Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Lazima Umpende Yehova Mungu Wako”

“Lazima Umpende Yehova Mungu Wako”

“Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.MT. 22:37.

1. Kwa nini upendo ulisitawi kati ya Mungu na Mwana wake?

YESU KRISTO, Mwana wa Yehova, alisema hivi: “Ninampenda Baba.” (Yoh. 14:31) Alisema hivi pia: “Baba anampenda Mwana.” (Yoh. 5:20) Hilo halipaswi kutushangaza kwa sababu kwa miaka mingi sana kabla ya kuwa mwanadamu, Yesu alikuwa “stadi wa kazi” wa Mungu. (Met. 8:30) Kadiri Yehova na Yesu walivyofanya kazi pamoja, ndivyo upendo wao ulivyositawi. Mwana alijifunza mengi kuhusu sifa za Baba yake na alikuwa na sababu nyingi sana za kumpenda.

2. (a) Upendo huhusisha nini? (b) Tutazungumzia maswali gani?

2 Upendo huhusisha kuwa na hisia nyingi za kutoka moyoni kumwelekea mtu. Mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: ‘Ninakupenda wewe, Ee Yehova nguvu zangu.’ (Zab. 18:1) Hivyo ndivyo tunavyopaswa kuhisi kumhusu Mungu, kwa kuwa yeye anatupenda pia. Tukimtii Yehova, ataonyesha kwamba anatupenda. (Soma Kumbukumbu la Torati 7:12, 13.) Lakini je, tunaweza kweli kumpenda Mungu tusiyeweza kumwona? Kumpenda Yehova humaanisha nini? Kwa nini tunapaswa kumpenda? Na tunawezaje kuonyesha kwamba tunampenda Mungu?

 KWA NINI TUNAWEZA KUMPENDA MUNGU?

3, 4. Kwa nini tunaweza kumpenda Mungu?

3 “Mungu ni Roho”; kwa hiyo, hatuwezi kumwona. (Yoh. 4:24) Hata hivyo, tunaweza kumpenda Yehova, na Maandiko yanatuamuru kumpenda. Kwa mfano, Musa aliwaambia hivi Waisraeli: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa nguvu zako zote.”Kum. 6:5.

4 Kwa nini tunaweza kumpenda sana Mungu? Kwa sababu alituumba tukiwa na uhitaji wa kiroho na uwezo wa kuonyesha upendo. Uhitaji wetu wa kiroho unapotoshelezwa vizuri, upendo wetu kumwelekea Mungu huongezeka na tunakuwa na sababu nzuri ya kuwa na furaha. Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.” (Mt. 5:3) Imesemwa hivi kuhusu ile inayoitwa tamaa ya kiasili ya wanadamu ya kuabudu: ‘Tunapoona jinsi wanadamu ulimwenguni pote wanavyomtafuta na kumwamini Mungu tunapaswa kustaajabu na kuonyesha hofu na heshima.’Man Does Not Stand Alone, kitabu kilichoandikwa na A. C. Morrison.

5. Tunajuaje kwamba kumtafuta Mungu si ubatili?

5 Je, kumtafuta Mungu ni ubatili? Hapana, kwa sababu anataka tumpate. Mtume Paulo alisema wazi jambo hilo alipohubiria umati uliokusanyika Areopago, karibu na hekalu la Parthenoni lililowekwa wakfu kwa Athena, mungu mlezi wa kike wa jiji la kale la Athene. Jiwazie ukiwa miongoni mwa watu wanaomsikiliza Paulo anapozungumza kumhusu “Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo,” na kueleza kwamba “hakai katika mahekalu yaliyofanywa kwa mikono.” Mtume huyo anasema pia kwamba Mungu “alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu, ili wakae juu ya uso wa dunia nzima, naye aliamuru nyakati na mipaka ya makao ya watu, ili wao wamtafute Mungu, ikiwa wangeweza kupapasa-papasa wakimtafuta na kwa kweli wampate, ijapokuwa, kweli, hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Mdo. 17:24-27) Naam, watu wanaweza kumpata Mungu. Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni saba na nusu ‘kwa kweli wamempata,’ nao wanampenda kikweli.

KUMPENDA MUNGU HUMAANISHA NINI?

6. Yesu alisema ni ‘amri gani iliyo kuu na ya kwanza’?

6 Tunapaswa kumpenda Yehova kutoka moyoni. Yesu alisema jambo hilo waziwazi Farisayo mmoja alipomuuliza hivi: “Mwalimu, amri iliyo kuu katika ile Sheria ni gani?” Yesu akamjibu: “‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri iliyo kuu na ya kwanza.”Mt. 22:34-38.

7. Ni nini maana ya kumpenda Mungu kwa (a) ‘moyo wetu wote’? (b) ‘nafsi yetu yote’? (c) ‘akili yetu yote’?

7 Yesu alimaanisha nini aliposema kwamba ni lazima tumpende Mungu kwa ‘moyo wetu wote’? Alimaanisha kwamba ni lazima tumpende Yehova kwa moyo wetu wote wa mfano, yaani, tamaa na hisia zetu zote. Ni lazima pia tumpende kwa ‘nafsi yetu yote,’ yaani, uhai wetu. Isitoshe, ni lazima tumpende Mungu kwa ‘akili yetu yote,’ au uwezo wetu wote wa kufikiri. Kimsingi, tunapaswa kumpenda Yehova kikamili, bila masharti.

8. Kumpenda Mungu kikamili kutatuchochea kufanya nini?

8 Ikiwa tunampenda Mungu kwa moyo, akili, na nafsi yetu yote, tutajifunza Neno lake kwa bidii, tutafanya mapenzi yake kwa moyo wetu wote, na kutangaza kwa bidii habari njema ya Ufalme. (Mt. 24:14; Rom. 12:1, 2) Kumpenda kikweli Yehova kutatuchochea kumkaribia zaidi. (Yak. 4:8) Kwa kweli, tuna sababu nyingi sana za kumpenda Mungu. Hata hivyo, acheni tuchunguze sababu chache.

 KWA NINI TUNAPASWA KUMPENDA YEHOVA?

9. Kwa nini unampenda Yehova akiwa Muumba na Mwandalizi wetu?

9 Yehova ni Muumba wetu na Mwandalizi wetu. Paulo alisema hivi: “Kupitia kwake tuna uhai na tunaenda na kuwako.” (Mdo. 17:28) Yehova ametupatia dunia, makao yetu maridadi sana. (Zab. 115:16) Yeye hutuandalia pia chakula na vitu vingine vinavyoendeleza uhai wetu. Ndiyo sababu Paulo aliwaambia hivi wakaaji wa Listra walioabudu sanamu: “Mungu aliye hai . . . hakujiacha mwenyewe bila ushahidi kwa kuwa alitenda mema, akiwapa ninyi mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda, akijaza mioyo yenu kikamili kwa chakula na uchangamfu.” (Mdo. 14:15-17) Je, hiyo si sababu nzuri ya kumpenda Muumba wetu Mkuu na Mwandalizi anayetupenda?Mhu. 12:1.

10. Tunapaswa kuhisije kuhusu uandalizi wa Mungu wa kuondoa kifo na dhambi?

10 Mungu ameandaa njia ya kuondoa kifo na dhambi tuliyorithi kutoka kwa Adamu. (Rom. 5:12) Kwa kweli, “Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Rom. 5:8) Bila shaka, tunampenda sana Yehova kutoka moyoni kwa sababu amefanya iwezekane kwetu kusamehewa dhambi tukitubu kikweli na kuonyesha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu.Yoh. 3:16.

11, 12. Yehova ametupatia tumaini katika njia zipi?

11 Yehova ‘anatoa tumaini linalotujaza shangwe na amani.’ (Rom. 15:13) Mungu hutupatia tumaini linalotuwezesha kuvumilia majaribu ya imani. Watiwa-mafuta wanaobaki ‘waaminifu hata kufikia kifo watapewa taji la uzima mbinguni.’ (Ufu. 2:10) Watu watimilifu walio na tumaini la kuishi milele duniani watafurahia baraka za milele katika Paradiso iliyoahidiwa ya ulimwenguni pote. (Luka 23:43) Tunahisije kuhusu matumaini hayo? Je, hayatujazi amani na shangwe, na kutuchochea kumpenda Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu”?Yak. 1:17.

12 Mungu ametupatia tumaini la ufufuo linalotia moyo. (Mdo. 24:15) Bila shaka, tunahuzunika sana mpendwa wetu anapokufa, lakini tumaini la ufufuo linatusaidia ‘kutokuwa na huzuni kama wale wasio na tumaini.’ (1 The. 4:13) Kwa sababu ya upendo, Yehova Mungu anatamani sana kuwafufua wafu, hasa watu waaminifu kama Ayubu aliyekuwa mwadilifu. (Ayu. 14:15) Wazia jinsi tutakavyowakaribisha kwa shangwe wapendwa wanapofufuliwa duniani. Kwa kweli, tunachochewa kumpenda kwa moyo wote Baba yetu wa mbinguni, ambaye ametupatia tumaini zuri sana la ufufuo!

13. Kuna uthibitisho gani kwamba Mungu anatujali kikweli?

13 Yehova anatujali kikweli. (Soma Zaburi 34:6, 18, 19; 1 Petro 5:6, 7.) Tunajua kwamba Mungu wetu mwenye upendo yuko tayari sikuzote kuwasaidia walio waaminifu kwake, hivyo, tunahisi tukiwa salama tukiwa sehemu ya ‘kundi la malisho yake.’ (Zab. 79:13) Isitoshe, mambo ambayo Mungu atatutimizia kupitia Ufalme wa Kimasihi yatathibitisha kwamba anatupenda. Baada ya Yesu Kristo, mfalme aliyechaguliwa na Mungu kuondoa jeuri, uonevu, na uovu duniani, wanadamu watiifu watafurahia ufanisi na amani ya kudumu. (Zab. 72:7, 12-14, 16) Je, hukubali kwamba matumaini hayo yanatuchochea kumpenda kwa moyo, nafsi, nguvu, na akili yote Mungu wetu anayejali?Luka 10:27.

14. Mungu ametupatia pendeleo gani lisilo na kifani?

14 Yehova ametupatia pendeleo lisilo na kifani la kuwa Mashahidi wake. (Isa. 43:10-12) Tunampenda Mungu kwa sababu ametupatia pendeleo la kuunga mkono enzi yake kuu na kuwapa watu tumaini la kweli katika  ulimwengu huu uliojaa taabu. Isitoshe, tunaongea kwa imani na usadikisho kwa sababu tunatangaza habari njema inayotegemea Neno la Mungu wa kweli. Ahadi zake zinazowapa watu tumaini hazikosi kamwe kutimia. (Soma Yoshua 21:45; 23:14.) Bila shaka, tuna baraka na sababu nyingi sana zinazotufanya tumpende Yehova. Lakini tunawezaje kuonyesha kwamba tunampenda?

UNAWEZAJE KUONYESHA KWAMBA TUNAMPENDA MUNGU?

15. Kujifunza na kutumia Neno la Mungu kunawezaje kutusaidia?

15 Jifunze Neno la Mungu kwa bidii na kulitumia. Tunapofanya hivyo tunaonyesha kwamba tunampenda Yehova na kwa kweli tunataka neno lake liwe ‘nuru katika barabara yetu.’ (Zab. 119:105) Tunapokabili matatizo, tunaweza kufarijiwa na maneno ya upendo yenye kutia moyo kama haya: “Moyo uliovunjika na kupondwa, Ee Mungu, hutaudharau.” “Fadhili zako zenye upendo, Ee Yehova, ziliendelea kunitegemeza. Fikira zangu zinazofadhaisha zilipokuwa nyingi ndani yangu, faraja zako mwenyewe zilianza kuikumbatia nafsi yangu.” (Zab. 51:17; 94:18, 19) Yehova huwahurumia wanaoteseka, na Yesu huwasikitikia pia. (Isa. 49:13; Mt. 15:32) Kujifunza Biblia kunaweza kutusaidia kuwa na uhakika kwamba Yehova hutuhangaikia kwa upendo na hilo hutuchochea tumpende sana.

16. Kusali kwa ukawaida kunawezaje kufanya upendo wetu kumwelekea Mungu uongezeke?

16 Sali kwa Mungu kwa ukawaida. Sala zetu hutufanya tumkaribie zaidi “msikiaji wa sala.” (Zab. 65:2) Tunapoona Mungu akijibu sala zetu, upendo wetu kumwelekea unaongezeka. Kwa mfano, huenda tumeona kwamba Mungu haachi tujaribiwe kupita tunavyoweza kuhimili. (1 Kor. 10:13) Tukitoa dua na kumweleza Yehova kwa unyoofu kuhusu mahangaiko yetu, tunaweza kupata “amani ya Mungu” isiyo na kifani. (Flp. 4:6, 7) Pindi nyingine, tunaweza kusali kimya-kimya kama Nehemia alivyofanya na kugundua kwamba sala yetu inajibiwa. (Neh. 2:1-6) Kadiri ‘tunavyodumu katika sala’ na kutambua kwamba Yehova anajibu maombi yetu, ndivyo upendo wetu kumwelekea unavyoongezeka, na pia uhakika wetu wa kwamba atatusaidia kukabiliana na majaribu mengine ya imani.Rom. 12:12.

17. Ikiwa tunampenda Mungu, tutakuwa na maoni gani kuhusu kuhudhuria mikutano?

 17 Uwe na desturi ya kuhudhuria makusanyiko na mikutano ya Kikristo. (Ebr. 10:24, 25) Waisraeli walikusanyika ili kusikiliza na kujifunza kumhusu Yehova ili wamwogope na kutii Sheria yake. (Kum. 31:12) Kufanya mapenzi ya Mungu si mzigo mzito ikiwa tunampenda kikweli. (Soma 1 Yohana 5:3.) Kwa hiyo, tusiruhusu kamwe chochote kitufanye tuone kuhudhuria mikutano kuwa jambo la kivivi hivi tu. Kwa hakika hatutaki jambo lolote litufanye tupoteze upendo tuliokuwa nao mwanzoni kumwelekea Yehova.Ufu. 2:4.

18. Kumpenda Mungu hutuchochea kufanya nini kuhusiana na habari njema?

18 Hubiri kwa bidii “kweli ya habari njema.” (Gal. 2:5) Upendo wetu kuelekea Mungu hutuchochea kuongea kuhusu Ufalme wa Kimasihi wa Mwana wake mpendwa, ‘atakayepanda kwa kutetea kweli’ katika vita vya Har–Magedoni. (Zab. 45:4; Ufu. 16:14, 16) Ni shangwe iliyoje kufanya wanafunzi kwa kuwafundisha watu kuhusu upendo wa Mungu na ulimwengu mpya alioahidi!Mt. 28:19, 20.

19. Kwa nini tunapaswa kuthamini mpango wa Yehova wa kulichunga kundi lake?

19 Onyesha kwamba unathamini mpango wa Mungu wa kulichunga kundi lake. (Mdo. 20:28) Wazee Wakristo ni uandalizi kutoka kwa Yehova, ambaye hufanya mambo kwa manufaa yetu sikuzote. Wazee ni “kama mahali pa kujificha kutokana na upepo na mahali pa kujificha kutokana na dhoruba ya mvua, kama vijito vya maji katika nchi isiyo na maji, kama kivuli cha mwamba mzito katika nchi iliyochoka.” (Isa. 32:1, 2) Sisi huthamini sana mahali pa kujikinga kutokana na upepo wenye nguvu na dhoruba yenye baridi kali. Jua linapokuwa kali tunathamini sana kusimama chini ya kivuli cha mwamba. Mifano hiyo inatusaidia kutambua kwamba wazee huandaa kitulizo na msaada wa kiroho tunaohitaji. Tunapowatii wale wanaoongoza miongoni mwetu, tunaonyesha jinsi tunavyothamini sana ‘zawadi hizo katika wanadamu.’ Tunaonyesha pia kwamba tunampenda Mungu na Kristo ambaye ni Kichwa cha kutaniko.Efe. 4:8; 5:23; Ebr. 13:17.

Yehova ameandaa wachungaji wanaopendezwa kikweli na kondoo (Tazama fungu la 19)

ENDELEA KUKUA KATIKA UPENDO WAKO KUELEKEA MUNGU

20. Ikiwa unampenda Mungu, utatendaje kupatana na andiko la Yakobo 1:22-25?

20 Ikiwa unampenda Yehova na una uhusiano mzuri pamoja naye, utakuwa ‘mtendaji wa neno, si msikiaji tu.’(Soma Yakobo1:22-25.) “Mtendaji” wa neno ana imani inayomchochea kufanya kazi kama vile kuhubiri kwa bidii na kushiriki katika mikutano ya Kikristo. Kwa kuwa unampenda Mungu kikweli, utatii ‘sheria kamilifu’ ya Yehova, inayotia ndani kila jambo analotaka ufanye.Zab. 19:7-11.

21. Sala zako zinazotoka moyoni zinaweza kufananishwa na nini?

21 Kumpenda Yehova Mungu kutakuchochea kusali kwake kwa ukawaida kutoka moyoni. Ni wazi kwamba mtunga-zaburi Daudi alikuwa akirejelea uvumba uliochomwa kila siku kulingana na agano la Sheria alipoimba hivi: “Sala yangu na itayarishwe kama uvumba mbele zako [Yehova], kuinuliwa kwa mikono yangu kama toleo la jioni la nafaka.” (Zab. 141:2; Kut. 30:7, 8) Maombi yako ya unyenyekevu, dua zako za bidii, na maneno yako ya kumsifu na kumshukuru Mungu kutoka moyoni, na yawe kama uvumba wenye harufu tamu unaofananisha sala zinazokubalika.Ufu. 5:8.

22. Ni upendo wa aina gani tutakaozungumzia katika makala inayofuata?

22 Yesu alisema kwamba ni lazima tumpende Mungu na jirani yetu pia. (Mt. 22:37-39) Tunapoendelea kuzungumzia sifa ya upendo katika makala inayofuata, tutaona kwamba kumpenda Yehova na kupenda kanuni zake kutatusaidia kuwa na uhusiano mzuri na wanadamu wenzetu na kumpenda jirani yetu.