Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Unamuona “Yeye Asiyeonekana”?

Unamuona “Yeye Asiyeonekana”?

‘Aliendelea kuwa imara kama mutu anayemuona Yeye asiyeonekana.’—EBR. 11:27.

1, 2. (a) Sababu gani ilionekana kwamba Musa alikuwa katika hatari? Eleza. (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.) (b) Sababu gani Musa hakuogopa hasira ya mufalme?

FARAO aliogopewa sana, na Wamisri walimuona kuwa mungu anayeishi. Kitabu kimoja kinasema kwamba Wamisri walimuona Farao ‘kuwa mwenye hekima na nguvu kuliko viumbe wote duniani.’ (When Egypt Ruled the East) Ili watu wake wamuogope, Farao alivaa taji iliyokuwa na sanamu ya nyoka anayeitwa swila (ao cobra) aliye tayari kushambulia. Sanamu hiyo ilionyesha kwamba alikuwa tayari kuangamiza haraka maadui wake. Wazia sasa namna Musa alivyojisikia wakati Yehova alimwambia hivi: ‘Nitakutuma kwa Farao, nawe utawatoa watu wangu wana wa Israeli kutoka Misri.’—Kut. 3:10.

2 Musa alienda Misri kutangaza ujumbe wa Mungu, na hivyo kufanya hasira ya Farao iwake. Kisha mapigo kenda kupiga inchi ya Misri, Farao alimutolea Musa angalisho kwa kusema hivi: ‘Jiangalie! Usijaribu kuuona uso wangu tena, kwa sababu siku utakapouona uso wangu utakufa.’ (Kut. 10:28) Mbele Musa aondoke machoni pa Farao, alitabiri kwamba muzaliwa wa kwanza wa mufalme atakufa. (Kut. 11:4-8) Mwishowe, Musa aliagiza familia za Waisraeli wachinje mbuzi ao kondoo-dume na kupakaa sehemu  ya damu yake juu ya nguzo za milango. Kondoo-dume alionwa kuwa mutakatifu kwa mungu wa Wamisri anayeitwa Ra. (Kut. 12:5-7) Farao angetenda namna gani? Musa hakuogopa. Sababu gani? Imani yake ilimuchochea amutii Yehova, ‘bila kuogopa hasira ya mufalme, kwa maana aliendelea kuwa imara kama mutu anayemuona Yeye asiyeonekana.’—Soma Waebrania 11:27, 28.

3. Tutazungumuzia nini kuhusu imani ya Musa?

3 Imani yako ni yenye nguvu ili ionekane kwamba ‘unamuona Mungu’? (Mt. 5:8) Ili kufanya hali yetu ya kiroho iwe nguvu na kumuona ‘Yeye asiyeonekana,’ acheni tuzungumuzie mufano wa Musa. Namna gani imani yake katika Yehova ilimusaidia asimuogope mwanadamu? Ni katika njia gani alionyesha imani katika ahadi za Mungu? Na namna gani uwezo wa Musa wa kumuona ‘Yeye asiyeonekana’ ulimutia nguvu wakati yeye na watu wake walikuwa katika hatari?

MUSA HAKUOGOPA ‘HASIRA YA MUFALME’

4. Kwa macho ya mwanadamu, Musa alionekana namna gani mbele ya Farao?

4 Kwa macho ya mwanadamu, Musa alionekana kuwa bure mbele ya Farao. Maisha ya Musa, na wakati wake ujao vilionekana kuwa katika mikono ya Farao. Musa mwenyewe alimuuliza Yehova hivi: “Mimi ni nani hata niende kwa Farao, nikawatoe wana wa Israeli kutoka Misri?” (Kut. 3:11) Miaka 40 hivi iliyopita, Musa alikuwa amekimbia kutoka Misri. Pengine angejiuliza hivi: ‘Ni jambo la hekima kurudia Misri na kumufanya mufalme akasirike tena?’

5, 6. Ni jambo gani lilimusaidia Musa asimuogope Farao lakini amuogope Yehova?

5 Mbele Musa arudi Misri, Mungu alimufundisha kanuni moja ya maana sana. Kisha Musa aliandika kanuni hiyo katika kitabu cha Ayubu inayosema hivi: ‘Kumuogopa Yehova—hiyo ndiyo hekima.’ (Ayu. 28:28) Ili kumusaidia Musa awe na woga huo na kutenda kwa hekima, Yehova alimuonyesha tofauti iliyo kati ya wanadamu na Mungu Mweza-Yote. Yehova alimuuliza hivi: ‘Ni nani aliyekifanya kinywa kwa ajili ya mwanadamu ao ni nani ambaye humufanya mutu kuwa bubu ao kiziwi ao mwenye kuona vizuri ao kipofu? Je, si mimi, Yehova?’—Kut. 4:11.

6 Yehova alipenda kumufundisha somo gani? Musa hakupaswa kuogopa. Ni Yehova aliyemutuma, na ni yeye aliyemupatia kila kitu alichohitaji ili kumutolea Farao ujumbe. Tena, Farao hakuwa kitu mbele ya Yehova. Zaidi ya hilo, hiyo haikuwa mara ya kwanza watumishi wa Yehova wakuwe katika hatari katika utawala wa Misri. Pengine Musa alifikiri namna Yehova alivyolinda Abrahamu, Yosefu, na Musa mwenyewe wakati wa utawala wa Farao wengine. (Mwa. 12:17-19; 41:14, 39-41; Kut. 1:22–2:10) Kwa kuwa alikuwa na imani katika Yehova, “Yeye asiyeonekana,” Musa alifika mbele ya Farao kwa ujasiri na kutangaza kila neno ambalo Yehova alimuagiza aseme.

7. Namna gani imani katika Yehova ilimulinda dada mumoja?

7 Vilevile imani katika Yehova ilimusaidia dada mumoja anayeitwa Ella asiogope wanadamu. Katika mwaka wa 1949, dada Ella alikamatwa katika Estonia na Shirika la Usalama wa Kitaifa la Sovieti (KGB), alitoshwa manguo, na kisha viongozi wa polisi vijana walimukazia macho kwa mazarau. Dada Ella anasema hivi: “Nilijisikia kwamba nimezarauliwa kabisa. Lakini, kisha kusali kwa Yehova, nilijisikia kuwa na amani na utulivu.” Kisha, dada Ella alifungwa katika chumba kidogo muda wa siku tatu akiwa peke yake. Anasema hivi: “Viongozi wa polisi walisema hivi kwa sauti kubwa: ‘Tutafanya yote tunayoweza ili jina Yehova lizimike katika Estonia! Utapelekwa katika kambi, na wengine watapelekwa Siberia!’ Waliongeza hivi kwa mazarau: ‘Yehova wako iko wapi?’” Je, dada Ella angeogopa wanadamu ao angemutegemea Yehova? Alipoulizwa, aliwaambia hivi bila woga wale waliomuzarau: “Nimefikiria sana jambo hili, na kuliko kupoteza uhusiano wangu pamoja na Yehova ili nifunguliwe, ni vizuri nibaki katika gereza nikiendelea kukubaliwa naye.”  Dada Ella alimuona Yehova kuwa mutu mwenye kuonekana kama alivyowaona wale wanaume waliosimama mbele yake. Kupitia imani yake, alibaki mushikamanifu.

8, 9. (a) Ni jambo gani linaloweza kukusaidia usimuogope mwanadamu? (b) Ikiwa wanadamu wanakuogopesha, unapaswa kumuweka nani katika akili?

8 Imani katika Yehova itakusaidia usiogope. Ikiwa viongozi wenye mamlaka wanajaribu kukukataza usimuabudu Mungu, itaonekana kwamba maisha yako, na wakati wako ujao viko katika mikono ya wanadamu. Unaweza hata kuanza kujiuliza ikiwa ni jambo la hekima kuendelea kumutumikia Yehova na kuwakisha hasira ya wenye mamlaka. Usisahau kwamba imani katika Mungu ndilo jambo linaloweza kukusaidia usimuogope mwanadamu. (Soma Methali 29:25.) Yehova anauliza hivi: ‘Sababu gani umuogope mwanadamu anayeweza kufa ambaye atakufa, na mwanadamu ambaye atafanywa kuwa majani mabichi tu?’—Isa. 51:12, 13.

9 Weka Baba yako Mweza-Yote katika akili. Yeye anaona wale wanaoteswa bila sababu na viongozi wabaya, anajitia pa nafasi yao na anawakomboa. (Kut. 3:7-10) Hata ikiwa unaweza kutetea imani yako mbele ya viongozi wenye mamlaka, ‘usihangaike juu ya jambo utakalosema ao jinsi utakavyolisema; kwa maana utapewa jambo la kusema katika saa hiyo.’ (Mt. 10:18-20) Watawala wanadamu hawako kitu mbele ya Yehova. Kwa kufanya imani yako iwe nguvu sasa, unaweza kumuona Yehova kama Mutu anayeonekana na aliye tayari kukusaidia.

ALIONYESHA IMANI KATIKA AHADI ZA MUNGU

10. (a) Ni maagizo gani ambayo Yehova aliwatolea Waisraeli katika mwezi wa Nisani ya mwaka wa 1513? (b) Sababu gani Musa alitii maagizo ya Mungu?

10 Katika mwezi wa Nisani ya mwaka wa 1513 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, Yehova aliwaambia Musa na Haruni watolee Waisraeli maagizo haya ya pekee: Muchague kondoo-dume ao mbuzi mwenye afya nzuri, mumuchinje, na mupakae damu yake kwenye nguzo za milango yenu. (Kut. 12:3-7) Musa aliitikia namna gani? Baadaye, mutume Paulo aliandika hivi: ‘Kwa imani alifanya sherehe ya Pasaka na upakaji wa damu, ili muangamizaji asiwaguse wazaliwa wao wa kwanza.’ (Ebr. 11:28) Musa alijua kwamba Yehova ni mwenye kutegemeka na alionyesha imani katika ahadi ya Yehova ya kuwaua wazaliwa wa kwanza katika Misri.

11. Sababu gani Musa aliwatolea wengine maagizo?

11 Inaonekana kwamba watoto wa Musa walikuwa Midiani, mbali na ‘muangamizaji.’ * (Kut. 18:1-6) Lakini, kwa kuwa alimutii Yehova, yeye alitoa maagizo hayo kwa familia ya Waisraeli wengine ambao watoto wao walikuwa katika hatari. Uzima ulikuwa katika hatari, na Musa aliwapenda Waisraeli wenzake. Biblia inasema: “Papo hapo, Musa akawaita wanaume wote na wazee wa Israeli na kuwaambia: . . . ‘Muchinje munyama wa Pasaka.’”—Kut. 12:21.

12. Yehova ametuagiza tutolee watu ujumbe gani wa maana sana?

12 Kwa musaada wa malaika, watu wa Yehova wanatangaza ujumbe huu wa maana sana: ‘Muogopeni Mungu na kumupa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yake imefika, na kwa hiyo muabuduni Yeye aliyezifanya mbingu na dunia na bahari na chemchemi za maji.’ (Ufu. 14:7) Huu ndio wakati wa kutangaza ujumbe huo. Tunapaswa kuwaonya majirani wetu watoke katika Babiloni Mukubwa, ili ‘wasipokee sehemu ya mapigo yake.’ (Ufu. 18:4) “Kondoo wengine” wanajiunga na Wakristo watiwa-mafuta ili kuwasihi wale ambao wametengwa na Mungu ‘wapatanishwe pamoja’ naye.​—Yoh. 10:16; 2 Kor. 5:20.

Imani katika ahadi za Yehova itaongeza hamu yako ya kuhubiri habari njema (Ona fungu la 13)

13. Ni jambo gani litaongeza hamu yetu ya kuhubiri habari njema?

13 Tuko hakika kwamba “saa ya hukumu” imefika kabisa. Na tuna imani kwamba Yehova  ana sababu nzuri za kusema kwamba kazi ya kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi inapaswa kufanywa kwa uharaka sana. Katika maono, mutume Yohana ‘aliona malaika wanne wakisimama juu ya pembe ine za dunia, wakizishika sana zile pepo ine za dunia.’ (Ufu. 7:1) Kwa imani, je, unawaona wale malaika wakiwa karibu kuachilia zile pepo za uharibifu za ziki kubwa juu ya ulimwengu huu? Ikiwa unawaona malaika hao kupitia macho yako ya imani, utakuwa tayari kuhubiri habari njema bila kuogopa.

14. Ni jambo gani linalotuchochea ‘tumuonye muovu ili aiache njia yake ya uovu’?

14 Leo, Wakristo wa kweli wanafurahia urafiki pamoja na Yehova na tumaini lao la uzima wa milele. Hata hivyo, tunajua kwamba ni daraka letu ‘kumuonya muovu aiache njia yake ya uovu ili kumuhifazi hai [ao aendelee kuishi].’ (Soma Ezekieli 3:17-19.) Bila shaka, hatuhubiri tu ili kuepuka hatia ya damu. Tunafanya hivyo kwa sababu tunamupenda Yehova na majirani wetu. Katika mufano wake wa Musamaria, Yesu alionyesha maana kabisa ya upendo na huruma. Tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Ninawasikilia watu huruma kama yule Musamaria kwa kuwahubiria?’ Bila shaka, hatupendi kuwa hata kidogo kama kuhani na Mulawi wa mufano huo kwa kujitafutia visababu ili tusiwahubirie wengine. (Lu. 10:25-37) Imani katika ahadi za Mungu na upendo kwa jirani vitatuchochea tuwe na mengi ya kufanya katika kazi ya kuhubiri kwa kuwa tungali na wakati wa kufanya hivyo.

“WALIPITA KATIKA BAHARI NYEKUNDU”

15. Sababu gani Waisraeli waliona kwamba hawataponyoka?

15 Imani ya Musa katika “Yeye asiyeonekana” ilimusaidia wakati Waisraeli  walipokuwa katika hatari kisha kuondoka Misri. Biblia inasema hivi: ‘Wana wa Israeli wakaanza kuinua macho yao, na tazama, Wamisri walikuwa wakipiga mwendo wakiwafuatilia; na wana wa Israeli wakaogopa sana na kuanza kumulilia Yehova.’ (Kut. 14:10-12) Bila shaka, Waisraeli wangepaswa kutazamia jambo hilo. Kwa sababu Yehova alikuwa amesema hivi: ‘Nitauacha moyo wa Farao uwe mukaidi [ao mugumu], naye hakika atawafuatilia wao nami nitajipatia utukufu kupitia kwa Farao na majeshi yake yote; nao Wamisri watajua hakika kwamba mimi ni Yehova.’ (Kut. 14:4) Hata hivyo, waliona tu yale ambayo macho ya mwanadamu yanaweza kuona, ni kusema, mbele yao, Bahari Nyekundu ambayo hawawezi kuvuka; nyuma yao, magari ya Farao yanayokimbia mbio sana; na muchungaji wao mwenye miaka 80 anayewaongoza! Waliona kwamba hawataponyoka.

16. Namna gani imani ilimutia Musa nguvu kwenye Bahari Nyekundu?

16 Hata hivyo Musa hakuyumba-yumba. Sababu gani? Kwa sababu macho yake ya imani yaliona jambo fulani lenye nguvu zaidi kuliko bahari ao majeshi ya Farao. Aliona “wokovu wa Yehova,” na alijua kwamba Yehova angewapigania Waisraeli. (Soma Kutoka 14:13, 14.) Imani ya Musa iliwatia moyo watu wa Mungu. Biblia inasema hivi: ‘Kwa imani walipita katikati ya Bahari Nyekundu kana kwamba ni juu ya inchi kavu, lakini Wamisri waliposubutu kuipitia wakamezwa.’ (Ebr. 11:29) Baadaye, ‘watu wakaanza kumwogopa Yehova na kuwa na imani katika Yehova na katika Musa mutumishi wake.’—Kut. 14:31.

17. Ni matukio gani ya wakati ujao yatakayojaribu imani yetu?

17 Hivi karibuni, maisha yetu yataonekana kwamba yako katika hatari. Kwenye sehemu ya mwisho ya ziki kubwa, serikali za ulimwengu huu zitakuwa zimeharibu na kuangamiza dini zote ambazo zilionekana kuwa kubwa na zilizokuwa na waamini wengi kuliko sisi. (Ufu. 17:16) Yehova alitabiri kwamba watu wake wataonekana kuwa kama hawana mutu wa kuwapigania, aliposema hivi: ‘Inchi iliyowazi . . . , iliyo bila ukuta, na bila hata milango na mapingo [ao kipande cha muti cha kufungia mulango kwa ndani].’ (Eze. 38:10-12, 14-16) Kwa macho ya mwanadamu itaonekana kwamba watumishi wa Mungu hawataponyoka hata kidogo. Utatenda namna gani?

18. Eleza sababu gani hatutahitaji kuyumba-yumba wakati wa ziki kubwa.

18 Hatutahitaji kuyumba-yumba kwa sababu ya woga. Sababu gani? Kwa sababu Yehova alitabiri kwamba watu wake watashambuliwa. Tena, ametabiri yale yatakayotokea siku hiyo. “‘Katika siku hiyo, katika siku ambayo Gogu atakuja juu ya inchi ya Israeli,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘kwamba gazabu [ao hasira] yangu itapanda puani mwangu. Na katika ukali wangu, katika moto wa gazabu yangu, nitalazimika kusema.’” (Eze. 38:18-23) Kisha, Mungu atawaharibu wale wote wanaotaka kushambulia watu wa Yehova. Imani yako katika “ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha” itakusaidia ‘kuona wokovu wa Yehova’ na kuendelea kubaki mushikamanifu.​—Yoe. 2:31, 32.

19. (a) Uhusiano kati ya Yehova na Musa ulikuwa wa karibu sana namna gani? (b) Ikiwa unamutambua Yehova katika njia zako, utapata baraka gani?

19 Uwe tayari sasa kwa ajili ya matukio hayo yenye kufurahisha kwa kuendelea ‘kuwa imara kama mutu anayemuona Yeye asiyeonekana’! Fanya uhusiano wako pamoja na Yehova Mungu uwe nguvu kwa kujifunza na kusali kwa ukawaida. Musa alikuwa na uhusiano kama huo, na Yehova alimutumia kwa njia kubwa hivi kwamba Biblia inasema kwamba Yehova alimujua “uso kwa uso.” (Kum. 34:10) Musa alikuwa nabii mukubwa. Hata hivyo, kwa imani wewe pia unaweza kumujua Yehova sana kama mutu unayemuona kabisa. Ikiwa unaendelea kumutambua Yehova “katika njia zako zote,” kama vile Neno la Mungu linavyokutia moyo kufanya, “atanyoosha mapito yako.”—Met. 3:6.

^ fu. 11 Bila shaka Yehova alituma malaika ili waangamize Wamisri.​—Zab. 78:49-51.