Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umesoma kwa makini matoleo ya hivi karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Ona ikiwa unaweza kujibu maswali yafuatayo:

Je, desturi ya kuchoma maiti inawafaa Wakristo?

Kuchoma au kutochoma maiti ni uamuzi wa mtu binafsi. Ingawa Biblia haitaji zoea hili moja kwa moja, tunapaswa kukumbuka kwamba miili ya Mfalme Sauli na mwana wake Yonathani ilichomwa, kisha ikazikwa. (1 Sam. 31:2, 8-13)—6/15, ukurasa wa 7.

Tunawezaje kuwa na uhakika kwamba si Mungu anayesababisha mambo mabaya?

Mungu ni mwadilifu katika njia zake zote. Yeye ni mwenye haki, mwaminifu, na mnyoofu. Yehova pia ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema. (Kum. 32:4; Zab. 145:17; Yak. 5:11)—7/1, ukurasa wa 4.

Mtu anaweza kukabiliana na changamoto gani anapohamia nchi nyingine ili kutumika katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi?

Kuna changamoto tatu, (1) kuishi maisha tofauti, (2) kutamani kurudi nyumbani, na (3) kuzoeana na ndugu katika eneo ambalo amehamia. Wengi ambao wamekabiliana na changamoto hizo wamepata baraka nyingi.—7/15, ukurasa wa 4-5.

Kwa nini ndugu za Yosefu walimchukia?

Kwa sababu Yakobo alimpenda sana Yosefu, na alimpa vazi la pekee. Ndugu za Yosefu walimwonea wivu na kumuuza utumwani.—8/1, ukurasa wa 11-13.

Kwa nini trakti mpya zina matokeo mazuri na ni rahisi kutumia?

Trakti zote mpya zina mpangilio uleule. Kila trakti hutuchochea kusoma andiko kutoka katika Biblia na ina swali kwa mwenye nyumba. Vyovyote vile mwenye nyumba atakavyojibu, tunaweza kufungua ukurasa wa pili na kumwonyesha yale ambayo Biblia inasema. Tunaweza pia kumwonyesha swali tutakalozungumzia tutakaporudi.—8/15, ukurasa wa 13-14.

Peshitta ya Kisiria ni nini?

Lugha ya Kisiria, ambayo ni lahaja ya Kiaramu, ilianza kutumiwa sana katika karne ya pili au ya tatu W.K. Inaonekana kwamba Kisiria ndiyo lugha iliyotumika kwanza kutafsiri sehemu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Biblia hiyo ya Kisiria iliitwa Peshitta.9/1, ukurasa wa 13-14.

Wazazi Wakristo wanawezaje kuwachunga watoto wao?

Ni muhimu kuwasikiliza watoto wako ili uwajue. Jitahidi kuwalisha kiroho. Waongoze kwa upendo, kwa mfano wanapokabiliana na mambo yanayowafanya watilie shaka mambo ya kiroho.—9/15, ukurasa wa 18-21.

Ni mambo gani hayatakuwapo tena Ufalme wa Mungu utakapotawala?

Hakutakuwapo tena na matatizo ya afya, kifo, ukosefu wa kazi, vita, upungufu wa chakula, na umaskini.—10/1, ukurasa wa 6-7.

Ni agano gani linalotajwa katika Biblia linaloruhusu watu wengine kutawala na Kristo?

Baada ya mlo wa mwisho wa Pasaka pamoja na mitume wake, Yesu alifanya agano pamoja na wanafunzi wake waaminifu ambalo linaweza kuitwa agano la Ufalme. (Luka 22:28-30) Agano hilo liliwahakikishia kwamba watatawala pamoja na Yesu mbinguni.—10/15, ukurasa wa 16-17.

Toa mifano miwili kutoka katika Biblia inayothibitisha kwamba Shetani ni kiumbe halisi.

Maandiko yanasema kwamba Shetani alizungumza na Yesu alipokuwa akimshawishi. Pia katika siku za Ayubu, Shetani alizungumza na Mungu. Masimulizi hayo yanathibitisha kwamba Shetani ni kiumbe halisi.—11/1, ukurasa wa 4-5.

Ni nani waliokuwa “watu kwa ajili ya jina lake” ambao Yakobo alizungumza juu yao kwenye Matendo 15:14?

Walikuwa Wayahudi na waamini wasio Wayahudi ambao Mungu alikuwa amewateua wawe jamii iliyochaguliwa ili ‘watangaze kotekote sifa bora’ za Yeye aliyewaita. (1 Pet. 2:9, 10)—11/15, ukurasa wa 24-25.

Jiji la Timgad lilikuwa wapi, na baadhi ya wakaaji wake walikuwa na mtazamo gani?

Timgad lilikuwa jiji kubwa la Waroma lililokuwa Afrika Kaskazini (leo ni nchi ya Algeria). Maandishi yaliyochimbuliwa katika eneo hilo ambayo yanasema: “Kuwinda, Kuoga, Kucheza, Kucheka—Haya Ndiyo Maisha!” yanaonyesha mtazamo ambao baadhi ya wakaaji wake walikuwa nao. Mtazamo kama huo unatajwa katika andiko la 1 Wakorintho 15:32.12/1, ukurasa 8-10.