Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU

Je, Mungu Anakujali?

Je, Mungu Anakujali?

“Mimi ninateseka nami ni maskini. Yehova mwenyewe ananijali.” *MFALME DAUDI WA ISRAELI, KARNE YA 11 K.W.K.

“Mataifa ni kama tone kutoka katika ndoo.”—ISAYA 40:15

Je, ilikuwa sawa kwa Daudi kutarajia Mungu amjali? Je, Mungu anakujali? Watu wengi hawaamini kwamba Mungu mweza-yote anawajali. Kwa nini?

Sababu moja ni kwamba Mungu ana uhai wa hali ya juu kuliko wanadamu. Akiwa kwenye makao yake yaliyotukuka, mataifa yote “ni kama tone kutoka katika ndoo; nayo yamehesabiwa kuwa kama mavumbi membamba juu ya mizani.” (Isaya 40:15) Mwandishi mmoja asiyeamini Mungu alisema kwamba “ni kiburi cha hali ya juu kuamini kwamba kuna Mungu anayekujali na anayehangaikia matendo yako.”

Kwa upande mwingine, baadhi ya watu huhisi kwamba tabia zao zinawafanya wasiwe na thamani machoni pa Mungu. Kwa mfano, mwanamume anayeitwa Jim mwenye umri wa makamo anasema hivi: “Kila mara nilisali ili nipate amani ya akili na kujidhibiti, lakini punde si punde, nilikasirika tena. Mwishowe niliamini kwamba nilikuwa mwovu sana na hivyo Mungu hangenisaidia.”

Je, Mungu yuko mbali sana na wanadamu hivi kwamba hawajali? Yeye huhisije kuhusu wanadamu wenye dhambi? Bila msaada wa Mungu hakuna mwanadamu anayeweza kujibu maswali hayo. Hata hivyo, ujumbe wa Mungu kwa wanadamu, yaani, Biblia hutuhakikishia kwamba yuko karibu na wanadamu na anawajali. Biblia inasema, “kweli, hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Katika makala nne zifuatazo, tutachunguza jinsi ambavyo Mungu amethibitisha kwamba anawajali wanadamu kutia ndani wewe.