangaisha. Yehova alimsaidiaje Musa kutimiza mgawo wake mgumu?

10. Yehova alimsaidiaje Musa kutimiza mgawo wake?

10 Kwanza, Yehova alimhakikishia Musa hivi: “Nitakuwa pamoja nawe.” (Kut. 3:12) Pili, Yehova alimwimarisha kwa kumweleza maana moja ya jina lake: “NITAKUWA KILE NITAKACHOKUWA.” * (Kut. 3:14) Tatu, alimpa Musa nguvu za kimuujiza zilizothibitisha kwamba alitumwa na Mungu. (Kut. 4:2-5) Nne, Yehova alimpa Musa msaidizi na msemaji, yaani, Haruni, ambaye angemsaidia kutimiza mgawo wake. (Kut. 4:14-16) Mwishoni mwa maisha yake, Musa alikuwa amesadiki kabisa kwamba Mungu huwasaidia watumishi Wake kutimiza migawo yoyote anayowapa. Ndiyo sababu Musa alimwambia hivi kwa uhakika Yoshua aliyechukua mahali pake: “Na Yehova ndiye anayepiga mwendo mbele yako. Yeye mwenyewe ataendelea kuwa pamoja nawe. Hatakutupa wala kukuacha kabisa. Usiogope wala usiingiwe na hofu.”—Kum. 31:8.

11. Kwa nini Musa alithamini sana mgawo wake?

11 Kwa msaada wa Yehova, Musa alithamini sana mgawo wake mgumu na kuuona kuwa “mkubwa kuliko hazina za Misri.” Kwa kweli, kumtumikia Farao hakungeweza kamwe kulinganishwa na kumtumikia Mungu Mweza-Yote. Je, kuwa mkuu katika nchi ya Misri kungeweza kulinganishwa na kuwa “Kristo,” au mtiwa-mafuta wa Yehova? Musa alithawabishwa kwa sababu ya kuthamini mapendeleo yake ya utumishi. Alikuwa na urafiki wa pekee pamoja na Yehova, aliyemsaidia kuonyesha “nguvu na hofu kuu” alipowaongoza Waisraeli kwenye Nchi ya Ahadi.—Kum. 34:10-12.

12. Tunapaswa kuthamini mapendeleo gani tuliyopewa na Yehova?

12 Sisi pia tuna mgawo. Kupitia Yesu, Yehova ametugawia huduma, kama alivyomgawia Paulo na wengine. (Soma 1 Timotheo 1:12-14.) Sisi sote tuna pendeleo la kutangaza habari njema. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Wengine  wanatumikia wakiwa watumishi wa wakati wote. Ndugu wakomavu waliobatizwa wanawatumikia wengine kutanikoni wakiwa watumishi wa huduma na wazee. Hata hivyo, huenda watu wa familia yako na wengine wasio waamini wasithamini mapendeleo hayo au huenda wakudhihaki kwa sababu ya kujidhabihu. (Mt. 10:34-37) Ukivunjika moyo, huenda ukaanza kufikiri kwamba hakuna faida yoyote ya kujidhabihu na huwezi kutimiza mgawo wako. Imani itakusaidiaje kuendelea kuvumilia?

13. Yehova hutusaidiaje kutimiza migawo ya kitheokrasi?

13 Kwa imani, msihi Yehova akusaidie. Mwambie mambo yanayokuogopesha na kukuhangaisha. Kwa kweli, Yehova ndiye aliyekupa mapendeleo hayo, atakusaidia kufanikiwa. Atakusaidiaje? Kama tu alivyomsaidia Musa. Kwanza, Yehova anakuhakikishia hivi: “Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli. Nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.” (Isa. 41:10) Pili, anakukumbusha kwamba ahadi zake zinategemeka: “Mimi nimesema hilo; pia nitalitimiza. Nimelifanyiza, pia nitalitenda.” (Isa. 46:11) Tatu, Yehova anakupa “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili utimize huduma yako. (2 Kor. 4:7) Nne, ili kukusaidia kuvumilia katika mgawo wako, Baba yetu mwenye kujali amekupa undugu wa ulimwenguni pote wa waabudu wa kweli ‘wanaoendelea kufarijiana na kujengana.’ (1 The. 5:11) Kadiri Yehova anavyokusaidia kutimiza migawo yako, ndivyo imani yako inavyoendelea kuongezeka na utathamini mapendeleo yako ya utumishi na kuyaona kuwa yenye thamani kuliko hazina yoyote duniani.

“ALIKAZA MACHO KWENYE MALIPO YA THAWABU”

14. Kwa nini Musa alikuwa na uhakika kwamba angethawabishwa?

14 Musa “alikaza macho kwenye malipo ya thawabu.” (Ebr. 11:26) Musa aliruhusu mambo machache aliyojua kuhusu wakati ujao yaongoze mtazamo wake. Kama Abrahamu, babu yake, Musa alikuwa na uhakika kwamba Yehova anaweza kuwafufua wafu. (Luka 20:37, 38; Ebr. 11:17-19) Kwa kuwa Musa aliamini ahadi za Yehova za wakati ujao, hakuona kwamba alipoteza miaka 40 aliyokuwa mkimbizi na miaka 40 aliyokaa nyikani. Ingawa hakujua kikamili jinsi ambavyo ahadi za Mungu zingetimizwa, kwa macho ya imani aliona thawabu isiyoonekana.

15, 16. (a) Kwa nini tunahitaji kukazia macho thawabu yetu? (b) Ni baraka gani unazotazamia kwa hamu chini ya utawala wa Ufalme?

 15 Je ‘unakaza macho kwenye malipo ya thawabu’? Sawa na Musa, hatujui kikamili jinsi ahadi za Mungu zitakavyotimia. Kwa mfano, ‘hatujui dhiki kuu itakuja wakati gani uliowekwa.’ (Marko 13:32, 33) Hata hivyo, tunajua mambo mengi kuhusu Paradiso itakayokuja kuliko Musa alivyojua. Hata ingawa hatujui mambo yote, tuna ahadi za kutosha tunazoweza ‘kukazia’ macho zinazoonyesha jinsi maisha yatakavyokuwa chini ya Ufalme wa Mungu. Tutachochewa kuutafuta Ufalme huo kwanza ikiwa ulimwengu mpya ni halisi akilini mwetu. Jinsi gani? Fikiria jambo hili: Je, unaweza kununua nyumba ikiwa hujui mengi kuihusu? La hasha! Vivyo hivyo, hatungependa kutumia maisha yetu kufuatilia tumaini lisilo halisi. Kwa imani, tunapaswa kuona kihalisi na wazi jinsi maisha yatakavyokuwa chini ya utawala wa Ufalme.

Tutasisimka sana kuzungumza na watumishi waaminifu kama Musa! (Tazama fungu la 16)

16 Ili Ufalme wa Mungu uwe halisi zaidi akilini mwako, ‘kazia’ macho jinsi maisha yako yatakavyokuwa katika Paradiso. Tumia uwezo wako wa kufikiri. Kwa mfano, unaposoma masimulizi ya Biblia kuhusu watu walioishi kabla ya Ukristo, fikiria maswali utakayowauliza wakifufuliwa. Fikiria maswali ambayo huenda watakuuliza kuhusu maisha yako katika siku za mwisho. Wazia jinsi utakavyosisimka utakapokutana na mababu zako na kuwafundisha mambo yote ambayo Mungu amewafanyia. Wazia jinsi utakavyofurahia kujifunza kuhusu wanyama mbalimbali wa mwituni wakiwa katika mazingira yenye amani. Fikiria jinsi utakavyokuwa na uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Yehova unapofikia ukamilifu hatua kwa hatua.

17. Thawabu yetu inatuchocheaje inapokuwa halisi akilini mwetu?

17 Thawabu yetu inapokuwa halisi akilini mwetu, inatuchochea kuendelea kuvumilia, kuwa na shangwe, na kufanya maamuzi yatakayotusaidia kupata uzima wa milele wakati ujao. Paulo aliwaandikia Wakristo watiwa-mafuta hivi: “Tukitumainia kile ambacho hatuoni, sisi huendelea kukingojea kwa uvumilivu.” (Rom. 8:25) Hilo linawahusu pia Wakristo wote wenye tumaini la kuishi milele. Ingawa hatujapokea thawabu yetu, imani yetu ni yenye nguvu sana hivi kwamba tunaendelea kungojea kwa subira “malipo ya thawabu.” Sawa na Musa, hatuoni kwamba tunapoteza wakati kumtumikia Yehova. Badala yake, tunasadiki kwamba “vitu vinavyoonekana ni vya muda, lakini vitu visivyoonekana ni vya milele.”Soma 2 Wakorintho 4:16-18.

18, 19. (a) Kwa nini ni lazima tupigane ili kudumisha imani yetu? (b) Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

18 Imani hutuwezesha kutambua “uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Ebr. 11:1) Mtu wa kimwili haoni thamani kubwa ya kumtumikia Yehova, na hazina za kiroho “ni upumbavu kwake.” (1 Kor. 2:14) Lakini sisi tunatumaini kuishi milele na kushuhudia watu wakifufuliwa, mambo ambayo ulimwengu hauoni. Sawa na wanafalsafa waliomwita Paulo “mpiga-domo” mpumbavu, watu wengi leo wanafikiri kwamba tumaini tunalohubiri ni upumbavu mtupu.Mdo. 17:18.

19 Kwa kuwa tumezungukwa na watu wengi wasio na imani, ni lazima tupigane ili kudumisha imani yetu. Toa dua kwa Yehova ili “imani yako isififie.” (Luka 22:32) Kazia macho thamani kubwa ya kumtumikia Yehova, tumaini lako la uzima wa milele, na ufikirie madhara ya dhambi. Hata hivyo, imani ya Musa ilimwezesha kuona mengi zaidi. Katika makala inayofuata, tutachunguza jinsi imani ilivyomsaidia Musa kumwona ‘Yule asiyeonekana.’Ebr. 11:27.

^ fu. 10 Msomi mmoja wa Biblia aliandika hivi kuhusu maneno ya Mungu yaliyo katika Kutoka 3:14: “Hakuna chochote kinachoweza kumzuia kutimiza mapenzi yake . . . Jina hili [Yehova] lingekuwa ngome kwa Waisraeli, chanzo cha tumaini na faraja milele.”