Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Namna “Fundisho la Yehova” Lilifikia Mataifa

Namna “Fundisho la Yehova” Lilifikia Mataifa

“Yule liwali . . . akawa mwamini, kwa kuwa alistaajabishwa na fundisho la Yehova.”​MDO. 13:12.

1-3. Sababu gani haikuwa mwepesi kwa wanafunzi wa Yesu kufanya kazi yao ya kuhubiri habari njema katika “mataifa yote”?

YESU KRISTO alipatia wafuasi wake kazi kubwa. Aliwaambia hivi: ‘Nendeni mukafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ Kupitia kazi hiyo, mwishowe “habari njema ya ufalme [ingehubiriwa] katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.”​—Mt. 24:14; 28:19.

2 Wanafunzi walimupenda Yesu na walipenda habari njema. Pengine walijiuliza namna gani watatimiza kazi yao. Tena, walikuwa wachache sana. Walikuwa wanatangaza kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu, lakini Yesu alikuwa ameuawa. Wanafunzi wake walionwa kuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu.” (Mdo. 4:13) Lakini walipaswa kutangaza ujumbe wenye kupinga mafundisho ya viongozi wa dini, hata kama viongozi hao waliheshimiwa sana, na walikuwa wamejifunza desturi za tangu zamani. Wanafunzi wa Yesu hawakuheshimiwa katika inchi yao. Tena, taifa lao la Israeli lilionekana kuwa bure, kwa kulilinganisha na utawala wote wa Roma wenye mamlaka.

3 Pia, Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba watachukiwa na kuteswa, na kwamba wamoja kati yao watauawa. (Lu. 21:16, 17) Tena, aliwaambia kwamba watu fulani watawatoa kwa maadui wao, kutakuwa manabii wa uongo, na kwamba uasi-sheria utaongezeka. (Mt. 24:10-12) Hata kama watu wangekubali ujumbe wao kila mahali, namna gani wangehubiri ujumbe huo ‘mupaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia’? (Mdo. 1:8) Bila shaka, mambo hayo yote yalionekana kuwa yenye kuogopesha sana!

4. Wanafunzi wa kwanza-kwanza walipata matokeo gani mazuri katika kazi yao ya kuhubiri?

4 Hata kama wanafunzi wa Yesu walijua kwamba kazi yao haitakuwa mwepesi, walihubiri habari njema kwa bidii. Walihubiri katika Yerusalemu na Samaria, lakini pia katika ulimwengu wote wenye ulijulikana wakati huo. Walipata magumu, lakini kisha miaka 30 hivi, habari njema ilikuwa ‘inahubiriwa katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu’ na ilikuwa ‘inazaa matunda na kuongezeka katika ulimwengu wote.’ (Kol. 1:6, 23) Kwa mufano, mambo yenye mutume Paulo alisema na kufanya kwenye kisiwa cha Kipro, ilifanya liwali mumoja mwenye kuitwa Sergio Paulo ‘akuwe mwamini, kwa kuwa alistaajabishwa [alishangazwa sana] na fundisho la Yehova.’​—Soma Matendo 13:6-12.

5. (a) Yesu aliambia wanafunzi wake nini? (b) Kitabu kimoja cha historia kilisema nini kuhusu wakati wa mitume?

5 Wanafunzi wa Yesu walijua kwamba hawataweza kutimiza kazi ya kuhubiri kwa nguvu zao wenyewe. Yesu aliwaambia kwamba atakuwa pamoja nao na kwamba roho takatifu itawasaidia. (Mt. 28:20) Katika njia fulani, hali zenye zilikuwa katika ulimwengu wa wakati ule zilisaidia wanafunzi ili waweze kuhubiri Ufalme. Kitabu kimoja cha historia kinasema hivi: “Wakati wa mitume ulikuwa wakati muzuri kuliko wakati mwengine wowote, ambao watu wangeweza kupokea Kanisa lenye lilikuwa tu linaanza . . . Katika miaka ya 101 mupaka 200, Wakristo . . . walianza kusema kwamba ni Mungu ndiye alitayarisha ulimwengu kwa ajili ya Ukristo.”

6. Tutachunguza nini (a) katika habari hii? (b) katika habari yenye kufuata?

6 Biblia haiseme ni kwa kadiri gani Mungu aliongoza mambo katika ulimwengu wakati wa mitume, ili kazi ya kuhubiri ifanyike kwa kiasi kikubwa. Lakini tuko hakika juu ya jambo hili: Yehova alipenda habari njema ihubiriwe, lakini Shetani hakupenda. Katika habari hii, tutachunguza mambo fulani yenye, pengine ilifanya kazi ya kuhubiri wakati wa mitume ikuwe mwepesi zaidi. Katika habari yenye kufuata, tutachunguza maendeleo yenye imefanyika leo katika ulimwengu, ambayo inatusaidia kutangaza habari njema mupaka sehemu ya mwisho ya dunia.

AMANI YA ROMA

7. Amani ya Roma ilikuwa nini, na sababu gani kipindi hicho kilikuwa tofauti na nyakati zingine?

7 Kwa njia fulani, hali zenye zilikuwa katika ulimwengu wenye ulitawaliwa na Roma wakati wa mitume, zilisaidia sana Wakristo. Kwa mufano, kulikuwa kipindi chenye kuitwa Amani ya Roma, ao Pax Romana katika Kilatini. Wakati huo, serikali ya Roma ilitia amani katika maeneo yote yenye ilikuwa chini ya utawala wake. Wakati fulani, kulikuwa “vita na habari za vita,” kama vile Yesu alikuwa amesema. (Mt. 24:6) Jeshi la Roma liliharibu muji wa Yerusalemu katika mwaka wa 70, na kulikuwa vita vidogo-vidogo kwenye mipaka ya Utawala wa Roma. Hata hivyo, kwa miaka 200 hivi kuanzia wakati Yesu alikuwa hapa duniani, kulikuwa amani ya kadiri katika eneo la Mediterania. Kitabu kimoja kinasema kwamba, wakati huo wanadamu wengi walikuwa na amani na usalama kwa muda murefu kuliko nyakati zingine.

8. Namna gani Wakristo wa kwanza-kwanza walifaidika na Amani ya Roma?

8 Miaka 300 hivi kisha Kristo, mwanateolojia mumoja mwenye kuitwa Origène aliandika hivi kuhusu kipindi hicho cha amani: “Ikiwa kungekuwa falme nyingi wakati ule, ingekuwa vigumu mafundisho ya Yesu ienee katika ulimwengu wote . . . kwa sababu kila mahali wanaume wangelazimishwa kufanya kazi ya askari ili kupigania inchi yao. . . . Kwa kweli, namna gani mafundisho ya Yesu yenye kufundisha amani na yenye kukataza watu kujilipizia kisasi juu ya adui zao ingekuwa na matokeo, ikiwa kila mahali watu hawangeishi kwa amani, na ikiwa watu wangekosa roho ya utulivu?” Wahubiri wa Ufalme waliteswa katika maeneo yenye ilitawaliwa na Roma, lakini walipenda amani na inaonekana walitumia vizuri kipindi hicho cha amani ya kadiri ili waweze kuhubiri.​—Soma Waroma 12:18-21.

ILIKUWA MWEPESI KUSAFIRI

9, 10. Sababu gani haikuwa vigumu kwa wanafunzi wa Yesu kusafiri katika maeneo yenye ilitawaliwa na Roma?

9 Wakristo walitumia vizuri barabara zenye zilitengenezwa na Roma. Ili kulinda na kuongoza raia wake vizuri, serikali ya Roma ilikuwa na jeshi lenye nguvu. Iliomba barabara nzuri ili kufanya maaskari waende haraka, na Waroma walijua vizuri kutengeneza barabara hizo. Mafundi wa Roma walijenga barabara zenye ziliunganisha karibu majimbo yote, na barabara zote pamoja zilikuwa na urefu wa kilometre zaidi ya 80 000. Barabara fulani zilipita katika pori, katika jangwa, na kwenye milima.

10 Waroma walitumia pia kilometre 27 000 ili kusafiri juu ya maji. Mashua (bateaux) za Roma zilitumia njia 900 hivi ili kusafiri juu ya bahari; njia hizo ziliunganisha mamia ya bandari (ports). Kwa hiyo, Wakristo wangeweza kusafiri bila magumu katika maeneo yote yenye ilitawaliwa na Roma. Kulikuwa magumu fulani, lakini mutume Paulo na Wakristo wengine wangeweza kusafiri katika maeneo yote yenye ilitawaliwa na Roma, bila kuwa na lazima ya vitambulisho kama vile pasipoti (passeport) ao viza. Hakuna watu wenye waliwekwa ili kuchunguza mizigo ao kuchunguza watu wenye walitoka katika maeneo mengine. Katika barabara zote kulikuwa usalama wa kadiri, kwa sababu wavunja-sheria waliogopa kuazibiwa na Roma. Watu walisafiri pia kwa usalama juu ya bahari, kwa sababu mashua za maaskari wa Roma zilikuwa juu ya maji ili kulinda watu wasishambuliwe na wanyanganyi. Mara nyingi mutume Paulo alivunjikiwa na mashua kwenye bahari, na kulikuwa hatari zingine za kusafiri juu ya maji. Lakini Biblia haiseme kwamba alishambuliwa na wanyanganyi wakati alisafiri kwa mashua.​—2 Kor. 11:25, 26.

LUGA YA KIGIRIKI

Ilikuwa mwepesi zaidi kupata andiko katika kodeksi

(Ona fungu la 12)

11. Sababu gani wanafunzi wa Yesu walitumia luga ya Kigiriki?

11 Kigiriki cha kawaida ao Koine, ni luga yenye ilisaidia Wakristo waelewane vizuri na wakuwe na umoja katika makutaniko ya Kikristo. Mutawala Mugiriki mwenye kuitwa Alexandre Mukubwa, alipata ushindi juu ya maeneo mengi. Hilo lilifanya watu wa maeneo hayo wajue kusema na kuelewa luga ya Kigiriki. Kwa hiyo, watumishi wa Mungu waliweza kuzungumuza na watu wa kila namna, na hilo lilisaidia ili habari njema ienee katika maeneo mengi. Zaidi ya hilo, Wayahudi wenye walikuwa wanaishi Misri walikuwa wametafsiri Maandiko ya Kiebrania katika luga ya Kigiriki. Watu walijua vizuri tafsiri hiyo yenye kuitwa Septante, na Wakristo wa kwanza-kwanza walikuwa wanataja maandiko ya tafsiri hiyo bila magumu. Pia, Wakristo walifurahia kutumia luga ya Kigiriki katika maandishi yao. Luga hiyo ilikuwa na maneno mengi sana, na ilisaidia Wakristo kupata maneno yenye kufaa ili kufasiria mafundisho ya maana sana ya Biblia.

12. (a) Kodeksi ni nini, na sababu gani ilikuwa nzuri kuliko kitabu cha kukunjwa? (b) Ni wakati gani Wakristo wengi walianza kutumia kodeksi?

12 Namna gani Wakristo waliweza kutumia Maandiko katika mahubiri? Haikuwa mwepesi kutumia kitabu cha kukunjwa. Iliomba kukikunja na kukikunjua, na mara nyingi maandishi yalipatikana tu kwenye upande mumoja. Kwa mufano, Injili ya Mathayo yenyewe ingeweza kuenea katika kitabu kimoja cha kukunjwa. Kisha watu wakaanza kutumia kodeksi. Kodeksi ilikuwa aina ya kwanza kabisa ya vitabu kama vya leo. Ilitengenezwa kwa kuunganisha makaratasi pamoja. Musomaji angeweza kufungua kodeksi na kupata andiko bila magumu. Hatujue ni wakati gani Wakristo walianza kutumia kodeksi, lakini kitabu kimoja kinasema hivi: “Kati ya mwaka wa 101 na 200, Wakristo wengi walikuwa wanatumia kodeksi; hilo linaonyesha kwamba ilianza kutumiwa mbele ya kipindi hicho.”

SHERIA YA ROMA

13, 14. (a) Mutume Paulo alipata ulinzi gani kwa sababu alikuwa raia wa Roma? (b) Namna gani Wakristo walifaidika na sheria ya Roma?

13 Sheria ya Roma ilikuwa inatumika katika maeneo yote yenye kutawaliwa na Roma, na ilipatia raia wa Roma haki za maana sana na ulinzi. Kwa mufano, mutume Paulo alikuwa raia wa Roma, na mara nyingi sheria ilimutolea ulinzi. Katika muji wa Yerusalemu, maaskari wa Roma walitaka kumupiga mijeledi, lakini Paulo akamuuliza hivi kiongozi mumoja wa jeshi: ‘Je, ni halali kwa ninyi watu kumupiga mijeledi mutu ambaye ni Muroma na ambaye hajahukumiwa kuwa mwenye hatia?’ Sheria ilikataza kufanya hivyo. Wakati mutume Paulo alisema kwamba yeye ni raia wa Roma tangu kuzaliwa, ‘watu waliokuwa karibu kumuhoji (kumuuliza) kwa kumutesa wakaondoka kwake; na kiongozi wa kijeshi akaogopa alipohakikisha kwamba [Paulo] alikuwa Muroma na kwamba alikuwa amemufunga.’​—Mdo. 22:25-29.

14 Katika muji wa Filipi, mutume Paulo alitendewa kulingana na haki zenye uraia wa Roma ulimutolea. (Mdo. 16:35-40) Katika Efeso, kiongozi wa muji alinyamazisha kikundi cha watu wenye hasira, kisha akawakumbusha mambo yenye sheria ya Roma inasema. (Mdo. 19:35-41) Wakati mutume Paulo alikuwa katika muji wa Kaisaria, alikata rufani na hilo likamupatia nafasi ya kutetea imani yake mbele ya Kaisari. (Mdo. 25:8-12) Kwa njia hiyo, sheria ya Roma ilifanya iwezekane ‘kutetea na kuisibitisha kisheria habari njema.’​—Flp. 1:7.

WAYAHUDI WALIISHI KATIKA INCHI NYINGI

15. Ni nini inaonyesha kwamba Wayahudi walikuwa wanaishi katika inchi nyingi wakati Yesu alikuwa hapa duniani na wakati wa mitume?

15 Wayahudi waliishi katika maeneo mengi yenye ilikuwa inatawaliwa na Roma, na inawezekana hilo lilifanya ikuwe mwepesi zaidi kwa Wakristo kufanya kazi ya kuhubiri. Miaka mingi mbele, Wayahudi walipelekwa katika inchi ya Waashuru, na kisha miaka fulani wengine wakapelekwa Babiloni. Katika miaka ya 400 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, Wayahudi walikuwa wanaishi katika majimbo 127 ya utawala wa Waperse. (Esta 9:30) Wakati Yesu alikuwa hapa duniani, Wayahudi fulani waliishi katika Asia Ndogo, Ugiriki, Mesopotamia, Misri na katika maeneo mengine ya Kaskazini mwa Afrika. Ilikadiriwa kwamba Utawala wa Roma ulikuwa na watu milioni 60, na watu zaidi ya milioni 4 kati yao walikuwa Wayahudi. Wayahudi walipeleka dini yao kila mahali walienda.​—Mt. 23:15.

16, 17. (a) Kwa sababu Wayahudi waliishi katika inchi nyingi, namna gani watu wasio Wayahudi walifaidika na jambo hilo? (b) Leo Wakristo wanafuata mufano gani wa Wayahudi?

16 Kwa sababu Wayahudi waliishi katika inchi nyingi, watu wengi wenye hawakuwa Wayahudi walijua vizuri Maandiko ya Kiebrania. Walijifunza kwamba kuna Mungu mumoja tu wa kweli, na kwamba watu wenye kumutumikia wanapaswa kutii sheria zake. Zaidi ya hilo, Maandiko ya Kiebrania yalikuwa na unabii mwingi juu ya Masiya. (Lu. 24:44) Wayahudi na Wakristo waliamini kwamba Maandiko ya Kiebrania ni Neno la Mungu na kwamba yaliongozwa na roho yake. Hilo lilimusaidia mutume Paulo aanzishe mazungumuzo kwa kutumia mambo yenye alikubaliana na wale wenye walikuwa tayari kumusikiliza. Ndio sababu, kulingana na desturi yake, mutume Paulo aliingia katika masinagogi ya Wayahudi na kufikiri nao kwa kutumia Maandiko.​—Soma Matendo 17:1, 2.

17 Wayahudi walikuwa na namna yao ya kufanya ibada. Walikuwa na programu ya kawaida ya kukusanyika pamoja katika masinagogi ao inje. Waliimba pamoja, walisali, na walizungumuzia Maandiko. Leo pia, tunafanya hivyo katika makutaniko ya Kikristo.

YOTE ILIWEZEKANA KWA MUSAADA WA YEHOVA

18, 19. (a) Mambo yenye tumezungumuzia ilisaidia Wakristo wa kwanza-kwanza kufanya nini? (b) Habari hii imekufundisha nini juu ya Yehova?

18 Mambo yote yenye tumezungumuzia ilisaidia ili kazi ya kuhubiri habari njema ikuwe na matokeo mazuri. Amani ya Roma, luga ya Kigiriki, kusafiri bila magumu, sheria ya Roma, na Wayahudi kupatikana katika inchi nyingi, vilisaidia wanafunzi wa Yesu ili waendelee kufanya kazi yenye Mungu aliwapatia, ni kusema, kazi ya kuhubiri habari njema.

19 Miaka 400 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, mwanafilozofia mumoja mwenye kuitwa Plato aliandika hivi: “Ingekuwa vigumu kumupata yule mwenye aliumba ulimwengu wote muzima, na hata kama tungemupata, haingewezekana kuelezea kila mutu juu yake.” Lakini, Yesu alisema hivi: “Mambo yasiyowezekana kwa wanadamu yanawezekana kwa Mungu.” (Lu. 18:27) Muumbaji wa ulimwengu wote muzima anapenda tumupate na tumujue. Tena, Yesu aliwaambia wanafunzi wake wafanye “wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mt. 28:19) Tunaweza kufanya kazi hiyo kwa musaada wa Yehova Mungu. Habari yenye kufuata itaonyesha namna gani kazi hiyo inafanyika leo.