Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tunapaswa Kuwa Watakatifu Katika Mwenendo Wetu Wote

Tunapaswa Kuwa Watakatifu Katika Mwenendo Wetu Wote

‘Mukuwe watakatifu katika mwenendo wenu wote.’—1 PET. 1:15.

1, 2. (a) Kuhusiana na mwenendo, Yehova anataka watumishi wake wafanye nini? (b) Tutajibu maulizo gani katika habari hii?

MUTUME Petro aliongozwa na roho ya Yehova ili aandike kwamba Wakristo wanapaswa kuwa watakatifu katika mwenendo wao wote. Utakatifu huo, unapatana na utakatifu wenye unazungumuziwa katika kitabu cha Mambo ya Walawi. (Soma 1 Petro 1:14-16.) Yehova ambaye ni ‘Mutakatifu’ anataka Wakristo watiwa-mafuta na “kondoo wengine” wafanye yao yote ili wakuwe watakatifu katika mwenendo wao wote.—Yoh. 10:16.

2 Katika habari hii, tutajifunza mambo mengine mazuri sana yenye kuapatikana katika kitabu cha Mambo ya Walawi. Mambo hayo yatatuletea faida kubwa sana. Pia kutumikisha mambo hayo kutatusaidia tukuwe watakatifu katika mwenendo wetu wote. Kwa hiyo, tutajibia maulizo haya: Tunapaswa kuwa na maoni gani juu ya kuvunja ushikamanifu? Kitabu cha Mambo ya Walawi kinatufundisha nini kuhusu kuunga mukono utawala mukubwa wa Yehova? Zabihu zenye Waisraeli walikuwa wanatoa zinaweza kutufundisha nini?

FANYA ANGALISHO USIVUNJE USHIKAMANIFU WAKO

3, 4. (a) Sababu gani Wakristo wanapaswa kuendelea kushikamana na sheria na kanuni za Biblia? (b) Sababu gani hatupaswe kulipiza kisasi ao kuwekea wengine kinyongo?

3 Ili kumufurahisha Yehova, tunapaswa kushikamana na sheria na kanuni zake, na tunapaswa kuepuka kabisa mwenendo usio safi wenye unaweza kutufanya tukose kushikamana na sheria na kanuni hizo. Ni kweli kwamba hatuongozwe na Sheria ya Musa. Lakini, mambo yenye kupatikana katika Sheria hiyo yanatusaidia kuelewa mambo yenye inaweza kumupendeza Mungu na ile yenye inaweza kumuchukiza. Kwa mufano, Waisraeli  walipewa amri hii: ‘Usilipize kisasi wala usikuwe na kinyongo juu ya wana wa watu wako; nawe umupende mwenzako kama wewe mwenyewe. Mimi ni Yehova.’—Law. 19:18.

4 Yehova anataka tuepuke kulipiza kisasi, na anapenda tuepuke kuwekea wengine kinyongo. (Rom. 12:19) Ikiwa tunapuuza sheria na kanuni za Mungu, Ibilisi atafurahi sana, na hilo linaweza kufanya jina la Yehova lichafuliwe. Hata kama mutu fulani alitukwaza kimakusudi, tuepuke kuwa vyombo vya kuwekea ndani kinyongo. Mungu ametupatia pendeleo la kuwa “vyombo vya udongo” vyenye kuwa na hazina ya huduma. (2 Kor. 4:1, 7) Kama vile aside ao sumu, kinyongo hakipaswe kuwa ndani ya vyombo kama hivyo!

5. Habari juu ya Haruni na kifo cha watoto wake inaweza kutufundisha nini? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

5 Andiko la Mambo ya Walawi 10:1-11 lina habari yenye kuhuzunisha kuhusu familia ya Haruni. Bila shaka familia hiyo ilisikia uchungu wakati moto ulitoka mbinguni na kuteketeza Nadabu na Abihu, watoto wa Haruni, kwenye hema ya ibada. Kwa kweli, imani ya Haruni na ya familia yake ilijaribiwa wakati Yehova aliwakataza wasifanye kilio kwa ajili ya Nadabu na Abihu wenye walikuwa wamekufa! Wewe pia, unaendelea kuwa mutakatifu kwa kuepuka kufanya urafiki pamoja na mutu wa familia yako ao mutu mwengine mwenye ametengwa na kutaniko?—Soma 1 Wakorintho 5:11.

6, 7. (a) Wakati tunaamua ikiwa tutakubali daraka fulani katika arusi yenye itafanywa katika kanisa, ni mambo gani ya lazima tunapaswa kufikiria? (Ona maelezo yaliyo chini.) (b) Namna gani tunaweza kufikiri na watu wa jamaa yetu ambao si Mashahidi kuhusu musimamo wetu kuelekea arusi yenye inafanywa katika kanisa?

6 Pengine hatutapata jaribu kama lile la Haruni na familia yake. Lakini, tutafanya nini ikiwa mutu wa jamaa yetu ambaye si Shahidi anatualika na kutuomba tufanye jambo fulani kwenye arusi yenye inafanywa katika kanisa? Tunajua kwamba Biblia haitutolee sheria iliyo wazi kuhusu jambo hilo; hata hivyo, kuna kanuni za Biblia zenye zinaweza kutusaidia kuamua? *

7 Kuchukua musimamo wa kuendelea kuwa watakatifu katika hali zenye tumezungumuzia kunaweza kuwashangaza watu wa jamaa yetu ambao si Mashahidi wa Yehova. (1 Pet. 4:3, 4) Kwa kweli hatupendi kuwaumiza. Hata hivyo, ni vizuri zaidi mara nyingi kuzungumuza nao waziwazi, lakini kwa njia ya upole. Pengine unaweza kufanya hivyo siku nyingi mbele tukio hilo lifanyike. Unaweza kwanza kuwashukuru na kuwaambia kwamba unafurahi kuona vile walikupatia daraka fulani katika arusi yao. Kisha unaweza kusema kwamba kwa sababu hautafanya mambo yenye inahusu ibada, kushugulikia daraka hilo kunaweza kufanya siku hiyo ya pekee isikuwe yenye furaha kabisa na kwamba hilo linaweza kusumbua wahuzuriaji wengine. Kufanya hivyo, ni njia moja yenye inaweza kutusaidia tuendelee kuwa washikamanifu kuelekea mafundisho na imani yetu.

UNGA MUKONO UTAWALA MUKUBWA WA YEHOVA

8. Namna gani kitabu cha Mambo ya Walawi kinakazia utawala mukubwa wa Yehova?

8 Kitabu cha Mambo ya Walawi kinakazia utawala mukubwa wa Yehova. Zaidi ya mara 30, sheria zenye kupatikana katika kitabu hicho zinaonyeshwa kuwa zinatoka kwa Yehova. Musa alijua vizuri jambo hilo na alifanya mambo yenye Yehova alimuomba afanye. (Law. 8:4, 5) Sisi pia, tunapaswa kuendelea kufanya mambo yenye Yehova, Mutawala wetu Mukubwa, anatuomba tufanye. Tengenezo la Mungu linatusaidia ili tuweze kufanya hivyo. Lakini tunaweza kujaribiwa wakati tuko peke yetu, kama vile Yesu alijaribiwa wakati alikuwa peke yake katika jangwa. (Lu. 4:1-13) Ikiwa tunakazia akili yetu juu ya utawala mukubwa wa Mungu na ikiwa tunamutegemea, hakuna mutu yeyote anaweza kutufanya tuvunje ushikamanifu wetu ao kutufanya tuogope sana.—Met. 29:25.

9. Sababu gani watu wa Mungu wanachukiwa katika mataifa yote?

 9 Sisi watu wa Yehova, tunateswa katika mataifa yote duniani kwa sababu ya imani yetu. Hilo si jambo la kushangaza, kwa sababu Yesu aliambia wanafunzi wake hivi: ‘Watu watawatia ninyi katika ziki na kuwaua ninyi, nanyi mutachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.’ (Mt. 24:9) Lakini hata kama tunachukiwa hivyo, tunaendelea kufanya kazi ya kuhubiri Ufalme na tunaendelea kujionyesha kuwa watakatifu mbele ya Yehova. Sisi Mashahidi wa Yehova tunajiendesha vizuri, tunaishi maisha safi, na tuko wanainchi wenye kuheshimu sheria; lakini sababu gani watu wanatuchukia? (Rom. 13:1-7) Kwa sababu tumekubali Yehova akuwe Mutawala wetu Mukubwa! Tunamutolea “yeye peke yake” utumishi mutakatifu na hatutavunja hata siku moja ushikamanifu wetu kuelekea sheria na kanuni zake za haki.—Mt. 4:10.

10. Ni jambo gani lilitokea wakati ndugu mumoja alivunja ushikamanifu wake?

10 Tena, sisi “si sehemu ya ulimwengu.” Ndiyo sababu hatujiingize katika mambo ya vita na mambo ya siasa. (Soma Yohana 15:18-21; Isaya 2:4.) Watu fulani wenye walijitoa kwa Mungu ili kumutumikia walivunja ushikamanifu wao kwa kujiingiza katika mambo ya vita na mambo ya siasa. Wengi kati yao walitubu na wakarudilia urafiki wao pamoja na Baba yetu wa mbinguni, ambaye ni Mungu mwenye rehema. (Zab. 51:17) Lakini wachache walikataa kutubu. Kwa mufano, wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu, wakubwa wa jeshi walikusanya ndugu 160 waliokuwa na miaka chini ya 45 wenye walifungwa bila sababu katika magereza ya Hungaria na kuwatia katika muji mumoja. Katika muji huo, wakubwa hao waliwakaza kufanya kazi ya jeshi. Ndugu wengi walibakia waaminifu, lakini kenda kati yao walifanya kiapo cha maaskari na wakakubali kuvaa mavazi ya maaskari. Kisha miaka mbili, mumoja wa wale wenye walivunja ushikamanifu wao, alijikuta kati ya maaskari wenye waliombwa kupiga masasi Mashahidi wenye walibakia waaminifu. Ndugu yake mukubwa alikuwa kati ya ndugu hao waaminifu! Hata hivyo, mauaji hayo yenye kuogopesha hayakufanyika.

UMUTOLEE YEHOVA KULINGANA NA UWEZO WAKO

11, 12. Maagizo yenye Yehova aliwapatia Waisraeli kuhusu zabihu yanafundisha nini Wakristo leo?

11 Sheria ya Musa ilisema kwamba Waisraeli walipaswa kutoa aina mbalimbali za zabihu. (Law. 9:1-4, 15-21) Zabihu hizo hazikupaswa kuwa na ulema wowote kwa sababu zilifananisha zabihu ya Yesu yenye kukamilika. Zaidi ya hilo, kulikuwa maagizo fulani yenye Waisraeli walipaswa kufuata ili kumutolea Mungu aina fulani ya sadaka, ao zabihu. Tuone kwa mufano mambo yenye mwanamuke mwenye alitoka tu kuzaa aliombwa kufanya. Andiko la Mambo ya Walawi 12:6 linasema hivi: ‘Kisha zitakapotimia siku za utakaso wake kwa ajili ya mwana ao binti ataleta mwana-kondoo dume katika mwaka wake wa kwanza kwa ajili ya toleo la kuteketezwa na hua muchanga ao njiwa-tetere kwa ajili ya toleo la zambi kwenye muingilio wa hema la mukutano kwa kuhani.’ Mambo yenye Yehova aliomba yalikuwa wazi, lakini Sheria inaonyesha kwamba Yehova alikuwa mwenye upendo na mwenye usawaziko. Ikiwa mwanamuke huyo hakuwa na uwezo wa kuleta kondoo, aliruhusiwa kutoa njiwa-tetere wawili ao hua wawili wachanga. (Law. 12:8) Hata kama alikuwa maskini, mwanamuke kama huyo alipendwa na Yehova na alionwa kuwa wa lazima sawasawa na yule alitoa kondoo. Jambo hilo linaweza kutufundisha nini?

12 Mutume Paulo alitia moyo waamini wenzake wamutolee Mungu ‘zabihu ya sifa.’ (Ebr. 13:15) Midomo yetu inapaswa kutangaza jina takatifu la Yehova mbele ya watu wote. Ndugu na dada viziwi wanatumia luga ya ishara ili kumusifu Mungu. Wakristo wenye hawana uwezo wa kutoka nyumbani wanamusifu Yehova kwa kutoa ushahidi kupitia barua, telefone, na kwa kuwahubiria wale walio karibu nao na wale wenye wanakuja kuwatembelea. Zabihu yetu ya sifa, ni kusema, sifa yenye tunamutolea Yehova wakati tunasaidia watu kujua jina lake na wakati tunahubiri habari njema, inategemea  afya na uwezo wetu. Inapaswa kulingana kabisa na hali yetu.—Rom. 12:1; 2 Tim. 2:15.

13. Sababu gani tunapaswa kutoa ripoti ya kazi yetu ya mahubiri?

13 Tunamutolea Mungu zabihu za sifa kwa kujipendea kwa sababu tunamupenda. (Mt. 22:37, 38) Lakini tunaombwa kutoa ripoti ya kazi yetu ya mahubiri. Kwa hiyo, tunapaswa kuona mupango huo namna gani? Ripoti yenye tunatoa kila mwezi inaonyesha kwamba tunashikamana na Mungu. (2 Pet. 1:7) Hata hivyo, haiombe tujisikie kwamba tunakazwa kuhubiri sana ili tuweze kuripoti saa nyingi. Ndio sababu muhubiri wa Ufalme mwenye anaishi katika nyumba za kuwatunzia wazee ao ule mwenye hana uwezo wa kutoka nyumbani anaombwa kuripoti hata dakika 15. Yehova anapendezwa sana na dakika hizo na anaona kwamba muhubiri wa Ufalme mwenye amezitoa amefanya kulingana na uwezo wake na kwamba muhubiri huyo anamupenda. Pia, Yehova anaona muhubiri huyo kuwa anafurahia pendeleo la pekee lenye amepewa la kuwa Shahidi Wake. Kama vile Yehova alikubali zabihu za Waisraeli wenye walikuwa maskini, anakubali pia watumishi wake wenye kuwa na matatizo fulani watoe ripoti kulingana na uwezo wao. Tena, ripoti ya kila Mukristo inahesabiwa pamoja na ripoti za wahubiri wa duniani pote na inasaidia tengenezo lipange kazi ya kuhubiri Ufalme kwa ajili ya wakati unaokuja. Kwa hiyo sasa, tunaweza kusema kwamba ni muzigo kutoa ripoti ya kazi yetu ya mahubiri?

TABIA ZETU ZA KUJIFUNZA NA KUMUTOLEA YEHOVA ZABIHU ZA SIFA

14. Eleza sababu gani tunapaswa kuchunguza tabia zetu za kujifunza.

14 Kisha kujifunza mambo mazuri sana yenye inapatikana katika kitabu cha Mambo ya Walawi, pengine unaweza kusema hivi: ‘Sasa, nimeelewa vizuri zaidi sababu zenye zilifanya kitabu hiki kiingizwe katika Neno la Mungu lenye liliongozwa na roho yake.’ (2 Tim. 3:16) Pengine sasa umeazimia kabisa kuwa mutakatifu, si kwa sababu tu Yehova anakuomba ukuwe mutakatifu, lakini pia kwa sababu anastahili kukuona unajikaza sana ili kumufurahisha. Pengine mambo yenye umejifunza kuhusu kitabu cha Mambo ya Walawi katika habari hizi mbili yamekufanya ukuwe na hamu ya kujifunza zaidi Biblia yote nzima. (Soma Methali 2:1-5.) Chunguza tabia zako za kujifunza, na usali kwa ajili ya jambo hilo. Bila shaka unapenda Yehova akubali zabihu zako za sifa. Je, programu za televizyo, michezo ya video, mazoezi, ao michezo ingine, vinakukengeusha na kukuzuia ufanye maendeleo ya kiroho? Ikiwa jibu lako ni ndiyo, ni lazima ufikiri sana juu ya maneno fulani ya mutume Paulo yenye inapatikana katika kitabu cha Waebrania.

Unatia funzo la Biblia na Ibada ya Familia pa nafasi ya kwanza katika maisha yako?(Ona fungu la 14)

15, 16. Sababu gani mutume Paulo alikuwa wazi sana wakati aliwaandikia Wakristo Waebrania?

15 Mutume Paulo alikuwa wazi sana wakati aliwaandikia Wakristo Waebrania. (Soma Waebrania 5:7, 11-14.) Kwa kweli, hakuwaficha kitu! Aliwaambia kwamba ‘walikuwa wazito’ katika namna yao ya kusikia. Sababu gani mutume Paulo  alikuwa wazi sana? Kama vile Yehova, mutume Paulo aliwapenda na kuwahangaikia Wakristo wenye waliendelea kutosheka na maziwa ya kiroho, ao mafundisho ya musingi ya Biblia. Ni lazima kujua mafundisho ya musingi ya Kikristo. Hata hivyo, tunapaswa kula “chakula kigumu” ili kufanya maendeleo ya kiroho na kufikia ukomavu wa Kikristo.

16 Waebrania walipaswa kufanya maendeleo ya kiroho ili waweze kufundisha wengine, lakini walihitaji tena mutu wa kuwafundisha. Sababu gani? Kwa sababu hawakupenda kula “chakula kigumu.” Ni lazima ujiulize hivi: ‘Niko na maoni mazuri kuelekea chakula kigumu cha kiroho? Ninakula chakula hicho? Ao, ninasita kusali na kujifunza Biblia kwa bidii? Ikiwa jibu ni ndiyo, ni kwa sababu sizoee kujifunza?’ Jua kwamba tunapaswa kuhubiria watu, lakini pia tunapaswa kuwafundisha na kuwasaidia wakuwe wanafunzi.—Mt. 28:19, 20.

17, 18. (a) Sababu gani tunapaswa kuendelea kula chakula kigumu cha kiroho? (b) Ni vibaya kunywa pombe mbele ya kuenda kwenye mikutano ya Kikristo? Eleza.

17 Wengi kati yetu wanaweza kuona kwamba ni vigumu kujifunza Biblia. Kwa kweli, Yehova hajaribu kutufanya tujisikie kwamba anatukaza tujifunze. Lakini, hata kama tunamutumikia Mungu tangu miaka mingi ao hapana, tunapaswa kuendelea kula chakula kigumu cha kiroho. Kufanya hivyo kutatusaidia tuendelee kuwa watakatifu.

18 Ili kuwa watakatifu, tunapaswa kuchunguza Maandiko kwa uangalifu na kufanya mambo yenye Mungu anatuomba tufanye. Fikiri kidogo juu ya Nadabu na Abihu, watoto wa Haruni, wenye waliuawa kwa sababu ya kumutolea Yehova “moto haramu,” pengine kwa sababu ya ulevi. (Law. 10:1, 2) Ona maneno yenye Mungu alimuambia Haruni kisha tukio hilo. (Soma Mambo ya Walawi 10:8-11.) Maneno ya andiko hilo yanamaanisha kwamba hatupaswe kunywa pombe mbele ya kuenda kwenye mikutano ya Kikristo? Fikiria mambo haya: Hatuongozwe na Sheria ya Musa. (Rom. 10:4) Katika inchi fulani, waamini wenzetu wanakunywa pombe kwa kiasi wakati wa kula chakula mbele ya kuenda kwenye mikutano. Kwenye Pasaka, Wayahudi walikuwa wanatumia vikombe ine vya divai. Na wakati wa kuanzisha Ukumbusho, Yesu aliwaomba mitume wake wakunywe divai yenye inafananisha damu yake. (Mt. 26:27) Biblia inakataza kunywa pombe kupita kiasi na ulevi. (1 Kor. 6:10; 1 Tim. 3:8) Pia, kwa sababu ya zamiri yao, Wakristo wengi wanaweza kuamua kujiepusha kabisa na pombe mbele ya kufanya kila namna ya utumishi mutakatifu. Hata hivyo, hali zinaachana kulingana na kila inchi, na jambo la lazima kwa kila Mukristo ni kujua “kufanya tofauti kati ya kitu kitakatifu na kile [kilicho] najisiu” ili akuwe mutakatifu kwa njia yenye kumupendeza Mungu.

19. (a) Tunapaswa kukumbuka kufanya nini wakati wa ibada ya familia na wakati wa funzo la pekee? (b) Ili ukuwe mutakatifu, umeazimia kufanya nini?

19 Ikiwa unajifunza Neno la Mungu kwa bidii, utapata mambo mengine mazuri sana. Tumia vyombo vya kutusaidia kutafuta habari ili ufaidike zaidi wakati wa ibada ya familia na wakati wa funzo lako la pekee. Ujikaze kujua vizuri zaidi Yehova na makusudi yake. Umukaribie zaidi. (Yak. 4:8) Sali kwa Mungu kama mutunga Zaburi mwenye aliimba hivi: “Ufunue macho yangu, ili nipate kutazama mambo ya ajabu kutoka katika sheria yako.” (Zab. 119:18) Usivunje hata siku moja ushikamanifu wako kuelekea sheria na kanuni za Biblia. Tukubali kwa moyo wote sheria ya juu zaidi ya ‘Mutakatifu,’ Yehova, na tufanye kwa bidii “kazi takatifu ya habari njema ya Mungu.” (1 Pet. 1:15; Rom. 15:16) Katika siku hizi za mwisho zenye kuyumba-yumba, ujikaze kuwa mutakatifu. Tunatiwa moyo kuwa watakatifu katika mwenendo wetu wote; kwa kufanya hivyo, tutamuunga mukono Yehova, ambaye ni Mungu wetu mutakatifu.

^ fu. 6 Ona habari, “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 5, 2002.