Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, ulijua?

Je, ulijua?

Wakati wa zamani, ilimaanisha nini mutu kupasua nguo zake mwenyewe?

MAANDIKO yanazungumuzia hali nyingi zilizowafanya watu fulani wayapasue manguo yao. Leo, wasomaji wa Biblia wanaweza kuona jambo hilo kuwa lenye kushangaza. Lakini kwa Wayahudi, kufanya hivyo kulionyesha kwamba mutu anaumia sana kwa sababu ya kukosa tumaini, kwa sababu ya huzuni, kuzarauliwa, hasira ao kwa sababu mutu amefiwa na mupendwa wake.

Kwa mufano, Rubeni “alirarua [ao kupasua]” nguo zake alipoona kwamba mipango yake ya kumuokoa ndugu yake Yosefu haikufanikiwa kwa sababu alikuwa ameuzishwa ili awe mutumwa. Baba yao Yakobo, “alirarua nguo zake” alipoambiwa kwamba munyama wa pori alimuua Yosefu mwana wake. (Mwa. 37:18-35) Ayubu “alirarua [ao kupasua] nguo zake” aliposikia kwamba watoto wake wote walikufa. (Ayu. 1:18-20) Mujumbe “aliyekuwa na mavazi yenye kuraruliwa [ao yenye kupasuka]” alifika mbele ya Eli, Kuhani Mukubwa, ili kumujulisha kwamba Waisraeli walishindwa kwenye vita, watoto wake wawili walikuwa wameuawa, na kwamba sanduku la agano lilinyanganywa. (1 Sam. 4:12-17) Yosia, ‘alirarua mavazi yake’ aliposikia maneno ya Sheria yakisomwa kwa ajili yake na kutambua makosa ya watu wake.​—2 Fal. 22:8-13.

Yesu alipokuwa akisambishwa, Kayafa, Kuhani Mukubwa ‘aliyararua mavazi yake ya inje’ aliposikia maneno ya Yesu ambayo alielewa kimakosa kuwa maneno ya kukufuru. (Mt. 26:59-66) Kulingana na desturi ya sheria ya dini iliyowekwa na marabi, yeyote aliyesikia mutu fulani akikufuru ao kutukana jina la Mungu, alipaswa kupasua nguo zake. Hata hivyo, wazo lingine ambalo marabi walitokeza kisha hekalu la Yerusalemu kuharibiwa, lilionyesha kwamba “mutu anayesikia makufuru juu ya Jina la Mungu katika siku zetu hapaswe kupasua nguo zake. Lakini nguo za mutu ambaye alikufuru jina la Mungu ndizo zingepaswa kupasuliwa vipande-vipande.”

Bila shaka, Mungu hakuona kwamba ni jambo la maana mutu kupasua nguo zake ikiwa huzuni ya mutu huyo haikuwa ya kweli ao ya kutoka moyoni. Ndiyo sababu Yehova aliwaambia watu wake ‘wairarue [ao waipasue] mioyo yao wala si mavazi yao, na warudie kwake.’—Yoe. 2:13.