Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

 Vitu Vya Maana Sana Vya Historia Yetu

‘Kungali Kazi Kubwa ya Mavuno’

‘Kungali Kazi Kubwa ya Mavuno’

George Young alifika katika muji wa Rio de Janeiro Mwezi wa 3, 1923

TUKO katika mwaka wa 1923. Jumba la maonyesho kwenye Masomo ya Drama na Muziki ya São Paulo linajaa watu wengi! Unaweza kumusikiliza ndugu George Young akisema kwa sauti yenye nguvu. Hotuba yake inatafsiriwa mustari kwa mustari katika Kireno (luga ya Ureno ao Portugal). Watu wote 585 wanaohuzuria wanasikiliza kwa uangalifu. Maandiko ya Biblia yaliyo katika Kireno yanaonyeshwa kwenye skrini (ao écran). Mukutano unapomalizika kila mutu anapewa kijitabu chenye kichwa: Des millions de personnes actuellement vivantes ne mourront jamais ! (Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe!) Kijitabu hicho kilikuwa katika Kiingereza, Kijerumani, na Kiitaliano. Hotuba hiyo ilitoa ushahidi mukubwa na habari yake ilienea sana! Kisha siku mbili, jumba hilo lilijaa tena watu wengi ili wasikilize hotuba nyingine. Mambo yalianza namna gani?

Katika mwaka wa 1867, Sarah Bellona Ferguson alitoka Amerika na kuhamia huko Brazili pamoja na familia yake. Katika mwaka wa 1899, Sarah alijua kwamba alikua amepata ukweli kisha kusoma vichapo fulani ambavyo ndugu yake mudogo alileta Brazili kutoka Amerika. Kwa kuwa Sarah alikuwa musomaji mwenye bidii, alijiandikisha ili kupata gazeti Munara wa Mulinzi kwa ukawaida. Kwa kuwa alipendezwa sana na ujumbe wa Biblia, alimuandikia Ndugu Russell, na kumuonyesha kwamba yeye anaweza kushuhudia kwamba hakuna mutu aliye mbali sana ili ujumbe usimufikie.”

Watu Wazima Wanaweza Kuzungumuza na Wafu? (katika Kireno)

Sarah Ferguson alifanya yote anayoweza ili kuwaelezea wengine ukweli wa Biblia, lakini mara kwa mara alijiuliza ikiwa atapata mutu wa kumusaidia ajue mengi zaidi, na vilevile kusaidia familia yake na watu wote wazuri huko Brazili. Katika mwaka wa 1912, Beteli ya Brooklyn ilimujulisha kwamba mutu fulani angetumwa São Paulo akiwa na maelfu ya trakte yenye kichwa Où sont les morts ? (Wafu wako wapi) katika Kireno. Katika mwaka wa 1915 alisema kwamba sikuzote alishangaa kusikia kwamba Wanafunzi wengi wa Biblia walitazamia kuenda mbinguni kisha siku chache. Ili kuonyesha maoni yake, aliandika hivi: “Namna gani kuhusu Brazili na Amerika ya Kusini? . . . Ikiwa unafikiria ukubwa wa eneo la Amerika Kusini, utaona kwamba kungali kazi kubwa ya mavuno inayopashwa kufanywa.” Bila shaka, kazi kubwa ya  mavuno ilipashwa kufanywa.

Katika mwaka wa 1920, vijana 8 wa Brazili waliokuwa wakifanya kazi katika mashua walihuzuria mikutano katika New York City wakati mashua yao ya vita ilikuwa ikirekebishwa. Waliporudia Rio de Janeiro, walielezea wengine kuhusu tumaini lao mupya walilojifunza katika Biblia. Muda mufupi baadaye, Mwezi wa 3, 1923, Ndugu George Young, aliyekuwa pilgrimu, ao mwangalizi mwenye kusafiri, alifika katika muji wa Rio de Janeiro, na huko alikutana na watu waliopendezwa. Alifanya mipango ili vichapo fulani vitafsiriwe katika Kireno. Kisha siku chache Ndugu Young alienda São Paulo, muji uliokuwa na watu 60000 hivi wakati huo. Alitoa hotuba katika muji huo na kutolea watu vijitabu Des millions de personnes actuellement vivantes ne mourront jamais !, kama tulivyoonyesha mwanzoni mwa habari hii. Alisema hivi: “Kwa kuwa nilikuwa pekee yangu, nilitumia sana hotuba zilizotangazwa katika magazeti ya habari.” Kisha, aliongeza hivi: “Hizo zilikuwa hotuba za watu wote za kwanza zilizotangazwa kwa jina la I.B.S.A. katika Brazili.” *

Maandiko ya Biblia yalionyeshwa kwenye skrini wakati Ndugu Young alikuwa akitoa hotuba zake

Katika ripoti moja kuhusu Brazili, Munara wa Mulinzi wa tarehe 15/12/1923, ulitoa maelezo yafuatayo: “Tunapofikiria kwamba kazi ilianza huko tarehe 1 Mwezi wa 6 na kwamba hakukuwa kichapo hata kimoja wakati huo, tunaona kabisa kwamba Bwana amebariki kazi yetu.” Ripoti hiyo inaendelea kusema kwamba hotuba ambazo Ndugu Young alitoa katika São Paulo zilikuwa hotuba 2 kati ya 21 ambazo zilitolewa kuanzia tarehe 1 Mwezi wa 6 mupaka tarehe 30 Mwezi wa 9, na ambazo zilihuzuriwa na watu 3600. Katika Rio de Janeiro, ujumbe wa Ufalme ulienea pole kwa pole. Na katika miezi michache tu, vichapo zaidi ya 7000 katika Kireno viligawanywa. Zaidi ya hilo, gazeti la kwanza la Munara wa Mulinzi katika Kireno lilikuwa la Mwezi wa 11 na 12, 1923.

Sarah Bellona Ferguson alikuwa wa kwanza kujiandikisha ili kupata kwa ukawaida magazeti ya Kiingereza ya Munara wa Mulinzi katika Brazili

Ndugu George Young alimutembelea Sarah Ferguson, na gazeti Munara wa Mulinzi lilisema hivi: “Dada huyo alikuja katika chumba cha kuikalisha wageni, na kwa muda fulani alibaki bila kusema kitu. Kisha, alishika mukono wa Ndugu Young, alimutazama katika uso, na kumuuliza hivi: ‘Je, wewe ni Pilgrimu kabisa?’” Kisha siku chache, yeye na watoto wake wane walibatizwa. Kwa kweli, alikuwa amengojea ubatizo kwa miaka 25! Munara wa Mulinzi wa tarehe 01/08/1924, ulionyesha kwamba watu 50 walibatizwa katika Brazili, wengi kati yao walikuwa katika muji wa Rio de Janeiro.

Leo, kisha miaka 90, hatuna tena sababu ya kuuliza hivi: “Namna gani kuhusu Brazili na Amerika ya Kusini?” Mashahidi wa Yehova zaidi ya 760000 wanahubiri habari njema katika Brazili. Na katika Amerika ya Kusini yote ujumbe wa Ufalme unasikika katika Kireno, Kihispania, na katika luga nyingi za kienyeji. Bila shaka, Sarah Ferguson hakudanganyika katika mwaka wa 1915, aliposema kwamba kulikuwa kungali kazi kubwa ya mavuno iliyopashwa kufanywa.—Kutoka katika vitu vya maana sana vya historia yetu vya Brazili.

^ fu. 6 I.B.S.A. inamaanisha International Bible Students Association