Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI KUBWA | YESU ANATUOKOA—NAMNA GANI?

Kifo cha Yesu na Ufufuo Wake—Vinaweza Kukuletea Faida Gani?

Kifo cha Yesu na Ufufuo Wake—Vinaweza Kukuletea Faida Gani?

‘Umuamini Bwana Yesu nawe utaokolewa.’—Matendo 16:31.

Maneno hayo yasiyosahaulika ni maneno yenye Mutume Paulo na Sila walimuambia mulinzi mumoja wa gereza katika muji wa Filipi, huko Makedonia. Maneno hayo yanamaanisha nini? Ili tuelewe sababu gani kuamini Yesu kunatuokoa kutoka katika kifo, tunapaswa kwanza kujua sababu gani tunakufa. Tuone mambo Biblia inafundisha.

Watu hawakuumbwa ili wakufe

Na Yehova Mungu akamuchukua mutu na kumuweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza. Pia Yehova Mungu akamuwekea mutu amri hii: Matunda ya kila muti wa bustani unaweza kula mupaka ushibe. Lakini kuhusu matunda ya muti wa ujuzi wa mema na mabaya usikule, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.’—Mwanzo 2:15-17.

Mungu alimuweka mutu wa kwanza, Adamu, katika bustani ya Edeni. Bustani hiyo ilikuwa paradiso ya duniani yenye ilikuwa inajaa wanyama wengi na mimea ya muzuri. Katika bustani hiyo kulikuwa miti yenye kutoa matunda ambayo Adamu angekula kwa uhuru. Lakini, Yehova Mungu alimuambia Adamu waziwazi asikule matunda ya muti mumoja, alimuonya Adamu kuwa atakufa ikiwa anakula matunda ya muti huo.

Adamu alielewa jambo hilo lenye alikatazwa? Alijua kifo ni nini kwa sababu alikuwa anaona wanyama wanakufa. Ikiwa Adamu aliumbwa ili akufe siku fulani, onyo la Mungu halingekuwa na maana yoyote. Lakini, alitambua kama ikiwa anamutii Mungu na anakosa kula matunda ya muti huo, angeishi milele, hangekufa hata siku moja.

Watu fulani wanaamini kama muti huo ulifananisha kitendo cha ndoa. Lakini haikukuwa hivyo kwa sababu Yehova alitaka Adamu na bibi yake Eva, ‘wazae na kuwa wengi’ na ‘wajaze dunia na kuitiisha.’ (Mwanzo 1:28) Jambo walikatazwa ulikuwa muti wa kweli-kweli. Yehova aliuita ‘muti wa ujuzi wa mema na mabaya’ kwa sababu ulifananisha haki yake ya kuamua yaliyo mema na yaliyo mabaya kwa ajili ya watu. Adamu hangekula matunda ya muti huo, angeonyesha utii na shukrani yake kwa Yule mwenye alimuumba na kumubariki sana.

Adamu alikufa kwa sababu alikosa kumutii Mungu

[Mungu] akamuambia Adamu: Kwa sababu . . . ulikula matunda ya muti ambao nilikupa amri hii kuuhusu, . . . kwa jasho la uso wako utakula mukate mupaka utakaporudi katika udongo, kwa kuwa ulitolewa katika huo.’—Mwanzo 3:17, 19.

Adamu alikula tunda la muti wenye alikatazwa. Tendo hilo la kukosa utii halikupaswa kukamatwa kwa muchezo. Huo ulikuwa uasi; alizarau kabisa mambo yote ya muzuri yenye Yehova alimufanyia. Wakati Adamu alikula tunda hilo, alimukataa Yehova, akachagua njia ya uhuru yenye ingemuletea matokeo mabaya.

Mwishowe Adamu alikufa, kama vile Mungu alikuwa amesema. Mungu alikuwa amemuumba Adamu ‘kutoka katika mavumbi ya inchi’ na alikuwa amemuambia kama ‘angerudi katika udongo.’ Adamu hakuendelea kuishi katika mwili mwingine ao mahali pengine. Wakati alikufa, hakukuwa tena na uzima, alikuwa kama vile mavumbi yenye yalitumiwa kumuumba.—Mwanzo 2:7; Mhubiri 9:5, 10.

Tunakufa kwa sababu tuko watoto wa Adamu

‘Kupitia mutu mumoja zambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia zambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya zambi.’—Waroma 5:12.

Kukosa utii kwa Adamu, ao zambi, kulileta matokeo mabaya sana. Wakati Adamu alifanya zambi, alipoteza tumaini lake la uzima wa milele haiko tu uzima wetu wa kawaida wa miaka 70 ao 80. Tena, wakati Adamu alifanya zambi, alipoteza ukamilifu na angeweza tu kuwapitishia watoto wake kutokamilika.

Sisi wote tuko watoto wa Adamu. Bila sisi kutaka, tumeriti kupitia yeye mwili usiokamilika na mwishowe tunakufa. Paulo alieleza muzuri hali yetu mbaya. Aliandika hivi: ‘Mimi ni wa kimwili, nimeuzwa chini ya zambi. Maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki?’ Kisha Paulo anajibu ulizo lake mwenyewe. Anasema hivi: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!”—Waroma 7:14, 24, 25.

Yesu alitoa uzima wake ili tuweze kuishi milele

Baba amemutuma Mwana wake kuwa Mwokozi wa ulimwengu.’—1 Yohana 4:14.

Yehova Mungu alifanya mupango wa kumaliza matokeo ya zambi na kutuweka huru kutoka katika hukumu ya kifo cha milele. Namna gani? Alimutuma Mwana wake mupendwa kutoka mbinguni azaliwe akiwa mutu mukamilifu kama Adamu. Lakini, tofauti na Adamu, Yesu ‘hakufanya zambi.’ (1 Petro 2:22) Kwa sababu alikuwa mukamilifu, hakukuwa chini ya hukumu ya kifo na pia angeweza kuishi milele akiwa mutu mukamilifu.

Lakini, Yehova aliacha maadui wa Yesu wamuue. Kisha siku tatu, Yehova alimufufua Yesu akiwa roho ili aweze kurudia tena mbinguni. Huko mbinguni, Yesu alimupatia Mungu bei ya uzima wake mukamilifu ambao alitoa ili kulipia mambo yenye Adamu alipoteza kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya watoto wake. Yehova alikubali zabihu hiyo na kupatia watu wenye kuamini Yesu nafasi ya kupata uzima wa milele.—Waroma 3:23, 24; 1 Yohana 2:2.

Kwa kufanya hivyo, Yesu alinunua mambo yenye Adamu alipoteza. Alikufa kwa ajili yetu ili tuweze kuishi milele. Biblia inasema hivi: ‘Yesu . . . alipatwa na kifo, ili kwa fazili zisizostahiliwa za Mungu aonje kifo kwa ajili ya kila mwanadamu.’—Waebrania 2:9.

Mupango huo unaonyesha mambo mengi juu ya Yehova. Kulingana na kanuni yake juu ya haki, haingewezekana wanadamu wasio wakamilifu wajikomboe wenyewe. Hata hivyo, upendo wake na huruma yake vilimuchochea atende kulingana na kanuni zake mwenyewe hata kama ilimuomba alipe bei kubwa, ni kusema, kutoa Mwana wake mwenyewe ili kulipa bei ya ukombozi.—Waroma 5:6-8.

Yesu alifufuliwa, watu wengine pia watafufuliwa

“Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu, matunda ya kwanza ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo. Kwa kuwa kifo ni kupitia mwanadamu, ufufuo wa wafu pia ni kupitia mwanadamu. Kwa maana kama vile katika Adamu wote wanakufa, vivyo hivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai [wazima].”—1 Wakorintho 15:20-22.

Bila shaka, Yesu aliishi na alikufa, lakini ni mambo gani yanahakikisha kuwa alifufuliwa? Kati ya mambo yenye kuhakikisha sana kuwa Yesu alifufuliwa kuna jambo hili: Kisha kufufuliwa alitokea watu wengi mahali na wakati mbalimbali. Wakati fulani, aliwatokea watu zaidi ya 500. Mutume Paulo aliandika juu ya jambo hilo katika barua yake kwa Wakorintho. Alionyesha kuwa kati ya watu wenye walijionea jambo hilo, watu fulani walikuwa hawajakufa, kwa hiyo wangeweza kushuhudia mambo yenye walikuwa wameona na kusikia.—1 Wakorintho 15:3-8.

Ni muzuri kujua kama wakati Paulo aliandika kuwa Kristo alikuwa “matunda ya kwanza” ya watu wenye watafufuliwa, alikuwa anaonyesha kuwa wengine pia wangefufuliwa kisha hapo. Yesu mwenyewe alisema kuwa wakati utakuja ambapo ‘wale wote walio ndani ya makaburi ya ukumbusho watatoka.’—Yohana 5:28, 29.

Ili tuishi milele, tunapaswa kumuamini Yesu

Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamutoa Mwana wake muzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali [lakini] akuwe na uzima wa milele.’—Yohana 3:16.

Kurasa za kwanza za Biblia zinazungumuzia wakati kifo kilianza na Paradiso ikapotea. Kurasa za mwisho zinazungumuzia wakati Mungu atamaliza kifo na kurudisha Paradiso duniani. Wakati huo, watu watakuwa na maisha yenye maana na yenye furaha. Andiko la Ufunuo 21:4 linasema hivi: ‘Kifo hakitakuwa tena.’ Ili kukazia kuwa ahadi hiyo ni ya kweli, mustari wa 5 unasema hivi: “Maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.” Yehova iko kabisa na uwezo wa kutimiza mambo yenye anaahidi.

Unaamini kuwa ‘maneno hayo ni ya uaminifu na ya kweli’? Kwa hiyo, ujifunze mambo mengi juu ya Yesu Kristo, na umuamini. Ikiwa unafanya hivyo, utakubaliwa na Yehova. Atakubariki sana leo na utakuwa na tumaini la uzima wa milele katika Paradiso duniani, kwenye ‘kifo hakitakuwa tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwa tena.’