Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Ni Lazima Tuwe Watakatifu?

Kwa Nini Ni Lazima Tuwe Watakatifu?

Mtakuwa watakatifu.”LAW. 11:45.

1. Kitabu cha Mambo ya Walawi kinawezaje kutusaidia?

KITABU cha Mambo ya Walawi kinataja sifa ya utakatifu mara nyingi zaidi kuliko kitabu kingine chochote cha Biblia. Kwa kuwa ni lazima waabudu wote wa kweli wa Yehova wawe watakatifu, kuelewa na kuthamini kitabu cha Mambo ya Walawi kutatusaidia kuwa watakatifu.

2. Ni baadhi ya mambo gani yaliyo katika kitabu cha Mambo ya Walawi?

2 Kitabu cha Mambo ya Walawi, kilichoandikwa na nabii Musa, ni sehemu ya “Andiko lote” ambalo ni lenye faida kwa kufundisha. (2 Tim. 3:16) Kwa wastani, jina la Yehova linapatikana mara kumi katika kila sura ya kitabu cha Mambo ya Walawi. Kuelewa kitabu cha Mambo ya Walawi kutatuimarisha ili tuepuke kufanya jambo lolote litakaloletea jina la Mungu suto. (Law. 22:32) Maneno “mimi ni Yehova” yanayotajwa tena na tena katika kitabu hicho yanapaswa kutukumbusha kumtii Mungu. Katika makala hii na inayofuata, tutachunguza baadhi ya hazina zenye thamani katika kitabu cha Mambo ya Walawi ambacho ni zawadi kutoka kwa Mungu inayotusaidia kumtolea ibada takatifu.

 TUNAPASWA KUWA WATAKATIFU

3, 4. Kuoshwa kwa Haruni na wanawe kulifananisha nini? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 8.)

3 Soma Mambo ya Walawi 8:5, 6Yehova alimchagua Haruni awe kuhani mkuu wa Israeli, na wanawe wawe makuhani wa taifa hilo. Haruni anafananisha Yesu Kristo na wana wa Haruni wanafananisha wafuasi watiwa-mafuta wa Yesu. Je, kuoshwa kwa Haruni kulifananisha kusafishwa kwa Yesu? Hapana, Yesu hakuwa na dhambi na alikuwa “bila dosari,” hivyo hakuhitaji kusafishwa. (Ebr. 7:26; 9:14) Hata hivyo, kuoshwa kwa Haruni kunafananisha usafi na uadilifu wa Yesu. Basi kuoshwa kwa wana wa Haruni kunafananisha nini?

4 Kuoshwa kwa wana wa Haruni kulifananisha kusafishwa kwa wale wanaochaguliwa kuwa washiriki wa ukuhani wa kimbingu. Je, ubatizo wa watiwa-mafuta unahusiana na kusafishwa kwa wana wa Haruni? Hapana, ubatizo hauoshi na kuondoa dhambi; badala yake, unaonyesha kwamba mtu amejiweka wakfu kwa Yehova Mungu bila masharti. Watiwa-mafuta wanaoshwa “kwa njia ya neno,” hivyo wanapaswa kufuata kwa moyo wote mafundisho ya Kristo maishani mwao. (Efe. 5:25-27) Kwa kufanya hivyo, wanatakaswa na kusafishwa. Lakini namna gani “kondoo wengine”?—Yoh. 10:16.

5. Kwa nini tunaweza kusema kwamba kondoo wengine wanasafishwa kwa njia ya Neno la Mungu?

5 Wana wa Haruni hawakufananisha “umati mkubwa” wa kondoo wengine. (Ufu. 7:9) Basi je, Wakristo hao waliobatizwa wanakuwa pia watakatifu na kusafishwa kwa njia ya Neno la Mungu? Ndiyo! Wale walio na tumaini la kuishi milele duniani wanaposoma yale ambayo Biblia inasema kuhusu umuhimu na nguvu za damu ya Yesu iliyomwagwa, wanaamini mambo hayo na kutoa “utumishi mtakatifu mchana na usiku.” (Ufu. 7:13-15) Watiwa-mafuta na kondoo wengine ‘wanadumisha mwenendo mzuri’ kwa sababu wanaendelea kusafishwa. (1 Pet. 2:12) Bila shaka Yehova anafurahi sana anapoona usafi na umoja wa watiwa-mafuta na kondoo wengine wanaomsikiliza na kumfuata kwa ushikamanifu Mchungaji wao, Yesu.

Je, umeazimia kutii sheria ya Yehova kuhusu damu? (Tazama fungu la 14 na 15)

6. Kwa nini tunapaswa kujichunguza kwa ukawaida?

6 Takwa la makuhani Waisraeli kuwa safi kimwili lina maana sana kwa watu wa Yehova leo. Mara nyingi wale tunaowafundisha Biblia huona kwamba mahali petu pa ibada ni safi na sisi wenyewe tuko safi na tunavalia vizuri. Isitoshe, usafi wa makuhani unatusaidia kutambua kwamba mtu yeyote anayepanda mlima uliokwezwa wa ibada ya Yehova ni lazima awe “safi moyoni.” (Soma Zaburi 24:3, 4; Isa. 2:2, 3.) Ni lazima tumtolee Mungu utumishi mtakatifu kwa akili, mioyo, na miili safi. Kwa hiyo, tunapaswa kujichunguza kwa ukawaida na huenda baadhi yetu tukahitaji kufanya mabadiliko makubwa ili kuwa watakatifu. (2 Kor. 13:5) Kwa mfano, Mkristo aliyebatizwa anayetazama ponografia kimakusudi anapaswa kujiuliza, ‘Je, mimi ni mtakatifu?’ Kisha anapaswa kutafuta msaada ili aache zoea hilo chafu.—Yak. 5:14.

IWENI WATAKATIFU KWA KUWA WATIIFU

7. Kulingana na Mambo ya Walawi 8:22-24, Yesu aliweka mfano gani?

7 Ukuhani ulipoanzishwa katika Israeli, damu ya kondoo-dume ilipakwa kwenye sikio la kuume, kidole gumba cha mkono wa kuume, na kidole kikubwa cha mguu wa kuume wa Kuhani Mkuu Haruni na wanawe. (Soma Mambo ya Walawi 8:22-24.) Damu ilitumiwa kwa njia hiyo kuonyesha kwamba makuhani wangetii na kujitahidi kabisa kutimiza majukumu yao. Vivyo hivyo, Kuhani Mkuu Yesu aliwawekea  watiwa-mafuta na kondoo wengine mfano mkamilifu. Sikio lake lilisikiliza mwongozo wa Mungu. Yesu alitumia mikono yake kufanya mapenzi ya Yehova, na miguu yake haikukengeuka kamwe kutoka kwenye njia takatifu.—Yoh. 4:31-34.

8. Ni lazima waabudu wote wa Yehova wafanye nini?

8 Ni lazima Wakristo watiwa-mafuta na kondoo wengine wa Yesu waige utimilifu wa Kuhani wao Mkuu. Ni lazima waabudu wote wa Yehova watii miongozo iliyo katika Neno la Mungu na hivyo kuepuka kuihuzunisha roho yake. (Efe. 4:30) Ni lazima ‘waifanyie miguu yao mapito yaliyonyooka.’—Ebr. 12:13.

9. Ndugu watatu ambao wamefanya kazi kwa ukaribu na washiriki wa Baraza Linaloongoza walisema nini, na maneno yao yanawezaje kukusaidia kuendelea kuwa mtakatifu?

9 Fikiria maelezo ya kutoka moyoni ya ndugu watatu wenye tumaini la kuishi milele duniani ambao kwa miaka mingi wamefanya kazi kwa ukaribu na washiriki wa Baraza Linaloongoza. Mmoja wao alisema hivi: “Ingawa kufanya kazi pamoja na ndugu hao ni pendeleo la pekee la utumishi, nimeona kwamba wao si wakamilifu licha ya kwamba wametiwa mafuta kwa roho. Hata hivyo, mojawapo ya miradi ambayo nimekuwa nayo kwa miaka mingi ni kuwatii wale wanaoongoza.” Ndugu wa pili alisema hivi: “Maandiko kama vile 2 Wakorintho 10:5 yanayotuhimiza ‘tumtii Kristo,’ yamenisaidia kutii na kushirikiana na wale wanaoongoza. Ninatii kutoka moyoni.” Ndugu wa tatu alisema hivi: “Tunaonyesha kwamba tunapenda mambo anayopenda Yehova na kuchukia anayochukia, na pia tunatafuta daima mwongozo wake na kufanya mambo yanayompendeza tunapotii tengenezo lake na wale anaowatumia kuendeleza kusudi lake duniani.” Ndugu huyo aliona kwamba Nathan Knorr, ambaye baadaye alikuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alikubali kwa utayari mambo yaliyozungumziwa kwenye makala yenye kichwa “Kuzaliwa kwa Taifa,” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la mwaka wa 1925 (la Kiingereza), hata ingawa wengine waliyatilia shaka. Ndugu huyo aliguswa moyo sana na utii wa Ndugu Knorr. Kutafakari maneno ya ndugu hao watatu kunaweza kukusaidia kuwa mtakatifu kwa kutii.

KUWA WATAKATIFU KWA KUTII SHERIA YA MUNGU KUHUSU DAMU

10. Kwa nini ni muhimu sana kutii sheria ya Mungu kuhusu damu?

10 Soma Mambo ya Walawi 17:10. Yehova aliwaamuru Waisraeli wasile “namna yoyote ya damu.” Kujiepusha na damu ya mnyama au ya mwanadamu ni takwa la Kikristo pia. (Mdo. 15:28, 29) Hatungependa kamwe Mungu ‘auweke uso wake dhidi yetu’ na kutukatilia mbali kutoka katika kutaniko lake. Tunampenda na tunataka kumtii. Hata tunapokabili hali inayohatarisha uhai wetu, tunaazimia kutokubali kushawishiwa na wale wasiomjua Yehova na wasiotaka kamwe kumtii. Naam, tunajua kwamba tutadhihakiwa kwa sababu ya kujiepusha na damu, lakini tumeamua kumtii Mungu. (Yuda 17, 18) Ni mambo gani yatakayotuimarisha ili ‘tuazimie kwa uthabiti’ kutokula damu au kutotiwa damu mishipani?—Kum. 12:23.

11. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Siku ya Upatanisho ya kila mwaka haikuwa tu desturi?

11 Kuchunguza jinsi kuhani mkuu katika taifa la kale la Israeli alivyotumia damu ya wanyama katika Siku ya Upatanisho ya kila mwaka kunatusaidia kuelewa maoni ya Mungu kuhusu damu. Damu ilitumiwa tu kwa njia ya pekee. Ilitumiwa kufanya upatanisho kwa ajili ya dhambi za wale waliotafuta msamaha wa Yehova. Damu ya ng’ombe-dume na mbuzi ilipaswa kutapanywa kukielekea kifuniko cha sanduku la agano na mbele yake. (Law. 16:14,  15, 19) Tendo hilo lilifungua njia ili Yehova asamehe dhambi za Waisraeli. Isitoshe, Yehova aliamuru kwamba mtu aliyemuua mnyama kwa ajili ya chakula, alipaswa kumwaga damu ya mnyama huyo na kuifunika kwa mavumbi, “kwa sababu nafsi ya kila mwili wa namna yoyote iko katika damu yake.” (Law. 17:11-14) Je, mambo yote hayo yalikuwa desturi isiyo na maana? Hapana. Matumizi ya damu katika Siku ya Upatanisho, na pia amri ya kumwaga damu ardhini, inapatana na amri ambayo Yehova alimpa Noa na wazao wake kuhusu damu. (Mwa. 9:3-6) Yehova Mungu aliwakataza kuendeleza uhai wao kwa kula damu. Hilo linamaanisha nini kwa Wakristo?

12. Barua ya Paulo kwa Wakristo Waebrania inahusianishaje damu na msamaha wa dhambi?

12 Mtume Paulo alipowaandikia Wakristo Waebrania kuhusu nguvu za kusafisha za damu, alieleza hivi: “Karibu vitu vyote husafishwa kwa damu kulingana na Sheria, na damu isipomwagwa hakuna msamaha unaotokea.” (Ebr. 9:22) Paulo alisema pia kwamba ingawa dhabihu za wanyama zilikuwa na thamani kwa kadiri fulani, ziliwakumbusha Waisraeli kwamba walikuwa watenda-dhambi na hazikutosha kuondolea mbali dhambi. Naam, Sheria ilikuwa “kivuli cha mambo mema yatakayokuja, lakini si umbo halisi la mambo hayo.” (Ebr. 10:1-4) Basi ni nini kilichohitajiwa ili dhambi zisamehewe?

13. Unahisije kujua kwamba Yesu alimtolea Yehova thamani ya damu yake?

13 Soma Waefeso 1:7. Kifo cha kidhabihu cha Yesu Kristo ambaye kwa hiari ‘alijitoa mwenyewe kwa ajili yetu,’ kina maana kubwa sana kwa wote wanaompenda yeye na Baba yake. (Gal. 2:20) Hata hivyo, jambo alilofanya Yesu baada ya kifo na ufufuo wake ndilo hasa lililotuachilia huru na kufungua njia ili dhambi zetu zisamehewe. Yesu alitimiza jambo lililoonyeshwa mapema na Sheria ya Musa katika Siku ya Upatanisho. Siku hiyo, kuhani mkuu alichukua sehemu ya damu ya wanyama waliotolewa dhabihu na kuingia nayo Mahali Patakatifu Zaidi katika maskani, na baadaye katika hekalu la Sulemani, na kuitoa mbele za Mungu, kana kwamba ni mbele za  macho yake. (Law. 16:11-15) Vivyo hivyo, Yesu aliingia mbinguni kwenyewe akiwa na thamani ya damu yake ya kibinadamu na kumtolea Yehova. (Ebr. 9:6, 7, 11-14, 24-28) Tunashukuru sana kwamba tunaweza kusamehewa dhambi zetu na kusafishwa dhamiri kwa sababu tunadhihirisha imani katika damu ya Yesu.

14, 15. Kwa nini ni muhimu kuelewa na kutii sheria ya Yehova kuhusu damu?

14 Je, sasa umeelewa vizuri kwa nini Yehova anatuamuru tusile “namna yoyote ya damu”? (Law. 17:10) Je, unaelewa kwa nini Mungu anaona damu kuwa takatifu? Kwa kweli, anaona damu kuwa sawa na uhai. (Mwa. 9:4) Je, unakubali kwamba tunapaswa kuwa na maoni kama ya Mungu kuhusu damu na kutii amri yake ya kujiepusha nayo? Kila mmoja wetu anaweza tu kuwa na amani pamoja na Mungu kwa kudhihirisha imani katika dhabihu ya Yesu ya fidia na kutambua kwamba damu ni yenye thamani sana kwa Muumba wetu.—Kol. 1:19, 20.

15 Yeyote kati yetu anaweza kukabili kwa ghafla suala la damu. Au huenda mshiriki wa familia yetu au rafiki yetu mpendwa akakabili suala la kukubali au kutokubali kutiwa damu mishipani. Katika hali kama hiyo ya dharura, mtu anahitaji pia kuamua ikiwa atakubali visehemu fulani vya damu na matibabu mengine. Kwa hiyo, ni muhimu sana kufanya utafiti na kujitayarisha kwa ajili ya hali ya dharura. Kusali na kufanya matayarisho hayo kutatusaidia kuwa thabiti kuhusiana na suala hilo na kutolegeza msimamo wetu. Bila shaka hatutaki kuhuzunisha moyo wa Yehova kwa kukubali kitu ambacho Neno lake linashutumu! Wataalamu wengi wa kitiba na watu wengine wanaotetea zoea la kutia damu mishipani wanawasihi watu wachangie damu ili kuokoa maisha. Hata hivyo, watu watakatifu wa Yehova wanatambua kwamba Muumba ana haki ya kusema jinsi damu inavyopaswa kutumiwa. Anaona “namna yoyote ya damu” kuwa takatifu. Ni lazima tuazimie kutii sheria yake kuhusu damu. Tunamthibitishia kupitia mwenendo wetu mtakatifu kwamba tunathamini sana nguvu zinazookoa uhai za damu ya Yesu—hiyo ndiyo damu pekee inayotuwezesha kupata msamaha wa dhambi na uzima wa milele.—Yoh. 3:16.

KWA NINI YEHOVA ANATAKA TUWE WATAKATIFU?

16. Kwa nini ni lazima watu wa Yehova wawe watakatifu?

16 Mungu alipokuwa akiwakomboa Waisraeli kutoka utumwani Misri, aliwaambia hivi: “Mimi ni Yehova anayewaongoza ninyi kutoka katika nchi ya Misri ili kujionyesha kuwa Mungu kwenu; nanyi mtakuwa watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.” (Law. 11:45) Waisraeli walipaswa kuwa watakatifu kwa sababu Yehova ni mtakatifu. Tukiwa Mashahidi wa Yehova, sisi pia ni lazima tuwe watakatifu. Kitabu cha Mambo ya Walawi kinasema jambo hilo waziwazi.

17. Unahisije sasa kuhusu kitabu cha Biblia cha Mambo ya Walawi?

17 Bila shaka tumenufaika kwa kuchunguza mambo machache katika kitabu cha Mambo ya Walawi. Ni wazi kwamba funzo hili limekusaidia kukithamini zaidi kitabu hicho cha Biblia kilichoandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu. Bila shaka kutafakari baadhi ya mambo yenye thamani sana yaliyo katika kitabu cha Mambo ya Walawi kumekusaidia kuelewa vizuri zaidi kwa nini ni lazima tuwe watakatifu. Hata hivyo, ni hazina gani nyingine za kiroho tunazoweza kupata katika sehemu hiyo ya Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho takatifu? Tunaweza kujifunza mambo gani mengine kuhusu kumtolea Yehova utumishi mtakatifu? Tutachunguza mambo hayo katika makala ifuatayo.