Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Yehova Anawajua Walio Wake”

“Yehova Anawajua Walio Wake”

“Ikiwa yeyote anampenda Mungu, huyo anajulikana naye.” —1 KOR. 8:3.

1. Ni simulizi gani la Biblia linaloonyesha jinsi baadhi ya watu wa Mungu walivyojidanganya? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

ASUBUHI moja, Kuhani Mkuu Haruni, alisimama kwenye mwingilio wa maskani ya Yehova akiwa amebeba chetezo cha kuchomea uvumba. Kora na wanaume 250, kila mmoja wao akiwa na chetezo chake, walikuwa pia wakimfukizia uvumba Yehova. (Hes. 16:16-18) Mwanzoni, wote walionekana kuwa waabudu washikamanifu wa Yehova. Hata hivyo, tofauti na Haruni, waasi hao wenye kiburi walikuwa wakijaribu kunyakua ukuhani. (Hes. 16:1-11) Walijidanganya wenyewe kwa kufikiri kwamba Mungu angekubali ibada yao. Hata hivyo, walimvunjia heshima Yehova anayeweza kusoma mioyo na kwa kweli aliona unafiki wao.—Yer. 17:10.

2. Musa alitabiri nini? Je, maneno yake yalitimia?

2 Siku iliyotangulia, Musa alitabiri hivi kwa kufaa: “Asubuhi Yehova atajulisha ni nani aliye wake.” (Hes. 16:5) Na kwa kweli Yehova alifunua wazi waabudu wa kweli na waabudu wa uwongo ‘moto ulipokuja kutoka kwa Yehova na kumteketeza Kora na wale wanaume 250 waliokuwa wakitoa uvumba.’ (Hes. 16:35; 26:10) Hata hivyo, Yehova hakumwangamiza Haruni na hivyo kuthibitisha kwamba Haruni alikuwa kuhani halali na alimwabudu kwa unyoofu.—Soma 1 Wakorintho 8:3.

3. (a) Ni hali gani iliyotokea katika siku za mtume Paulo? (b) Yehova alionyeshaje karne nyingi zilizopita kwamba yeye huwachukulia hatua waasi?

 3 Hali kama hiyo ilitokea miaka 1,500 hivi baadaye katika siku za mtume Paulo. Watu fulani waliodai kuwa Wakristo walifuata mafundisho ya uwongo huku wakishirikiana na kutaniko. Huenda waasi-imani hao hawakuonekana kuwa tofauti na washiriki wengine wa kutaniko. Hata hivyo, uasi-imani wao ulikuwa hatari kwa Wakristo waaminifu. Mbwa-mwitu hao waliojivika mavazi ya kondoo walianza ‘kupindua imani ya wengine.’ (2 Tim. 2:16-18) Hata hivyo, Yehova huona na kuchukua hatua na Paulo alijua hilo kutokana na jinsi Mungu alivyomwadhibu Kora na waasi wenzake karne nyingi zilizopita. Kuhusiana na hilo, acheni tuchunguze maneno fulani katika Biblia yanayotia moyo na tuone mambo tunayoweza kujifunza.

‘MIMI NI YEHOVA; SIBADILIKI’

4. Paulo alikuwa na uhakika gani? Alionyeshaje uhakika huo alipomwandikia Timotheo?

4 Paulo alikuwa na hakika kwamba Yehova anatambua ibada ya kinafiki, na anatambua pia wale Wanaomtii. Paulo alipomwandikia Timotheo chini ya mwongozo wa roho takatifu, alitumia maneno yaliyoonyesha kwamba alikuwa na uhakika kabisa kuhusu jambo hilo. Baada ya kutaja madhara ya kiroho ambayo tayari baadhi ya washiriki wa kutaniko walikuwa wamepata kwa sababu ya waasi-imani, Paulo aliandika hivi: “Hata hivyo, msingi imara wa Mungu unakaa ukiwa umesimama, ukiwa na muhuri huu: ‘Yehova anawajua walio wake,’ na: ‘Kila mtu anayelitaja jina la Yehova na aukatae ukosefu wa uadilifu.’”—2 Tim. 2:18, 19.

5, 6. Maneno “msingi imara wa Mungu” aliyotumia Paulo ni ya pekee kwa njia gani, na inaelekea yalimchocheaje Timotheo?

5 Maneno aliyotumia Paulo katika andiko hilo ni ya pekee kwa njia gani? Katika Biblia, maneno “msingi imara wa Mungu” yanatajwa katika mstari huo tu. Biblia hutumia neno “msingi” kwa njia ya mfano kumaanisha vitu tofauti-tofauti kama vile Yerusalemu halisi, jiji kuu la taifa la kale la Israeli. (Zab. 87:1, 2) Daraka analotimiza Yesu katika kusudi la Yehova linafananishwa pia na msingi. (1 Kor. 3:11; 1 Pet. 2:6) Hivyo, Paulo alimaanisha nini alipoandika kuhusu “msingi imara wa Mungu”?

6 Paulo alitaja “msingi imara wa Mungu” katika muktadha ambamo alinukuu maneno ya Musa katika Hesabu 16:5 kuhusu Kora na wale waliomuunga mkono. Bila shaka, Paulo alikuwa akirejelea matukio katika siku za Musa ili kumtia moyo Timotheo na kumkumbusha kuhusu uwezo wa Yehova wa kutambua na kukomesha matendo ya uasi. Kora hangeweza kuzuia kusudi la Yehova karne nyingi zilizopita, vivyo hivyo, waasi-imani waliokuwa katika kutaniko hawangeweza kulizuia lisitimie. Paulo hakufafanua kwa undani maana ya “msingi imara wa Mungu.” Hata hivyo, ni wazi kwamba maneno aliyotumia yalimchochea Timotheo kuamini kwa uhakika njia za Yehova.

7. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatenda kwa uadilifu na ukweli au uaminifu?

7 Kanuni bora za Yehova hazibadiliki. Andiko la Zaburi 33:11 linasema hivi: “Shauri la Yehova litasimama milele; mawazo ya moyo wake ni kwa kizazi kimoja baada ya kizazi kingine.” Maandiko mengine yanasema kwamba utawala wa Yehova, fadhili zake zenye upendo, uadilifu, na ukweli au uaminifu wake ni wa milele. (Kut. 15:18; Zab. 106:1; 112:9; 117:2) Andiko la Malaki 3:6 linasema hivi: ‘Mimi ni Yehova; sibadiliki.’ Andiko la Yakobo 1:17 linasema pia kwamba Yehova “habadiliki, kama kugeuka kwa kivuli.”

 “MUHURI” UNAOJENGA IMANI KATIKA YEHOVA

8, 9. Tunaweza kujifunza nini kutokana na “muhuri” wa mfano aliotaja Paulo?

8 Katika 2 Timotheo 2:19, Paulo anataja msingi wa mfano wenye ujumbe. Ni kana kwamba ujumbe huo umepigwa kwa muhuri. Katika nyakati za kale, kwa kawaida maneno yalichongwa kwenye msingi wa jengo ili kuonyesha mjenzi au mmiliki wa jengo hilo. Paulo ndiye mwandikaji wa kwanza katika Biblia kutumia mfano huo hususa. * Muhuri ulio kwenye “msingi imara wa Mungu” una matangazo mawili. Kwanza, “Yehova anawajua walio wake,” na pili, “Kila mtu anayelitaja jina la Yehova na aukatae ukosefu wa uadilifu.” Maneno hayo ya Paulo yanatukumbusha tunachosoma katika Hesabu 16:5.—Soma.

9 Tunaweza kujifunza nini kutokana na “muhuri” wa mfano aliotaja Paulo? Kwa wale walio wa Mungu, viwango na kanuni za Yehova zinaweza kutegemea kweli mbili za msingi: (1) Yehova anawapenda wale walio washikamanifu kwake, na (2) Yehova anachukia ukosefu wa uadilifu. Hilo linahusianaje na suala la uasi-imani kutanikoni?

10. Wakristo waaminifu katika siku za Paulo waliathiriwaje na matendo ya waasi-imani?

10 Inawezekana kwamba Timotheo na watumishi wengine waaminifu walihangaishwa sana na matendo ya waasi-imani waliokuwa miongoni mwao. Huenda baadhi ya Wakristo walishangaa kuona Yehova akiruhusu watu hao waendelee kuwa kutanikoni. Labda Wakristo waaminifu walijiuliza ikiwa kwa kweli Yehova aliona kwamba ushikamanifu wao thabiti ni tofauti na ibada ya kinafiki ya waasi-imani.—Mdo. 20:29, 30.

Timotheo hangeweza kupotoshwa na matendo ya wale waliokuwa na mielekeo ya uasi-imani (Tazama fungu la 10-12)

11, 12. Barua ya Paulo iliimarishaje imani ya Timotheo?

11 Ni wazi kwamba barua ya Paulo iliimarisha imani ya Timotheo kwa kumkumbusha kilichotokea wakati Yehova alipothibitisha kwamba alimkubali Haruni aliyekuwa mwaminifu. Lakini Kora na wenzake walifunuliwa wazi kuwa wanafiki, wakakataliwa, na kuangamizwa. Kwa njia fulani, Paulo alikuwa akisema kwamba ijapokuwa Wakristo wa uwongo walikuwa miongoni mwao, Yehova angejua walio wake kikweli, kama tu alivyofanya katika siku za Musa.

12 Yehova habadiliki kamwe; anategemeka. Anachukia ukosefu wa uadilifu, na  kwa wakati unaofaa anawahukumu wakosaji wasiotubu. Kwa kuwa Timotheo ‘alilitaja jina la Yehova,’ alikumbushwa pia wajibu wake wa kukataa ukosefu wa uadilifu wa Wakristo wa uwongo. *

IBADA YA KWELI SI YA BURE KAMWE

13. Tunaweza kuwa na uhakika gani?

13 Maneno ya Paulo yaliyoongozwa na roho yanaweza kutuimarisha sisi pia kiroho. Kwanza kabisa, inatia moyo kujua kwamba Yehova anajua vizuri ushikamanifu wetu kwake. Mbali na kwamba anajua ushikamanifu wetu, Yehova anapendezwa sana na wale walio wake. Biblia inasema hivi: “Kwa habari ya Yehova, macho yake yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.” (2 Nya. 16:9) Kwa hiyo, tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba lolote tunalofanya kwa ajili ya Yehova “kutokana na moyo safi,” si bure kamwe.—1 Tim. 1:5; 1 Kor. 15:58.

14. Yehova havumilii ibada ya aina gani?

14 Kujua kwamba Yehova havumilii ibada ya kinafiki kunapaswa pia kuwa onyo kwetu. Kwa kuwa “macho yake yanaenda huku na huku duniani,” anaweza kutambua wale ambao moyo wao si “mkamilifu kumwelekea yeye.” Andiko la Methali 3:32 linasema kwamba “mtu mwenye hila ni chukizo kwa Yehova,” kwa kuwa, mtu wa namna hiyo hujifanya mtiifu lakini anatenda dhambi kwa siri. Ingawa mtu mwenye hila anaweza kwa ujanja kuwadanganya wanadamu kwa muda, Yehova aliye Mweza-Yote na mwadilifu anatuhakikishia kwamba “anayefunika makosa yake hatafanikiwa.”—Met. 28:13; soma 1 Timotheo 5:24; Waebrania 4:13.

15. Tunapaswa kuepuka nini, na kwa nini?

15 Watumishi wengi wa Yehova wanamtumikia kwa unyoofu. Si kawaida kwa Mkristo kutanikoni kuamua kimakusudi kuwa mnafiki katika ibada yake. Hata hivyo, ikiwa hilo lilitokea katika siku za Musa na katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, linaweza pia kutokea leo. (2 Tim. 3:1, 5) Lakini je, tuwatilie shaka Wakristo wenzetu na kufikiri kwamba unyoofu na ushikamanifu wao kwa Yehova si wa kweli? La hasha! Ni kosa kuwatilia shaka ndugu na dada zetu bila msingi. (Soma Waroma 14:10-12; 1 Wakorintho 13:7.) Isitoshe, mwelekeo wa kutilia shaka utimilifu wa wengine kutanikoni utatudhuru kiroho.

16. (a) Kila mmoja wetu anaweza kufanya nini ili unafiki usitie mizizi moyoni mwake? (b) Tunajifunza nini kutokana na sanduku lenye kichwa “ Endeleeni Kujijaribu . . . Endeleeni Kuthibitisha . . . ”?

16 Kila Mkristo anapaswa “athibitishe kazi yake mwenyewe.” (Gal. 6:4) Kwa sababu ya mwelekeo wetu wa kutenda dhambi, tunakabili daima hatari ya kutokuwa wanyoofu. (Ebr. 3:12, 13) Hivyo, tunapaswa kuchunguza mara kwa mara nia yetu ya kumtumikia Yehova. Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninamwabudu Yehova kwa sababu ninampenda na ninatambua enzi yake kuu? Au ninakazia zaidi baraka za kimwili ninazotazamia kufurahia katika Paradiso?’ (Ufu. 4:11) Kwa kweli, sote tunaweza kunufaika tukichunguza matendo yetu na kuondoa unafiki wowote moyoni mwetu.

USHIKAMANIFU UNAOLETA FURAHA

17, 18. Kwa nini tunapaswa kumwabudu Yehova kwa unyoofu na uaminifu?

17 Tunanufaika sana tunapojitahidi kumwabudu Yehova kwa unyoofu na uaminifu. Mtunga-zaburi alisema hivi: “Mwenye furaha ni mtu ambaye Yehova hamhesabii kosa, na ambaye katika roho yake hamna  udanganyifu.” (Zab. 32:2) Naam, wale wanaoondoa unafiki moyoni mwao ni wenye furaha zaidi, na wanatumaini kupata furaha kamili wakati ujao.

18 Hivi karibuni, Yehova atawafunua wote wanaozoea kutenda mabaya au wanaoishi maisha ya kinafiki. Ataonyesha wazi ‘tofauti kati ya mwadilifu na mwovu, kati ya mtu anayemtumikia Mungu na mtu ambaye hamtumikii.’ (Mal. 3:18) Kwa sasa, inatia moyo kujua kwamba “macho ya Yehova yako juu ya waadilifu, na masikio yake yanaielekea dua yao.”—1 Pet. 3:12.

^ fu. 8 Andiko la Ufunuo 21:14 lililoandikwa miaka mingi baada ya barua za Paulo kwa Timotheo, linataja ‘mawe kumi na mawili ya msingi’ yaliyoandikwa majina kumi na mawili ya mitume.

^ fu. 12 Katika makala inayofuata tutachunguza jinsi tunavyoweza kumwiga Yehova kwa kukataa kabisa ukosefu wa uadilifu.