Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tufuate Mufano wa Yesu: Tukuwe na Uhodari na Utambuzi

Tufuate Mufano wa Yesu: Tukuwe na Uhodari na Utambuzi

‘Ninyi munamupenda, ingawa hamukumuona yeye kamwe. Ingawa hamumuone wakati wa sasa, bado munaonyesha imani katika yeye.’​1 PET. 1:8.

1, 2. (a) Tunapaswa kufanya nini ili tupate uzima wa milele? (b) Ni nini inaweza kutusaidia tuendelee na safari yetu yenye kupeleka kwenye uzima wa milele?

WAKATI tunakubali kuwa wanafunzi wa Kristo, tunaanza safari ya mufano. Safari hiyo inaweza kutupeleka kwenye uzima wa milele, mbinguni ao duniani. Yesu alisema hivi: ‘Yule ambaye atavumilia mupaka mwisho [mwisho wa maisha yake ya sasa ao mwisho wa ulimwengu huu] ndiye atakayeokolewa.’ (Mt. 24:13) Ikiwa tunaendelea kuwa waaminifu, bila shaka tutapata uzima wa milele. Hata hivyo, katika safari yetu tunapaswa kuwa waangalifu ili tusikengeushwe na ili tusipotee. (1 Yoh. 2:15-17) Ni nini inaweza kutusaidia tuendelee na safari yetu?

2 Yesu ambaye ni mufano wetu, alifanya pia safari hiyo. Habari juu ya safari yake zinapatikana katika Biblia. Ikiwa tunajifunza habari hizo, tutamujua Yesu muzuri, tutamupenda na tutaonyesha imani katika yeye. (Soma 1 Petro 1:8, 9.) Kumbuka kwamba mutume Petro alisema kama Yesu alituachia mufano ili tufuate hatua zake kwa ukaribu [kwa uaminifu]. (1 Pet. 2:21) Ikiwa tunafuata mufano wake kwa uaminifu, tutafikia kusudi la imani yetu, ni kusema, uzima wa milele. * Katika habari yenye ilitangulia, tuliona namna gani tunaweza kumuiga Yesu kwa kuonyesha unyenyekevu na kutendea wengine kwa huruma. Tuone sasa namna gani tunaweza kumuiga Yesu kwa kuonyesha uhodari na utambuzi.

YESU ALIONYESHA UHODARI

3. Uhodari ni nini, na namna gani tunaweza kuupata?

3 Uhodari ni hali fulani ya kutokuwa na woga, yenye inatupatia nguvu na kututegemeza. Mutu mwenye kuwa na uhodari “anaendelea kupambana na majaribu,” “anatetea mambo yaliyo sawa,” na “anaendelea kupambana na mateso bila kupoteza imani yake ao heshima.” Uhodari unahusiana sana na woga, tumaini, na upendo. Namna gani? Kumuogopa Mungu kunatusaidia tukuwe na uhodari ili tusiogope mwanadamu. (1 Sam. 11:7; Met. 29:25) Kuwa na tumaini la kweli kunatusaidia tuone mbele kuliko kukaza akili juu ya majaribu yenye tunapata na kunatusaidia tusiogope wakati unaokuja. (Zab. 27:14) Wakati tuko na upendo wa kweli, tutakuwa na uhodari hata kama tuko katika hatari. (Yoh. 15:13) Ikiwa tunamutegemea Mungu na ikiwa tunaiga Mwana wake, bila shaka tutapata uhodari.​—Zab. 28:7.

4. Namna gani Yesu alionyesha uhodari wakati alikuwa ndani ya hekalu “katikati ya walimu”? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

4 Hata wakati Yesu alikuwa na miaka 12, alionyesha uhodari kwa kutetea mambo yaliyo sawa. Tuone mambo yenye ilitokea wakati Yesu alikuwa ndani ya hekalu, “katikati ya walimu.” (Soma Luka 2:41-47.) Walimu hao walijua sana Sheria ya Musa, lakini walijua pia mapokeo ao desturi za wanadamu ambazo zilifanya ikuwe vigumu kuheshimu Sheria hiyo. Hata hivyo, Yesu hakunyamaza kwa sababu ya kuogopa; alikuwa ‘anawauliza maswali [maulizo].’ Hakuwa anauliza maulizo kama vile mutoto mwenye anapenda kujua jambo fulani. Wazia namna Yesu anauliza maulizo yenye kuwafanya walimu hao wafikiri sana na washangae sana. Inawezekana walimu hao walimuuliza Yesu maulizo ili kumutega katika maneno yake, lakini walishindwa. Ndio sababu watu wote wenye walimusikiliza, hata walimu, ‘walishangazwa sana na uelewaji wake na majibu yake,’ ambayo bila shaka ilionyesha kwamba Neno la Mungu ni kweli.

5. Wakati alikuwa anahubiri, namna gani Yesu alionyesha uhodari?

5 Wakati alikuwa anahubiri, Yesu alionyesha uhodari katika njia mbalimbali. Hakuogopa kuonyesha wazi kwamba viongozi wa dini walipoteza watu kupitia mafundisho ya uongo. (Mt. 23:13-36) Alikataa kabisa kuambukizwa na roho ya ulimwengu. (Yoh. 16:33) Aliendelea kuhubiri hata kama maadui wake walimupinga. (Yoh. 5:15-18; 7:14) Tena, alisafisha mara mbili hekalu kwa kuwafukuza watu wote wenye walikuwa wanachafua ibada ya kweli.​—Mt. 21:12, 13; Yoh. 2:14-17.

6. Katika siku ya mwisho ya maisha yake hapa duniani, namna gani Yesu alionyesha uhodari?

6 Tukiiga mufano wa Yesu wa uhodari wakati wa mateso, imani yetu itakuwa yenye nguvu. Tufikirie kwa mufano namna alionyesha uhodari katika siku ya mwisho ya maisha yake hapa duniani. Alijua vizuri kwamba mutume wake mumoja atamutoa kwa maadui na alijua vizuri namna mambo itafuatana. Ndio sababu wakati wa chakula cha Pasaka, Yesu alimuambia Yuda hivi: “Lile unalofanya lifanye upesi [mbio] zaidi.” (Yoh. 13:21-27) Wakati alikuwa katika bustani ya Gethsemane, Yesu hakuogopa kujitambulisha kwa maaskari wenye walikuja kumukamata. Hata kama maisha yake ilikuwa katika hatari, alisema jambo fulani ili kulinda wanafunzi wake. (Yoh. 18:1-8) Na wakati alisambishwa mbele ya Sanhedrini, hakuogopa kusema kwamba yeye ni Kristo na ni Mwana wa Mungu. Hakuogopa hata kama alijua kwamba kuhani mukubwa alikuwa anatafuta sababu ya kumuua. (Mk. 14:60-65) Yesu alibakia mwaminifu mupaka kifo chake kwenye muti wa mateso. Mbele akate pumuzi, alisema hivi kwa sauti ya ushindi: “Imetimizwa!”​—Yoh. 19:28-30.

TUMUIGE YESU KWA KUONYESHA UHODARI

7. Vijana, munajisikia namna gani kwa sababu ya kuitwa kwa jina la Yehova, na namna gani munaweza kuonyesha kwamba muko na uhodari?

7 Namna gani tunaweza kumuiga Yesu kwa kuonyesha uhodari? Kwenye masomo. Vijana wanaonyesha kwamba wako na uhodari wakati wanakuwa tayari kujitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova, hata kama wanafunzi wenzao ao watu wengine watawacheka. Kwa kufanya hivyo, wanaonyesha kwamba wanafurahia kuitwa kwa jina la Yehova. (Soma Zaburi 86:12.) Pengine unakazwa ili uamini fundisho la mageuzi. Lakini uko na sababu nzuri zenye zinakufanya uamini fundisho la Biblia kuhusu uumbaji. Unaweza kutumia broshua Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai ili kujibu kwa njia yenye kusadikisha wale wote wenye wanapenda kujua ‘sababu ya tumaini lililo ndani yako.’ (1 Pet. 3:15) Kwa kufanya hivyo, utafurahi kwa sababu unajua kwamba umetetea kweli ya Neno la Mungu.

8. Sababu gani tunahubiri kwa uhodari?

8 Katika mahubiri. Kwa sababu tuko Wakristo wa kweli, tunapaswa kuendelea ‘kusema kwa ujasiri [bila kuogopa] kwa mamlaka ya Yehova.’ (Mdo. 14:3) Sababu gani tunahubiri kwa ujasiri, ao kwa uhodari? Kwanza, tunajua kwamba mambo yenye tunahubiri ni ya kweli kwa sababu inatoka katika Biblia. (Yoh. 17:17) Pili, tunajua kwamba tuko “wafanyakazi wenzi wa Mungu” na kwamba roho takatifu inatusaidia. (1 Kor. 3:9; Mdo. 4:31) Tatu, wakati tunahubiri kwa bidii tunaonyesha kwamba tunashikamana na Yehova na kwamba tunapenda majirani wetu. (Mt. 22:37-39) Uhodari utatusaidia tusiache kuhubiri. Lakini, tumeazimia kuonyesha wazi uongo wa dini ambao unazuia watu wasijue kweli. (2 Kor. 4:4) Tutaendelea kuhubiri habari njema hata kama watu hawapendezwe, wanatuzarau, ao wanatupinga.​—1 Tes. 2:1, 2.

9. Wakati wa mateso, namna gani tunaweza kuonyesha uhodari?

9 Wakati wa mateso. Kumutegemea Mungu kunatusaidia tukuwe na imani na uhodari ili tuweze kupambana na mateso. Ikiwa mutu mwenye tunapenda anakufa, tutahuzunika, lakini hatutapoteza tumaini. Tutamutegemea “Mungu wa faraja yote” ili atupatie nguvu. (2 Kor. 1:3, 4; 1 Tes. 4:13) Ikiwa tunapambana na ugonjwa hatari ao tumeumia sana, tunaweza kusikia maumivu, lakini hatutavunja ushikamanifu wetu. Tunakataa matunzo yoyote yenye kupingana na kanuni za Biblia. (Mdo. 15:28, 29) Ikiwa tumevunjika moyo, “huenda mioyo yetu ikatuhukumu,” lakini kwa sababu tunamutegemea Mungu ambaye “yuko karibu na wale waliovunjika moyo,” tutaendelea kuvumilia. *​—1 Yoh. 3:19, 20; Zab. 34:18.

YESU ALIONYESHA UTAMBUZI

10. Utambuzi ni nini, na namna gani Mukristo mwenye utambuzi anasema na kutenda?

10 Mutu mwenye utambuzi anatumia akili yake vizuri, ni kusema, anajua kutofautisha mambo yaliyo sawa na yaliyo makosa, na kisha anachukua uamuzi wenye hekima. (Ebr. 5:14) Neno utambuzi linafasiriwa kuwa “uwezo wa kutumia akili vizuri katika mambo ya kiroho.” Mukristo mwenye utambuzi, anasema na kutenda kwa namna yenye kumupendeza Mungu. Anachagua maneno yenye inaweza kusaidia wengine kuliko kuwaumiza. (Met. 11:12, 13) Yeye “si mwepesi wa hasira.” (Met. 14:29) ‘Anaenda mbele moja kwa moja,’ na anashikamana na safari yake yenye kupeleka kwenye uzima wa milele. (Met. 15:21) Tunaweza kufanya nini ili tukuwe na utambuzi? Tunapaswa kujifunza Neno la Mungu na kutumikisha mambo yenye tunajifunza. (Met. 2:1-5, 10, 11) Jambo lenye linaweza kutusaidia zaidi, ni kuchunguza mufano wa Yesu, mutu mwenye alionyesha utambuzi kwa ukamilifu.

11. Katika maneno yake, namna gani Yesu alionyesha utambuzi?

11 Yesu alionyesha utambuzi katika mambo yote yenye alisema na kufanya. Katika maneno yake. Alitumia utambuzi wakati alikuwa anahubiri habari njema, na alichagua “maneno yenye kuvutia sana” yenye ilifanya watu wenye kumusikiliza washangae sana. (Lu. 4:22; Mt. 7:28) Mara nyingi aliacha Neno la Mungu liseme; alisoma maandiko, aliyataja, ao alichagua maandiko vizuri ili kukazia jambo lenye alikuwa anazungumuzia. (Mt. 4:4, 7, 10; 12:1-5; Lu. 4:16-21) Tena, Yesu alifasiria Maandiko kwa njia yenye kugusa mioyo ya watu wenye walimusikiliza. Kisha kufufuliwa kwake, Yesu alizungumuza na wanafunzi wake wawili ambao walikuwa wanaenda Emau. Wakati huo, ‘aliwafasiria mambo yanayomuhusu yeye mwenyewe katika Maandiko yote.’ Kisha hapo, wanafunzi hao walisema hivi: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka . . . alipokuwa akitufungulia Maandiko?”—Lu. 24:27, 32.

12, 13. Ni mifano gani inaonyesha kwamba Yesu hakuwa mwepesi wa hasira na kwamba aliwaelewa wengine?

12 Alijizuia na aliwaelewa wengine. Utambuzi ulimusaidia Yesu akuwe mwenye kujizuia, na ulimufanya asikuwe “mwepesi wa hasira.” (Met. 16:32) Alikuwa “mwenye tabia-pole.” (Mt. 11:29) Kila mara, alivumilia uzaifu wa wanafunzi wake. (Mk. 14:34-38; Lu. 22:24-27) Aliendelea kuwa mupole hata wakati alitendewa bila haki.​—1 Pet. 2:23.

13 Utambuzi ulimusaidia pia Yesu awaelewe watu wengine. Yesu alielewa mambo ya lazima yenye ilikuwa katika Sheria ya Musa; alielewa sababu gani Sheria ilitolewa na alitenda kulingana na hilo. Kwa mufano, tuchunguze habari yenye kupatikana katika andiko la Marko 5:25-34. (Soma.) Mwanamuke mwenye alikuwa na ugonjwa wa kutokwa damu alipita katikati ya watu wengi ili kuenda kugusa vazi la Yesu, kisha akapona. Kulingana na Sheria, mwanamuke huyo hakuwa safi; kwa hiyo, hakupaswa kugusa mutu yeyote. (Law. 15:25-27) Lakini kwa sababu Yesu alijua kwamba “rehema na uaminifu” vilikuwa kati ya “mambo mazito zaidi ya Sheria,” hakumutombokea kwa sababu aligusa vazi lake. (Mt. 23:23) Lakini, alimuambia hivi kwa upole: ‘Binti yangu, imani yako imekuponya. Enda kwa amani, na ukuwe na afya njema kutokana na ugonjwa wako wenye kuhuzunisha.’ Inagusa moyo sana kuona namna utambuzi ulimuchochea Yesu awatendee wengine kwa wema!

14. Yesu alichagua kufanya nini, na ni nini ilimusaidia aendelee kufanya kazi ya kuhubiri?

14 Namna alitumia maisha yake. Yesu alionyesha utambuzi kwa kuchagua njia nzuri ya kutumia maisha yake, na akashikamana na njia hiyo. Alifanya kwa bidii kazi ya kuhubiri habari njema, na alifanya kazi hiyo ikuwe ya kwanza katika maisha yake. (Lu. 4:43) Pia, Yesu alifanya maamuzi yenye ilimusaidia aendelee kufanya kazi ya kuhubiri na amalize mugao wake vizuri. Alichagua kuishi maisha mepesi ili aweze kutumia wakati wake na nguvu zake ili kufanya kazi ya kuhubiri. (Lu. 9:58) Alitambua kwamba ni lazima awazoeze wengine wenye watafanya kazi hiyo kisha yeye kufa. (Lu. 10:1-12; Yoh. 14:12) Aliwaambia wanafunzi wake kwamba atawasaidia katika kazi hiyo ‘mupaka umalizio wa mufumo wa mambo.’​—Mt. 28:19, 20.

TUMUIGE YESU KWA KUONYESHA UTAMBUZI

Ujikaze kuelewa ni mambo gani inaweza kuwapendeza watu, na uchague maneno yenye kupatana na hali yao(Ona fungu la 15)

15. Katika maneno yetu, namna gani tunaweza kuonyesha utambuzi?

15 Tuone tena namna tunaweza kumuiga Yesu. Katika maneno yetu. Wakati tunazungumuza na Wakristo wenzetu, tunapaswa kutumia maneno yenye kujenga kuliko kutumia maneno ya kubomoa. (Efe. 4:29) Wakati tunahubiria wengine juu ya Ufalme wa Mungu, tunapaswa kukoleza maneno yetu na “chumvi.” (Kol. 4:6) Tujikaze kuelewa ni mambo gani inahangaisha watu ao mambo yenye inaweza kuwapendeza, na kisha tuchague maneno yenye kupatana na hali yao. Ikiwa tunatumia maneno mazuri, watu watapenda kutusikiliza, na ujumbe wetu utagusa mioyo yao. Zaidi ya hilo, tunajikaza kutumia Biblia ili kuelezea watu mambo yenye tunaamini. Ikiwa tunataja maandiko ao kuyasoma wakati hali inaruhusu, tunaonyesha kwamba mambo yenye tunaamini inatoka katika Biblia. Tunajua kwamba ujumbe wa Biblia ni wenye nguvu zaidi kuliko neno lolote lenye tunaweza kusema.​—Ebr. 4:12.

16, 17. (a) Namna gani tunaweza kuonyesha kwamba hatuko wepesi wa hasira na kwamba tunawaelewa wengine? (b) Ni nini itatusaidia tuendelee kufanya kazi ya kuhubiri?

16 Tukuwe wenye kujizuia na kuwaelewa wengine. Utambuzi unatusaidia tukuwe wenye kujizuia, na unatufanya tusikuwe ‘wepesi wa gazabu [hasira].’ (Yak. 1:19) Wakati watu wanatukosea, tujikaze kutambua sababu gani wamesema ao wamefanya jambo fulani. Kufanya hivyo kunaweza kutusaidia tusikuwe na hasira, na kunaweza kutusaidia ‘tusamehe kosa.’ (Met. 19:11, La Sainte Bible en swahili de la R.D. Congo.) Pia, utambuzi unatusaidia tuwaelewe wengine. Kwa hiyo, tujikaze kuelewa ndugu na dada zetu wakati hawafikie kufanya mambo yenye tulipenda wafanye, na tukumbuke kwamba pengine wanapambana na magumu yenye tunashindwa kabisa kuelewa. Tukuwe tayari kusikiliza mawazo yao, na wakati inawezekana tukubali maoni yao.​—Flp. 4:5.

17 Namna ya kutumia maisha yetu. Sisi wanafunzi wa Yesu, tunatambua kwamba ni pendeleo kubwa sana kufanya kazi ya kuhubiri habari njema. Kwa hiyo, tunapaswa kufanya maamuzi yenye itatusaidia tuendelee kufanya kazi hiyo kwa bidii. Tuchague kutia mambo ya kiroho pa nafasi ya kwanza na tuendelee kuishi maisha mepesi ili tuweze kujitoa kabisa katika kazi ya kuhubiri ambayo ni ya maana sana, na tufanye hivyo mbele mwisho ukuje.​—Mt. 6:33; 24:14.

18. Tunaweza kufanya nini ili tuendelee na safari yetu yenye kupeleka kwenye uzima wa milele, na umeazimia kufanya nini?

18 Bila shaka tumefurahi sana kwa kuchunguza sifa fulani za Yesu zenye kuvutia. Wazia faida yenye unaweza kupata ikiwa unajifunza sifa zingine za Yesu, na ikiwa unajifunza namna unaweza kumuiga. Kwa hiyo, tuazimie kufuata hatua zake kwa uaminifu. Ikiwa tunafanya hivyo, tutaendelea na safari yetu yenye kupeleka kwenye uzima wa milele na tutamukaribia Yehova, Yule mwenye Yesu aliiga kwa ukamilifu.

^ fu. 2 Andiko la 1 Petro 1:8, 9 liliandikwa kwa ajili ya Wakristo wenye kuwa na tumaini la kuenda mbinguni. Hata hivyo, kanuni ya andiko hilo inahusu pia wale wenye kuwa na tumaini la kuishi hapa duniani.

^ fu. 9 Ili kupata mifano ya watu wenye walionyesha uhodari wakati wa mateso, ona Munara wa Mulinzi, wa tarehe 1 Mwezi wa 12, 2000, ukurasa wa 24-28; Amuka! ya tarehe 22 Mwezi wa 4, 2003, ukurasa wa 18-21; na ya tarehe 22 Mwezi wa 1, 1995, ukurasa 11-15.