Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hakuna Anayeweza Kuwatumikia Mabwana Wawili

Hakuna Anayeweza Kuwatumikia Mabwana Wawili

Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili . . . Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.”MT. 6:24.

1-3. (a) Watu wengi wanakabili matatizo gani ya kifedha, na baadhi yao hujaribu kuyatatua jinsi gani? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.) (b) Wazazi wanaohama huwa na mahangaiko gani kuhusu kulea watoto wao?

“MUME wangu, James, alirudi nyumbani kila siku akiwa amechoka sana baada ya kazi. Isitoshe, mshahara wake haukutosha mahitaji yetu ya kila siku,” akasema Marilyn. * Aliendelea kusema hivi: “Nilitaka kumpunguzia mzigo na kumnunulia mwana wetu, Jimmy, baadhi ya vitu vizuri ambavyo wanashule wenzake walikuwa navyo.” Marilyn alitaka pia kuwasaidia watu wao wa ukoo na kuweka pesa zitakazowasaidia wakati ujao. Tayari rafiki zake wengi walikuwa wamehamia nchi nyingine kufanya kazi ili wapate pesa zaidi. Hata hivyo, alikuwa na wasiwasi kuhusu uamuzi wake wa kuhamia nchi nyingine. Kwa nini?

2 Marilyn aliogopa kuiacha familia yake aliyoithamini sana na kuacha ratiba yao ya mambo ya kiroho. Hata hivyo, akawaza kwamba wengine wamehamia nchi nyingine kwa muda na familia zao zinaonekana zinaendelea vizuri kiroho. Hata hivyo, alifikiria pia jinsi ambavyo angemlea Jimmy akiwa mbali. Je, angefanikiwa kumlea mwana wake “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova” kwa kutumia Intaneti?—Efe. 6:4.

3 Marilyn alitafuta ushauri. Mume wake alimwambia kwamba  hangependa ahamie nchi nyingine, lakini hatamzuia kufanya hivyo. Wazee na wengine kutanikoni walimshauri asiende, lakini dada kadhaa walimtia moyo ahamie nchi nyingine. Dada hao walimwambia hivi: “Nenda ikiwa unaipenda familia yako. Unaweza kuendelea kumtumikia Yehova huko.” Ijapokuwa alikuwa na shaka, Marilyn alimwacha James na Jimmy na kuhamia nchi nyingine ili kufanya kazi. Aliwaahidi hivi: “Nitarudi karibuni.”

WAJIBU WA FAMILIA NA KANUNI ZA BIBLIA

4. Kwa nini watu wengi huhamia nchi nyingine? Na mara nyingi ni nani huwatunza watoto wao?

4 Yehova hataki watumishi wake wawe maskini kabisa, na tangu zamani watu wamekuwa wakihamia maeneo mengine ili kukabiliana na umaskini. (Zab. 37:25; Met. 30:8) Ili familia yake isife njaa, Yakobo, mzee wa ukoo aliwatuma wanawe Misri kununua chakula. * (Mwa. 42:1, 2) Hata hivyo, watu wengi leo hawahamii nchi nyingine ili kukabiliana na njaa. Huenda wakafanya hivyo ili kulipa deni kubwa. Wengine huhama kwa kuwa wanatamani tu kuboresha hali ya kifedha ya familia yao. Ili kufanya hivyo, wengi huhamia eneo au nchi nyingine mbali na familia zao. Watu wengi wanapohama, wanawaacha watoto wao wadogo watunzwe na mzazi anayebaki, mtoto wao mkubwa, babu na nyanya (bibi), watu wengine wa ukoo, au marafiki. Ijapokuwa watu wengi wanaohamia nchi nyingine huhuzunika sana kumwacha mwenzi wa ndoa au watoto wao, wanahisi kwamba hawana budi kufanya hivyo.

5, 6. (a) Yesu alifundisha nini kuhusu furaha na usalama? (b) Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali kuhusu mambo gani ya kimwili? (c) Yehova anatubariki kwa njia gani?

5 Katika siku za Yesu pia, watu wengi walikuwa maskini na huenda walifikiri kwamba wangekuwa na furaha na usalama zaidi ikiwa wangepata pesa nyingi. (Marko 14:7) Lakini Yesu hakutaka watu watumaini pesa. Alitaka wamtegemee Yehova, Chanzo cha utajiri wa kudumu. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema kwamba furaha na usalama wa kweli hautegemei vitu vya kimwili au jitihada zetu, badala yake unategemea urafiki wetu pamoja na Baba yetu wa mbinguni.

6 Katika sala yake ya kielelezo, Yesu hakutufundisha tusali tupate usalama wa kifedha, alitufundisha tuombe mahitaji yetu ya kila siku, yaani, “mkate wetu kwa ajili ya siku hii.” Aliwaambia wasikilizaji wake hivi waziwazi: “Acheni kujiwekea hazina duniani . . . Badala yake, jiwekeeni hazina mbinguni.” (Mt. 6:9, 11, 19, 20) Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatubariki kama alivyoahidi. Baraka za Mungu si kibali chake tu, bali pia anahakikisha kwamba tunapata vitu tunavyohitaji kikweli. Kwa kweli, njia pekee ya kupata furaha na usalama wa kweli ni kumtegemea Baba yetu anayetujali badala ya kutegemea pesa.—Soma Mathayo 6:24, 25, 31-34.

7. (a) Yehova amewapa nani daraka la kuwalea watoto? (b) Kwa nini wazazi wote wawili wanahitaji kushirikiana katika kuwalea watoto?

7 ‘Kuutafuta kwanza uadilifu wa Mungu’ kunatia ndani kuwa na maoni kama ya Yehova kuhusu wajibu wa kutunza familia. Sheria ya Musa ina kanuni hii inayowahusu pia Wakristo: Wazazi wanahitaji kuwapa watoto wao mazoezi ya kiroho. (Soma Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.) Mungu amewapa daraka hilo wazazi, bali si babu, nyanya, au mtu mwingine yeyote. Mfalme Sulemani alisema hivi: “Mwanangu, sikiliza nidhamu ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.” (Met. 1:8) Yehova alikusudia wazazi wote wawili wawepo ili kuwaongoza na kuwafundisha watoto wao. (Met. 31:10, 27, 28) Watoto hujifunza mambo mengi, hasa mambo ya kiroho, kwa kuwasikiliza wazazi wakiongea  kumhusu Yehova kila siku na kupitia mfano wao.

MATOKEO YASIYOTARAJIWA

8, 9. (a) Inakuwaje mzazi anapoishi mbali na familia? (b) Ni madhara gani ya kihisia na kimaadili yanayotokea wazazi wanapoishi mbali na watoto wao?

8 Kabla ya kuhamia nchi nyingine, watu hujaribu kufikiria mambo watakayohitaji kudhabihu na hatari zinazohusika, lakini ni wachache tu wanaofikiria madhara ya kuiacha familia yao. (Met. 22:3) * Baada ya kuhama, Marilyn alianza kuumia sana moyoni kwa sababu ya kuiacha familia yake. Mume na mtoto wake waliumia pia. Mtoto wake, Jimmy, alimuuliza hivi tena na tena: “Kwa nini uliniacha?” Na kadiri miaka ilivyopita, Marilyn alishtuka alipogundua kwamba familia yake imebadilika. Hisia na upendo wa Jimmy kumwelekea ulipungua. Marilyn anasema hivi kwa huzuni: “Hakunipenda tena kama zamani.”

9 Wazazi wanapoishi mbali na watoto wao, wote wanaweza kuathiriwa kihisia na kimaadili. * Watoto wenye umri mdogo zaidi ndio huumia zaidi mzazi anapoishi mbali kwa muda mrefu. Marilyn alimwambia Jimmy kwamba alihamia nchi nyingine kwa faida yake. Hata hivyo, Jimmy alihisi kwamba mama amemwacha. Mwanzoni, alimkosa sana mama yake. Lakini baadaye, Jimmy hakutaka kumwona mama yake alipowatembelea. Kama ilivyo kawaida kwa watoto walioachwa, Jimmy alihisi kwamba mama yake hakustahili tena kupendwa na kuonyeshwa utii.—Soma Methali 29:15.

Huwezi kumkumbatia mtoto wako kupitia Intaneti (Tazama fungu la 10)

10. (a) Matokeo yanakuwa nini mzazi akimpa mtoto zawadi badala ya kutumia wakati pamoja naye? (b) Watoto hukosa nini mzazi akiishi mbali nao?

10 Ijapokuwa Marilyn alimtumia mwana wake pesa na zawadi ili ahisi kwamba hajamwacha, aliona kwamba alikuwa akijitenga na mtoto wake na bila kukusudia alikuwa akimfundisha kutanguliza mambo ya kimwili badala ya mambo ya kiroho na mahusiano ya familia. (Met. 22:6) Jimmy alimwambia hivi: “Usirudi. Endelea tu kunitumia zawadi.” Marilyn alianza kugundua kwamba hangeweza ‘kumlea mwana wake kupitia vyombo vya mawasiliano,’ kama vile barua, simu, au kuwasiliana naye kupitia video. Anasema hivi: “Huwezi kumkumbatia au kumbusu mtoto wako kupitia Intaneti.”

Unaweza kukabili hatari gani ukiishi mbali na mwenzi wako? (Tazama fungu la 11)

11. (a) Ndoa itaathiriwaje ikiwa wenzi wa ndoa hawaishi pamoja kwa sababu ya kazi ya kimwili? (b) Dada mmoja alitambuaje umuhimu wa kurudi ili kuishi na familia yake?

11 Uhusiano wa Marilyn na Yehova, na  uhusiano wake na mume wake, James, ulidhoofika pia. Alishirikiana na kutaniko na kuhubiri siku moja kwa juma au nyakati nyingine alishindwa kufanya hivyo, naye alilazimika kukabiliana daima na mwajiri wake aliyekuwa akimtongoza. Kwa kuwa walikuwa mbali wasiweze kutegemezana wakati wa matatizo, Marilyn na James walisitawisha mahusiano ya kimahaba nje ya ndoa na karibu wafanye uzinzi. Marilyn aligundua kwamba ingawa yeye na mume wake hawakufanya uzinzi, kuishi mbali kuliwafanya wasifuate shauri la Biblia kuhusu kutosheleza mahitaji ya kihisia na ya kingono ya mwenzi wao wa ndoa. Hawakuweza kuzungumza wakati wowote, kutazamana, kutabasamu, kushikana mikono kwa wororo, kukumbatiana kwa uchangamfu, ‘kuonyeshana mapenzi,’ au kumpa mwenzi wao “haki” ya ndoa. (Wim. 1:2; 1 Kor. 7:3, 5) Pia hawakuweza kumwabudu Yehova kikamili wakiwa na mwana wao. Marilyn anasema hivi: “Niliposikia katika kusanyiko kwamba ni muhimu sana kufanya ibada ya familia kwa ukawaida ili tuokoke siku kuu ya Yehova, niliona wazi kwamba ninahitaji kurudi nyumbani. Nilihitaji kuanza kujenga tena hali yangu ya kiroho na maisha yangu ya familia.”

MASHAURI MAZURI NA MABAYA

12. Ni mashauri gani ya Kimaandiko tunayoweza kuwapa wale wanaoishi mbali na familia zao?

12 Kila mtu alikuwa na maoni tofauti kuhusu uamuzi wa Marilyn wa kurudi nyumbani. Wazee wa kutaniko katika nchi aliyohamia walimpongeza kwa sababu ya imani na ujasiri wake. Hata hivyo, baadhi ya wale waliohamia nchi nyingine mbali na wenzi wao wa ndoa na familia yao hawakufurahishwa na uamuzi wake. Badala ya kuiga mfano wake mzuri, walijaribu kumshauri asirudi nyumbani. Walimwambia hivi: “Utarudi huku hivi karibuni. Utapataje riziki ukirudi nyumbani?” Badala ya kusema maneno kama hayo yenye kuvunja moyo, Wakristo wenzetu wanapaswa “kuziamsha akili za wanawake vijana wawapende waume zao, wawapende watoto wao, wawe . . . wafanyakazi nyumbani,” yaani, katika nyumba zao wenyewe, “ili neno la Mungu lisitukanwe.”—Soma Tito 2:3-5.

13, 14. Kwa nini imani inahitajiwa ili kumtanguliza Yehova badala ya mapendezi ya watu wa ukoo? Toa mfano.

13 Wengi wanaoacha familia zao na kuhamia nchi nyingine ili kufanya kazi, wamelelewa katika nchi zenye utamaduni unaoheshimu sana desturi na mapendezi ya watu wa ukoo, hasa wazazi. Kwa kweli, Mkristo anaonyesha imani anapoamua kumpendeza Yehova badala ya kufuata desturi au mapendezi ya familia.

14 Carin anasema hivi: “Mwana wetu Don alipozaliwa, mimi na mume wangu tulikuwa  tukifanya kazi katika nchi nyingine, na nilikuwa nimeanza tu kujifunza Biblia. Kila mtu katika familia yetu alitarajia kwamba ningempeleka Don nyumbani ili wazazi wangu wamlee hadi hali yetu ya kiuchumi itakapokuwa nzuri.” Carin aliposisitiza kwamba anataka kumlea Don, watu wa ukoo pamoja na mume wake walimcheka na kusema kwamba yeye ni mvivu. Carin anasema hivi: “Kusema kweli, wakati huo sikuelewa kikamili kwa nini haikufaa kumpeleka Don kwa wazazi wangu ili wamlee kwa miaka michache. Hata hivyo, nilijua kwamba tukiwa wazazi, Yehova ametupatia kazi ya kumlea mwana wetu.” Carin alipokuwa mjamzito tena, mume wake asiye mwamini alisisitiza atoe mimba hiyo. Lakini uamuzi mzuri aliofanya Carin mwanzoni uliimarisha imani yake, na kwa mara nyingine tena alishikamana na sheria za Yehova. Sasa yeye, mume wake, na watoto wao, wanafurahi kwamba waliendelea kukaa pamoja. Huenda mambo yangekuwa tofauti kabisa ikiwa Carin angewapeleka watoto wake wakalelewe na watu wengine.

15, 16. (a) Dada mmoja aliyelelewa na watu wa ukoo alikabili hali gani? (b) Kwa nini aliamua kumlea binti yake?

15 Shahidi anayeitwa Vicky anasema hivi: “Nililelewa na nyanya yangu kwa miaka kadhaa na dada yangu mdogo alilelewa na wazazi wangu. Niliporudi nyumbani, upendo wangu kuwaelekea wazazi wangu ulikuwa umepungua. Dada yangu alikuwa na uhusiano wa karibu na wazazi wetu, aliwakumbatia na kuongea nao kwa uhuru. Hata hivyo, sikuwa na uhusiano wa karibu na wazazi wangu, na hata nikiwa mtu mzima bado si rahisi kuwaeleza ninavyohisi. Mimi na dada yangu tumewahakikishia wazazi wetu kwamba tutawatunza watakapozeeka. Lakini nitawatunza ili kutimiza wajibu tu, tofauti na dada yangu atakayewatunza kwa sababu anawapenda.”

16 Vicky anaendelea kusema hivi: “Sasa mama yangu anataka kumlea binti yangu kama nyanya alivyonilea. Nilikataa kwa busara. Mimi na mume wangu tunataka kumlea mtoto wetu katika njia za Yehova. Singependa kuharibu uhusiano wangu na binti yangu.” Vicky ametambua kwamba njia pekee ya kufanikiwa ni kumtanguliza Yehova na kanuni zake badala ya mali au mapendezi ya watu wa ukoo. Yesu alisema hivi waziwazi: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili,” Mungu na Utajiri.—Mt. 6:24; Kut. 23:2.

YEHOVA ‘HUFANIKISHA’ JITIHADA ZETU

17, 18. (a) Sikuzote Wakristo wana uhuru wa kuchagua nini? (b) Ni maswali gani tutakayozungumzia katika makala inayofuata?

17 Baba yetu, Yehova, ameazimia kutusaidia kupata mahitaji yetu ya lazima ikiwa tunatanguliza masilahi ya Ufalme na uadilifu wake maishani mwetu. (Mt. 6:33) Hivyo, sikuzote Wakristo wa kweli wana uhuru wa kuchagua jambo la kutanguliza. Yehova anaahidi kuandaa “njia ya kutokea” na hivyo hatuhitaji kulegeza kanuni za Biblia hata tukikabili hali yoyote ngumu. (Soma 1 Wakorintho 10:13.) Tukiendelea ‘kumngojea Yehova kwa kutamani’ na ‘tukimtegemea’ kwa kusali ili atupatie hekima na mwongozo wake na tukifuata amri na kanuni zake, yeye “mwenyewe atatenda.” (Zab. 37:5, 7) Atatubariki kabisa tukijitahidi kutoka moyoni kumtumikia yeye peke yake akiwa Bwana wa pekee wa kweli. Tukimtanguliza, ‘atafanikisha’ maisha yetu.—Linganisha na Mwanzo 39:3.

18 Tunaweza kufanya nini ili kuondoa madhara yanayosababishwa na familia kutengana? Tunaweza kuchukua hatua gani zinazofaa ili kuandaa mahitaji ya kimwili ya familia yetu bila kuishi mbali nao? Na tunawezaje kuwatia wengine moyo kwa upendo kufanya maamuzi yanayofaa kuhusiana na jambo hilo? Makala inayofuata itazungumzia maswali hayo.

^ fu. 1 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 4 Kila mara waliposafiri kwenda Misri, huenda wana wa Yakobo walikaa mbali na familia zao kwa muda usiozidi majuma matatu. Baadaye, Yakobo na wanawe walihamia Misri pamoja na wake na watoto wao.—Mwa. 46:6, 7.

^ fu. 8 Tazama makala yenye kichwa “Kuhamia Nchi Nyingine​—Matarajio na Mambo Halisi” katika gazeti la Amkeni! la Februari 2013.

^ fu. 9 Ripoti kutoka nchi mbalimbali zinaonyesha kwamba kuishi mbali na mwenzi wa ndoa au watoto ili kufanya kazi kumesababisha matatizo makubwa kama vile, wenzi wa ndoa kukosa uaminifu, ngono kati ya watu wa jinsia moja, au ngono kati ya watu wa ukoo, watoto kuwa na tabia mbaya, hasira, mahangaiko, kushuka moyo, kutaka kujiua, na kutofanya vizuri katika masomo yao.