Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Usiogope—Yehova Atakusaidia!

Usiogope—Yehova Atakusaidia!

“Uwe hodari na kusema: ‘Yehova ni musaidizi wangu.’”—EBR. 13:6.

1, 2. Watu wengi wanaohamia katika inchi zingine, wanapambana na matatizo gani wanaporudi nyumbani? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.)

NDUGU Eduardo alisema hivi: “Nilipokuwa nikitumikia katika inchi nyingine, nilikuwa na kazi nzuri na nilipata feza nyingi. Lakini nilipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, nilifikia kuelewa kwamba nilikuwa na daraka kubwa, ni kusema, kutimizia familia yangu mahitaji ya kiroho, wala si mahitaji ya kimwili tu. Kwa hiyo, nilirudia nyumbani ili nibaki na familia yangu.” *Efe. 6:4.

2 Ndugu Eduardo alijua kwamba ili amupendeze Yehova, alipaswa kurudilia familia yake. Lakini kama vile Marilyn ambaye tulizungumuzia katika habari iliyopita, Eduardo alipaswa kufanya mambo mengi ili uhusiano wake na familia yake uwe muzuri. Pia, alipambana na tatizo la kutunza bibi na watoto wake katika hali ya umaskini kabisa. Namna gani angetimiza mahitaji ya familia yake? Je, kutaniko lingewasaidia?

KUFANYA MAISHA NA HALI YA KIROHO YA FAMILIA IWE NZURI

3. Watoto wanajisikia namna gani muzazi anapoishi mbali nao?

3 Eduardo anasema hivi: “Nilielewa kwamba nilikuwa nimewaachilia watoto wangu walipokuwa na lazima zaidi ya uongozi na upendo wangu. Singeweza kuwasomea hadisi za Biblia, kusali  pamoja nao, kuwakumbatia, na kucheza pamoja nao.” (Kum. 6:7) Binti yake mukubwa, anayeitwa Anna anasema hivi: “Niliumia moyoni kwa sababu baba alikuwa mbali na sisi. Aliporudi nyumbani, tulimutambua tu kupitia sauti na sura yake. Aliponikumbatia, sikujisikia kama nilikumbatiwa na baba yangu.”

4. Sababu gani si rahisi kwa baba kuongoza vizuri familia yake anapoishi mbali?

4 Tena, baba anapokuwa mbali na familia yake, anakuwa na matatizo ya kutimiza vizuri daraka lake la ukichwa. Ruby, bibi ya Eduardo, anasema hivi: “Nilipaswa kutimiza madaraka mawili, ni kusema, daraka la baba na la mama, na nilikuwa nikichukua maamuzi mengi ya familia. Wakati Eduardo alirudi nyumbani, nilipaswa kujifunza maana kabisa ya kujitiisha. Hata sasa, wakati fulani ninapaswa kujikumbusha kwamba bwana yangu iko pamoja nami.” (Efe. 5:22, 23) Eduardo anaongezea hivi: “Binti zetu walizoea kumuendea mama yao ili kumuomba ruhusa ya kufanya mambo fulani. Mimi na bibi yangu, tulitambua kwamba tulihitaji kuungana mukono ili kulea watoto wetu, na nilipaswa kujifunza kuongoza familia yangu nikiwa Baba Mukristo.”

5. Namna gani Eduardo alifanya hali ya familia yake iwe nzuri kisha kurudi nyumbani, na matokeo yalikuwa nini?

5 Eduardo aliazimia kufanya yote anayoweza ili awe tena na uhusiano muzuri na washiriki wa familia yake na kuwasaidia wawe nguvu kiroho. Anasema hivi: “Muradi wangu ulikuwa kukazia kweli za Biblia katika mioyo ya watoto wangu kupitia maneno na matendo, wala si kusema tu kwamba ninamupenda Yehova, lakini kuonyesha hilo kwa matendo.” (1 Yoh. 3:18) Yehova alibariki jitihada za Eduardo? Binti wao Anna anasema hivi: “Nilipoona namna baba yangu alijikaza ili kuwa baba muzuri na kuwa tena karibu nasi, hilo lilisaidia sana. Alipojikaza kufikia mapendeleo katika kutaniko, tulifurahi sana. Ulimwengu ulikuwa ukijaribu kutuchochea tumuache Yehova. Lakini tulipoona wazazi wetu wakishika sana kweli, tulijaribu kuwaiga. Baba alituahidi kwamba hawezi kutuacha tena, na alitimiza ahadi yake. Ikiwa angetuacha tena, pengine singekuwa tena katika tengenezo la Yehova.”

KUBALI KOSA LAKO

6. Wazazi wengi walijifunza somo gani wakati wa vita?

6 Habari fulani zinaonyesha kwamba wakati wa vita katika maeneo ya Balkani, watoto wa Mashahidi wa Yehova walioishi huko walikuwa na furaha hata ikiwa maisha yalikuwa magumu sana. Sababu gani? Wazazi ambao hawakuenda kutumika, walibaki nyumbani na walijifunza, walicheza, na kutembea pamoja na watoto wao. Wazazi wanapata somo gani? Haitoshe tu kuwatolea watoto feza ao zawadi; jambo ambalo watoto wanahitaji sana ni kuwa pamoja na wazazi wao. Kwa hiyo, Neno la Mungu linaonyesha kwamba watoto watafaidika ikiwa wazazi wao wanawahangaikia na kuwafundisha.​—Met. 22:6.

7, 8. (a) Wazazi fulani wanafanya kosa gani wanaporudi nyumbani? (b) Namna gani wazazi wanaweza kuwasaidia watoto wao wawapende na kuwaheshimu tena?

7 Jambo la kuhuzunisha ni kwamba wazazi fulani wanaporudi nyumbani na kukutana watoto wao wanawawekea kinyongo na hawawahangaikie tena, wanawaambia hivi: “Hamushukuru hata kidogo juu ya mambo yote ambayo nimewafanyia?” Hata hivyo, ikiwa watoto wanaonyesha hali hiyo, ni kwa sababu tu wazazi wao walikuwa mbali nao. Muzazi anaweza kufanya nini ili kumaliza tatizo hilo?

8 Umuombe Yehova akusaidie uwaelewe washiriki wa familia yako. Kisha, unapozungumuza nao, tambua na ukubali makosa yako. Ukiwaomba musamaha wa kweli, hilo linaweza kusaidia. Wakati bibi ao bwana yako na watoto wanatambua kwamba unafanya yote unayoweza ili kutengeneza mambo, watakuamini kabisa. Ukiazimia kabisa kufanya hivyo kwa uvumilivu, polepole familia yako itaanza tena kukupenda na kukuheshimu.

 KUWATIMIZIA WATU WA FAMILIA MAHITAJI YAO

9. Sababu gani si lazima kutafuta sana vitu vingi vya kimwili ili kuwatimizia watu wa familia yetu mahitaji yao?

9 Mutume Paulo aliandika kwamba wakati Wakristo wenye kuzeeka hawawezi tena kujitimizia mahitaji yao, watoto wao na wajukuu wao wanapaswa ‘kuwalipa malipo yanayowastahili.’ Lakini mutume Paulo aliendelea kuwatia moyo Wakristo wote watosheke na mahitaji yao ya kila siku, ni kusema, chakula, mavazi, na makao, kuliko kuendelea kutafuta maisha ya hali ya juu ao feza nyingi kwa ajili ya wakati ujao. (Soma 1 Timotheo 5:4, 8; 6:6-10.) Ili ‘kuwaandalia [ao kuwatimizia]’ watu wa jamaa yake mahitaji yao, si lazima Mukristo ajitafutie utajiri katika ulimwengu huu ambao utaharibiwa hivi karibuni. (1 Yoh. 2:15-17) Hatupaswi kuruhusu ‘nguvu za utajiri’ ao ‘mahangaiko ya maisha’ yazuie familia yetu ‘kushika uzima ulio wa kweli’ katika ulimwengu mupya wenye haki!—Mk. 4:19; Lu. 21:34-36; 1 Tim. 6:19.

10. Sababu gani ni jambo la hekima kuepuka madeni?

10 Yehova anajua kwamba tunahitaji feza. Lakini, feza haziwezi kutulinda na kututegemeza kama vile hekima inayotoka kwa Mungu. (Mhu. 7:12; Lu. 12:15) Mara nyingi watu hawatambue garama ya kuenda kutumikia katika inchi nyingine, na hakuna uhakika kwamba watapata feza huko. Bila shaka, kuenda kutumika katika inchi nyingine kuna hatari kubwa. Watu wengi wanaohamia katika inchi nyingine wanarudia na madeni mengi. Wanakuwa watumwa wa wale waliowakopesha kuliko kumutumikia Mungu kwa uhuru. (Soma Methali 22:7.) Jambo la hekima ni kujikaza kuepuka madeni.

11. Namna gani kupangia feza kunaweza kusaidia familia?

11 Ndugu Eduardo alijua kwamba ili uamuzi wake wa kurudilia familia yake uwe na matokeo mazuri, alipaswa kutumia feza vizuri. Yeye na bibi yake walipanga namna ya kutumia vizuri feza zao ili kununua tu vitu ambavyo walihitaji kabisa. Kufanya hivyo kuliwasaidia wasinunue vitu vingi sana kama walivyokuwa wakifanya zamani. Lakini wote waliungana mukono na walitumia feza ili kununua tu vitu vya lazima. * Eduardo anasema hivi: “Kwa mufano, niliwatosha watoto wangu kwenye masomo isiyokuwa ya serikali ao ya dini na niliwaandikisha katika masomo mazuri ya serikali.” Yeye na familia yake walisali ili apate kazi ambayo haingezuia programu yao ya kumuabudu Yehova. Namna gani Yehova alijibu sala zao?

12, 13. Ni hatua gani nzuri ambazo Eduardo alichukua ili kutegemeza familia yake, na namna gani Yehova amebariki uamuzi wake wa kuendelea kuishi maisha rahisi?

12 Eduardo anasema hivi: “Katika miaka miwili ya kwanza-kwanza ilikuwa vigumu. Feza zangu zilikuwa zimepunguka na mushahara wangu mudogo haungetimiza mahitaji yetu yote, na nilikuwa sina nguvu tena. Lakini, tulikuwa tunakusanyika na kuhubiri pamoja kwa ukawaida.” Eduardo hakutaka kufikiria hata kidogo kazi yoyote ambayo ingemufanya aache tena familia yake kwa miezi ao miaka mingi. Anasema hivi: “Lakini, nilijifunza kazi mbalimbali ili, ikiwa ningekosa kazi moja, ningefanya ingine.”

Je, unaweza kujifunza kazi mbalimbali ili kutunza familia yako? (ona fungu la 12)

13 Kwa kuwa Eduardo alipaswa kulipa madeni yake polepole, alipaswa kuhangaikia sana namna ya kulipa madeni hayo. Lakini, alijikaza kulipa madeni yake yote ili awe huru kumutumikia Yehova pamoja na familia yake. Eduardo anasema hivi: “Sasa ninapata feza ndogo kuliko feza nilizokuwa nikipata katika inchi ya kigeni, lakini hatujalala njaa hata siku moja. ‘Mukono wa Yehova si mufupi.’ Kwa hiyo, tuliamua kuwa mapainia. Kisha, hali ya feza ilikuwa nzuri na ikawa rahisi sana kutunza familia yangu.”—Isa. 59:1.

 WATU WA JAMAA WANAPOKUSUMBUA

14, 15. Familia zinaweza kufanya nini watu wa jamaa wanapowasumbua watafute kwanza feza kuliko ibada ya Yehova, na matokeo yanaweza kuwa nini ikiwa tunatia Yehova pa nafasi ya kwanza?

14 Katika maeneo mengi, watu wanaona kwamba wanalazimika kuwapatia watu wa jamaa na marafiki zao feza na zawadi. Eduardo anasema hivi: “Hiyo ni tabia ya kwetu na tunafurahia kupana. Lakini hatufanye hivyo kila siku. Ninawaambia kwa upole watu wa jamaa yangu kwamba nitawapatia kulingana na uwezo wangu, lakini siwezi kuzarau mahitaji ya kiroho na ya kimwili ya familia yangu ili kuwasaidia.”

15 Mara nyingi watu wa jamaa wanawakasirikia na kuwatukana wale wanaorudi nyumbani na wale wanaokataa kuenda katika inchi nyingine kwa sababu hawapendi kuacha familia zao. Watu fulani wa jamaa wanavunjika moyo kwa sababu walikuwa wakifikiri kwamba wao ndio watawatumia feza na zawadi. Wengine wanawaambia kwamba hawana upendo. (Met. 19:6, 7) Anna, binti wa Eduardo, anasema hivi: “Ijapokuwa hivyo, tunapoamua kuacha faida za kimwili kwa sababu ya kumuabudu Yehova, watu fulani wa jamaa yetu wanaweza kuona kwamba tunatia Yehova pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu. Lakini, tukitenda tofauti na hilo, wataelewa namna gani musimamo wetu?”—Linganisha 1 Pet. 3:1, 2.

ONYESHA IMANI KATIKA MUNGU

16. (a) Namna gani mutu anaweza ‘kujidanganya mwenyewe kwa mawazo yasiyo ya kweli’? (Yak. 1:22) (b) Yehova anabariki maamuzi ya namna gani?

16 Kisha kufika katika inchi moja tajiri bila bwana yake na watoto wake, dada mumoja aliwaambia wazee wa kutaniko hivi: “Familia yangu ilifanya yote inayoweza ili nifike hapa. Bwana yangu aliacha hata daraka lake la muzee. Kwa hiyo, ninaamini kabisa kwamba Yehova atanibariki kwa sababu nimefika hapa.” Kila mara Yehova anabariki maamuzi yanayoonyesha kwamba mutu anamutumainia. Lakini Yehova hatatubariki ikiwa uamuzi ambao tunachukua haupatane na mapenzi yake, zaidi sana ikiwa uamuzi huo unamufanya mutu aache mapendeleo yake katika kutaniko bila sababu nzuri.​—Soma Waebrania 11:6; 1 Yohana 5:13-15.

17. Sababu gani tunapaswa kutafuta muongozo wa Yehova mbele ya kuchukua maamuzi, na namna gani tunaweza kufanya hivyo?

17 Tafuta muongozo wa Yehova kwanza mbele ya kuchukua uamuzi wowote, wala si kisha kufanya hivyo ili usijute baadaye. Muombe Yehova roho takatifu, hekima, na  muongozo. (2 Tim. 1:7) Ujiulize hivi: ‘Niko tayari kumuheshimu Yehova katika hali gani? Niko tayari kumuheshimu hata wakati ninateswa kwa sababu ya imani yangu?’ Ikiwa ndiyo, niko tayari kubaki na familia yangu hata kama hilo litafanya tuishi maisha ya hali ya chini? (Lu. 14:33) Omba wazee wa kutaniko mashauri ya Biblia, na uonyeshe kwamba unamutumainia kabisa Yehova na utegemee ahadi yake ya kukusaidia ikiwa unafuata shauri lake. Wazee wa kutaniko hawawezi kuchukua maamuzi pa nafasi yako, lakini wanaweza tu kukusaidia uchukue maamuzi ambayo yatafanya uwe na maisha yenye furaha.​—2 Kor. 1:24.

18. Kutimizia familia mahitaji ni daraka la nani, lakini ni hali gani zinazoweza kuwachochea wengine wasaidie?

18 Yehova ametolea kichwa cha familia daraka nzito la kuwatimizia kila siku watu wa familia yake mahitaji yao. Tunapaswa kupongeza na kusali kwa ajili ya wale wanaotimiza daraka hilo bila kuacha bibi na watoto, ijapokuwa wanasumbuliwa na watu wa jamaa zao. Zaidi ya kusali kwa ajili yao, tunapaswa kuwahangaikia wanapopatwa na hali zisizotazamiwa, kama vile misiba ao magonjwa yanayoomba kutunziwa haraka. Hali hizo zinatutolea nafasi ya kuonyesha ndugu hao waaminifu upendo wa kweli. (Gal. 6:2, 5; 1 Pet. 3:8) Unaweza kumutimizia ndugu yako mahitaji ya haraka kama vile feza ao chakula ao kumusaidia apate kazi katika eneo lenu? Ukifanya hivyo, unaweza kupunguza mikazo inayoweza kumuchochea ndugu ao dada aende kutumikia katika inchi nyingine.​—Met. 3:27, 28; 1 Yoh. 3:17.

KUMBUKA KWAMBA YEHOVA ATAKUSAIDIA!

19, 20. Sababu gani Wakristo wanaweza kuwa hakika kwamba Yehova atawasaidia?

19 Maandiko yanatutia moyo hivi: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa feza, huku mukirizika [ao kutosheka] na vitu vya sasa. Kwa maana yeye [Mungu] amesema: ‘Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.’ Hivi kwamba tuwe hodari na kusema: ‘Yehova ni musaidizi wangu; sitaogopa. Mwanadamu anaweza kunitendea nini?’” (Ebr. 13:5, 6) Namna gani tunaweza kutumia shauri hilo?

20 Muzee mumoja ambaye ametumikia katika kutaniko kwa miaka mingi anayeishi katika inchi moja maskini anasema hivi: “Mara nyingi watu wanasema mambo mengi kuhusu Mashahidi wa Yehova. Wanatambua pia kwamba hata Mashahidi walio maskini wanavaa vizuri kila siku na wanaonekana kuwa na maisha mazuri kuliko watu wengine.” Hilo linapatana na ahadi ambayo Yesu aliwatolea wale wanaotia Ufalme pa nafasi ya kwanza. (Mt. 6:28-30, 33) Bila shaka, Baba yako wa mbinguni, Yehova, anakupenda na anakutakia wewe na watoto wako mema. ‘Macho yake [Yehova] yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mukamilifu kumuelekea yeye.’ (2 Nya. 16:9) Ametutolea amri zake. Amri hizo zinatia ndani mashauri yanayohusu maisha na mahitaji ya kimwili ya familia. Yote hayo ni kwa faida yetu. Tunapotii amri hizo, tunaonyesha kwamba tunamupenda na kumutegemea Yehova. ‘Kumupenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si muzigo muzito.’—1 Yoh. 5:3.

21, 22. Sababu gani umeazimia kumutegemea Yehova?

21 Eduardo anasema hivi: “Ninajua kwamba wakati niliopitisha nikiwa mbali na bibi yangu na watoto wangu umekwisha kupita na hautarudi tena, lakini sifikirie sana wakati huo. Wengi ambao tulitumika nao ni matajiri lakini hawana furaha. Familia zao zina matatizo mengi. Lakini, familia yetu ni yenye furaha kabisa! Na ninashangaa kuona namna ndugu wengine katika inchi hii wanatia ibada ya Yehova pa nafasi ya kwanza katika maisha yao, hata kama wao ni maskini. Sisi wote tunaendelea kujionea ukweli wa ahadi ya Yesu.”—Soma Mathayo 6:33.

22 Usiogope! Azimia kumutii na kumutegemea Yehova. Acha upendo wako kwa Mungu, kwa bibi yako, na kwa watoto wako ukuongoze utimize vizuri daraka lako la kutunza familia yako. Ukifanya hivyo, Yehova atakusaidia.

^ fu. 1 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 11 Ona habari “Jinsi ya Kupangia Matumizi ya Pesa Zako” katika Amuka! ya Mwezi wa 9, 2011.