Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Lazima Tuwe Watakatifu Katika Mwenendo Wetu Wote

Ni Lazima Tuwe Watakatifu Katika Mwenendo Wetu Wote

Iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote.1 PET. 1:15.

1, 2. (a) Mungu anatazamia watu wake wawe na mwenendo wa aina gani? (b) Makala hii inajibu maswali gani?

YEHOVA alimwongoza mtume Petro kunukuu kitabu cha Mambo ya Walawi kinachokazia utakatifu na kueleza kwamba tukiwa Wakristo tunapaswa kuwa watakatifu katika mwenendo wetu. (Soma 1 Petro 1:14-16.) Yehova ambaye ni “Mtakatifu” anatazamia watiwa-mafuta na “kondoo wengine” wajitahidi kabisa kuwa watakatifu katika mwenendo wao wote, si katika mambo fulani tu!—Yoh. 10:16.

2 Tutanufaika sana tukiendelea kuchunguza hazina za kiroho zilizo katika kitabu cha Mambo ya Walawi, na kufuata tunayojifunza kutatusaidia kuwa watakatifu katika mwenendo wetu wote. Tutachunguza maswali yafuatayo: Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu kulegeza msimamo wetu? Kitabu cha Mambo ya Walawi kinatufundisha nini kuhusu kuunga mkono enzi kuu ya Yehova? Tunaweza kujifunza nini kutokana na dhabihu zilizotolewa?

JIHADHARI USILEGEZE MSIMAMO WAKO

3, 4. (a) Kwa nini Wakristo hawapaswi kulegeza msimamo wao kuelekea sheria na kanuni za Biblia? (b) Kwa nini hatupaswi kulipiza kisasi au kuwa na kinyongo?

3 Ili tumpendeze Yehova, ni lazima tutii kabisa sheria na  kanuni zake, na hatupaswi kamwe kuziona si takatifu na hivyo kulegeza msimamo wetu. Ingawa hatuko chini ya Sheria ya Musa, matakwa yake yanatusaidia kuelewa mambo yanayokubalika na yasiyokubalika machoni pa Mungu. Kwa mfano, Waisraeli waliamriwa hivi: “Usilipize kisasi wala usiwe na kinyongo juu ya wana wa watu wako; nawe mpende mwenzako kama wewe mwenyewe. Mimi ni Yehova.”—Law. 19:18.

4 Yehova anataka tujizuie kulipiza kisasi, na pia anataka tuepuke kuwa na kinyongo. (Rom. 12:19) Ibilisi atafurahi sana tukipuuza sheria na kanuni za Mungu, na huenda tukamletea Yehova suto. Hata ikiwa tumeumizwa kimakusudi na mtu fulani, tusikubali kamwe kuwa vyombo vinavyobeba kinyongo. Mungu ametupatia pendeleo la kuwa “vyombo vya udongo” ambavyo vina hazina ya huduma. (2 Kor. 4:1, 7) Kinyongo ni kama asidi au tindikali ambayo haipaswi kuwekwa katika vyombo vya aina hiyo!

5. Tunajifunza nini kutokana na simulizi kumhusu Haruni na vifo vya wanawe? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 13.)

5 Andiko la Mambo ya Walawi 10:1-11 linasimulia kisa chenye kuhuzunisha sana kilichoikumba familia ya Haruni. Bila shaka walihuzunika sana moto ulipotoka mbinguni na kuwateketeza Nadabu na Abihu, wana wa Haruni, wakiwa katika maskani. Imani ya Haruni na familia yake ilijaribiwa sana walipoagizwa wasiomboleze vifo vya jamaa zao! Je, unajitahidi kibinafsi kuwa mtakatifu kwa kutoshirikiana na watu wa familia au watu wengine waliotengwa na ushirika?—Soma 1 Wakorintho 5:11.

6, 7. (a) Ni mambo gani muhimu tunayopaswa kuzingatia tunapoamua ikiwa tutashiriki au kutoshiriki katika arusi kanisani? (Angalia maelezo ya chini.) (b) Tunawezaje kuwaeleza watu wetu wa ukoo wasio Mashahidi msimamo wetu kuhusu kushiriki katika arusi kanisani?

6 Huenda tusikabili jaribu kali kama la Haruni na familia yake. Lakini tufanye nini tukialikwa kuhudhuria na kushiriki katika arusi ya mtu wa ukoo asiye Shahidi itakayofanyiwa kanisani? Hakuna amri ya moja kwa moja katika Maandiko inayotukataza kuhudhuria, lakini je, kuna kanuni za Biblia zinazopaswa kutuongoza kufanya uamuzi kama huo? *

7 Huenda watu wetu wa ukoo wasio Mashahidi wakashangazwa na azimio letu la kuwa watakatifu machoni pa Yehova katika hali tulizotaja. (1 Pet. 4:3, 4) Bila shaka, tunajitahidi kuepuka kuwaudhi, lakini itafaa kuzungumza nao kwa fadhili, lakini waziwazi. Tunaweza kufanya hivyo mapema kabla ya sherehe. Tunaweza kuwashukuru na kuwaambia tunafurahi kwamba wametupatia mgawo katika arusi yao. Kisha tunaweza kuwaambia kwamba kwa sababu masuala ya dini yanahusika, hatutashiriki katika arusi yao ili tusiharibu siku yao ya pekee yenye furaha na huenda tukawaaibisha wao na wahudhuriaji wengine. Tunaweza kutumia njia hiyo kuepuka kulegeza msimamo wetu kuhusu mafundisho na imani yetu.

UNGA MKONO ENZI KUU YA YEHOVA

8. Kitabu cha Mambo ya Walawi kinakaziaje enzi kuu ya Yehova?

8 Kitabu cha Mambo ya Walawi kinakazia enzi kuu ya Yehova. Kinataja zaidi ya mara 30 kwamba Yehova ndiye chanzo cha sheria zilizomo. Musa alikiri jambo hilo na kufanya kama Yehova alivyomwamuru. (Law. 8:4, 5) Sisi pia tunapaswa sikuzote kufanya yale ambayo Mwenye Enzi Kuu wetu, Yehova, anataka tufanye. Tengenezo la Mungu linatusaidia kufanya hivyo. Hata hivyo, huenda imani yetu ikajaribiwa tunapokuwa peke yetu, kama Yesu alivyojaribiwa nyikani. (Luka 4:1-13) Tukikazia fikira  enzi kuu ya Mungu na kumtegemea, hakuna yeyote anayeweza kutufanya tulegeze msimamo wetu na kunaswa na woga usiofaa.—Met. 29:25.

9. Kwa nini watu wa Mungu wanachukiwa katika mataifa yote?

9 Tukiwa wafuasi wa Kristo na Mashahidi wa Yehova, tunateswa katika mataifa mbalimbali ulimwenguni. Tunatazamia mateso kwa sababu Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: ‘Watu watawatia ninyi katika dhiki na kuwaua ninyi, nanyi mtachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.’ (Mt. 24:9) Hata ingawa tunachukiwa, tunavumilia katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kuendelea kuwa watakatifu mbele za Yehova. Kwa nini tunachukiwa sana licha ya kwamba sisi ni raia wanyoofu, wanaoishi maisha safi, na wanaotii sheria? (Rom. 13:1-7) Kwa sababu tumemfanya Yehova kuwa Bwana Mwenye Enzi Kuu wetu! Tunamtolea “yeye peke yake” utumishi mtakatifu na hatutalegeza kamwe msimamo wetu kuhusu sheria na kanuni zake za uadilifu.—Mt. 4:10.

10. Ni nini kilichotokea ndugu mmoja alipolegeza msimamo wake wa kutounga mkono upande wowote?

10 Sisi pia “si sehemu ya ulimwengu.” Kwa hiyo, hatuungi mkono upande wowote katika vita wala siasa za ulimwengu huu. (Soma Yohana 15:18-21; Isaya 2:4.) Baadhi ya watu waliojiweka wakfu kwa Mungu wamelegeza msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote. Wengi wao wametubu na kuwa tena na uhusiano mzuri na Baba yetu wa mbinguni mwenye rehema. (Zab. 51:17) Wachache hawakutubu. Kwa mfano, wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, maofisa waliwachukua ndugu zetu 160 waliofungwa isivyo haki katika magereza yote nchini Hungaria na kuwapeleka katika mji mmoja. Ndugu hao wenye umri usiozidi miaka 45 waliamriwa wajiunge na jeshi. Ndugu waaminifu walikataa kwa uthabiti, lakini ndugu tisa walikubali kiapo na kuvaa mavazi ya jeshi. Miaka miwili baadaye, ndugu mmoja aliyelegeza msimamo wake aliwekwa kwenye kikosi cha kuwapiga risasi Mashahidi waaminifu. Ndugu yake wa kimwili alikuwa miongoni mwao! Lakini hawakutekeleza mauaji hayo.

MTOLEE YEHOVA KILICHO BORA ZAIDI

11, 12. Wakristo wanajifunza nini leo kutokana na matakwa ya Yehova kuhusu dhabihu zilizotolewa katika taifa la kale la Israeli?

11 Kulingana na Sheria ya Musa, Waisraeli walipaswa kutoa dhabihu hususa. (Law. 9:1-4, 15-21) Dhabihu hizo hazikupaswa kuwa na kasoro yoyote kwa sababu zilifananisha dhabihu kamilifu ya Yesu. Isitoshe, Waisraeli walipaswa kufuata utaratibu fulani hususa walipotoa kila toleo au dhabihu. Kwa mfano, fikiria matakwa yaliyopaswa kutimizwa na mama mwenye mtoto mchanga. Andiko la Mambo ya Walawi 12:6 linasema hivi: “Zitakapotimia siku za utakaso wake kwa ajili ya mwana au binti ataleta mwana-kondoo dume katika mwaka wake wa kwanza kwa ajili ya toleo la kuteketezwa na hua mchanga au njiwa-tetere kwa ajili ya toleo la dhambi kwenye mwingilio wa hema la mkutano kwa kuhani.” Mungu alitoa matakwa hususa, lakini Sheria inaonyesha waziwazi upendo na usawaziko wake. Ikiwa mama hangeweza kutoa kondoo, aliruhusiwa kutoa njiwa-tetere wawili au hua wawili wachanga. (Law. 12:8) Mwabudu huyo maskini, alipendwa na kuthaminiwa kama yule aliyeleta toleo la gharama kubwa zaidi. Tunajifunza nini kutokana na hilo?

12 Mtume Paulo aliwahimiza waabudu wenzake wamtolee Mungu “dhabihu ya sifa.” (Ebr. 13:15) Midomo yetu inapaswa kutangaza hadharani jina takatifu la Yehova. Ndugu na dada viziwi hutumia lugha ya ishara au ya alama kumtolea Mungu sifa hiyo. Wakristo wagonjwa wasioweza  kutoka nyumbani humsifu kwa kuhubiri kupitia barua na simu, na pia kwa kuwahubiria wageni na watu wanaowahudumia. Tunapaswa kutoa dhabihu bora zaidi ya sifa, yaani, kumsifu Yehova kwa kulitangaza jina lake na kuhubiri habari njema kadiri afya na uwezo wetu unavyoruhusu.—Rom. 12:1; 2 Tim. 2:15.

13. Kwa nini tunapaswa kutoa ripoti ya utendaji wetu katika utumishi wa shambani?

13 Dhabihu zetu za sifa ni matoleo ya kibinafsi tunayomtolea Mungu kwa hiari kwa sababu tunampenda. (Mt. 22:37, 38) Lakini tumeombwa tutoe ripoti ya utendaji wetu katika huduma. Basi, tunapaswa kuwa na mtazamo gani kuelekea jambo hilo? Ripoti tunayotoa kila mwezi inahusiana na ujitoaji-kimungu wetu. (2 Pet. 1:7) Bila shaka, hatupaswi kuhisi kwamba ni lazima tuhubiri kwa saa nyingi ili turipoti tu saa nyingi za utumishi wa shambani. Ndiyo sababu mhubiri wa Ufalme ambaye amedhoofika kimwili au aliye hospitalini anaweza kuripoti utumishi wa dakika 15, 30, na 45 badala ya saa nzima. Yehova anathamini dakika hizo na kuona kwamba mhubiri huyo wa Ufalme ametoa toleo bora zaidi na Anampenda na kuthamini pendeleo lisilo na kifani la kumtumikia akiwa Shahidi Wake. Sawa na Waisraeli ambao hali zao hazikuwaruhusu kumtolea Yehova dhabihu zenye gharama kubwa, watumishi wa Yehova wenye thamani ambao hawawezi kutimiza mengi bado wanaweza kutoa ripoti. Na ripoti za kila mmoja wetu zinajumlishwa katika ripoti ya ulimwenguni pote, ambayo inasaidia tengenezo kupanga jinsi kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme itakavyofanywa. Basi, je, tengenezo linadai mengi mno linapotuomba tutoe ripoti ya utendaji wetu katika kazi ya kuhubiri?

MAZOEA YETU YA KUJIFUNZA NA DHABIHU ZA SIFA

14. Eleza kwa nini tunapaswa kuchunguza mazoea yetu ya kujifunza.

14 Baada ya kuchunguza hazina chache za kiroho kutoka katika kitabu cha Mambo ya Walawi, huenda ukasema, ‘Sasa ninaelewa vizuri kwa nini kitabu hiki ni sehemu ya Neno la Mungu lililoongozwa na roho.’ (2 Tim. 3:16) Huenda sasa umeazimia zaidi kuwa mtakatifu, si kwa sababu tu Yehova anataka uwe mtakatifu bali kwa sababu anastahili kutumikiwa kwa moyo wote. Huenda mambo ambayo umejifunza kuhusu kitabu cha Mambo ya Walawi katika makala hizi mbili yameongeza tamaa yako ya kuchimba ndani zaidi ya Maandiko yote. (Soma Methali 2:1-5.) Sali na uchunguze mazoea yako ya kujifunza. Bila shaka ungependa dhabihu zako za sifa zikubaliwe na Yehova. Je, unaruhusu vipindi vya televisheni, michezo ya video au michezo mingine, au mapendezi mengine yakukengeushe na kukuzuia kufanya maendeleo ya kiroho? Ikiwa ndivyo, huenda ukanufaika sana ukitafakari mambo fulani yaliyoandikwa na mtume Paulo katika kitabu cha Waebrania.

Je, unatanguliza funzo la Biblia na Ibada ya Familia maishani mwako? (Tazama fungu la 14)

15, 16. Kwa nini Paulo alisema mambo waziwazi alipowaandikia Wakristo Waebrania?

15 Paulo alisema mambo waziwazi alipowaandikia Wakristo wenzake Waebrania. (Soma Waebrania 5:7, 11-14.) Mtume huyo hakuwaficha ukweli wa mambo! Aliwaambia  kwamba ‘wamekuwa wazito’ katika kusikia kwao. Kwa nini Paulo aliwapa shauri kali la moja kwa moja? Alikuwa akimwiga Yehova kwa kuwaonyesha upendo na kuwahangaikia Wakristo hao waliofikiri kwamba wangeweza kuendelea kuwa hai kiroho kwa kunywa tu maziwa ya kiroho. Ni muhimu kujua mafundisho ya msingi ya Kikristo. Hata hivyo, Mkristo anahitaji “chakula kigumu” ili aendelee kukua kiroho na kufikia ukomavu wa Kikristo.

16 Badala ya kufanya maendeleo na kuwafundisha wengine, Waebrania walihitaji kufundishwa. Kwa nini? Kwa sababu waliepuka “chakula kigumu.” Jiulize hivi: ‘Je, nina mtazamo unaofaa kuelekea chakula kigumu cha kiroho? Je, ninakula chakula kigumu? Au ninaepuka kusali na kujifunza Biblia kwa kina? Ikiwa ndivyo, je, huenda ikawa kwamba sina mazoea mazuri ya kujifunza?’ Hatupaswi tu kuwahubiria watu bali pia kuwafundisha na kufanya wanafunzi.—Mt. 28:19, 20.

17, 18. (a) Kwa nini tunapaswa kula chakula kigumu cha kiroho kwa ukawaida? (b) Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu kunywa kileo kabla ya kuhudhuria mikutano?

17 Huenda isiwe rahisi kwa wengi wetu kujifunza Biblia. Bila shaka, Yehova hawalazimishi watu wake wajifunze kwa kuwafanya wahisi wana hatia. Hata hivyo, iwe tumejiweka wakfu kwa Mungu na tumekuwa tukimtumikia kwa miaka mingi au muda mfupi, tunapaswa kuendelea kula chakula kigumu cha kiroho. Ni muhimu kufanya hivyo ili tuendelee kuwa watakatifu maishani.

18 Ili tuwe watakatifu, ni lazima tuchunguze Maandiko kwa makini na kufanya yale ambayo Mungu anataka tufanye. Fikiria Nadabu na Abihu, wana wa Haruni, ambao waliangamizwa kwa sababu ya kutoa “moto haramu,” labda wakiwa wamelewa. (Law. 10:1, 2) Ona yale ambayo Mungu alimwambia Haruni katika pindi hiyo. (Soma Mambo ya Walawi 10:8-11.) Je, andiko hilo linamaanisha kwamba hatupaswi kunywa kileo chochote kabla ya kuhudhuria mkutano wa Kikristo? Fikiria hoja hizi: Hatuko chini ya Sheria. (Rom. 10:4) Katika nchi fulani, waamini wenzetu hunywa vileo kwa kiasi wakati wa mlo kabla ya kuhudhuria mikutano. Vikombe vinne vya divai vilitumiwa katika sherehe ya Pasaka. Yesu alipoanzisha Ukumbusho, aliwapa mitume wake divai iliyofananisha damu yake ili wanywe. (Mt. 26:27) Biblia inashutumu zoea la kunywa kupita kiasi na ulevi. (1 Kor. 6:10; 1 Tim. 3:8) Na Wakristo wengi huongozwa na dhamiri yao kuepuka kabisa kunywa kileo kabla ya kushiriki katika utumishi wowote mtakatifu. Hata hivyo, hali zinatofautiana katika kila nchi, lakini jambo muhimu ni Wakristo “kufanya tofauti kati ya kitu kitakatifu na kile najisi” ili mwenendo wao mtakatifu umpendeze Mungu.

19. (a) Tunapaswa kukumbuka nini kuhusu ibada ya familia na funzo la kibinafsi? (b) Unawezaje kuonyesha kwamba umeazimia kuendelea kuwa mtakatifu?

19 Unaweza kuchimba na kupata hazina nyingi za kiroho katika Neno la Mungu. Tumia vifaa vya utafiti vilivyopo kuboresha ibada ya familia na funzo lako la kibinafsi. Jifunze mengi zaidi kumhusu Yehova na makusudi yake. Endelea kumkaribia. (Yak. 4:8) Sali kwa Mungu kama mtunga-zaburi aliyeimba hivi: “Ufunue macho yangu, ili nipate kutazama mambo ya ajabu kutoka katika sheria yako.” (Zab. 119:18) Usilegeze kamwe msimamo wako kuhusu sheria na kanuni za Biblia. Tii kwa hiari sheria bora ya Yehova, aliye “Mtakatifu,” na ushiriki kwa bidii katika “kazi takatifu ya habari njema ya Mungu.” (1 Pet. 1:15; Rom. 15:16) Endelea kuwa mtakatifu katika siku hizi za mwisho zenye misukosuko. Acheni sote tuwe watakatifu katika mwenendo wetu na hivyo kuunga mkono enzi kuu ya Mungu wetu mtakatifu, Yehova.

^ fu. 6 Tazama “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika Mnara wa Mlinzi, Mei 15, 2002.