Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutayarisha Mataifa kwa Ajili ya “Fundisho la Yehova”

Kutayarisha Mataifa kwa Ajili ya “Fundisho la Yehova”

“Yule liwali . . . akawa mwamini, kwa kuwa alistaajabishwa na fundisho la Yehova.” —MDO. 13:12.

1-3. Kwa nini haikuwa rahisi kwa wanafunzi wa Yesu kuhubiri habari njema katika “mataifa yote”?

YESU KRISTO aliwapa wafuasi wake kazi kubwa sana ya kufanya. Aliwaamuru hivi: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” Wanafunzi hao wangefanya kazi hiyo, na mwishowe ‘habari njema ya ufalme ingehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.’—Mt. 24:14; 28:19.

2 Wanafunzi walimpenda Yesu na habari njema. Hata hivyo, huenda walijiuliza, ‘Tutatimizaje kazi hii?’ Kwanza, walikuwa wachache. Kisha Yesu, ambaye walimtangaza kuwa Mwana wa Mungu, alikuwa ameuawa. Isitoshe, wanafunzi wake walionwa kuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu.” (Mdo. 4:13) Lakini walipaswa kutangaza ujumbe ambao ulipinga mafundisho ya viongozi maarufu wa kidini waliofundishwa desturi zilizokuwepo kwa miaka mingi sana. Wanafunzi wa Yesu hawakuheshimiwa katika nchi yao ya Israeli. Na taifa la Israeli halingeweza kamwe kulinganishwa na Milki ya Roma yenye nguvu.

3 Isitoshe, Yesu alikuwa amewaonya wanafunzi wake kwamba wangechukiwa na kuteswa na baadhi yao wangeuawa. (Luka 21:16, 17) Wangekabili wasaliti, manabii wa uwongo, na kuongezeka kwa uasi-sheria. (Mt. 24:10-12) Hata kama ujumbe wao ungepokewa vizuri kila mahali, wangewezaje kuhubiri “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia”? (Mdo. 1:8) Bila shaka, matatizo hayo yalionekana kuwa makubwa sana!

4. Wanafunzi wa karne ya kwanza walifanikiwa kadiri gani katika kazi yao ya kuhubiri?

4 Licha ya mahangaiko waliyokuwa nayo, wanafunzi hao walihubiri habari njema kwa bidii Yerusalemu na Samaria, na pia katika ulimwengu mzima wa wakati huo. Ijapokuwa walikabili matatizo, katika kipindi cha miaka 30, habari njema “ilihubiriwa katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu” na ilikuwa ‘ikizaa matunda na kuongezeka katika ulimwengu wote.’ (Kol. 1:6, 23) Kwa mfano: Kwa sababu ya mambo ambayo mtume Paulo alisema na kufanya kwenye kisiwa cha Kipro, liwali Mroma Sergio Paulo “akawa mwamini, kwa kuwa alistaajabishwa na fundisho la Yehova.”—Soma Matendo 13:6-12.

5. (a) Yesu aliwahakikishia nini wanafunzi wake? (b) Watu fulani wamefikia mkataa gani kuhusu hali katika karne ya kwanza?

5 Wanafunzi wa Yesu walijua kwamba hawangeweza kutimiza kazi ya kuhubiri kwa uwezo wao wenyewe. Yesu alisema kwamba angekuwa pamoja nao na kwamba roho takatifu ingewasaidia. (Mt. 28:20) Huenda hali fulani zilizokuwepo wakati huo ziliwawezesha wanafunzi kuhubiri kuhusu Ufalme. Kitabu kimoja (Evangelism in the Early Church) kinasema hivi: “Huenda hakuna kipindi kingine katika historia ya ulimwengu ambacho kilifaa zaidi kuanzishwa kwa Kanisa changa la Kikristo kuliko karne ya kwanza AD . . . Kufikia karne ya pili, Wakristo . . . walianza kusema kwamba Mungu ndiye aliyeutayarisha ulimwengu kwa ajili ya kuanzishwa kwa Ukristo.”

6. Tutachunguza nini (a) katika makala hii? (b) katika makala inayofuata?

6 Biblia haisemi ni kwa kadiri gani Mungu aliongoza matukio ya ulimwengu katika karne ya kwanza ili Wakristo waweze kuhubiri katika eneo kubwa. Lakini tuna hakika kuhusu jambo hili: Yehova alitaka habari njema ihubiriwe, lakini Shetani hakutaka. Katika makala hii, tutachunguza mambo fulani ambayo huenda yalifanya kazi ya kuhubiri iwe rahisi zaidi katika karne ya kwanza kuliko wakati mwingine wowote katika historia. Katika makala inayofuata, tutachunguza matukio fulani katika nyakati zetu ambayo yametusaidia kutangaza habari njema duniani pote.

JINSI AMBAVYO HUENDA AMANI YA ROMA ILISAIDIA

7. Pax Romana ilikuwa nini, na kwa nini ilikuwa ya pekee?

7 Kwa njia fulani, Milki ya Roma iliwanufaisha Wakristo katika karne ya kwanza. Kwa mfano, kulikuwa na Pax Romana au Amani ya Roma. Milki kubwa ya Roma ilidumisha amani miongoni mwa raia wake. Nyakati nyingine, kulikuwa na “vita na habari za vita,” kama Yesu alivyotabiri. (Mt. 24:6) Majeshi ya Roma yaliharibu Yerusalemu katika mwaka wa 70 W.K., na kulikuwa na vita vidogo-vidogo kwenye mipaka ya milki hiyo. Hata hivyo, kwa miaka 200 hivi tangu siku za Yesu, eneo lote la Mediterania lilikuwa na amani kwa kadiri fulani. Kitabu kimoja cha marejeo kinasema hivi: “Hakuna kipindi kingine katika historia ya wanadamu kilichokuwa na amani kwa muda mrefu hivyo, na amani hiyo ilidumu miongoni mwa watu wengi sana.”

8. Amani iliyokuwepo katika Milki ya Roma iliwanufaishaje Wakristo wa mapema?

8 Akieleza maoni yake, Origen, mwanatheolojia wa karne ya tatu aliandika hivi: “Mafundisho ya Yesu hayangeenea kotekote ulimwenguni ikiwa kungekuwa na falme nyingi . . . kwa sababu kila mahali wanaume wangelazimishwa kujiunga na jeshi na kupigana ili kulinda nchi yao. . . . Kwa hiyo, fundisho hilo linalohubiri amani na ambalo hata haliwaruhusu watu kulipiza kisasi dhidi ya adui zao, lingefanikiwaje ikiwa hali ya ulimwengu haingebadilika na ikiwa hakungekuwa na amani wakati Yesu alipoanza huduma yake?” Watangazaji wa Ufalme waliteswa katika Milki ya Roma, lakini walikuwa wafanya-amani na ni wazi kwamba amani ya kadiri iliyokuwapo wakati huo iliwanufaisha.—Soma Waroma 12:18-21.

JINSI MFUMO MZURI WA USAFIRI ULIVYOWASAIDIA WAKRISTO

9, 10. Kwa nini ilikuwa rahisi zaidi kwa wanafunzi kusafiri katika Milki ya Roma?

9 Wakristo walitumia vizuri barabara nzuri za Roma kusafiri kotekote. Roma ilikuwa na jeshi lenye nguvu na bidii ili kuwalinda na kuwadhibiti raia wake. Barabara nzuri zilihitajika ili kuwasafirisha haraka askari-jeshi, na Waroma walikuwa wajenzi stadi wa barabara. Mainjinia Waroma walijenga barabara zilizofikia umbali wa kilomita zaidi ya 80,000 na ziliunganisha karibu wilaya zote. Barabara hizo zilipita misituni, jangwani, na hata milimani.

10 Mbali na barabara, Waroma wangeweza kusafiri umbali wa kilomita 27,000 hivi kupitia mito na mifereji. Meli za Waroma zilisafiri kupitia njia 900 hivi za baharini zilizounganisha mamia ya bandari. Kwa hiyo, Wakristo wangeweza kusafiri kotekote katika Milki ya Roma. Matatizo yalikuwepo, lakini mtume Paulo na wengine waliweza kusafiri katika Milki yote ya Roma bila pasipoti wala viza. Hakukuwa na ofisi za uhamiaji au za forodha. Wahalifu waliogopa kuadhibiwa na serikali ya Roma, kwa hiyo barabara zilikuwa na usalama wa kadiri fulani. Usafiri wa baharini ulikuwa salama pia kwa sababu majeshi ya wanamaji ya Roma yalihakikisha kwamba hakuna maharamia. Ingawa Paulo alivunjikiwa na meli mara kadhaa na kukabili hatari baharini, Maandiko hayasemi kihususa kwamba alivamiwa na maharamia katika safari zake.—2 Kor. 11:25, 26.

JINSI LUGHA ILIVYOSAIDIA

Ilikuwa rahisi zaidi kupata andiko katika kodeksi (Tazama fungu la 12)

11. Kwa nini wanafunzi wa Kristo walitumia Kigiriki?

11 Kigiriki cha kawaida, yaani, Koine, kilisaidia makutaniko ya Kikristo kuwa na mawasiliano mazuri na umoja. Baada ya Aleksanda Mkuu kuteka maeneo mengi, watu wengi sana walielewa na kuzungumza Kigiriki. Kwa hiyo, watumishi wa Mungu wangeweza kuwasiliana na watu wa kila aina, na hilo lilisaidia kueneza habari njema. Isitoshe, Wayahudi walioishi nchini Misri walikuwa wametafsiri Maandiko ya Kiebrania katika Kigiriki. Watu waliijua tafsiri hiyo ya Septuajinti, na wafuasi wa mapema wa Kristo waliinukuu mara nyingi. Pia, Wakristo walitumia Kigiriki katika maandishi yao. Lugha hiyo ina msamiati au maneno mengi na iliwasaidia sana kufafanua mambo ya kiroho.

12. (a) Kodeksi ni nini, na ilikuwa na manufaa gani ikilinganishwa na kitabu cha kukunjwa? (b) Kodeksi ilianza kutumiwa sana na Wakristo wakati gani?

12 Wakristo walitumiaje Maandiko katika huduma yao? Vitabu vya kukunjwa vilikuwa vikubwa na haikuwa rahisi kuvitumia kwa sababu vilihitaji kukunjwa na kukunjuliwa, na kwa kawaida vilikuwa na maandishi upande mmoja tu. Injili ya Mathayo peke yake ingejaza kitabu kizima cha kukunjwa. Lakini baadaye kitabu cha kwanza kabisa kilibuniwa, kiliitwa kodeksi. Kurasa zake ziliunganishwa pamoja. Msomaji angeweza kufungua kodeksi na kupata andiko kwa urahisi. Ingawa haijulikani kwa uhakika ni lini Wakristo walipoanza kutumia kodeksi, kitabu kimoja cha marejeo kinasema hivi: “Wakristo walitumia sana kodeksi ulimwenguni pote katika karne ya pili, hivyo inaonekana kwamba ilibuniwa kabla ya mwaka wa 100 A.D.”

JINSI SHERIA YA ROMA ILIVYOSAIDIA

13, 14. (a) Paulo alitumiaje uraia wake wa Roma? (b) Sheria ya Roma iliwanufaishaje Wakristo?

13 Sheria ya Roma ilifuatwa katika milki yote, na uraia wa Roma uliwapa watu ulinzi na haki fulani. Paulo alitumia uraia wake wa Roma pindi kadhaa. Ofisa Mroma alipoagiza mtume Paulo apigwe mijeledi Yerusalemu, mtume huyo alimuuliza hivi: “Je, ni halali kwa ninyi watu kumpiga mijeledi mtu ambaye ni Mroma na ambaye hajahukumiwa kuwa mwenye hatia?” Haikuwa halali. Paulo aliposema kwamba alizaliwa akiwa raia Mroma, “watu waliokuwa karibu kumhoji kwa kumtesa wakaondoka kwake; na kiongozi wa kijeshi akaogopa alipohakikisha kwamba [Paulo] alikuwa Mroma na kwamba alikuwa amemfunga.”—Mdo. 22:25-29.

14 Maofisa hao walipogundua kwamba Paulo alikuwa raia wa Roma walimtendea kwa njia tofauti. (Mdo. 16:35-40) Katika jiji la Efeso, karani wa jiji alirejelea sheria ya Roma baada ya kuutuliza umati wenye hasira. (Mdo. 19:35-41) Paulo alipokata rufani akiwa Kaisaria, alipata nafasi ya kutetea imani yake mbele ya Kaisari. (Mdo. 25:8-12) Kwa hiyo, sheria ya Roma iliwawezesha Wakristo “kutetea na kuithibitisha kisheria habari njema.”—Flp. 1:7.

MATOKEO YA KUTAWANYIKA KWA WAYAHUDI

15. Vikundi vya Wayahudi vilienea kwa kadiri gani katika karne ya kwanza?

15 Huenda kutawanyika kwa Wayahudi kotekote katika Milki ya Roma kulirahisisha kazi ya Wakristo ya kueneza injili. Karne nyingi mapema, Waashuru na baadaye Wababiloni walikuwa wamewapeleka Wayahudi uhamishoni. Mapema kabisa katika karne ya tano K.W.K., kulikuwa na vikundi vya Wayahudi katika wilaya 127 za Milki ya Uajemi. (Esta 9:30) Yesu alipokuwa duniani, kulikuwa na vikundi vya Wayahudi nchini Misri na sehemu nyingine za Afrika Kaskazini, na pia Ugiriki, Asia Ndogo, na Mesopotamia. Milki ya Roma ilikuwa na watu 60,000,000 na inakadiriwa kwamba mtu 1 kati ya watu 14 alikuwa Myahudi. Wayahudi walieneza dini yao popote walipoenda.—Mt. 23:15.

16, 17. (a) Kutawanyika kwa Wayahudi kuliwanufaishaje watu wengi wasio Wayahudi? (b) Wanafunzi walifuata utaratibu gani wa Wayahudi?

16 Kwa kuwa Wayahudi walikuwa wametawanyika kotekote, watu wengi wasio Wayahudi walifahamu Maandiko ya Kiebrania. Walijifunza kwamba kuna Mungu mmoja tu wa kweli na kwamba wale wanaomtumikia wanapaswa kufuata viwango vya juu vya mwenendo na maadili. Isitoshe, Maandiko ya Kiebrania yalikuwa na unabii mwingi kumhusu Masihi. (Luka 24:44) Wayahudi na Wakristo walielewa kwamba Maandiko ya Kiebrania yalikuwa Neno la Mungu lililoongozwa na roho takatifu, na hivyo Paulo alitumia jambo hilo kuwa msingi wa mazungumzo yake na watu waliokuwa na mwelekeo wa kupenda uadilifu. Kwa hiyo, mtume Paulo alikuwa na desturi ya kuingia katika masinagogi ya Wayahudi na kujadiliana nao kwa kutumia Maandiko.—Soma Matendo 17:1, 2.

17 Wayahudi walifuata utaratibu hususa wa ibada. Walikutana kwa ukawaida katika masinagogi au hadharani. Waliimba nyimbo, walisali, na kuzungumzia Maandiko. Makutaniko ya Kikristo leo yanafuata utaratibu huohuo.

YANAWEZEKANA KWA MSAADA WA YEHOVA

18, 19. (a) Hali zilizokuwepo katika karne ya kwanza zilifanya jambo gani liwezekane? (b) Makala hii inakufanya uhisije kumhusu Yehova?

18 Kwa hiyo, hali fulani za pekee zilichangia kufanikiwa kwa kazi ya kuhubiri habari njema. Mambo kama vile Pax Romana, mfumo mzuri wa usafiri, lugha iliyozungumzwa ulimwenguni pote, sheria ya Roma, na kutawanyika kwa Wayahudi yaliwasaidia wanafunzi wa Yesu kutimiza kazi ya kuhubiri waliyokabidhiwa na Mungu.

19 Miaka 400 hivi mapema, Plato, mwanafalsafa Mgiriki alisema hivi katika kitabu chake kimoja: “Ni vigumu kumpata mfanyi na baba ya ulimwengu huu wetu, na hata ikiwa tungempata, haingewezekana kumwambia kila mtu kumhusu.” Hata hivyo, Yesu alisema hivi: “Mambo yasiyowezekana kwa wanadamu yanawezekana kwa Mungu.” (Luka 18:27) Muumba wa ulimwengu anataka watu wampate na kumjua. Isitoshe, Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake: ‘Mfanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mt. 28:19) Kwa msaada wa Yehova Mungu, kazi hiyo inaweza kutimizwa. Makala ifuatayo itaonyesha jinsi kazi hiyo inavyofanywa katika siku zetu.