Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Majibu ya Maswali ya Biblia

Majibu ya Maswali ya Biblia

Je, inawezekana ulimwengu wote kutawaliwa na serikali moja?

Serikali ya ulimwenguni pote inawezaje kuwaunganisha watu wa mataifa yote? Isaya 32:1, 17; 54:13

Fikiria faida ambazo wanadamu wangepata ikiwa kungekuwa na serikali moja tu duniani pote. Leo watu wengi wanateseka kwa sababu ya umaskini ilhali wengine ni matajiri sana. Hata hivyo, serikali inayowajali watu itahakikisha kwamba kila mtu duniani anapata mahitaji yake. Je, wanadamu wanaweza kuunda serikali kama hiyo?—Soma Yeremia 10:23.

Historia inaonyesha kwamba serikali za wanadamu zimeshindwa kuwatimizia mahitaji raia na hasa maskini. Serikali nyingine zinatawala kwa ukatili. (Mhubiri 4:1; 8:9) Hata hivyo, Mungu Mweza-Yote ameahidi kwamba serikali yake itachukua mahali pa serikali za wanadamu. Mtawala wa serikali hiyo atawatimizia watu mahitaji yao yote.—Soma Isaya 11:4; Danieli 2:44.

Ufalme wa Mungu utafanya nini?

Yehova Mungu amemchagua Mtawala anayefaa kabisa kuutawala ulimwengu, yaani, Mwana wake Yesu. (Luka 1:31-33) Alipokuwa duniani, Yesu alipenda kuwasaidia watu. Akiwa Mfalme, ataleta umoja miongoni mwa watu wa mataifa yote na kuwaondolea mateso.—Soma Zaburi 72:8, 12-14.

Je, watu wote wanamkubali Yesu kuwa Mtawala? La hasha! Hata hivyo, Yehova ni mwenye subira. (2 Petro 3:9) Anawapa watu nafasi ya kumkubali Yesu kuwa Mtawala. Hivi karibuni, Yesu atawaondoa waovu na kuleta amani na usalama ulimwenguni pote.—Soma Mika 4:3, 4.