Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Sikiliza, Upate Maana’

‘Sikiliza, Upate Maana’

“Nisikilizeni, ninyi nyote, mpate maana.”—MARKO 7:14.

1, 2. Kwa nini watu wengi waliomsikiliza Yesu hawakupata maana ya maneno yake?

UNAWEZA kusikia sauti ya mtu anayeongea na hata kutambua hisia zake. Lakini kuna faida gani ya kufanya hivyo ikiwa huelewi au hupati maana ya maneno anayosema? (1 Kor. 14:9) Vivyo hivyo, maelfu ya watu walisikia maneno ya Yesu. Hata alizungumza nao katika lugha ambayo wangeweza kuelewa. Hata hivyo, si wote waliopata maana ya maneno yake. Ndiyo sababu Yesu aliwaambia hivi watu waliokuwa wakimsikiliza: “Nisikilizeni, ninyi nyote, mpate maana.”—Marko 7:14.

2 Kwa nini watu wengi hawakupata maana ya maneno ya Yesu? Baadhi yao walishikilia maoni yao na walikuwa na nia mbaya. Yesu aliwaambia hivi: “Kwa ustadi mnaweka kando amri ya Mungu kusudi mbaki na mapokeo yenu.” (Marko 7:9) Kwa kweli watu hao hawakujaribu kupata maana ya maneno yake. Hawakutaka kubadili njia na maoni yao. Huenda masikio yao yalikuwa wazi, lakini mioyo yao ilikuwa imefungwa kabisa, yaani, ilikuwa migumu! (Soma Mathayo 13:13-15.) Lakini tunawezaje kuhakikisha kwamba mioyo yetu inabaki ikiwa imefunguka ili tunufaike na mafundisho ya Yesu?

JINSI YA KUNUFAIKA NA MAFUNDISHO YA YESU

3. Kwa nini wanafunzi walielewa maneno ya Yesu?

3 Tunahitaji kufuata mfano wa wanafunzi wa Yesu waliokuwa wanyenyekevu. Alisema hivi kuwahusu: “Yenye furaha ni  macho yenu kwa sababu hayo yanaona, na masikio yenu kwa sababu hayo yanasikia.” (Mt. 13:16) Kwa nini walielewa maneno yake ilhali watu wengine hawakuyaelewa? Kwanza, walikuwa tayari kuuliza maswali na kujitahidi kuelewa maana ya maneno ya Yesu. (Mt. 13:36; Marko 7:17) Pili, walikuwa tayari kuongeza ujuzi wao kuhusu mambo ambayo walikuwa wamekubali mioyoni mwao. (Soma Mathayo 13:11, 12.) Tatu, walikuwa tayari kutumia katika maisha yao mambo waliyosikia na kuelewa, na pia kuyatumia pia kuwasaidia wengine.—Mt. 13:51, 52.

4. Ili kuelewa mifano ya Yesu, tunapaswa kufanya mambo gani matatu?

4 Ikiwa tunataka kuelewa mifano ya Yesu, tunahitaji kufuata mfano wa wanafunzi wake waaminifu. Tunahitaji pia kufanya mambo matatu yafuatayo. Kwanza, tunahitaji kutumia wakati kujifunza na kutafakari mambo ambayo Yesu alisema, kufanya utafiti, na kujiuliza maswali. Tunapofanya hivyo, tunapata ujuzi. (Met. 2:4, 5) Kisha, tunahitaji kuona jinsi ujuzi huo unavyohusiana na mambo ambayo tayari tunajua, na kutambua jinsi yanavyotunufaisha sisi binafsi. Tunapofanya hivyo, tunapata uelewaji. (Met. 2:2, 3) Mwishowe, tunapaswa kutumia mambo tuliyojifunza, na kutenda kupatana nayo maishani mwetu. Tunapofanya hivyo, tunaonyesha kwamba tuna hekima.Met. 2:6, 7.

5. Toa mfano ambao unaonyesha tofauti kati ya ujuzi, uelewaji, na hekima.

5 Kuna tofauti gani kati ya ujuzi, uelewaji, na hekima? Tunaweza kutumia mfano huu: Wazia kwamba umesimama katikati ya barabara na basi linakuja kwa kasi. Kwanza, unatambua kwamba basi linakuja—huo ni ujuzi. Kisha, unatambua kwamba ukiendelea kusimama barabarani litakugonga—huo ni uelewaji! Kwa hiyo, unaondoka haraka barabarani—hiyo ni hekima! Ndiyo sababu Biblia inatuhimiza ‘tulinde hekima inayotumika’ kwa kuwa inaweza kuokoa uhai wetu.—Met. 3:21, 22; 1 Tim. 4:16.

6. Ni maswali gani manne tutakayouliza tunapochunguza mifano saba aliyotumia Yesu? (Tazama  sanduku kwenye ukurasa wa 8.)

6 Katika makala hii na ifuatayo, tutachunguza mifano saba ambayo Yesu alitumia. Tunapofanya hivyo, tutauliza maswali yafuatayo: Mfano huu unamaanisha nini? (Swali hili linatusaidia kupata ujuzi.) Kwa nini Yesu alitoa mfano huu? (Swali hili linatusaidia kupata uelewaji.) Tunawezaje kutumia habari hii kwa manufaa yetu na ya wengine? (Hiyo ni hekima.) Mwishowe, mfano huu unatufundisha nini kumhusu Yehova na Yesu?

MBEGU YA HARADALI

7. Mfano wa mbegu ya haradali unamaanisha nini?

7 Soma Mathayo 13:31, 32. Mfano wa Yesu wa mbegu ya haradali unamaanisha nini? Mbegu hiyo inafananisha ujumbe wa Ufalme na pia matokeo ya kuhubiriwa kwa ujumbe huo, yaani, kutaniko la Kikristo. Sawa na mbegu ya haradali ambayo ndiyo “mbegu ndogo zaidi kuliko zote,” kutaniko la Kikristo lilikuwa na mwanzo mdogo katika mwaka wa 33 W.K. Hata hivyo, baada ya miaka michache, kutaniko hilo lilikua haraka sana. Wengi hawakutarajia kwamba lingepanuka kwa kasi sana hivyo. (Kol. 1:23) Ukuzi huo ulikuwa na manufaa kwa sababu Yesu anatuambia kwamba “ndege wa mbinguni” waliweza “kupata makao katikati ya matawi yake.” Ndege hao wa mfano wanafananisha watu wenye mioyo minyoofu wanaopata chakula cha kiroho, kivuli, na makao katika kutaniko la Kikristo.—Linganisha na Ezekieli 17:23.

8. Kwa nini Yesu alitumia mfano wa mbegu ya haradali?

 8 Kwa nini Yesu alitumia mfano huu? Alitumia ukuzi unaostaajabisha wa mbegu ya haradali kuonyesha jinsi Ufalme wa Mungu ulivyo na nguvu za kupanuka, kulinda, na kushinda vipingamizi vyote. Kuanzia mwaka wa 1914, sehemu inayoonekana ya tengenezo la Mungu imekua kwa njia kubwa ajabu! (Isa. 60:22) Wale wanaoshirikiana na tengenezo hilo wamefurahia ulinzi mzuri sana wa kiroho. (Met. 2:7; Isa. 32:1, 2) Isitoshe, hakuna upinzani wowote ambao umezuia ukuzi unaoendelea wa kazi ya Ufalme.—Isa. 54:17.

9. (a) Tunajifunza nini kutokana na mfano wa mbegu ya haradali? (b) Jambo hilo linatufundisha nini kumhusu Yehova na Yesu?

9 Tunajifunza nini kutokana na mfano wa mbegu ya haradali? Labda tunaishi katika eneo ambalo lina Mashahidi wachache au ambalo kwa sasa hatupati matokeo mengi katika kazi yetu ya kuhubiri. Hata hivyo, kukumbuka kwamba Ufalme unaweza kushinda vipingamizi vyote kutatuimarisha ili tuweze kuvumilia. Kwa mfano, Ndugu Edwin Skinner alipofika India mwaka wa 1926, Mashahidi walikuwa wachache sana nchini humo. Mwanzoni, kazi ya kuhubiri “ilikuwa ngumu sana” kwa sababu ukuzi ulikuwa wa polepole. Lakini aliendelea kuhubiri na kuona ujumbe wa Ufalme ukishinda vipingamizi vikubwa. Sasa kuna Mashahidi zaidi ya 37,000 wenye bidii nchini India, na watu zaidi ya 108,000 walihudhuria Ukumbusho mwaka uliopita. Fikiria mfano mwingine unaoonyesha jinsi ambavyo kazi ya Ufalme imepanuka sana. Mashahidi walianza kuhubiri nchini Zambia mwaka uleule ambao Ndugu Skinner alifika India. Sasa kuna wahubiri zaidi ya 170,000 nchini Zambia, na watu 763,915 walihudhuria Ukumbusho mwaka wa 2013. Hilo linamaanisha kwamba mtu 1 kati ya kila watu 18 nchini Zambia alihudhuria Ukumbusho. Huo ni ukuzi wenye kustaajabisha kama nini!

CHACHU

10. Mfano wa chachu unamaanisha nini?

10 Soma Mathayo 13:33. Mfano wa chachu  unamaanisha nini? Mfano huo unahusu pia ujumbe wa Ufalme na matokeo yake. “Tonge lote” la unga linafananisha mataifa yote, na kuchacha kwa tonge hilo kunafananisha kuenea kwa ujumbe wa Ufalme kupitia kazi ya kuhubiri. Ukuzi wa mbegu ya haradali unaonekana waziwazi lakini kuenea kwa chachu hakuonekani mwanzoni. Matokeo yake yanaonekana baadaye.

11. Kwa nini Yesu alitumia mfano wa chachu?

11 Kwa nini Yesu alitumia mfano huu? Alikuwa akionyesha kwamba ujumbe wa Ufalme una nguvu za kuenea sana na kuleta mabadiliko. Ujumbe wa Ufalme umefika “sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Hata hivyo, nyakati nyingine mabadiliko yanayoletwa na ujumbe huo hayaonekani waziwazi, na huenda hata yasionekane mwanzoni. Lakini kuna mabadiliko, na si mabadiliko tu ya idadi bali pia mabadiliko katika utu wa wale wanaokubali ujumbe huo unaoenea.—Rom. 12:2; Efe. 4:22, 23.

12, 13. Toa mifano inayoonyesha jinsi ambavyo kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme imekua kama inavyoelezwa katika mfano wa chachu.

12 Mara nyingi matokeo ya kazi ya kuhubiri huonekana miaka mingi baada ya watu kuhubiriwa. Kwa mfano, wenzi wa ndoa, Franz na Margit, ambao sasa wanatumika katika ofisi nyingine ya tawi walikuwa wakitumika katika ofisi ya tawi nchini Brazili mwaka wa 1982. Wakati huo, walihubiri katika mji fulani mdogo wa mashambani. Mama fulani na watoto wake wanne walikuwa miongoni mwa wanafunzi wao wa Biblia. Mwanaye mkubwa aliyekuwa na umri wa miaka 12 tu wakati huo, alikuwa mwenye haya sana na mara nyingi alijaribu kujificha kabla ya funzo. Wenzi hao walipewa mgawo mpya na hivyo hawakuendelea kujifunza nao. Lakini walitembelea mji huo miaka 25 baadaye. Walipata nini? Walipata kutaniko lenye wahubiri 69, na 13 kati yao walikuwa mapainia wa kawaida, na walikutana katika Jumba jipya la Ufalme. Vipi yule mvulana mwenye haya? Sasa yeye ni mratibu wa baraza la wazee! Kama ile chachu katika mfano wa Yesu, ujumbe wa Ufalme ulikua na kubadili maisha ya wengi na hilo liliwaletea shangwe wenzi hao!

13 Nguvu zisizoonekana za ujumbe wa Ufalme za kubadili watu zimeonekana waziwazi katika nchi ambazo zimepiga marufuku kazi yetu ya Ufalme. Ni vigumu kujua ujumbe huo umeenea kadiri gani katika nchi hizo, na mara nyingi tunashangazwa na matokeo yake. Kwa mfano, fikiria nchi ya Kuba. Ujumbe wa Ufalme ulifika nchini humo mwaka wa 1910, na Ndugu Russell alitembelea Kuba mwaka wa 1913. Hata hivyo, mwanzoni ukuzi ulikuwa wa polepole sana. Sasa hali ikoje nchini Kuba? Kuna wahubiri zaidi ya 96,000 wanaohubiri habari njema, na watu 229,726 walihudhuria Ukumbusho mwaka wa 2013, yaani, mtu 1 kwa kila watu 48 katika kisiwa hicho. Hata hivyo, katika nchi ambazo haziko chini ya marufuku, huenda ujumbe wa Ufalme umefika katika maeneo ambayo Mashahidi wanafikiri kwamba hauwezi kufika. *Mhu. 8:7; 11:5.

14, 15. (a) Tunaweza kunufaikaje kibinafsi na mfano wa chachu? (b) Mfano huo unatufundisha nini kumhusu Yehova na Yesu?

14 Mambo aliyofundisha Yesu katika mfano wa chachu yanaweza kutunufaishaje? Tunapotafakari maana ya mfano  huo wa Yesu, tunatambua kwamba hatuhitaji kuhangaika kupita kiasi kuhusu jinsi ujumbe wa Ufalme utakavyowafikia mamilioni ya watu ambao bado hawajausikia. Yehova ndiye anayeongoza mambo yote. Lakini kazi yetu ni nini? Neno la Mungu linajibu hivi: “Asubuhi panda mbegu zako na mpaka jioni usiache mkono wako upumzike; kwa maana hujui ni wapi hii itafanikiwa, hapa au pale, au ikiwa zote mbili zitakuwa njema.” (Mhu. 11:6) Hata hivyo, hatupaswi kamwe kusahau kusali ili kazi yetu ya kuhubiri ifanikiwe, hasa katika nchi ambazo zimepiga marufuku kazi yetu.—Efe. 6:18-20.

15 Zaidi ya hayo, hatupaswi kuvunjika moyo tusipopata matokeo mazuri mwanzoni. Hatupaswi kamwe kudharau “siku ya mambo madogo.” (Zek. 4:10) Mwishowe huenda tukapata matokeo mengi mazuri kuliko tulivyotarajia!—Zab. 40:5; Zek. 4:7.

MWANABIASHARA MSAFIRI NA HAZINA ILIYOFICHWA

16. Mfano wa mwanabiashara msafiri na mfano wa hazina iliyofichwa unamaanisha nini?

16 Soma Mathayo 13:44-46. Mfano wa mwanabiashara msafiri na mfano wa hazina iliyofichwa unamaanisha nini? Katika siku za Yesu, baadhi ya wanabiashara walisafiri mpaka Bahari ya Hindi ili kupata lulu bora zaidi. Mwanabiashara katika mfano huo anafananisha watu wenye mioyo minyoofu wanaofanya yote wawezayo ili kutosheleza mahitaji yao ya kiroho. “Lulu moja ya thamani kubwa” inafananisha kweli ya Ufalme yenye thamani. Baada ya kutambua thamani ya lulu hiyo, mwanabiashara huyo alikuwa tayari kuuza “mara moja” vitu vyote alivyokuwa navyo ili ainunue. Pia, Yesu alisimulia kuhusu mtu aliyekuwa akifanya kazi shambani na kupata hazina “iliyofichwa.” Tofauti na yule mwanabiashara, mtu huyo hakuwa akitafuta hazina. Hata hivyo, sawa na yule mwanabiashara, alikuwa tayari kuuza “vitu vyote” ili apate hazina hiyo.

17. Kwa nini Yesu alitoa mfano wa mwanabiashara anayesafiri na mfano wa hazina iliyofichwa?

17 Kwa nini Yesu alitoa mifano hiyo miwili? Alikuwa akionyesha kwamba kweli hupatikana kwa njia mbalimbali. Baadhi ya watu wanaitafuta na wamejidhabihu sana ili kuipata. Wengine wamepata kweli—huenda kwa kuhubiriwa—hata ingawa hawakuwa wakiitafuta. Vyovyote vile, kila mmoja wao alitambua thamani ya alichopata, naye alikuwa tayari kujidhabihu sana ili kukipata.

18. (a) Tunawezaje kunufaika kutokana na mifano hiyo miwili? (b) Inatufundisha nini kumhusu Yehova na Yesu?

18 Tunawezaje kunufaika kutokana na mifano hiyo miwili? (Mt. 6:19-21) Jiulize hivi: ‘Je, nina mtazamo kama wa watu hao? Je, ninathamini sana kweli kama walivyoithamini? Je, niko tayari kujidhabihu ili kuipata, au ninaruhusu vitu vingine kama vile mahangaiko ya maisha, vinikengeushe kutoka katika kweli?’ (Mt. 6:22-24, 33; Luka 5:27, 28; Flp. 3:8) Kadiri shangwe yetu ya kupata kweli inavyozidi kuongezeka, ndivyo tutakavyoazimia kutanguliza kweli maishani mwetu.

19. Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

19 Acheni tuonyeshe kwamba tumesikiliza na kuelewa kikweli maana ya mifano hiyo ya Ufalme. Kumbuka kwamba hatufanyi hivyo kwa kuelewa tu maana yake bali pia kwa kutumia mambo tunayojifunza kutokana nayo. Katika makala inayofuata, tutachunguza mifano mingine mitatu na kuona mambo tunayoweza kujifunza kutokana nayo.

^ fu. 13 Kumekuwa na ukuzi kama huo katika nchi kama vile Argentina (Kitabu cha Mwaka wa 2001, ukurasa wa 186, Kiingereza); Ujerumani Mashariki (Kitabu cha Mwaka wa 1999, ukurasa wa 83, Kiingereza); Papua New Guinea (Kitabu cha Mwaka wa 2005, ukurasa wa 63); na Kisiwa cha Robinson Crusoe (Mnara wa Mlinzi, Juni 15, 2000, ukurasa wa 9).