Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Wazee na watumishi wa huduma huwekwaje rasmi katika kila kutaniko?

Katika karne ya kwanza W.K., mtume Paulo aliwaambia hivi wazee waliotumika katika kutaniko la Efeso: “Jiangalieni ninyi wenyewe na kundi lote, ambalo roho takatifu imewaweka ninyi rasmi kuwa waangalizi kati yake, kulichunga kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.” (Mdo. 20:28) Roho takatifu inatimiza sehemu gani katika kuwekwa rasmi kwa wazee na watumishi wa huduma leo?

Kwanza, roho takatifu iliwaongoza waandikaji wa Biblia kuandika sifa za kustahili za wazee na watumishi wa huduma. Matakwa 16 ya wazee yameorodheshwa katika 1 Timotheo 3:1-7. Sifa nyingine za kustahili zinapatikana katika maandiko kama vile Tito 1:5-9 na Yakobo 3:17 na 18. Sifa za kustahili za watumishi wa huduma zimeorodheshwa katika 1 Timotheo 3:8-10, 12 na 13. Pili, wale wanaowapendekeza wazee na watumishi wa huduma hutoa sala hususa ili roho ya Yehova iwaongoze wanapochunguza ikiwa ndugu anatimiza matakwa ya Kimaandiko kwa kadiri inayofaa. Tatu, yule anayependekezwa anahitaji kudhihirisha tunda la roho takatifu ya Mungu maishani mwake. (Gal. 5:22, 23) Kwa hiyo, roho ya Mungu inahusika katika hatua zote za kumweka rasmi ndugu kuwa mzee au mtumishi wa huduma.

Lakini ni nani hasa anayewaweka rasmi ndugu hao? Awali, mapendekezo yote ya kuwaweka rasmi wazee na watumishi wa huduma yalitumwa kwenye ofisi ya tawi. Katika ofisi ya tawi, ndugu waliowekwa rasmi na Baraza Linaloongoza walipewa mgawo wa kuchunguza mapendekezo hayo na kuwaweka rasmi wanaostahili. Kisha, ofisi ya tawi ilijulisha baraza la wazee kuhusu mapendekezo hayo. Halafu wazee waliwajulisha ndugu hao kwamba wamewekwa rasmi na kuwauliza ikiwa walikuwa tayari na ikiwa kwa kweli walistahili kukubali mgawo huo. Mwishowe, tangazo lilitolewa kutanikoni.

Lakini ndugu waliwekwaje rasmi katika karne ya kwanza? Nyakati nyingine, mitume waliwaweka rasmi wanaume ili kushughulikia mambo fulani hususa, kama wale wanaume saba waliowekwa rasmi ili kuwagawia wajane chakula kila siku. (Mdo. 6:1-6) Hata hivyo, huenda tayari wanaume hao walitumikia wakiwa wazee kabla ya kupewa mgawo huo wa ziada.

Ingawa Maandiko hayaelezi kwa undani jinsi kila mzee na mtumishi wa huduma alivyowekwa rasmi wakati huo, kuna madokezo yanayoonyesha utaratibu uliofuatwa. Tunaambiwa kwamba Paulo na Barnaba walipokuwa wakirudi nyumbani baada ya safari yao ya kwanza ya umishonari, ‘waliwaweka  rasmi wanaume wazee kwa ajili yao katika kila kutaniko, wakitoa sala pamoja na kufunga, na kuwakabidhi kwa Yehova ambaye walikuwa wamemwamini.’ (Mdo. 14:23) Miaka mingi baadaye, Paulo alimwandikia hivi Tito, msafiri mwenzake: “Nilikuacha wewe Krete, ili uyarekebishe mambo yaliyokuwa na kasoro na uweke rasmi wanaume wazee katika jiji baada ya jiji, kama nilivyokupa maagizo.” (Tito 1:5) Vivyo hivyo, inaonekana kwamba Timotheo, aliyesafiri kotekote na mtume Paulo, alipewa mamlaka hayo. (1 Tim. 5:22) Basi ni wazi kwamba wanaume hao wazee hawakuwekwa rasmi na mitume na wanaume wazee waliokuwa Yerusalemu bali waliwekwa rasmi na waangalizi wanaosafiri.

Kwa kuzingatia kielelezo hicho kilicho katika Biblia, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova limerekebisha utaratibu wa kuwaweka rasmi wazee na watumishi wa huduma. Kuanzia Septemba 1, 2014, utaratibu ufuatao wa kuwaweka ndugu rasmi umekuwa ukifuatwa: Kila mwangalizi wa mzunguko huchunguza kwa makini mapendekezo yanayofanywa katika mzunguko wake. Anapotembelea makutaniko, atajitahidi kuwajua wale waliopendekezwa na kushiriki nao katika huduma ikiwezekana. Baada ya kuzungumzia mapendekezo hayo na baraza la wazee kutanikoni, mwangalizi wa mzunguko ana daraka la kuwaweka rasmi wazee na watumishi wa huduma katika makutaniko yaliyo katika mzunguko wake. Wanapofanya hivyo wanafuata kwa ukaribu zaidi kielelezo cha karne ya kwanza.

Wazee wanazungumza na mwangalizi wa mzunguko kuhusu sifa za ndugu za kustahili zinazoonyeshwa katika Maandiko (Malawi)

Ni nani wanaoshughulikia majukumu mbalimbali katika utaratibu huo? Sikuzote, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ana jukumu la msingi la kuwalisha watumishi wa nyumbani. (Mt. 24:45-47) Hilo linatia ndani kuchunguza Maandiko kwa msaada wa roho takatifu ili kutoa mwongozo kuhusu njia inayofaa ya kutumia kanuni za Biblia zinazoongoza utaratibu wa kutaniko la ulimwenguni pote. Mtumwa mwaminifu pia huwaweka rasmi waangalizi wote wa mzunguko na washiriki wa Halmashauri ya Tawi. Na kila ofisi ya tawi husaidia kutekeleza mwongozo unaotolewa. Kila baraza la wazee lina wajibu mzito wa kuchunguza kwa makini sana ili kuhakikisha kwamba ndugu wanaowapendekeza katika kutaniko la Mungu wanatimiza sifa za kustahili zinazoonyeshwa katika Maandiko. Kila mwangalizi wa mzunguko ana daraka zito la kusali na kuchunguza kwa uangalifu mapendekezo yanayofanywa na wazee na kisha kuwaweka rasmi wanaume wanaostahili.

Tunapoelewa jinsi wazee na watumishi wa huduma wanavyowekwa rasmi, tunaelewa kikamili zaidi jukumu la roho takatifu katika utaratibu huo. Na hilo linatusaidia kuwatumaini zaidi na kuwaheshimu wale waliowekwa rasmi katika kutaniko la Kikristo.—Ebr. 13:7, 17.

Ni nani wale mashahidi wawili wanaotajwa katika Ufunuo sura ya 11?

Andiko la Ufunuo 11:3 linasema kwamba mashahidi wawili wangetoa unabii kwa siku 1,260. Kisha, simulizi hilo linasema kwamba mnyama-mwitu ‘angewashinda na kuwaua.’ Lakini baada ya “siku tatu na nusu,” mashahidi hao wawili wangerudishwa kwenye uhai, na hilo lingewashangaza watu wote waliokuwa wakiwatazama.—Ufu. 11:7, 11.

Mashahidi hao wawili ni nani? Mambo yanayotajwa katika simulizi hilo yanatusaidia kuwatambua. Kwanza, tunaambiwa kwamba “wanafananishwa na ile mizeituni miwili na vile vinara viwili vya taa.” (Ufu. 11:4) Hilo linatukumbusha kile kinara cha taa na mizeituni miwili inayotajwa katika unabii wa Zekaria. Biblia inasema kwamba mizeituni hiyo ilifananisha “wale watiwa-mafuta wawili,” yaani, Gavana Zerubabeli na Kuhani Mkuu Yoshua, “wanaosimama kando ya Bwana wa dunia yote.” (Zek. 4:1-3, 14) Pili, Biblia inasema kwamba hao mashahidi wawili wanafanya miujiza kama ile iliyofanywa na Musa na Eliya.—Linganisha na Ufunuo 11:5, 6 na Hesabu 16:1-7, 28-35 na 1 Wafalme 17:1; 18:41-45.

Marejeo hayo yanahusianaje na Ufunuo sura ya 11 na Zekaria 4:1-3, na 14? Kila simulizi linawarejelea watiwa-mafuta wa Mungu waliokuwa wakiongoza katika wakati huo mgumu wa majaribu. Basi Ufalme wa Mungu ulipoanza kutawala mbinguni mwaka wa 1914, ndugu watiwa-mafuta waliokuwa wakiongoza wakati huo walitimiza andiko la Ufunuo sura ya 11 kwa kuhubiri kwa miaka mitatu na nusu wakiwa wamevikwa “nguo za magunia.”

Baada ya kuhubiri wakiwa wamevikwa nguo za magunia, watiwa-mafuta hao waliuawa kwa njia ya mfano walipofungwa gerezani kwa muda mfupi, yaani, kwa siku tatu na nusu za mfano. Maadui wa watu wa Mungu walishangilia sana kwa sababu waliona kwamba kazi yao ilikuwa imekomeshwa au kuuawa kwa njia ya mfano.—Ufu. 11:8-10.

Hata hivyo, kama ilivyotabiriwa, baada ya siku tatu na nusu, mashahidi hao wawili walirudishwa kwenye uhai. Watiwa-mafuta hao waliwekwa huru kutoka gerezani na wale waliobaki waaminifu wakapokea mgawo wa pekee kutoka kwa Mungu kupitia Bwana wao, Yesu Kristo. Mwaka wa 1919, walikuwa miongoni mwa wale waliowekwa rasmi kutumika wakiwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ili kushughulikia mahitaji ya kiroho ya watu wa Mungu katika siku za mwisho.—Mt. 24:45-47; Ufu. 11:11, 12.

Kwa kweli, andiko la Ufunuo 11:1 na 2 linahusianisha matukio hayo na wakati ambapo hekalu la kiroho lingepimwa, au kukaguliwa. Andiko la Malaki sura ya 3 linataja ukaguzi kama huo wa hekalu la kiroho, uliofuatwa na kipindi cha kutakasa. (Mal. 3:1-4) Kazi hiyo ya kukagua na kutakasa ilichukua muda gani? Ilianza mwaka wa 1914 mpaka mwanzoni mwa 1919. Kipindi hicho kinatia ndani siku 1,260 (miezi 42) na siku tatu na nusu za mfano zinazotajwa katika Ufunuo sura ya 11.

Tunafurahi sana kwamba Yehova alipanga kazi hiyo ya usafishaji wa kiroho ifanywe ili ajisafishie mwenyewe watu walio wake kwa njia ya pekee, walio na bidii kwa ajili ya kazi njema! (Tito 2:14) Isitoshe, tunathamini mfano uliowekwa na watiwa-mafuta waaminifu walioongoza wakati huo wa majaribu na hivyo kutumikia wakiwa wale mashahidi wawili wa mfano. *