Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | KWA NINI WATU WAZURI HUPATWA NA MAMBO MABAYA?

Mungu Atafanya Nini ili Kuondoa Mambo Mabaya

Mungu Atafanya Nini ili Kuondoa Mambo Mabaya

Biblia inatuambia waziwazi kile ambacho Yehova na Mwanaye, Yesu Kristo, watafanya kuhusiana na mateso yanayoletwa na Shetani Ibilisi. “Kwa kusudi hili Mwana wa Mungu [Yesu] alifunuliwa,” inasema Biblia, “ili azivunje kazi za Ibilisi.” (1 Yohana 3:8) Mfumo wa mambo wa sasa uliojaa pupa, chuki, na uovu utavunja-vunjwa. Yesu aliahidi kwamba “mtawala wa ulimwengu huu”—Shetani Ibilisi—“atatupwa nje.” (Yohana 12:31) Bila uvutano wa Shetani, ulimwengu mpya wenye uadilifu utaanzishwa, na dunia hii itakuwa mahali salama.—2 Petro 3:13.

Namna gani wale ambao wanakataa kubadili njia zao na kuendelea kufanya mabaya? Hebu fikiria ahadi hii iliyo wazi: “Wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake. Nao waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila, watang’olewa kutoka ndani yake.” (Methali 2:21, 22) Hakutakuwa tena na wanadamu waovu. Chini ya hali hiyo ya amani, wanadamu watiifu watawekwa huru hatua kwa hatua kutokana na hali ya kutokamilika waliyorithi.—Waroma 6:17, 18; 8:21.

Mungu ataondoaje ubaya katika ulimwengu huo mpya? Si kwa kuwanyima wanadamu uhuru wa kujiamulia na kuwaongoza kama mashine. Badala yake, atawafundisha wanadamu watiifu njia zake, na kuwasaidia waache mawazo na matendo mabaya.

Mungu ataondoa mambo yote yanayosababisha kuteseka

Mungu atafanya nini kuhusu misiba isiyotazamiwa? Ameahidi kwamba serikali ya Ufalme wake itaitawala dunia hivi karibuni. Mfalme wa Ufalme huo aliyechaguliwa na Mungu ni Yesu Kristo, na ana uwezo wa kuwaponya wagonjwa. (Mathayo 14:14) Vilevile, Yesu ana uwezo wa kudhibiti nguvu za asili. (Marko 4:35-41) Hivyo, hakutakuwa tena na misiba inayosababishwa na “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhubiri 9:11) Chini ya utawala wa Kristo, wanadamu hawatakumbwa tena na misiba.Methali 1:33.

Namna gani mamilioni ya watu wasio na hatia ambao wamekufa katika misiba? Kabla tu ya kumfufua rafiki yake Lazaro, Yesu alisema: “Mimi ndiye ufufuo na uzima.” (Yohana 11:25) Naam, Yesu ana nguvu za kuwafufua, au kuwarudisha wale waliokufa kwenye uhai!

Ikiwa ungependa kuishi katika ulimwengu ambao watu wazuri hawatapatwa na mabaya, tunakusihi ujifunze mengi kumhusu Mungu wa kweli na kusudi lake kwa kujifunza Biblia. Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu watafurahi kukusaidia upate ujuzi huo. Tunakuomba uwasiliane nao katika eneo lenu au uwaandikie wachapishaji wa gazeti hili.