Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe na Imani Isiyotikisika Katika Ufalme

Uwe na Imani Isiyotikisika Katika Ufalme

“Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa.”—EBR. 11:1.

1, 2. Ni nini kitakachoimarisha usadikisho wetu kwamba Ufalme utatimiza kusudi la Mungu kuelekea wanadamu, na kwa nini? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

TUKIWA Mashahidi wa Yehova, mara nyingi tunasema kwamba Ufalme wa Mungu ndio suluhisho pekee la matatizo yetu yote, na tunawahubiria wengine kwa bidii kuhusu kweli hiyo muhimu ya Kimaandiko. Pia, tumaini hilo la Ufalme linatufariji sana. Hata hivyo, tuna usadikisho thabiti kadiri gani kwamba Ufalme huo ni halisi na utatimiza kusudi lake? Kwa nini tunahitaji kuwa na imani isiyotikisika katika Ufalme huo?—Ebr. 11:1.

2 Ufalme wa Kimasihi ulianzishwa na Mweza-Yote mwenyewe ili kutimiza kusudi lake kuelekea viumbe wake. Ufalme huo unategemea msingi usiotikisika, yaani, haki kamili ya Yehova ya kutawala. Mambo yote muhimu ya Ufalme huo, yaani, mfalme wake, watawala wenzake, na eneo watakalotawala, yamethibitishwa kisheria kupitia maagano—mikataba au mipango ya kisheria inayomhusisha Mungu au Mwana wake, Yesu Kristo. Kutafakari kuhusu maagano hayo kutatusaidia kuelewa vizuri zaidi jinsi kusudi la Mungu litakavyotimia kwa  uhakika na jinsi mpango wa Ufalme ulivyo imara.—Soma Waefeso 2:12.

3. Tutachunguza nini katika makala hii na inayofuata?

3 Biblia inataja maagano sita ya msingi yanayohusiana na Ufalme wa Kimasihi ulio mikononi mwa Kristo Yesu. Maagano hayo ni (1) agano la Abrahamu, (2) agano la Sheria, (3) agano la Daudi, (4) agano la kuhani aliye kama Melkizedeki, (5) agano jipya, na (6) agano la Ufalme. Acheni tuchunguze jinsi kila agano linavyohusiana na Ufalme na kutimizwa kwa kusudi la Mungu kuelekea dunia na wanadamu.—Tazama makala yenye kichwa “ Jinsi Mungu Atakavyotimiza Kusudi Lake.”

AHADI YAFUNUA JINSI KUSUDI LA MUNGU LITAKAVYOTIMIA

4. Kulingana na kitabu cha Mwanzo, ni maagizo gani aliyotoa Yehova kuhusiana na wanadamu?

4 Baada ya kuitayarisha sayari yetu maridadi ili wanadamu waishi humo, Yehova alitoa maagizo matatu yanayowahusu wanadamu: Mungu wetu angewaumba wanadamu kwa mfano wake, wanadamu wangepanua Paradiso ili ienee duniani pote na kuijaza wazao wao waadilifu, na wanadamu walikatazwa kula matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya. (Mwa. 1:26, 28; 2:16, 17) Maagizo hayo matatu yalitosha kutimiza kusudi la Mungu. Baada ya wanadamu kuumbwa, walihitaji tu kufuata yale maagizo mawili yaliyobaki ili kusudi la Mungu litimie. Basi, kwa nini maagano yalihitajiwa?

5, 6. (a) Shetani alijaribu jinsi gani kuzuia kusudi la Mungu lisitimie? (b) Yehova alijibuje madai ya Shetani katika Edeni?

5 Akiwa na nia mbaya sana ya kuzuia kusudi la Mungu lisitimie, Shetani Ibilisi alianzisha uasi. Alikazia fikira agizo la wanadamu kumtii Mungu kwa kuwa alijua kwamba angewanasa kwa urahisi zaidi kupitia njia hiyo. Alimshawishi mwanamke wa kwanza, Hawa, kutotii sheria iliyowakataza kula matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya. (Mwa. 3:1-5; Ufu. 12:9) Kwa kufanya hivyo, Shetani alipinga haki ya Mungu ya kutawala viumbe Wake. Baadaye, Shetani pia alidai kwamba watumishi washikamanifu wa Mungu humtumikia kwa sababu za kichoyo.—Ayu. 1:9-11; 2:4, 5.

6 Yehova angejibuje madai aliyotoa Shetani katika Edeni? Kwa kweli, kuwaangamiza waasi hao kungekomesha uasi wao. Hata hivyo, kusudi alilotangaza Mungu la kuijaza dunia wazao watiifu wa Adamu na Hawa lisingetimia pia. Badala ya kuwaua waasi hao papo hapo, Muumba mwenye hekima alitoa unabii muhimu sana, ile ahadi ya Edeni, ili kuhakikisha kwamba kila jambo alilosema lingetimia.—Soma Mwanzo 3:15.

7. Ahadi ya Edeni inatuhakikishia nini kuhusu nyoka na uzao wake?

7 Kupitia ahadi aliyotoa katika Edeni, Yehova alimhukumu nyoka na uzao wake, yaani, Shetani Ibilisi pamoja na wote ambao wangemuunga mkono katika suala la haki ya Mungu ya kutawala. Mungu wa kweli aliupa uzao wa mwanamke wake wa kimbingu mamlaka ya kumwangamiza Shetani. Hivyo, ahadi ya Edeni ilikazia kwamba yule aliyeanzisha uasi katika bustani ya Edeni angeangamizwa na madhara ya matendo yake kuondolewa kabisa. Isitoshe, inaonyesha njia itakayotumiwa kutimiza mambo hayo.

8. Tunaweza kusema nini kuhusu utambulisho wa mwanamke na uzao wake?

8 Ni nani angekuwa uzao wa mwanamke? Kwa kuwa uzao huo ungeponda kichwa cha nyoka, yaani, “kumwangamiza” yule kiumbe wa roho Shetani Ibilisi, uzao huo ungekuwa pia kiumbe wa roho. (Ebr.  2:14) Kwa hiyo, mwanamke ambaye angetokeza uzao huo angekuwa wa kiroho pia. Uzao wa nyoka uliendelea kuongezeka, lakini utambulisho wa mwanamke na uzao wake ulibaki kuwa siri kwa karibu miaka 4,000 baada ya Yehova kutoa ahadi ya Edeni. Katika kipindi hicho, Yehova alifanya maagano kadhaa yanayotambulisha uzao wa mwanamke na kuwahakikishia watumishi Wake kwamba Angetumia uzao huo kuondoa msiba ambao Shetani aliwaletea wanadamu.

AGANO LAUTAMBULISHA ULE UZAO

9. Agano la Abrahamu ni nini, na lilianza kufanya kazi lini?

9 Miaka elfu mbili hivi baada ya kutangaza hukumu dhidi ya Shetani, Yehova alimwamuru mzee wa ukoo, Abrahamu, aondoke nyumbani kwake Uru, Mesopotamia, na kuhamia nchi ya Kanaani. (Mdo. 7:2, 3) Yehova alimwambia hivi: “Nenda zako kutoka katika nchi yako na kutoka kwa watu wa jamaa yako na kutoka kwa nyumba ya baba yako mpaka katika nchi ambayo nitakuonyesha; nami nitafanya taifa kubwa kutokana nawe, nitakubariki na kulifanya jina lako kuwa kuu; nawe uwe baraka. Nami nitawabariki wale wanaokubariki, na yule anayekulaani nitamlaani, na familia zote za nchi zitajibariki kupitia kwako.” (Mwa. 12:1-3) Hilo ndilo simulizi la kwanza kabisa kuandikwa kuhusu Agano la Abrahamu, ambalo Yehova Mungu alifanya na Abrahamu. Haijulikani kihususa ni lini Yehova alipofanya agano hilo kwa mara ya kwanza pamoja na Abrahamu. Hata hivyo, lilianza kufanya kazi mwaka wa 1943 K.W.K., Abrahamu alipoondoka Harani na kuvuka Mto Efrati akiwa na umri wa miaka 75.

10. (a) Abrahamu alionyeshaje kwamba ana imani isiyotikisika katika ahadi za Mungu? (b) Yehova alifunua hatua kwa hatua habari gani kuhusu uzao wa yule mwanamke?

10 Yehova alitaja tena ahadi yake kwa  Abrahamu mara kadhaa, akimweleza mambo mengi zaidi. (Mwa. 13:15-17; 17:1-8, 16) Na Abrahamu alipoonyesha imani isiyotikisika katika ahadi za Mungu kwa kuwa tayari kumtoa mwanawe wa pekee, Yehova aliimarisha agano hilo kwa kutoa ahadi isiyo na masharti yoyote. (Soma Mwanzo 22:15-18; Waebrania 11:17, 18.) Baada ya agano la Abrahamu kuanza kufanya kazi, Yehova alifunua hatua kwa hatua habari muhimu kuhusu uzao wa yule mwanamke. Uzao huo ungetoka kwa Abrahamu, ungetia ndani watu wengi, ungekuwa wa kifalme, ungewaangamiza maadui wote, na ungewaletea baraka watu wengine wengi.

Abrahamu alionyesha kwamba ana imani isiyotikisika katika ahadi za Mungu (Tazama fungu la 10)

11, 12. Maandiko yanaonyeshaje kwamba agano la Abrahamu lina utimizo mkubwa zaidi, na hilo linamaanisha nini kwetu?

11 Ingawa agano la Abrahamu lilitimizwa kihalisi wazao wa Abrahamu waliporithi Nchi ya Ahadi, Maandiko yanaonyesha kwamba masharti ya agano hilo yana utimizo wa kiroho pia. (Gal. 4:22-25) Kama mtume Paulo alivyoeleza kwa mwongozo wa roho, katika utimizo mkubwa zaidi wa kiroho, Kristo ndiye sehemu ya msingi ya uzao wa Abrahamu na sehemu ya pili ni Wakristo 144,000 waliotiwa mafuta kwa roho. (Gal. 3:16, 29; Ufu. 5:9, 10; 14:1, 4) Mwanamke anayetokeza uzao huo ni “Yerusalemu la juu,” yaani, sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Mungu, inayofanyizwa na viumbe wa roho walio washikamanifu. (Gal. 4:26, 31) Kama agano la Abrahamu lilivyoahidi, uzao wa mwanamke ungewaletea wanadamu baraka.

12 Agano la Abrahamu linatufunulia kuhusu Mfalme na watawala wenzake katika Ufalme wa Mungu, na ndilo msingi wa kisheria wa Ufalme wa mbinguni. (Ebr. 6:13-18) Agano hilo litaendelea kufanya kazi kwa muda gani? Andiko la Mwanzo 17:7 linasema kwamba ni “agano la mpaka wakati usio na kipimo,” au milele. Litaendelea kufanya kazi mpaka Ufalme wa Kimasihi utakapowaangamiza maadui wote wa Mungu na familia zote duniani kubarikiwa. (1 Kor. 15:23-26) Kwa kweli, wale watakaoishi duniani wakati huo watanufaika milele. Agano ambalo Mungu alifanya na Abrahamu linaonyesha kwamba Yehova ameazimia kutimiza kusudi lake la wanadamu waadilifu ‘kuijaza dunia’!—Mwa. 1:28.

AGANO LINALOHAKIKISHA KWAMBA UFALME UTADUMU

13, 14. Agano la Daudi linatuhakikishia nini kuhusu utawala wa Kimasihi?

13 Ahadi ya Edeni na agano la Abrahamu huthibitisha jambo muhimu la kwamba Enzi Kuu ya Yehova inayodhihirishwa kupitia Ufalme wa Kimasihi inategemea kabisa viwango vya Mungu vya uadilifu. (Zab. 89:14) Je, kuna uwezekano kwamba serikali ya Kimasihi itakuwa na ufisadi na hivyo kuondolewa? Agano lingine la kisheria linahakikisha kwamba jambo hilo halitatokea kamwe.

14 Fikiria ahadi ambayo Yehova alimpa Mfalme Daudi wa Israeli kupitia agano la Daudi. (Soma 2 Samweli 7:12, 16.) Yehova alifanya agano hilo pamoja na Daudi alipokuwa akitawala Yerusalemu, na alimwahidi kwamba Masihi angekuwa mzao wake. (Luka 1:30-33) Hivyo, Yehova aliendelea kufunua ukoo hususa ambao ungetokeza ule uzao na kuthibitisha kwamba mrithi wa Daudi angekuwa na “haki ya kisheria” ya kumiliki kiti cha Ufalme wa Kimasihi. (Eze. 21:25-27) Kupitia Yesu, ufalme wa Daudi ‘utafanywa imara mpaka wakati usio na kipimo.’ Kwa kweli, uzao wa Daudi “utakuwako mpaka wakati  usio na kipimo, na kiti chake cha ufalme kama vile jua.” (Zab. 89:34-37) Naam, utawala wa Masihi hautakuwa kamwe na ufisadi, na mambo utakayotimiza yatadumu milele!

AGANO LATOSHELEZA UHITAJI WA UKUHANI

15-17. Kulingana na agano la kuhani aliye kama Melkizedeki, ule uzao ungekuwa na jukumu gani lingine, na kwa nini?

15 Ingawa agano la Abrahamu na agano la Daudi yanathibitisha kwamba uzao wa mwanamke ungekuwa wa kifalme, jukumu hilo peke yake halingeweza kuwaletea baraka watu wa mataifa yote. Ili wabarikiwe kikweli, wangehitaji kuwekwa huru kutokana na hali yao ya dhambi na kuingizwa katika familia ya Mungu ya ulimwengu mzima. Ili hilo litimie, ni lazima uzao huo utimize jukumu la kikuhani. Muumba mwenye hekima alitosheleza uhitaji huo kupitia mpango mwingine wa kisheria, lile agano la kuhani aliye kama Melkizedeki.

16 Yehova alifunua kupitia Mfalme Daudi kwamba Angefanya agano la kibinafsi na Yesu ili kutimiza malengo haya mawili: kuhakikisha kwamba ‘anaketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu’ mpaka awatiishe adui zake na kuwa “kuhani mpaka wakati usio na kipimo kwa mfano wa Melkizedeki.” (Soma Zaburi 110:1, 2, 4.) Kwa nini awe kuhani “kwa mfano wa Melkizedeki”? Kwa sababu muda mrefu kabla ya mzao yeyote wa Abrahamu kurithi Nchi ya Ahadi, Melkizedeki, mfalme wa Salemu, alitumika akiwa “kuhani wa Mungu Aliye Juu Zaidi.” (Ebr. 7:1-3) Aliwekwa rasmi moja kwa moja na Yehova ili kutimiza jukumu hilo. Ni yeye peke yake anayetajwa katika Maandiko ya Kiebrania aliyetumika akiwa mfalme na kuhani. Isitoshe, kwa kuwa hakuna mtu mwingine aliyetumika katika mgawo huo kabla au baada yake, anaweza kuitwa “kuhani daima,” au milele.

17 Yesu anawekwa rasmi moja kwa moja kuwa kuhani kupitia agano hilo la kibinafsi alilofanya na Yehova, naye atadumu akiwa “kuhani milele kwa mfano wa Melkizedeki.” (Ebr. 5:4-6) Hilo linaonyesha wazi kwamba Yehova amejipa wajibu wa kisheria wa kutumia Ufalme wa Kimasihi kutimiza kusudi lake la mwanzoni kuelekea wanadamu duniani.

MAAGANO NDIYO MSINGI WA KISHERIA WA UFALME

18, 19. (a) Maagano ambayo tayari tumezungumzia yanaonyesha nini kuhusu Ufalme? (b) Ni maswali gani yanayobaki?

18 Tunapofikiria maagano ambayo tumechunguza, tunaweza kuona jinsi yanavyohusiana na Ufalme wa Kimasihi na jinsi mpango wa Ufalme unavyotegemea kabisa mikataba ya kisheria. Ahadi ya Edeni inampa Yehova wajibu wa kutimiza kusudi lake kuelekea dunia na wanadamu kupitia uzao wa yule mwanamke. Uzao huo ni nani, nao ungetimiza jukumu gani? Agano la Abrahamu linaweka msingi wa mambo hayo yote.

19 Agano la Daudi linatoa habari zaidi hususa kuhusu ukoo ambao ungetokeza sehemu ya msingi ya uzao huo na kumpa haki ya kutawala juu ya dunia ili mambo yanayotimizwa na Ufalme huo yadumu milele. Agano la kuhani aliye mfano wa Melkizedeki ndio msingi unaowezesha uzao huo kutumika kama kuhani. Hata hivyo, Yesu hatawasaidia wanadamu kufikia ukamilifu akiwa peke yake. Wengine wanatiwa mafuta pia ili kutumika wakiwa wafalme na makuhani. Wangetoka wapi? Jambo hilo litazungumziwa katika makala inayofuata.