Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Watu Ambao Mungu Wao Ni Yehova”

“Watu Ambao Mungu Wao Ni Yehova”

“Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova!”—ZAB. 144:15.

1. Watu fulani wanaamini nini kuhusu wale wanaomwabudu Mungu?

WATU wengi leo hukiri waziwazi kwamba dini kubwa za Kikristo na zisizo za Kikristo haziwasaidii sana wanadamu. Wengine wanakubali kwamba dini hizo hufundisha uwongo kumhusu Mungu na kufanya mambo yasiyompendeza na hivyo haziwezi kuwa na kibali chake. Hata hivyo, wanaamini kwamba kuna watu wanyoofu katika dini zote na kwamba Mungu anawaona na anawakubali kuwa waabudu wake duniani. Wanasema kwamba si lazima watu hao waache kushirikiana na dini ya uwongo ili wamwabudu Mungu wakiwa watu wake. Lakini, je, hayo ndiyo maoni ya Mungu? Acheni tupate jibu kwa kuchunguza yale ambayo Biblia inasema kuhusu historia ya waabudu wa kweli wa Yehova.

WATU WALIOFANYA AGANO NA MUNGU

2. Baada ya muda, ni nani waliokuja kuwa watu wa Yehova, na ni nini kilichowatofautisha na watu wengine? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

2 Tangu karne ya 20 K.W.K., Yehova alikuwa na kikundi cha watu wake duniani. Abrahamu, aliyeitwa “baba ya wale wote walio  na imani,” alikuwa kichwa cha familia yenye mamia ya watu. (Rom. 4:11; Mwa. 14:14) Watawala wa Kanaani walimwita “mkuu” na walimheshimu. (Mwa. 21:22; 23:6) Yehova alifanya agano na Abrahamu na wazao wake. (Mwa. 17:1, 2, 19) Mungu alimwambia hivi Abrahamu: ‘Hili ndilo agano langu ambalo ninyi mtashika, kati yangu na ninyi, hata uzao wako baada yako. Kila mwanamume wa kwenu lazima atahiriwe. Na iwe ishara ya agano kati yangu mimi na ninyi.’ (Mwa. 17:10, 11) Kwa hiyo, Abrahamu na wanaume wote wa nyumba yake walitahiriwa. (Mwa. 17:24-27) Tohara iliwatambulisha wazao wa Abrahamu kuwa watu pekee waliofanya agano na Yehova.

3. Wazao wa Abrahamu walikujaje kuwa kundi kubwa?

3 Yakobo, au Israeli, mjukuu wa Abrahamu alikuwa na wana 12. (Mwa. 35:10, 22b-26) Baada ya muda, wana hao wangekuwa vichwa vya makabila 12 ya Israeli. (Mdo. 7:8) Kwa sababu ya njaa, Yakobo na familia yake walikimbilia Misri, ambako Yosefu, mmoja wa wana wa Yakobo alikuwa amewekwa kuwa msimamizi wa chakula na msaidizi wa Farao. (Mwa. 41:39-41; 42:6) Wazao wa Yakobo wakawa wengi mno, “kutaniko la vikundi vya watu.”—Mwa. 48:4; soma Matendo 7:17.

WATU WALIOKOMBOLEWA

4. Mwanzoni, wazao wa Yakobo walikuwa na uhusiano gani na Wamisri?

4 Wazao wa Yakobo walikaa Misri kwa zaidi ya karne mbili, katika eneo la Mto Nile lililoitwa Gosheni. (Mwa. 45:9, 10) Inaonekana kwamba kwa miaka 100 hivi waliishi kwa amani na Wamisri, nao walikaa katika miji midogo na kulisha mifugo yao. Walikuwa wamekaribishwa kwa uchangamfu na Farao, ambaye alimjua na kumpenda Yosefu. (Mwa. 47:1-6) Lakini Wamisri waliwachukia sana watu waliofuga kondoo. (Mwa. 46:31-34) Hata hivyo, ilibidi wawavumilie Waisraeli.

5, 6. (a) Hali ya watu wa Mungu nchini Misri ilibadilikaje? (b) Musa aliokolewaje, na Yehova aliwafanyia nini watu Wake wote?

5 Lakini hali ya watu wa Mungu ingebadilika kabisa. “Baada ya muda mfalme mpya ambaye hakumjua Yosefu akainuka juu ya Misri. Naye akawaambia watu wake: ‘Tazama! Watu wa wana wa Israeli ni wengi zaidi na wenye nguvu kuliko sisi.’ Kwa hiyo Wamisri wakawatumikisha wana wa Israeli chini ya uonevu. Nao wakazidi kuyafanya maisha yao yawe machungu kwa utumwa mgumu wa kutengeneza saruji ya udongo na matofali na kwa kila namna ya utumwa shambani, ndiyo, kila namna ya utumwa wao ambao kwa huo waliwatumia wakiwa watumwa chini ya uonevu.”—Kut. 1:8, 9, 13, 14.

6 Farao hata aliamuru kwamba watoto wote wa kiume wa Waebrania wauawe mara tu wanapozaliwa. (Kut. 1:15, 16) Musa alizaliwa wakati huo. Alipokuwa na umri wa miezi mitatu, mama yake alimficha katikati ya matete ya Mto Nile, ambapo binti ya Farao alimpata. Baadaye binti ya Farao alimchukua akawa mwana wake. Kwa mwongozo wa Mungu, Musa alipokuwa mtoto alilelewa na Yokebedi, mama yake aliyekuwa mwaminifu, na akawa mtumishi mshikamanifu wa Yehova. (Kut. 2:1-10; Ebr. 11:23-25) Yehova ‘aliona’ mateso ya watu wake akaamua kumtumia Musa kuwakomboa kutoka kwa wakandamizaji. (Kut. 2:24, 25; 3:9, 10) Kwa hiyo, wangekuwa watu ‘waliokombolewa’ na Yehova.—Kut. 15:13; soma Kumbukumbu la Torati 15:15.

WATU WA MUNGU WANAKUWA TAIFA

7, 8. Watu wa Yehova walikujaje kuwa taifa takatifu?

7 Ingawa Yehova hakuwa amewapanga  Waisraeli kuwa taifa, aliwatambua kuwa watu wake. Kwa hiyo, aliwaagiza Musa na Haruni wamwambie hivi Farao: “Hivi ndivyo Yehova Mungu wa Israeli amesema, ‘Waruhusu watu wangu waende zao, wakanifanyie sherehe nyikani.’”—Kut. 5:1.

8 Ili kuwakomboa wana wa Waisraeli kutoka kwa ukandamizaji wa Wamisri, Yehova alitumia mapigo kumi na kisha akamwangamiza Farao na majeshi yake katika Bahari Nyekundu. (Kut. 15:1-4) Baada ya miezi isiyozidi mitatu, Yehova alifanya agano na Waisraeli kwenye Mlima Sinai na kuwapa ahadi hii ya pekee: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kabisa na kulishika kwa kweli agano langu, ndipo hakika mtakapokuwa mali yangu ya pekee kutoka kati ya vikundi vingine vyote vya watu, . . . taifa takatifu.”—Kut. 19:5, 6.

9, 10. (a) Kulingana na Kumbukumbu la Torati 4:5-8, Sheria iliwatofautishaje Waisraeli na watu wengine? (b) Waisraeli wangethibitishaje kwamba walikuwa “kikundi cha watu kilicho kitakatifu kwa Yehova”?

9 Walipokuwa Misri, kabla ya kuwa watumwa, Waebrania walikuwa wamepangwa katika makabila ambayo yalisimamiwa na vichwa vya familia. Sawa na watumishi wa Yehova walioishi kabla yao, vichwa vya familia walikuwa ndio watawala, waamuzi, na makuhani katika familia zao. (Mwa. 8:20; 18:19; Ayu. 1:4, 5) Hata hivyo, kupitia Musa, Yehova aliwapa Waisraeli mfumo wa sheria ambao ungewatofautisha na mataifa mengine yote. (Soma Kumbukumbu la Torati 4:5-8; Zab. 147:19, 20.) Chini ya Sheria, kulikuwa na watu waliotumika wakiwa makuhani, na haki ilitekelezwa na “wanaume wazee” ambao waliheshimiwa kwa sababu ya ujuzi na hekima yao. (Kum. 25:7, 8) Sheria ilikuwa na maagizo yaliyoongoza utendaji wa kidini na wa kijamii katika taifa hilo changa.

10 Kabla tu ya Waisraeli kuingia katika Nchi ya Ahadi, Yehova aliwakumbusha sheria zake, na Musa aliwaambia hivi: “Yehova, amekufanya useme leo kwamba utakuwa kikundi cha watu wake, mali ya pekee, kama vile alivyokuahidi, na kwamba utashika amri zake zote, na kwamba atakuweka wewe juu kuliko mataifa mengine yote ambayo ameyafanya, hilo likitokeza sifa na heshima na uzuri, huku ukijithibitisha kuwa kikundi cha watu kilicho kitakatifu kwa Yehova Mungu wako, kama vile ambavyo ameahidi.”—Kum. 26:18, 19.

WAKAAJI WAGENI WAKARIBISHWA

11-13. (a) Ni nani waliojiunga na watu wa Mungu waliochaguliwa? (b) Mtu asiye Mwisraeli alipaswa kufanya nini ikiwa alitaka kumwabudu Yehova?

11 Ingawa sasa Yehova alikuwa na taifa lake duniani, hakuwazuia watu wasio Waisraeli wasijiunge na watu wake. Aliruhusu “jamii kubwa iliyochangamana” ya watu wasio Waisraeli, kutia ndani Wamisri, kuandamana na watu wake alipowakomboa kutoka Misri. (Kut. 12:38) Wakati wa pigo la saba, wengine “kati ya watumishi wa Farao” waliogopa neno la Yehova, na huenda walijiunga na jamii iliyochangamana ambayo ilitoka Misri pamoja na Waisraeli.—Kut. 9:20.

12 Kabla tu ya Waisraeli kuvuka Mto Yordani ili kuimiliki nchi ya Kanaani, Musa aliwaambia kwamba ni ‘lazima wampende mkaaji mgeni’ aliye miongoni mwao. (Kum. 10:17-19) Watu waliochaguliwa na Mungu walipaswa kumkubali mgeni yeyote ambaye alikuwa tayari kutii sheria za msingi walizopewa na Musa. (Law. 24:22) Baadhi ya wakaaji wageni walikuja kuwa waabudu wa Yehova, na kuwa na maoni kama ya Ruthu, yule Mmoabu, ambaye alimwambia hivi Naomi aliyekuwa Mwisraeli: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu.” (Rut. 1:16)  Wakaaji hao wageni wakawa wageuzwa-imani, na wanaume wakakubali kutahiriwa. (Kut. 12:48, 49) Yehova aliwakaribisha wageni hao kujiunga na watu wake aliowachagua.—Hes. 15:14, 15.

Waisraeli waliwapenda wakaaji wageni (Tazama fungu la 11-13)

13 Hekalu la Sulemani lilipowekwa wakfu kwa Yehova, mpango ulifanywa kwa manufaa ya waabudu ambao hawakuwa Waisraeli, kama sala ya Sulemani inavyoonyesha: “Kwa mgeni ambaye si sehemu ya watu wako Israeli na ambaye anatoka katika nchi ya mbali kwa sababu ya jina lako kuu na mkono wako wenye nguvu na mkono wako ulionyooshwa, nao kwa kweli waje na kusali kuelekea nyumba hii, basi na usikilize ukiwa mbinguni, katika makao yako yaliyofanywa imara, nawe ufanye kulingana na yote ambayo mgeni huyo anakuomba; kusudi watu wote wa dunia wapate kulijua jina lako nao wakuogope kama vile watu wako Israeli wanavyokuogopa, na ili wajue kwamba jina lako limeitwa juu ya nyumba hii ambayo nimeijenga.” (2 Nya. 6:32, 33) Kama ilivyokuwa katika siku za Yesu, mtu yeyote ambaye hakuwa Mwisraeli na aliyetaka kumwabudu Yehova angejiunga na watu waliofanya agano na Mungu.—Yoh. 12:20; Mdo. 8:27.

TAIFA LA MASHAHIDI

14-16. (a) Waisraeli wangekuwa taifa la mashahidi wa Yehova katika njia gani? (b) Watu wa Mungu katika siku zetu wana wajibu wa kufanya nini?

14 Waisraeli walimwabudu Mungu wao, Yehova, lakini mataifa mengine yaliabudu miungu yao. Katika siku za nabii Isaya, Yehova alitumia mfano wa kesi mahakamani kuonyesha hali ya ulimwengu. Aliiambia miungu ya mataifa ilete mashahidi wa kuthibitisha kwamba hiyo ni miungu aliposema hivi: “Mataifa yote na yakusanywe mahali pamoja, na vikundi vya mataifa vikusanywe pamoja. Ni nani kati [ya miungu] yao anayeweza kutangaza haya? Au, je, wanaweza kutufanya tusikie mambo ya kwanza? Na watoe mashahidi wao, ili watangazwe kuwa waadilifu, au wasikie na kusema, ‘Ni kweli!’”—Isa. 43:9.

15 Miungu ya mataifa ilishindwa kutoa uthibitisho wowote kwamba hiyo ni miungu. Ilikuwa tu sanamu zisizoweza  kusema ambazo zilihitaji kubebwa kila mahali. (Isa. 46:5-7) Kwa upande mwingine, Yehova aliwaambia hivi watu wake Israeli: “Ninyi ni mashahidi wangu, . . . mtumishi wangu ambaye nimemchagua, ili mjue na kuwa na imani katika mimi, na ili mwelewe kwamba mimi ni Yeye yuleyule. Kabla yangu hakuna Mungu yeyote aliyefanyizwa, na baada yangu hapakuendelea kuwapo yeyote. Mimi—mimi ni Yehova, na zaidi ya mimi hakuna mwokozi. . . . Basi ninyi ni mashahidi wangu, . . . nami ni Mungu.”—Isa. 43:10-12.

16 Wakiwa kama mashahidi katika kesi ya ulimwengu mzima inayohusu suala la “Ni nani aliye Mungu Mkuu Zaidi?,” watu waliochaguliwa na Yehova walipaswa kutoa uthibitisho ulio wazi kabisa kwamba Yehova tu ndiye Mungu wa kweli. Aliwaita “watu ambao nimejifanyia, ili wasimulie sifa zangu.” (Isa. 43:21) Hao ndio watu walioitwa kwa jina lake. Kwa kuwa Yehova aliwakomboa kutoka Misri, walikuwa na wajibu wa kutetea enzi yake kuu mbele ya watu wengine duniani. Hivyo, wangekuwa na mtazamo ambao nabii Mika alisema watu wa Mungu wangekuwa nao katika siku zetu. Alisema hivi: “Vikundi vyote vya watu vitatembea kila kimoja katika jina la mungu wake; bali sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.”—Mika 4:5.

WATU WAASI

17. Kwa nini Yehova aliwaona Waisraeli kuwa ‘mzabibu wa kigeni unaoharibika’?

17 Kwa kusikitisha, Waisraeli hawakuwa waaminifu kwa Mungu wao, Yehova. Walijiruhusu waathiriwe na mataifa yaliyoabudu miungu ya mbao na mawe. Katika karne ya nane K.W.K., nabii Hosea aliandika hivi: “Israeli ni mzabibu unaoharibika . . . Amezidisha madhabahu zake . . . Moyo wao umekuwa na unafiki; sasa watapatikana na hatia.” (Hos. 10:1, 2) Karne moja na nusu hivi baadaye, Yeremia aliandika maneno haya ambayo Yehova aliwaambia watu Wake wasio waaminifu: “Nilikuwa nimekupanda kama mzabibu bora mwekundu, wote ukiwa mbegu ya kweli. Basi ni jinsi gani umebadilika kunielekea ukawa machipukizi yaliyoharibika ya mzabibu wa kigeni? . . . Iko wapi miungu yako ambayo umejifanyia? Na isimame ikiwa inaweza kukuokoa wakati wa msiba wako . . . Watu wangu mwenyewe—wamenisahau.”—Yer. 2:21, 28, 32.

18, 19. (a) Yehova alitabirije kwamba angetokeza kikundi kipya cha watu kwa ajili ya jina lake? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

18 Badala ya kuzaa matunda mazuri kwa kumtolea Yehova ibada safi na kuwa mashahidi wake waaminifu, taifa la Israeli lilizaa matunda yaliyooza ya ibada ya sanamu. Kwa hiyo, Yesu aliwaambia hivi viongozi Wayahudi wanafiki katika siku zake: “Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa taifa lenye kuzaa matunda yake.” (Mt. 21:43) Ni wale tu waliokuwa katika “agano jipya,” lililotabiriwa na Yehova kupitia nabii Yeremia, ndio wangekuwa sehemu ya taifa hilo jipya, Israeli wa kiroho. Yehova alitabiri hivi kuhusu Waisraeli wa kiroho ambao wangeletwa katika agano hilo jipya: “Nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.”—Yer. 31:31-33.

19 Baada ya Waisraeli wa asili kukosa kuwa waaminifu, Yehova alifanya Israeli wa kiroho kuwa watu wake katika karne ya kwanza kama tulivyozungumzia awali. Lakini watu wake leo ni nani? Watu wenye mioyo minyoofu wanawezaje kuwatambua waabudu wa kweli wa Mungu? Maswali hao yatajibiwa katika makala inayofuata.