Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Yehova Ni Mungu Anayepanga Mambo Vizuri

Yehova Ni Mungu Anayepanga Mambo Vizuri

“Mungu si Mungu wa machafuko, bali ni wa amani.” 1 KOR. 14:33.

1, 2. (a) Ni nani aliyekuwa kiumbe wa kwanza wa Mungu, na namna gani Yehova alimutumia? (b) Ni jambo gani linaloonyesha kwamba malaika wanapangwa vizuri?

YEHOVA, Muumbaji wa ulimwengu wote, anapanga mambo vizuri. Kiumbe wake wa kwanza alikuwa Mwana wake muzaliwa-pekee anayeitwa “Neno” kwa sababu yeye ni musemaji mukubwa wa Mungu. Kwa kuwa Neno amemutumikia Yehova kwa miaka mingi sana, Biblia inasema hivi: “Hapo mwanzo Neno alikuwako, na Neno alikuwa pamoja na Mungu.” Biblia inaongezea hivi: “Vitu vyote vilikuja kuwako kupitia kwake, na bila yeye [Neno] hakuna hata kitu kimoja kilichokuja kuwako.” Miaka zaidi ya 2000 iliyopita, Mungu alimutuma Neno duniani. Alipokuwa duniani alifanya mapenzi ya Baba yake kwa uaminifu akiwa mwanadamu mukamilifu Yesu Kristo.—Yoh. 1:1-3, 14.

2 Mbele afike duniani, Mwana wa Mungu alitumika kwa uaminifu akiwa “fundi [wake] wa kazi.” (Met. 8:30 Verbum Bible) Kupitia yeye, Yehova aliumba mamilioni ya malaika huko mbinguni. (Kol. 1:16) Kuhusu malaika hao, Biblia inatuambia hivi: ‘Maelfu elfu waliendelea kumutumikia [Yehova], na elfu kumi mara elfu kumi waliendelea kusimama mbele zake.’ (Dan. 7:10) Viumbe wengi wa kiroho wa Mungu wanaitwa “majeshi” ya Yehova yanayopangwa vizuri sana.—Zab. 103:21.

3. Nyota na planete zinaweza kufikia hesabu gani, na zimepangwa namna gani?

 3 Tunaweza kusema nini kuhusu uumbaji unaoonekana kama vile nyota na sayari ao planete nyingi sana? Kuhusu nyota, gazeti moja la Houston, Texas, linaloitwa Chronicle, linasema kwamba kulingana na uchunguzi uliofanywa hivi karibuni, inaonekana kwamba kuna nyota trilioni tatu mara miliare mia moja, ni kusema, kutia zero 23 nyuma ya namba 3. Hesabu hiyo inazidi mara tatu hesabu ambayo wanasayansi walitoa hapo mbele. Nyota zimepangwa katika vikundi vinavyoitwa galaksi. Kila galaksi ina mamiliare ao hata matrilioni ya nyota, na planete nyingi. Galaksi nyingi zinapangwa katika vikundi-vikundi, na vikundi hivyo vinapangwa katika makundi makubwa-makubwa zaidi.

4. Sababu gani inaeleweka kusema kwamba watumishi wa Mungu wanapashwa kupangwa vizuri hapa duniani?

4 Kama viumbe waaminifu wa kiroho huko mbinguni, mbingu zenye nyota zimepangwa vizuri sana. (Isa. 40:26) Kwa hiyo, inaeleweka kusema kwamba Yehova anapashwa kuwapanga vizuri watumishi wake wanaomutumikia hapa duniani. Anataka watumishi wake wapangwe vizuri, na jambo hilo ni la maana sana kwa sababu wana kazi ya lazima sana ya kufanya. Kwa miaka mingi, Yehova amewapanga vizuri watumishi wake ili wamuabudu kwa uaminifu. Kuna mifano mingi inayohakikisha kwamba amekuwa pamoja nao na kwamba yeye “si Mungu wa machafuko, bali ni wa amani.”—Soma 1 Wakorintho 14:33, 40.

MUNGU ALIWAPANGA VIZURI WATUMISHI WAKE WA ZAMANI

5. Namna gani mupango wa Mungu wa kuijaza dunia ulisimamishwa kwa muda?

5 Yehova alipowaumba wanadamu wa kwanza, aliwaambia hivi: ‘Zaeni, muwe wengi, muijaze dunia na kuitiisha, na mutawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.’ (Mwa. 1:28) Wanadamu wangeendelea kuongezeka wakiwa wenye kupangwa vizuri ili waijaze dunia na kuifanya dunia nzima iwe Paradiso. Lakini utimizo wa mupango huo ulisimamishwa kwa muda kwa sababu Adamu na Eva hawakuendelea kumutii Mungu. (Mwa. 3:1-6) Kadiri wakati ulivyopita, ‘Yehova aliona kuwa ubaya wa mwanadamu ulikuwa mwingi duniani na kila muelekeo wa fikira za moyo wake ulikuwa mubaya tu wakati wote.’ Kwa hiyo, ‘dunia iliharibika machoni pa Mungu wa kweli, dunia ilijaa jeuri.’ Basi, Mungu aliamua kuleta garika katika dunia yote ambayo iliwaua watu wabaya wote.—Mwa. 6:5, 11-13, 17.

6, 7. (a) Sababu gani Yehova alimukubali Noa? (Ona picha mwanzoni wa habari hii.) (b) Watu wote ambao hawakuwa waaminifu katika siku za Noa, walipatwa na nini?

6 Hata hiyo, ‘Noa alipata kibali machoni pa Yehova’ kwa sababu ‘alikuwa mutu mwadilifu [ao mwenye haki]’ na ‘aliyeonekana kuwa mutu asiye na kosa kati ya watu wa siku zake.’ Kwa kuwa “Noa alitembea na Mungu wa kweli,” Yeye alimuambia ajenge safina kubwa sana. (Mwa. 6:8, 9, 14-16) Safina hiyo ilijengwa ili kuokoa uzima wa wanadamu na wanyama pia. Kwa kuwa alimutii Mungu, ‘Noa alifanya kulingana na yote ambayo Yehova alikuwa amemuamuru,’ na akisaidiwa na familia yake, alimaliza kazi ya kujenga kulingana na maagizo ambayo Yehova alimutolea. Kisha Noa kutia kila kitu chenye uzima ndani ya safina, ‘Yehova alifunga mulango.’—Mwa. 7:5, 16.

7 Garika ilipofika katika mwaka wa 2370 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, Yehova ‘alifutilia mbali kila kitu kilicho hai ambacho kilikuwa juu ya uso wa inchi,’ lakini alilinda salama mutumishi wake muaminifu Noa na familia yake ndani ya safina. (Mwa. 7:23) Kila mutu anayeishi duniani leo anatoka katika kizazi cha Noa, ni kusema, watoto wake na bibi zao. Lakini wale wote waliokosa imani waliokuwa inje ya safina waliharibiwa kwa sababu walikataa kumusikiliza Noa, ‘muhubiri wa uadilifu [ao wa haki].’—2 Pet. 2:5.

Kupanga mambo vizuri kuliwasaidia watu munane waokoke Garika(Ona fungu la 6, 7)

8. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Waisraeli walipangwa vizuri wakati Mungu aliwaagiza waingie katika Inchi ya Ahadi?

 8 Zaidi ya miaka 800 kisha Garika, Mungu aliwapanga Waisraeli vizuri ili wawe taifa. Mambo yao yote yalipashwa kupangwa vizuri, zaidi sana ibada yao. Kwa mufano, zaidi ya makuhani na Walawi wengi, kulikuwa pia wanawake waliopangwa vizuri ili watumikie kwenye muingilio wa hema la mukutano. (Kut. 38:8) Yehova Mungu aliwaagiza Waisraeli waingie katika inchi ya Kanaani. Lakini wengi kati yao walikosa uaminifu. Kwa hiyo, Yehova aliwaambia hivi: ‘Nanyi hamutaingia katika inchi ambayo niliinua mukono wangu katika kiapo ya kwamba nitakaa pamoja nanyi, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune na Yoshua mwana wa Nuni’ kwa sababu walileta ripoti nzuri kisha kuipeleleza Inchi ya Ahadi. (Hes. 14:30, 37, 38) Kulingana na agizo la Mungu, baadaye Musa alimuachia Yoshua kazi ya kuwaongoza Waisraeli. (Hes. 27:18-23) Yoshua alipokaribia kuwaingiza Waisraeli katika inchi ya Kanaani, Mungu alimuambia hivi: “Uwe hodari na mwenye nguvu. Usitetemeke wala usiwe na hofu, kwa maana Yehova Mungu wako yupo pamoja nawe kila mahali unapoenda.”—Yos. 1:9.

9. Namna gani Rahabu alimuona Yehova na watu wake?

9 Kwa kweli Yehova Mungu alikuwa pamoja na Yoshua kila mahali alipoenda. Kwa mufano, fikiria yale yaliyotokea Waisraeli walipopiga kambi karibu na Yeriko muji wa Wakanani. Katika mwaka wa 1473 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, Yoshua aliwatuma wanaume wawili kupeleleza muji wa Yeriko, na walimukuta kahaba aliyeitwa Rahabu. Aliwaficha wapelelezi hao katika dari ao sehemu ya juu ya nyumba yake, ili wanaume ambao mufalme wa Yeriko alituma ili kuwakamata wasiwaone. Rahabu aliwaambia Wapelelezi hao hivi: ‘Najua hakika ya kwamba Yehova atawapa inchi hii . . . , kwa maana tumesikia jinsi ambavyo Yehova aliyakausha maji ya Bahari Nyekundu mbele yenu . . . na yale muliyowatendea wale wafalme wawili wa Waamori.’ Aliongezea hivi: “Yehova Mungu wenu ni Mungu juu mbinguni na chini duniani.” (Yos. 2:9-11) Kwa kuwa Rahabu aliunga mukono tengenezo la Yehova la  wakati huo, Mungu alifanya mupango ili yeye na watu wa jamaa yake walindwe wakati wa kuharibiwa kwa muji wa Yeriko. (Yos. 6:25) Rahabu alionyesha imani, alimuogopa sana Yehova, na aliwaheshimia watu wake.

TENGENEZO LENYE BIDII KATIKA SIKU ZA MITUME

10. Yesu aliwaambia nini viongozi wa dini ya Wayahudi katika siku zake, na sababu gani aliwaambia hivyo?

10 Wakiongozwa na Yoshua, Waisraeli walishinda muji mumoja baada ya mwengine na kuchukua inchi ya Kanaani. Lakini, kulitokea nini katika miaka iliyofuata? Kwa miaka mingi, Waisraeli walivunja sheria ya Mungu tena na tena. Wakati Yehova alimutuma Mwana wake duniani, Waisraeli hawamukutii kabisa Mungu na hawakumusikiliza musemaji wake. Ndiyo sababu Yesu aliita muji wa Yerusalemu kuwa “muuaji wa manabii.” (Soma Mathayo 23:37, 38.) Mungu aliwakataa viongozi wa dini ya Wayahudi kwa sababu walikosa uaminifu. Kwa hiyo, Yesu aliwaambia hivi: “Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa taifa lenye kuzaa matunda yake.”—Mt. 21:43.

11, 12. (a) Katika siku za mitume, ni nini iliyoonyesha kwamba Yehova alikuwa amehamisha baraka zake kwa tengenezo lingine? (b) Tengenezo mupya ambalo Mungu alikubali katika siku za mitume lilifanyizwa na wanani?

11 Katika siku za Yesu, Yehova alikataa taifa la Israeli kwa sababu lilikosa uaminifu. Hata hivyo, hilo halikumaanisha kwamba Yehova hangekuwa tena na watumishi waaminifu duniani. Yehova alihamishia baraka zake kwa tengenezo mupya lenye bidii lililofuata Yesu Kristo na kusikiliza mafundisho yake. Tengenezo hilo lilianza siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33. Wakati huo, wafuasi wa Yesu 120 hivi walikuwa wamekusanyika nafasi fulani huko Yerusalemu na kwa ‘gafula kukatokea kutoka mbinguni kelele kama ile ya upepo wenye nguvu unaovuma, nao ukaijaza nyumba yote. Nao wakaona ndimi kama za moto, nazo zikagawanyika huku na huku, na mumoja ukaketi juu ya kila mumoja wao, nao wote wakajazwa roho takatifu wakaanza kusema katika luga tofauti, kama vile roho ilivyokuwa ikiwawezesha kusema.’ (Mdo 2:1-4) Jambo hilo lenye kushangaza lilionyesha kabisa kwamba Yehova alikuwa akiongoza tengenezo hilo jipya lililofanyizwa na wanafunzi wa Kristo.

12 Katika siku hiyo ya furaha, ‘watu karibu 3000 waliongezeka’ juu ya hesabu ya wafuasi wa Yesu. Zaidi ya hilo, ‘Yehova aliendelea kuongezea kwao kila siku wale waliokuwa wakiokolewa.’ (Mdo. 2:41, 47) Kazi ya kuhubiri katika siku za mitume ilikuwa na matokeo mazuri sana na hivyo ‘neno la Mungu liliendelea kukua, na hesabu ya wanafunzi ilizidi kuongezeka sana katika Yerusalemu.’ Hata ‘umati mukubwa wa makuhani ulianza kuitii imani.’ (Mdo. 6:7) Kwa hiyo, wengi waliokuwa na moyo wa kupenda haki walikubali kweli ambayo washiriki wa tengenezo hilo mupya walitangaza. Baadaye, Yehova alitoa uhakikisho mwengine ulioonyesha kwamba alikuwa akiwaongoza alipoanza kuwaleta “watu wa mataifa” katika kutaniko la Kikristo.—Soma Matendo 10:44, 45.

13. Tengenezo mupya ambalo Mungu alikubali lilipewa kazi gani?

13 Bila shaka ni wafuasi wa Kristo ndio walipewa kazi ya kuhubiri. Yesu mwenyewe aliwaachia wafuasi wake mufano, kwa kuwa kisha tu kubatizwa, alianza kuhubiri kuhusu “Ufalme wa mbinguni.” (Mt. 4:17) Yesu aliwafundisha wanafunzi wake namna ya kufanya kazi hiyo. Aliwaambia hivi: ‘Mutakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mupaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.’ (Mdo. 1:8) Wafuasi wa Kristo walielewa  vizuri yale waliyopashwa kufanya. Kwa mufano, katika Antiokia ya Pisidia, Paulo na Barnaba hawakuogopa kuwaambia hivi Wayahudi waliowapinga: “Ilikuwa lazima neno la Mungu lihubiriwe kwenu kwanza. Kwa kuwa munalisukumia mbali kutoka kwenu na hamujione kuwa munastahili uzima wa milele, tazameni! tunawageukia mataifa. Kwa kweli, Yehova ameweka amri juu yetu kwa maneno haya: ‘Nimewaweka ninyi kuwa nuru ya mataifa, ili muwe wokovu mupaka sehemu ya mwisho ya dunia.’” (Mdo. 13:14, 45-47) Tangu siku za mitume, sehemu ya duniani ya tengenezo la Mungu imekuwa ikiwajulisha watu mupango ambao Mungu amefanya ili kuwaokoa.

WENGI WANAANGAMIA, LAKINI WATUMISHI WA MUNGU WANAOKOKA

14. Muji wa Yerusalemu ulipatwa na nini, lakini ni nani ambao waliokoka?

14 Wayahudi wengi hawakukubali habari njema na kwa hiyo, wangepatwa na musiba. Yesu alikuwa amewaonya wanafunzi wake hivi: ‘Mutakapoona Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi, ndipo jueni kwamba kufanywa ukiwa kwake kumekaribia. Ndipo wale walio katika Yudea waanze kukimbilia milimani, na wale walio katikati yake na waondoke, nao wale walio katika sehemu za mashambani wasiingie ndani.’ (Lu. 21:20, 21) Maneno ya Yesu yalitimia. Kwa kuwa Wayahudi waliasi, jeshi la Roma lilizunguka Yerusalemu mwaka wa 66. Hata hivyo, kwa gafula jeshi hilo liliondoka katika muji na hilo liliwatolea wafuasi wa Yesu nafasi ya kutoka katika Yerusalemu na Yudea. Kulingana na mwana-historia Eusebio, Wayahudi wengi walivuka Muto Yordani na kuenda huko Pela katika Perea. Katika mwaka wa 70, jeshi la Roma lenye kuongozwa na Jenerali Tito lilirudia na kuharibu Yerusalemu. Hata hivyo, Wakristo waaminifu waliokoka kwa sababu walitii onyo la Yesu.

15. Wakristo walikuwa katika hali nzuri ya kiroho ijapokuwa hali gani?

15 Ijapokuwa wafuasi wa Kristo walipatwa na magumu, mateso, na majaribu mengine ya imani, Ukristo ulienea sana katika siku za mitume. (Mdo. 11:19-21; 19:1, 19, 20) Wakristo hao wa kwanza-kwanza walikuwa katika hali nzuri ya kiroho kwa sababu Mungu alikuwa akiwabariki.—Met. 10:22.

16. Ili kuwa na uhusiano muzuri pamoja na Mungu, kila Mukristo alipashwa kufanya nini?

16 Ili kuwa na uhusiano muzuri na Mungu, kila Mukristo alipashwa kujikaza kufanya mambo fulani. Ilikuwa jambo la maana sana kujifunza Maandiko kwa bidii, kukusanyika kikawaida ili kumuabudu Yehova, na kuhubiri kwa bidii. Mambo hayo yalisaidia watumishi wa Yehova wa wakati huo wawe na hali nzuri ya kiroho na umoja kama yanavyotusaidia leo. Wale waliojiunga na makutaniko ya kwanza-kwanza yaliyopangwa vizuri walisaidiwa sana na wazee na watumishi wa huduma waliokuwa na roho ya kujitoa. (Flp. 1:1; 1 Pet. 5:1-4) Wakristo hao walifurahi sana wakati wazee wenye kusafiri, kama vile Paulo, walitembelea makutaniko! (Mdo.15:36, 40, 41) Namna yetu ya kuabudu inafanana kabisa na ile ya Wakristo wa kwanza-kwanza. Tunafurahia sana namna Yehova amekuwa akiwapanga vizuri watumishi wake tangu zamani na hata leo! *Wanaendelea Kutembea Katika Kweli

17. Tutazungumuzia nini katika habari inayofuata?

17 Ulimwengu wa Shetani unapokaribia mwisho wake, sehemu ya duniani ya tengenezo la Yehova inaendelea kusonga mbele sana katika siku hizi za mwisho. Unaendelea kusonga mbele pamoja na tengenezo hilo? Unaendelea kufanya maendeleo ya kiroho? Habari inayofuata itatuonyesha namna ya kufanya hivyo.

^ fu. 16 Ona habari “Wakristo Huabudu kwa Roho na Kweli” na “” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15/07/2002. Mafasirio zaidi kuhusu sehemu ya duniani ya tengenezo la Mungu yamechapishwa katika kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu ya Ufalme.