Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Sasa Ninyi Ni Watu wa Mungu”

“Sasa Ninyi Ni Watu wa Mungu”

Wakati mmoja ninyi mlikuwa si watu, lakini sasa ninyi ni watu wa Mungu.”—1 PET. 2:10.

1, 2. Ni badiliko gani lililotokea Pentekoste ya 33 W.K., na ni nani waliokuja kuwa washiriki wa taifa jipya la watu wa Yehova? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

PENTEKOSTE ya 33 W.K. ilikuwa siku muhimu katika historia ya watu wa Yehova duniani. Badiliko kubwa sana lilitokea. Siku hiyo, kupitia roho yake, Yehova alitokeza taifa jipya—Israeli wa kiroho, “Israeli wa Mungu.” (Gal. 6:16) Kwa mara ya kwanza tangu siku za Abrahamu, tohara haingewatambulisha tena watu wa Mungu. Badala yake, Paulo aliandika hivi kuhusu kila mshiriki wa taifa hilo jipya: “Kutahiriwa kwake ni kule kwa moyo kupitia roho.”—Rom. 2:29.

2 Washiriki wa kwanza wa taifa hilo jipya la Mungu walikuwa mitume na wanafunzi wengine wa Kristo zaidi ya mia moja ambao walikuwa wamekutana katika chumba cha juu kule Yerusalemu. (Mdo. 1:12-15) Walimiminiwa roho takatifu, na hivyo wakawa wana wa Mungu waliozaliwa kwa roho. (Rom. 8:15, 16; 2 Kor. 1:21) Hilo lilithibitisha kwamba lile agano jipya, ambalo lilipatanishwa na Kristo na kuhalalishwa kwa damu yake, lilikuwa limeanza kufanya kazi. (Luka 22:20; soma Waebrania 9:15.) Hivyo wanafunzi hao wakawa washiriki wa taifa jipya la Yehova, yaani, kikundi kipya cha watu wake. Roho takatifu iliwawezesha kuhubiri katika lugha mbalimbali zilizozungumzwa  na Wayahudi na wageuzwa-imani kutoka sehemu mbalimbali za Milki ya Roma. Watu hao walikuja Yerusalemu kwa ajili ya Sherehe ya Kiyahudi ya Majuma, au Pentekoste. Watu hao walisikia na kuelewa katika lugha zao wenyewe “mambo makuu ya Mungu” yaliyohubiriwa na Wakristo hao waliozaliwa kwa roho.—Mdo. 2:1-11.

TAIFA JIPYA LA WATU WA MUNGU

3-5. (a) Petro aliwaambia nini Wayahudi katika siku ya Pentekoste? (b) Ni hatua gani zilizochangia ukuzi wa taifa jipya la Yehova katika miaka yake ya kwanza?

3 Yehova alimtumia mtume Petro kuongoza kazi ya kuwafungulia njia Wayahudi na wageuzwa-imani ili wawe washiriki wa taifa hilo jipya, yaani, kutaniko la Kikristo. Katika siku ya Pentekoste, kwa ujasiri Petro aliwaambia Wayahudi kwamba lazima wamkubali Yesu, yule mwanamume ambaye ‘walimfunga kwenye mti,’ kwa sababu “Mungu alimfanya Bwana na pia Kristo.” Watu walipouliza wafanye nini, Petro akajibu: “Tubuni, na acheni kila mmoja wenu abatizwe katika jina la Yesu Kristo kwa msamaha wa dhambi zenu, nanyi mtapokea zawadi ya bure ya roho takatifu.” (Mdo. 2:22, 23, 36-38) Siku hiyo, watu 3,000 hivi walijiunga na taifa jipya la Israeli wa kiroho. (Mdo. 2:41) Baadaye, mitume walihubiri kwa bidii na watu wengi wakakubali kweli. (Mdo. 6:7) Taifa hilo jipya lilizidi kukua.

4 Baadaye, walianza kuwahubiria Wasamaria, na kukawa na matokeo mazuri. Wengi walibatizwa na mweneza-injili Filipo, lakini hawakupokea roho takatifu papo hapo. Baraza linaloongoza kule Yerusalemu lilimtuma mtume Petro na Yohana kwa Wasamaria hao waliogeuzwa imani, nao ‘wakaweka mikono yao juu yao, wakaanza kupokea roho takatifu.’ (Mdo. 8:5, 6, 14-17) Kwa hiyo, Wasamaria hao pia wakawa washiriki waliozaliwa kwa roho wa taifa la Israeli wa kiroho.

Petro alimhubiria Kornelio na watu wa nyumba yake (Tazama fungu la 5)

5 Katika mwaka wa 36 W.K., kwa mara nyingine tena, Mungu alimtumia Petro kuwaalika wengine ili wajiunge na taifa jipya la Israeli wa kiroho. Hilo lilitokea Petro alipomhubiria Kornelio, ofisa wa jeshi la Roma pamoja na jamaa na rafiki zake. (Mdo. 10:22, 24, 34, 35) Biblia inasema hivi: “Petro alipokuwa bado akisema . . . , roho takatifu ikawaangukia wote [wasio Wayahudi] waliokuwa wakisikia lile neno. Na waaminifu waliokuwa wamekuja pamoja na Petro ambao walikuwa kati ya wale waliotahiriwa wakashangaa, kwa sababu zawadi ya bure ya roho takatifu ilikuwa ikimiminwa pia juu ya watu wa mataifa.” (Mdo. 10:44, 45) Kuanzia wakati huo, Watu wa Mataifa wasiotahiriwa wangeweza kuwa washiriki wa taifa jipya la Israeli wa kiroho.

“WATU KWA AJILI YA JINA LAKE”

6, 7. Washiriki wa taifa jipya wangekuwa “watu kwa ajili ya jina [la Yehova]” katika njia gani, nao walifanya hivyo kwa kadiri gani?

6 Katika mkutano wa baraza linaloongoza  la Wakristo wa karne ya kwanza uliofanywa mwaka wa 49 W.K., mwanafunzi Yakobo alisema hivi: “Simioni [Petro] ameeleza kikamili jinsi Mungu kwa mara ya kwanza alivyoelekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake.” (Mdo. 15:14) Kikundi hicho kipya cha watu walioitwa kwa jina la Yehova kingetia ndani waamini walio Wayahudi na wasio Wayahudi. (Mdo. 11:25, 26a) Baadaye, Petro aliwaandikia hivi: “Wakati mmoja ninyi mlikuwa si watu, lakini sasa ninyi ni watu wa Mungu.” Petro alitaja utume wao aliposema: “Ninyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa kuwa mali ya pekee, ili mtangaze kotekote sifa bora’ zake yeye aliyewaita ninyi kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.” (1 Pet. 2:9, 10) Walipaswa kumsifu yule waliyemwakilisha na kutukuza jina lake hadharani. Walipaswa kuwa mashahidi jasiri wa Yehova, Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote.

7 Kama ilivyokuwa kwa Israeli wa asili, Yehova aliwaita washiriki wa Israeli wa kiroho “watu ambao nimejifanyia, ili wasimulie sifa zangu.” (Isa. 43:21) Wakristo hao wa mapema walitangaza kwa ujasiri kwamba Yehova tu ndiye Mungu wa kweli na kufunua kwamba miungu mingine yote ilikuwa ya uwongo. (1 The. 1:9) Walitoa ushahidi kumhusu Yehova na Yesu “katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”—Mdo. 1:8; Kol. 1:23.

8. Mtume Paulo aliwapa onyo gani watu wa Mungu katika karne ya kwanza?

8 Paulo alikuwa mmojawapo wa “watu kwa ajili ya jina [la Yehova]” katika karne ya kwanza, naye alihubiri kwa ujasiri. Akiwa mbele ya wanafalsafa wapagani, alitetea kwa ujasiri enzi kuu ya Yehova, “Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, akiwa, kama Huyu alivyo, Bwana wa mbingu na dunia.” (Mdo. 17:18, 23-25) Alipokuwa akikaribia mwisho wa safari yake ya tatu ya umishonari, Paulo aliwaonya hivi watu walioitwa kwa jina la Mungu: “Ninajua kwamba baada ya kuondoka kwangu mbwa-mwitu wenye kukandamiza wataingia katikati yenu nao hawatalitendea kundi kwa wororo, na kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Mdo. 20:29, 30) Uasi-imani huo uliotabiriwa ulikuwa umeonekana wazi kufikia mwishoni mwa karne ya kwanza.—1 Yoh. 2:18, 19.

9. Ni nini kilichowapata “watu kwa ajili ya jina [la Yehova]” baada ya mitume kufa?

9 Baada ya mitume kufa, uasi-imani huo ulienea na kutokeza dini zinazodai kuwa za Kikristo. Badala ya kuwa “watu kwa ajili ya jina [la Yehova],” Wakristo waasi-imani hata wameliondoa jina la Mungu katika tafsiri zao nyingi za Biblia. Wamefuata desturi za kipagani na kumvunjia Mungu heshima kwa mafundisho yao yasiyo ya kimaandiko, vita vyao “vitakatifu,” na mwenendo wao mpotovu. Kwa hiyo, kwa karne nyingi Yehova alikuwa na waabudu wachache sana waaminifu duniani lakini hakuwa na watu waliopangwa kitengenezo “kwa ajili ya jina lake.”

WATU WA MUNGU WAZALIWA UPYA

10, 11. (a) Yesu alitabiri nini katika mfano wake wa ngano na magugu? (b) Mfano wa Yesu ulitimizwaje baada ya mwaka wa 1914, na matokeo yamekuwa nini?

10 Katika mfano wake wa ngano na magugu, Yesu alitabiri giza la kiroho ambalo lingetokana na uasi-imani. Alisema  kwamba “watu wakiwa wamelala usingizi,” Ibilisi angepanda magugu katikati ya mbegu za ngano ambazo Mwana wa binadamu alikuwa amepanda shambani. Ngano na magugu zingekua pamoja mpaka “umalizio wa mfumo wa mambo.” Yesu alieleza kwamba “mbegu nzuri” inafananisha “wana wa ufalme” na “magugu” ni “wana wa yule mwovu.” Wakati wa mwisho, Mwana wa binadamu atatuma “wavunaji,” yaani, malaika, ili watenganishe ngano ya mfano na magugu ya mfano. Kisha wana wa Ufalme watakusanywa. (Mt. 13:24-30, 36-43) Hilo lilitimiaje, na linahusianaje na kuwepo kwa watu wa Yehova duniani?

11 “Umalizio wa mfumo wa mambo” ulianza mwaka wa 1914. Vita vilipotokea mwaka huo, “wana wa ufalme,” yaani, Wakristo wachache watiwa-mafuta ambao walikuwa 5,000 hivi, walikuwa katika utekwa wa kiroho wa Babiloni Mkubwa. Katika mwaka wa 1919, Yehova aliwakomboa, na hivyo akaonyesha wazi tofauti kati yao na “magugu,” au Wakristo bandia. Aliwakusanya “wana wa ufalme” na kuwapanga kitengenezo na hivyo kutimiza unabii huu wa Isaya: “Je, nchi itazaliwa kwa uchungu katika siku moja? Au, je, taifa litazaliwa wakati uleule mmoja? Kwa maana Sayuni ameshikwa na uchungu wa kuzaa naye vilevile amezaa wanawe.” (Isa. 66:8) Sayuni, yaani, tengenezo la Yehova la viumbe wa roho, lilizaa wana waliotiwa mafuta kwa roho na kuwapanga kuwa taifa.

12. Watiwa-mafuta wameonyeshaje kwamba wao ndio “watu kwa ajili ya jina [la Yehova]” leo?

12 Kama Wakristo wa karne ya kwanza, “wana wa ufalme” watiwa-mafuta wangekuwa mashahidi wa Yehova. (Soma Isaya 43:1, 10, 11.) Hivyo, wangekuwa tofauti kwa sababu ya mwenendo wao wa Kikristo na kazi yao ya kuhubiri “hii habari njema ya ufalme . . . kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14; Flp. 2:15) Kwa njia hiyo, wamewasaidia mamilioni kuwa na msimamo wenye uadilifu mbele za Yehova.—Soma Danieli 12:3.

 “TUTAKWENDA PAMOJA NANYI”

13, 14. Ili kumwabudu na kumtumikia Yehova kwa njia inayokubalika, ni lazima watu wasio Waisraeli wa kiroho wafanye nini, na hilo lilitabiriwaje katika Biblia?

13 Tuliona katika makala iliyotangulia kwamba katika taifa la kale la Israeli, wageni wangemwabudu Yehova kwa njia inayokubalika ikiwa tu wangejiunga na watu waliofanya agano na Yehova. (1 Fal. 8:41-43) Vivyo hivyo leo, wale ambao si Waisraeli wa kiroho lazima waabudu pamoja na watu wa Yehova, yaani, “wana wa ufalme”—Mashahidi wa Yehova waliotiwa mafuta.

14 Manabii wawili wa kale walitabiri kwamba watu wengi wangemiminika ili kumwabudu Yehova pamoja na watu wake wakati huu wa mwisho. Isaya alitabiri hivi: “Vikundi vingi vya watu hakika vitaenda na kusema: ‘Njooni, twendeni juu kwenye mlima wa Yehova, kwenye nyumba ya Mungu wa Yakobo; naye atatufundisha njia zake, nasi tutatembea katika mapito yake.’ Kwa maana sheria itatoka katika Sayuni, na neno la Yehova katika Yerusalemu.” (Isa. 2:2, 3) Pia, nabii Zekaria alitabiri kwamba “vikundi vingi vya watu na mataifa yenye nguvu watakuja kumtafuta Yehova wa majeshi katika Yerusalemu na kuutuliza uso wa Yehova.” Aliwafananisha na “watu kumi kutoka katika lugha zote za mataifa” ambao kwa njia ya mfano, wangeshika nguo ya Israeli wa kiroho, na kusema: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.”—Zek. 8:20-23.

15. “Kondoo wengine” ‘wanakwenda pamoja’ na Waisraeli wa kiroho kufanya kazi gani?

15 “Kondoo wengine” ‘wanakwenda pamoja’ na Waisraeli wa kiroho katika kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme. (Marko 13:10) Wanakuwa sehemu ya watu wa Mungu, “kundi moja” pamoja na watiwa-mafuta, chini ya “mchungaji mwema,” Kristo Yesu.—Soma Yohana 10:14-16.

PATA ULINZI MIONGONI MWA WATU WA YEHOVA

16. Yehova ataletaje sehemu ya mwisho ya ile “dhiki kuu”?

16 Baada ya Babiloni Mkubwa kuharibiwa, watu wa Yehova watashambuliwa vikali, na wakati huo tutahitaji ulinzi wa Yehova. Kwa kuwa shambulizi hilo litaanzisha sehemu ya mwisho ya ile “dhiki kuu,” Yehova ndiye atakayeamua jinsi na ni lini shambulizi hilo litakapotukia. (Mt. 24:21; Eze. 38:2-4) Wakati huo, Gogu atashambulia “kikundi cha watu waliokusanywa pamoja kutoka katika mataifa,” yaani, watu wa Yehova. (Eze. 38:10-12) Shambulizi hilo litaonyesha kwamba wakati umefika wa Yehova kutekeleza hukumu yake dhidi ya Gogu na majeshi yake. Yehova ataitukuza enzi yake kuu na kulitakasa jina lake, kwa kuwa anasema: ‘Nami hakika nitajijulisha mwenyewe mbele ya macho ya mataifa mengi; nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’—Eze. 38:18-23.

Wakati wa ile “dhiki kuu,” tutahitaji kushirikiana kwa ukaribu na kutaniko letu (Tazama fungu la 16-18)

17, 18. (a) Yehova atawapa watu wake maagizo gani Gogu atakapowashambulia? (b) Ni lazima tufanye nini ili Yehova atulinde?

17 Gogu atakapoanza kushambulia, Yehova atawaambia hivi watumishi wake: “Nendeni, watu wangu, ingia katika vyumba vyako vya ndani, na ufunge milango nyuma yako. Jifiche kwa kitambo kidogo mpaka hukumu itakapopita.” (Isa. 26:20) Wakati huo, Yehova atatupatia maagizo yatakayookoa uhai wetu, na huenda ‘vyumba vya ndani’ vikahusianishwa na makutaniko yetu.

18 Hivyo basi, ikiwa tunataka Yehova atulinde wakati wa dhiki kuu, ni lazima tutambue kwamba ana watu wake duniani waliopangwa katika makutaniko. Ni lazima tuendelee kushikamana nao na kuendelea kushirikiana kwa ukaribu na kutaniko letu. Acheni tujiunge na mtunga-zaburi kutangaza hivi kwa moyo wetu wote: “Wokovu ni wa Yehova. Baraka yako iko juu ya watu wako.”—Zab. 3:8.