Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unamwona ‘Yule Asiyeonekana’?

Je, Unamwona ‘Yule Asiyeonekana’?

Aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yeye asiyeonekana.”EBR. 11:27.

1, 2. (a) Kwa nini ilionekana kwamba Musa alikuwa hatarini? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.) (b) Kwa nini Musa hakuogopa hasira ya mfalme?

FARAO alikuwa mtawala mwenye kutisha aliyeonwa na Wamisri kuwa mungu aliye hai. Kitabu Misri Ilipotawala Mashariki (cha Kiingereza) kinasema kwamba machoni pao “alikuwa na hekima na nguvu kuliko viumbe wote duni.” Ili kuwaogopesha raia wake, Farao alivaa kofia ya mfalme yenye sanamu ya swila aliye tayari kushambulia. Sanamu hiyo iliwakumbusha maadui wa mfalme kwamba wataangamizwa haraka. Basi wazia jinsi Musa alivyohisi Yehova alipomwambia hivi: ‘Nitakutuma kwa Farao, nawe uwatoe watu wangu wana wa Israeli kutoka Misri.’Kut. 3:10.

2 Musa alienda Misri kutangaza ujumbe wa Mungu uliomkasirisha sana Farao. Baada ya Misri kupata mapigo tisa, Farao alimwonya Musa hivi: “Jiangalie! Usijaribu kuuona uso wangu tena, kwa sababu siku utakayouona uso wangu utakufa.” (Kut. 10:28) Kabla ya kuondoka mbele ya Farao, Musa alitabiri kwamba mwana mzaliwa wa kwanza wa mfalme angekufa. (Kut. 11:4-8) Hatimaye, Musa akaiagiza kila familia ya Waisraeli ichinje mbuzi au kondoo dume na kuipaka damu yake juu ya milango yao. Wamisri  walimwona kondoo dume kuwa mnyama mtakatifu kwa mungu wao Ra. (Kut. 12:5-7) Farao angetendaje? Musa hakuogopa. Kwa nini? Kwa imani, alimtii Yehova “bila kuogopa hasira ya mfalme, kwa maana aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yeye asiyeonekana.”Soma Waebrania 11:27, 28.

3. Ni mambo gani tutakayochunguza kuhusu imani ya Musa katika ‘Yule asiyeonekana’?

3 Je, imani yako ni yenye nguvu sana kana kwamba ‘unamwona Mungu’? (Mt. 5:8) Ili kutusaidia kuboresha macho yetu ya kiroho yaweze kumwona ‘Yule asiyeonekana,’ acheni tuzungumze kuhusu Musa. Imani yake katika Yehova ilimsaidiaje kutowaogopa wanadamu? Alionyeshaje imani katika ahadi za Mungu? Na uwezo wa Musa wa kumwona ‘Yule asiyeonekana’ ulimwimarishaje alipokabili hatari akiwa na Waisraeli wenzake?

HAKUOGOPA “HASIRA YA MFALME”

4. Musa alionekanaje akilinganishwa na Farao?

4 Kwa macho halisi, Musa alionekana duni akilinganishwa na Farao. Ilionekana kwamba masilahi, maisha, na wakati ujao wa Musa ulikuwa mikononi mwa Farao. Musa alimuuliza Yehova hivi: “Mimi ni nani hata niende kwa Farao, nikawatoe wana wa Israeli kutoka Misri?” (Kut. 3:11) Miaka 40 hivi mapema, Musa alikimbia kutoka Misri. Huenda aliwaza hivi: ‘Je, kweli ni jambo la hekima kwangu kurudi Misri na kumkasirisha mfalme?’

5, 6. Ni nini kilichomsaidia Musa kumwogopa Yehova badala ya Farao?

5 Kabla ya Musa kurudi Misri, Mungu alimfundisha kanuni hii muhimu sana ambayo Musa aliandika baadaye katika kitabu cha Ayubu: “Kumwogopa Yehova—hiyo ndiyo hekima.” (Ayu. 28:28) Ili kumsaidia Musa kusitawisha woga huo na kutenda kwa hekima, Yehova alionyesha tofauti iliyopo kati ya wanadamu na Mungu Mweza-Yote. Aliuliza hivi: “Ni nani aliyekifanya kinywa kwa ajili ya mwanadamu au ni nani ambaye humfanya mtu kuwa bubu au kiziwi au mwenye kuona vizuri au kipofu? Je, si mimi, Yehova?”Kut. 4:11.

6 Musa alijifunza nini? Alijifunza kwamba hakuhitaji kuogopa. Alitumwa na Yehova, ambaye angempa Musa chochote alichohitaji ili kumtangazia Farao ujumbe Wake. Isitoshe, Farao hangeweza kamwe kulinganishwa na Yehova. Kwa kweli, hiyo haikuwa mara ya kwanza kwa watumishi wa Mungu kutishwa na utawala wa Misri. Huenda Musa alitafakari kuhusu jinsi Yehova alivyomlinda Abrahamu, Yosefu, na hata kumlinda yeye wakati wa utawala uliopita wa Mafarao. (Mwa. 12:17-19; 41:14, 39-41; Kut. 1:22–2:10) Akiwa na imani katika Yehova, ‘Yule asiyeonekana,’ Musa alienda kwa ujasiri mbele za Farao na kumwambia kila neno ambalo Yehova alimwamuru Musa.

7. Imani katika Yehova ilimlinda jinsi gani dada mmoja?

7 Vivyo hivyo, imani katika Yehova ilimlinda dada anayeitwa Ella kutokana na woga wa wanadamu. Mnamo mwaka wa 1949, Ella alikamatwa nchini Estonia na askari wa KGB na kuvuliwa nguo mbele ya maofisa vijana. Alisema hivi: “Niliaibika sana. Hata hivyo, baada ya kusali kwa Yehova, nilipata amani na utulivu moyoni.” Kisha, Ella aliwekwa katika kifungo cha upweke kwa siku tatu. Anasema hivi: “Maofisa hao walipaaza sauti hivi: ‘Tutahakikisha kwamba jina Yehova halikumbukwi tena nchini Estonia! Utapelekwa kambini, na wengine watapelekwa Siberia!’ Wakauliza hivi kwa dhihaka: ‘Yehova wenu yuko wapi?’” Je, Ella angewaogopa wanadamu au angemtegemea Yehova? Alipohojiwa, aliwaambia hivi kwa ujasiri waliomdhihaki: “Nimefikiria sana jambo hilo, afadhali niishi gerezani nikiwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu badala ya kuwa huru na kupoteza kibali chake.”  Ni kana kwamba Ella alimwona Yehova kihalisi kama tu alivyowaona wanaume waliosimama mbele yake. Imani yake ilimsaidia kudumisha utimilifu wake.

8, 9. (a) Ni nini kinachoweza kukusaidia kuushinda woga wa wanadamu? (b) Unapaswa kumkazia nani fikira ikiwa unawaogopa wanadamu?

8 Imani katika Yehova itakusaidia kushinda woga wowote ulionao. Maofisa wenye mamlaka wakijaribu kukuzuia kumwabudu Mungu, huenda ikaonekana kwamba maisha, masilahi, na wakati wako ujao uko mikononi mwa wanadamu. Huenda hata ukaanza kufikiri kwamba si jambo la hekima kuendelea kumtumikia Yehova na hivyo kuwakasirisha wenye mamlaka. Kumbuka kwamba imani katika Mungu itakusaidia kuushinda woga wa wanadamu. (Soma Methali 29:25.) Yehova anauliza hivi: ‘Wewe ni nani umwogope mwanadamu anayeweza kufa na ambaye atakufa, na mwanadamu ambaye atafanywa kuwa majani mabichi tu?’Isa. 51:12, 13.

9 Mkazie fikira Baba yako mweza-yote. Anawahurumia, anawaona na huwasaidia wote wanaoteswa na watawala wasiofuata haki. (Kut. 3:7-10) Hata ukilazimika kutetea imani yako mbele ya maofisa wenye mamlaka, ‘usihangaike juu ya jambo utakalosema au jinsi utakavyolisema; kwa maana utapewa jambo la kusema katika saa hiyo.’ (Mt. 10:18-20) Yehova ana nguvu nyingi zaidi ya watawala na maofisa wa serikali. Ukiimarisha imani yako sasa, unaweza kumwona Yehova kuwa Mungu halisi anayetaka sana kukusaidia.

ALIONYESHA IMANI KATIKA AHADI ZA MUNGU

10. (a) Yehova aliwapa Waisraeli maagizo gani katika mwezi wa Nisani, mwaka wa 1513 K.W.K.? (b) Kwa nini Musa alitii maagizo ya Mungu?

10 Katika mwezi wa Nisani, mwaka wa 1513 K.W.K., Yehova aliwaambia Musa na Haruni wawape Waisraeli maagizo haya yasiyo ya kawaida: Chagueni kondoo dume au mbuzi mwenye afya nzuri, mumchinje, na kuipaka damu yake juu ya milango yenu. (Kut. 12:3-7) Musa alitendaje? Baadaye mtume Paulo aliandika hivi kumhusu: “Kwa imani alifanya sherehe ya pasaka na upakaji wa damu, ili mwangamizaji asiwaguse wazaliwa wao wa kwanza.” (Ebr. 11:28) Musa alijua kwamba Yehova anategemeka, na hivyo alionyesha imani katika ahadi ya Yehova ya kuwaangamiza wana wazaliwa wa kwanza wa Wamisri.

11. Kwa nini Musa aliwaonya wengine?

11 Wana wa Musa walikuwa Midiani, mbali na “mwangamizaji.” * (Kut. 18:1-6) Hata hivyo, alitii na kuwapa maagizo hayo Waisraeli wengine ambao wana wao wazaliwa wa kwanza walikuwa hatarini. Uhai wao ulikuwa hatarini, na Musa aliwapenda wanadamu wenzake. Biblia inasema hivi: “Papo hapo Musa akawaita wanaume wote wazee wa Israeli na kuwaambia: ‘Mchinjeni mnyama wa pasaka.’”Kut. 12:21.

12. Yehova ametuagiza tutangaze ujumbe gani muhimu?

12 Watu wa Yehova wanatangaza ujumbe huu muhimu wakiongozwa na malaika: “Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yake imefika, na kwa hiyo mwabuduni Yeye aliyezifanya mbingu na dunia na bahari na chemchemi za maji.” (Ufu. 14:7) Huu ndio wakati wa kutangaza ujumbe huo. Ni lazima tuwaonye jirani zetu watoke katika Babiloni Mkubwa ili ‘wasipokee sehemu ya mapigo yake.’ (Ufu. 18:4) “Kondoo wengine” wanawasaidia Wakristo watiwa-mafuta kuwaomba wale waliotengwa mbali na Mungu ‘wapatanishwe’ naye.Yoh. 10:16; 2 Kor. 5:20.

Imani katika ahadi za Yehova itakuchochea kuwa na hamu zaidi ya kuhubiri habari njema (Tazama fungu la 13)

13. Ni nini kitakachotuchochea kuwa na hamu zaidi ya kuhubiri habari njema?

13 Tunasadiki kwamba kwa kweli “saa  ya hukumu yake imefika.” Pia, tuna imani kwamba Yehova hasemi uwongo kuhusu uharaka wa kazi yetu ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Mtume Yohana aliona katika maono “malaika wanne wamesimama juu ya pembe nne za dunia, wakizishika sana zile pepo nne za dunia.” (Ufu. 7:1) Je, unawaona kwa imani malaika hao wakiwa tayari kuachilia pepo za uharibifu za dhiki kuu juu ya ulimwengu huu? Ukiona malaika hao kwa macho ya imani, utaweza kuhubiri habari njema ukiwa na uhakika.

14. Ni nini kinachotuchochea ‘kumwonya mwovu ili aiache njia yake ya uovu’?

14 Tayari Wakristo wa kweli wanafurahia urafiki pamoja na Yehova na tumaini la kuishi milele. Hata hivyo, tunatambua kwamba ni jukumu letu ‘kumwonya mwovu aiache njia yake ya uovu ili ahifadhiwe hai.’ (Soma Ezekieli 3:17-19.) Bila shaka, hatuhubiri ili kuepuka tu hatia ya damu. Tunampenda Yehova, na tunawapenda jirani zetu. Yesu alitumia mfano wa Msamaria mwema kuonyesha maana halisi ya upendo na huruma. Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, mimi ni kama yule Msamaria, “ninawasikitikia” watu na hivyo kuwahubiria?’ Hatutaki kamwe kutoa visingizio na ‘kupita kando upande wa pili’ kama kuhani na Mlawi wanaotajwa katika mfano huo. (Luka 10:25-37) Kuonyesha imani katika ahadi za Mungu na kuwapenda jirani zetu kutatuchochea kushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri kabla mwisho haujafika.

“WALIPITA KATIKATI YA BAHARI NYEKUNDU”

15. Kwa nini Waisraeli walihisi kwamba wamenaswa?

15 Imani ya Musa katika ‘Yule asiyeonekana’ ilimsaidia wakati ambapo  Waisraeli walikabili hatari baada ya kuondoka Misri. Biblia inasema hivi: “Wana wa Israeli wakaanza kuinua macho yao, na tazama, Wamisri walikuwa wakipiga mwendo wakiwafuatilia; na wana wa Israeli wakaogopa sana na kuanza kumlilia Yehova.” (Kut. 14:10-12) Je, walitarajia jambo hilo? Bila shaka, kwa sababu Yehova alikuwa ametabiri hivi: “Nitauacha moyo wa Farao uwe mkaidi, naye hakika atawafuatilia wao nami nitajipatia utukufu kupitia kwa Farao na majeshi yake yote; nao Wamisri watajua hakika kwamba mimi ni Yehova.” (Kut. 14:4) Hata hivyo, Waisraeli waliona tu kilichoonekana kwa macho halisi, waliona Bahari Nyekundu iliyokuwa mbele yao kama kizuizi, waliona magari ya kivita ya Farao yaliyokuwa yakiwafuata kwa kasi, na Musa, mchungaji mwenye umri wa miaka 80 aliyekuwa akiwaongoza! Walihisi kwamba wamenaswa.

16. Imani ilimwimarishaje Musa kwenye Bahari Nyekundu?

16 Hata hivyo, Musa hakuogopa. Kwa nini? Kwa sababu kwa macho yake ya imani aliona jambo lenye nguvu zaidi kuliko bahari au jeshi. Aliuona “wokovu wa Yehova,” naye alijua kwamba Yehova angewapigania Waisraeli. (Soma Kutoka 14:13, 14.) Imani ya Musa iliwaimarisha watu wa Mungu. Biblia inasema hivi: “Kwa imani walipita katikati ya Bahari Nyekundu kana kwamba ni juu ya nchi kavu, lakini Wamisri walipothubutu kuipitia wakamezwa.” (Ebr. 11:29) Kisha, “watu wakaanza kumwogopa Yehova na kuwa na imani katika Yehova na katika Musa mtumishi wake.”Kut. 14:31.

17. Ni tukio gani la wakati ujao litakalojaribu imani yetu?

17 Hivi karibuni, itaonekana kwamba uhai wetu uko hatarini. Kwenye upeo wa dhiki kuu, serikali za ulimwengu huu zitakuwa zimeharibu na kuangamiza kabisa dini nyingi zilizo kubwa kuliko yetu. (Ufu. 17:16) Yehova anatabiri hatari tunayokabili kwa kusema sisi ni ‘nchi iliyo wazi ya mashambani, isiyo na ukuta, mapingo au milango.’ (Eze. 38:10-12, 14-16) Kwa macho halisi, itaonekana kwamba hatuwezi kuokoka. Utafanya nini?

18. Eleza kwa nini tunaweza kuwa imara wakati wa dhiki kuu.

18 Hatupaswi kuyumbayumba kwa woga. Kwa nini? Kwa sababu Yehova ndiye aliyetabiri kwamba watu wake watashambuliwa. Ametabiri pia matokeo yake. “‘Katika siku hiyo, katika siku ambayo Gogu atakuja juu ya nchi ya Israeli,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘ghadhabu yangu itapanda puani mwangu. Na katika ukali wangu, katika moto wa ghadhabu yangu, nitalazimika kusema.’” (Eze. 38:18-23) Kisha, Mungu atawaharibu wote wanaotaka kuwadhuru watu wa Yehova. Kuwa na imani kwamba utalindwa katika “ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha” kutakusaidia ‘kuuona wokovu wa Yehova’ na kudumisha utimilifu wako.—Yoe. 2:31, 32.

19. (a) Musa alikuwa na uhusiano wa karibu kadiri gani pamoja na Yehova? (b) Utafurahia baraka gani ukimtambua Yehova katika njia zako zote?

19 Jitayarishe sasa kwa ajili ya matukio hayo yenye kusisimua kwa kuendelea ‘kuwa imara kama mtu anayemwona Yule asiyeonekana’! Imarisha urafiki wako pamoja na Yehova Mungu kwa kusali na kujifunza kwa ukawaida. Musa alikuwa na urafiki wa karibu sana pamoja na Yehova na alimpa nguvu za kutenda miujiza hivi kwamba Biblia inasema Yehova alimjua Musa “uso kwa uso.” (Kum. 34:10) Musa alikuwa nabii asiye wa kawaida. Hata hivyo, kwa imani, unaweza pia kumjua Yehova vizuri sana hivi kwamba itakuwa ni kana kwamba unamwona kihalisi. Ukiendelea kumtambua “katika njia zako zote,” kama Neno la Mungu linavyokuhimiza ufanye, “atanyoosha mapito yako.”Met. 3:6.

^ fu. 11 Hapana shaka kwamba Yehova aliwatuma malaika kutekeleza hukumu yake juu ya Wamisri.Zab. 78:49-51.