Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe Hodari—Yehova Ni Msaidizi Wako!

Uwe Hodari—Yehova Ni Msaidizi Wako!

“Tuwe hodari na kusema: ‘Yehova ni msaidizi wangu.’”—EBR. 13:6.

1, 2. Wahamiaji wengi hukabili changamoto gani wanaporudi nyumbani? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

“NILIPATA pesa nyingi sana nilipokuwa nikifanya kazi katika nchi nyingine. Hata hivyo, nilipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, nilitambua kwamba nina daraka muhimu zaidi la kuitunza familia yangu kiroho wala si kimwili tu. Hivyo, nilirudi nyumbani,” anasema Eduardo. *Efe. 6:4.

2 Eduardo alijua kwamba Yehova alipendezwa na uamuzi wake wa kurudi ili kuishi na familia yake. Hata hivyo, sawa na Marilyn aliyetajwa katika makala iliyotangulia, Eduardo alihitaji kujitahidi sana kurekebisha uhusiano wake na familia yake. Alikabili pia changamoto ya kuiandalia familia yake mahitaji yao chini ya hali ngumu zaidi ya kiuchumi. Angepataje riziki? Washiriki wengine wa kutaniko wangemsaidiaje?

KUREKEBISHA HALI YA KIROHO NA MAISHA YA FAMILIA

3. Watoto huathiriwaje mzazi anapoishi mbali?

3 Eduardo anasema hivi: “Nilitambua kwamba niliwapuuza watoto wangu walipohitaji sana mwongozo na upendo. Sikuwapo ili kuwasomea masimulizi ya Biblia, kusali nao, kuwakumbatia,  na kucheza nao.” (Kum. 6:7) Anna, binti yake mkubwa, anasema hivi: “Baba alipoondoka nyumbani sikuhisi nikiwa salama. Aliporudi, tulimwona kama mgeni tu. Aliponikumbatia, nilihisi ni kana kwamba ninakumbatiwa na mtu nisiyemjua.”

4. Kwa nini mume hawezi kutimiza daraka lake akiwa kichwa cha familia ikiwa anaishi mbali?

4 Baba hawezi kutimiza daraka lake akiwa kichwa cha familia ikiwa anaishi mbali. Ruby, mke wa Eduardo, anasema hivi: “Nililazimika kutimiza daraka la Mama na Baba hivyo nikazoea kufanya maamuzi mengi katika familia. Eduardo aliporudi, nilihitaji kujifunza kujitiisha chini yake nikiwa mke Mkristo. Hata sasa, nyakati nyingine ninahitaji kujikumbusha kwamba mume wangu yupo.” (Efe. 5:22, 23) Eduardo anaongezea hivi: “Binti zangu walizoea kumwomba mama yao ruhusa kabla ya kufanya jambo fulani. Tukiwa wazazi, tuligundua kwamba watoto wetu walihitaji kuona kwamba tuna umoja, nami nilihitaji kujifunza kuiongoza familia yangu kwa njia ya Kikristo.”

5. Baba mmoja alianzaje kurekebisha uhusiano wake na familia yake? Matokeo yalikuwa nini?

5 Eduardo aliazimia kufanya yote awezayo ili kurekebisha uhusiano wake pamoja na familia yake na kuimarisha hali yao ya kiroho. Anasema hivi: “Lengo langu lilikuwa kuwafundisha kweli watoto wangu kwa maneno na matendo, yaani, kuonyesha kwamba ninampenda Yehova badala ya kusema tu.” (1 Yoh. 3:18) Je, Yehova alimbariki Eduardo kwa sababu ya kutenda kwa imani? Anna anasema hivi: “Ninatiwa moyo sana ninapomwona akifanya yote awezayo ili kuwa baba mzuri na kujitahidi kuwa tena na uhusiano wa karibu pamoja nasi. Tulifurahi pia kumwona akijitahidi kufikia mapendeleo kutanikoni. Ulimwengu ulijaribu kututenganisha na Yehova. Lakini tuliona wazazi wetu wakichukua kweli kwa uzito, nasi pia tulijitahidi kufanya hivyo. Baba alituahidi kwamba hatatuacha tena, na hajatuacha. Ikiwa angetuacha, huenda leo nisingekuwa katika tengenezo la Yehova.”

KUKUBALI MAJUKUMU

6. Baadhi ya wazazi walijifunza nini kuhusu kulea watoto katika kipindi cha vita?

6 Mambo yaliyoonwa yanaonyesha kwamba wakati wa vita katika nchi za Balkani, watoto wa Mashahidi wa Yehova walikuwa na furaha licha ya kwamba waliishi chini ya hali ngumu. Kwa nini? Kwa sababu wazazi ambao hawangeweza kwenda kazini walibaki nyumbani na kujifunza, kucheza, na kuzungumza nao. Tunajifunza nini? Wazazi wanahitaji kutumia wakati pamoja na watoto wao badala ya kuwapa tu pesa au zawadi. Kwa kweli, kama Neno la Mungu linavyosema, watoto watanufaika wakitunzwa na kuzoezwa na wazazi wao.—Met. 22:6.

7, 8. (a) Baadhi ya wazazi wanaorudi wanafanya kosa gani? (b) Wazazi wanaorudi wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia watoto wao kushinda hisia zisizofaa?

7 Inasikitisha kwamba baadhi ya wazazi wanaporudi na kukataliwa na watoto wao, wanasema hivi: “Mbona huna shukrani licha ya kwamba nimejidhabihu sana kwa ajili yako?” Hata hivyo, huenda watoto wao wana mtazamo huo usiofaa kwa sababu wazazi waliwaacha. Mzazi atafanya nini ili kurekebisha hali hiyo?

8 Mwombe Yehova akusaidie kuelewa vizuri hisia za familia yako. Kisha, unapozungumza na familia yako, kubali kwamba umechangia tatizo hilo. Kuwaomba msamaha kutoka moyoni kunaweza kusaidia. Mwenzi wako na watoto wanapoona kwamba unajitahidi sana kurekebisha hali, watatambua unyoofu wako. Ukiazimia na kuonyesha subira, huenda familia yako ikaanza tena kukupenda na kukuheshimu.

‘KUWAANDALIA MAHITAJI WALIO WAKO MWENYEWE’

9. Kwa nini hatuhitaji kutafuta vitu vingi vya kimwili ili ‘tuwaandalie mahitaji walio wetu’?

9 Mtume Paulo aliagiza kwamba Wakristo waliozeeka wakishindwa kupata riziki, watoto wao na wajukuu watahitaji “kuwalipa wazazi na wazazi wa wazazi wao malipo yanayowastahili.” Lakini Paulo aliwahimiza pia Wakristo wote waridhike na mahitaji yao ya kila siku, yaani, chakula, mavazi, na makao. Hatupaswi kujitahidi daima kuwa na maisha ya hali ya juu au kupata usalama wa kifedha. (Soma 1 Timotheo 5:4, 8; 6:6-10.) Ili ‘kuwaandalia mahitaji walio wake mwenyewe,’ Mkristo hahitaji kutafuta utajiri katika ulimwengu huu utakaopitilia mbali hivi karibuni. (1 Yoh. 2:15-17) Hatupaswi kuruhusu “nguvu za udanganyifu za utajiri” au “mahangaiko ya maisha” yahatarishe azimio la familia yetu la ‘kuushika imara uzima ulio wa kweli’ katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu!—Marko 4:19; Luka 21:34-36; 1 Tim. 6:19.

10. Tunawezaje kuonyesha hekima ya Mungu inapohusu madeni?

10 Yehova anajua kwamba tunahitaji kiasi fulani cha pesa. Hata hivyo, pesa haziwezi kutulinda na kututegemeza kama hekima ya Mungu inavyoweza kutulinda. (Mhu. 7:12; Luka 12:15) Watu wengi hupuuza hatari ya kwenda kufanya kazi katika nchi nyingine na uhakika wa kwamba huenda wasipate pesa. Ukweli ni kwamba kuna hatari kubwa sana. Watu wengi hurudi nchini mwao wakiwa na madeni makubwa hata zaidi. Badala ya kuwa huru kumtumikia Mungu, wanawatumikia tu wale wanaowadai pesa. (Soma Methali 22:7.) Jambo la hekima ni kuepuka madeni.

11. Kufuata bajeti kunaisaidiaje familia kupunguza matatizo ya kiuchumi?

11 Eduardo aligundua kwamba alihitaji kuwa na maoni yanayofaa kuhusu pesa ili akae na familia yake kama alivyoazimia. Yeye na mke wake walipanga bajeti ya vitu walivyohitaji kikweli. Ni kweli kwamba hawakuzoea bajeti kama hiyo yenye vitu vichache. Hata hivyo, wote walishirikiana kwa kutonunua vitu wasivyohitaji. * Eduardo anasema hivi: “Kwa mfano, niliwapeleka watoto wangu katika shule nzuri ya serikali badala ya shule ya kibinafsi.” Eduardo na familia yake walisali ili apate kazi ya kimwili ambayo haingevuruga ratiba yao ya kiroho. Yehova alijibuje sala zao?

12, 13. Baba mmoja alichukua hatua gani zinazofaa ili kuandaa mahitaji ya familia yake? Yehova alibarikije azimio lake la kuishi maisha rahisi?

12 Eduardo anakumbuka hivi: “Mambo hayakuwa rahisi miaka miwili ya kwanza. Pesa zilianza kupungua, mshahara wangu mdogo haukuweza kulipia gharama zetu zote, na nilichoka kimwili. Hata hivyo, tuliweza kuhudhuria mikutano yote na kushiriki pamoja katika huduma.” Eduardo aliazimia kutokubali kazi yoyote itakayomfanya aiache familia yake kwa miezi au miaka kadhaa. Anasema hivi: “Badala yake, nilijifunza kazi tofauti-tofauti ili nifanye kazi yoyote ninayopata.”

Je unaweza kujifunza kufanya kazi za aina mbalimbali ili kuitegemeza familia yako? (Tazama fungu la  12)

13 Eduardo alilazimika kulipa riba kubwa kwa sababu alilipa madeni yake kidogo-kidogo. Hata hivyo, aliona kwamba kuwa na familia yake, kama Yehova anavyotaka wazazi wafanye, hakuwezi kulinganishwa na riba anayolipa. Eduardo anasema hivi: “Ingawa sasa ninapata mshahara ambao hauzidi asilimia 10 ya mshahara niliopata katika nchi nyingine, hatujawahi kulala njaa. ‘Mkono wa Yehova si mfupi.’ Hata tuliamua kufanya upainia. Jambo la kushangaza ni kwamba baada ya kufanya hivyo, hali yetu ya kifedha iliboreka na ikawa rahisi zaidi kupata mahitaji muhimu ya kimwili.”—Isa. 59:1.

 KUKABILIANA NA SHINIKIZO LA FAMILIA

14, 15. Familia zinawezaje kukabiliana na shinikizo la kutafuta mali badala ya kutanguliza mambo ya kiroho? Na mfano wao mzuri huenda ukawa na matokeo gani?

14 Katika nchi nyingi, watu wanahisi kwamba wana daraka la kuwapa pesa na zawadi watu wao wa ukoo na marafiki. Eduardo anasema hivi: “Hiyo ni sehemu ya utamaduni wetu, nasi tunafurahia sana kutoa. Hata hivyo kuna mipaka. Kwa busara, mimi huwaambia watu wangu wa ukoo kwamba nitawasaidia kadiri niwezavyo bila kuhatarisha hali yetu ya kiroho na kuvuruga ratiba ya familia yangu.”

15 Wale wanaokataa kuacha familia zao ili kufanya kazi nchi nyingine na pia wahamiaji wanaorudi nyumbani, mara nyingi hudhihakiwa na kukasirikiwa na watu wa ukoo waliotamauka kwa sababu walitarajia kwamba wangewaandalia riziki. Baadhi yao husema kwamba watu hao hawapendi familia zao. (Met. 19:6, 7) Anna, binti ya Eduardo anasema hivi: “Hata hivyo, tunapokataa kutafuta mali ili kufuatilia mambo ya kiroho, hatimaye baadhi ya watu wetu wa ukoo huenda wakatambua kwamba maisha yetu ya Kikristo ni muhimu sana. Lakini watajuaje jambo hilo tukifanya wanavyotaka?”—Linganisha na 1 Petro 3:1, 2.

KUDHIHIRISHA IMANI KATIKA MUNGU

16. (a) Mtu anawezaje ‘kujidanganya mwenyewe kwa mawazo yasiyo ya kweli’? (Yak. 1:22) (b) Yehova hubariki maamuzi ya aina gani?

16 Dada mmoja aliyehamia nchi nyingine yenye ufanisi na kuwaacha watoto na mwenzi wake, aliwaambia hivi wazee wa kutaniko lake jipya: “Familia yetu imejidhabihu sana ili nije hapa. Hata mume wangu aliacha pendeleo la kuwa mzee. Hivyo, ninatumaini kabisa kwamba Yehova atabariki uamuzi wangu wa kuhamia hapa.” Sikuzote Yehova hubariki maamuzi yanayoonyesha kwamba tuna imani kumwelekea, lakini atabariki namna gani uamuzi usiopatana na mapenzi yake, hasa ikiwa tunaacha mapendeleo matakatifu kwa sababu zisizofaa?—Soma Waebrania 11:6; 1 Yohana 5:13-15.

17. Kwa nini tunahitaji kutafuta mwongozo wa Yehova kabla ya kufanya maamuzi, na tutafanyaje hivyo?

17 Tafuta mwongozo wa Yehova kabla ya kufanya maamuzi wala si baada ya kufanya maamuzi. Sali ili akupe roho yake takatifu,  hekima, na mwongozo. (2 Tim. 1:7) Jiulize hivi: ‘Je, niko tayari kumtii Yehova chini ya hali zozote zile? Hata nikiteswa?’ Ikiwa ni hivyo, je, uko tayari kumtii hata ikimaanisha kuishi maisha rahisi zaidi? (Luka 14:33) Waombe wazee mashauri na ufuate mashauri yao yanayotegemea Biblia. Ukifanya hivyo, utaonyesha kwamba unaamini ahadi ya Yehova ya kukusaidia. Wazee hawatakufanyia maamuzi, lakini wanaweza kukusaidia kufanya maamuzi ambayo mwishowe yatakuletea furaha.—2 Kor. 1:24.

18. Ni nani mwenye daraka la kuiandalia familia? Wakristo wengine wanaweza kusaidia katika hali gani?

18 Yehova amempa kichwa cha familia “mzigo” wa kuiandalia familia yake mahitaji ya kila siku. Tunapaswa kuwapongeza na kusali kwa ajili ya wote wanaotimiza daraka lao bila kumwacha mwenzi au watoto wao hata ingawa wanashinikizwa na kushawishiwa kufanya hivyo. Hali zisizotarajiwa, kama vile misiba au matatizo ya kiafya, zinatupa nafasi ya kuonyeshana upendo wa kweli wa Kikristo na hisia-mwenzi. (Gal. 6:2, 5; 1 Pet. 3:8) Je, unaweza kutoa michango ya pesa wakati wa dharura au kumsaidia Mkristo mwenzako kupata kazi katika eneo lenu? Ukifanya hivyo, unaweza kupunguza mkazo ambao huenda anakabili wa kutaka kuiacha familia ili kutafuta kazi katika eneo au nchi nyingine.—Met. 3:27, 28; 1 Yoh. 3:17.

KUMBUKA KWAMBA YEHOVA NI MSAIDIZI WAKO!

19, 20. Kwa nini Wakristo wanaweza kuridhika kwa kujua kwamba Yehova atawasaidia?

19 Maandiko yanatuhimiza hivi: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu vya sasa. Kwa maana [Mungu] amesema: ‘Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.’ Hivi kwamba tuwe hodari na kusema: ‘Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa. Mwanadamu anaweza kunitenda nini?’” (Ebr. 13:5, 6) Hilo linawezekanaje?

20 Ndugu ambaye amekuwa mzee wa kutaniko kwa miaka mingi katika nchi inayositawi anasema hivi: “Mara nyingi watu husema kwamba Mashahidi wa Yehova wana furaha. Husema pia kwamba hata Mashahidi walio maskini huvaa na kuonekana wakiwa nadhifu kuliko watu wengine.” Hilo linapatana na ahadi ya Yesu kwa wale wanaotafuta kwanza Ufalme. (Mt. 6:28-30, 33) Naam, Baba yetu wa mbinguni, Yehova, anakupenda na anataka wewe na watoto wako muwe na maisha bora. “Macho yake [Yehova] yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.” (2 Nya. 16:9) Ametupatia amri zake kwa faida yetu, kutia ndani amri kuhusu maisha ya familia na mahitaji ya kimwili. Tunapozifuata, tunaonyesha kwamba tunampenda na tunamtegemea. “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.”—1 Yoh. 5:3.

21, 22. Kwa nini umeazimia kumtegemea Yehova?

21 Eduardo anasema hivi: “Ninajua kwamba sitaupata tena wakati niliopoteza nilipoishi mbali na mke na watoto wangu, lakini sikazii fikira jambo hilo. Rafiki zangu wengi ni matajiri lakini hawana furaha. Familia zao zina matatizo makubwa lakini familia yetu ina furaha sana! Ninatiwa moyo kuona ndugu wengine katika nchi hii wakitanguliza mambo ya kiroho maishani mwao ijapokuwa ni maskini. Sote tunajionea ukweli wa ahadi ya Yesu.”—Soma Mathayo 6:33.

22 Uwe hodari! Chagua kumtii na kumtegemea Yehova. Acha upendo wako kumwelekea Mungu, mwenzi wako wa ndoa, na watoto wako ukuchochee kutimiza daraka lako la kiroho kuelekea familia yako. Ukifanya hivyo, utajionea wazi kwamba ‘Yehova ni msaidizi wako.’

^ fu. 1 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 11 Tazama mfululizo wa makala zenye kichwa “Jinsi ya Kupangia Matumizi ya Pesa” katika gazeti la Amkeni! la Septemba 2011