Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jifunze Kutokana na Mfano wa Talanta

Jifunze Kutokana na Mfano wa Talanta

“Akampa mmoja talanta tano, mwingine mbili, na mwingine moja.—MT. 25:15.

1, 2. Kwa nini Yesu alisimulia mfano wa talanta?

KATIKA mfano wa talanta, Yesu anafunua waziwazi jukumu ambalo wafuasi wake watiwa-mafuta wamekabidhiwa. Tunahitaji kuelewa maana ya mfano huo kwa sababu unawahusu Wakristo wote wa kweli, iwe wana tumaini la kupata thawabu mbinguni au duniani.

2 Yesu alisimulia mfano wa talanta alipokuwa akijibu swali la wanafunzi wake kuhusu “ishara ya kuwapo [kwake] na ya umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 24:3) Kwa hiyo, mfano huo unatimizwa katika siku zetu na ni sehemu ya ishara inayoonyesha kuwapo kwa Yesu na kwamba anatawala akiwa Mfalme.

3. Tunajifunza nini kutokana na mifano iliyoandikwa katika Mathayo sura ya 24 na 25?

3 Mfano wa talanta ni mojawapo ya mifano minne inayohusiana ambayo iliandikwa katika Mathayo 24:45 hadi 25:46. Mifano mingine mitatu, yaani, mfano wa mtumwa mwaminifu na mwenye busara, mabikira kumi, na ule wa kondoo na mbuzi, ilisimuliwa pia na Yesu alipokuwa akijibu swali kuhusu kuwapo kwake. Katika mifano yote minne, Yesu anakazia sifa ambazo zingewatambulisha wafuasi wake wa kweli katika siku hizi za mwisho. Mifano ya mtumwa, mabikira, na talanta inawahusu wafuasi wake watiwa-mafuta. Katika mfano wa mtumwa mwaminifu, Yesu anakazia kwamba kikundi kidogo cha watiwa-mafuta waliokabidhiwa jukumu la kuwalisha watumishi wake wa nyumbani katika siku za mwisho, wanapaswa kuwa waaminifu na wenye busara. Katika mfano wa mabikira, Yesu anakazia kwamba wafuasi wake wote watiwa-mafuta wanapaswa kuwa tayari na kuwa macho, kwa kuwa wanajua anakuja lakini hawajui siku wala saa atakayokuja. Katika mfano wa talanta, Yesu anaonyesha kwamba watiwa-mafuta wanahitaji kuwa na bidii wanapotimiza majukumu yao ya Kikristo. Yesu anaelekeza mfano wake wa mwisho unaohusu kondoo na mbuzi kwa wale walio na tumaini la kuishi duniani. Anakazia kwamba wanapaswa kuwa washikamanifu na kuwaunga mkono kikamili ndugu za Yesu watiwa-mafuta walio duniani. * Acheni sasa tukazie fikira mfano wa talanta.

BWANA AWAKABIDHI PESA WATUMWA WAKE

4, 5. Yule mtu, au bwana, anafananisha nani, na talanta halisi ina thamani gani?

4 Soma Mathayo 25:14-30. Kwa muda mrefu, machapisho yetu yameeleza kwamba mtu, au bwana, anayetajwa katika mfano huo ni Yesu na alisafiri ng’ambo alipopanda kwenda mbinguni mwaka wa 33 W.K. Katika mfano mwingine unaolingana na huo, Yesu anafunua kusudi lake la kusafiri ng’ambo, yaani, alisafiri “ili ajipatie mamlaka ya kifalme kwa ajili yake mwenyewe.” (Luka 19:12) Yesu hakupata mamlaka kamili ya Ufalme mara tu baada ya kurudi mbinguni. * Badala yake, ‘aliketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu, tangu wakati huo na kuendelea akingojea mpaka adui zake wawekwe kuwa kiti cha miguu yake.’—Ebr. 10:12, 13.

5 Mtu anayetajwa katika mfano huo alikuwa na talanta nane; hicho kilikuwa kiasi kikubwa sana cha pesa wakati huo. * Kabla ya kusafiri ng’ambo, aliwagawia watumwa wake talanta hizo, akitarajia kwamba wangefanya biashara akiwa safarini. Sawa na mtu huyo, Yesu alikuwa na kitu chenye thamani kubwa sana kabla ya kwenda mbinguni. Kitu gani hicho? Ni kazi aliyofanya maishani mwake.

6, 7. Talanta zinafananisha nini?

6 Yesu aliona kazi yake ya kuhubiri na kufundisha kuwa muhimu sana. (Soma Luka 4:43.) Kupitia kazi hiyo, alilima shamba ambalo lingekuwa na mazao mengi sana. Awali, aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Inueni macho yenu myatazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.” (Yoh. 4:35-38) Alikuwa akifikiria kukusanywa kwa watu wengine wengi wenye mioyo minyofu ambao wangekuwa wanafunzi wake. Yesu alikuwa kama mkulima bora, hangelipuuza shamba ambalo lilikuwa tayari kuvunwa. Hivyo, muda mfupi baada ya kufufuliwa na kabla ya kupanda mbinguni, aliwapa wanafunzi wake mgawo huu mzito: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi.” (Mt. 28:18-20) Hivyo, Yesu aliwakabidhi hazina yenye thamani sana, yaani, huduma ya Kikristo.—2 Kor. 4:7.

7 Basi tufikie mkataa gani? Yesu alipowapa wafuasi wake kazi ya kufanya wanafunzi, ni kana kwamba alikuwa akiwakabidhi “mali zake,” yaani, talanta zake. (Mt. 25:14) Kwa ufupi, talanta zinafananisha jukumu la kuhubiri na kufanya wanafunzi.

8. Bwana alitarajia nini licha ya kwamba kila mtumwa alipokea idadi tofauti ya talanta?

8 Katika mfano wa talanta, bwana alimpa mtumwa mmoja talanta tano, mwingine mbili, na mwingine moja tu. (Mt. 25:15) Ingawa kila mtumwa alipokea idadi tofauti ya talanta, bwana alitarajia kwamba wote wangekuwa na bidii katika kuzitumia talanta hizo, yaani, wangefanya yote wawezayo katika huduma. (Mt. 22:37; Kol. 3:23) Katika karne ya kwanza, kuanzia Pentekoste ya 33 W.K., wafuasi wa Kristo walianza kufanya biashara kwa kutumia talanta hizo. Kitabu cha Biblia cha Matendo kinaonyesha waziwazi bidii yao katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. *Mdo. 6:7; 12:24; 19:20.

KUTUMIA ZILE TALANTA KUFANYA BIASHARA KATIKA SIKU ZA MWISHO

9. (a) Wale watumwa wawili waaminifu walifanya nini na zile talanta, na hilo linaonyesha nini? (b) “Kondoo wengine” wanatimiza sehemu gani?

9 Katika siku za mwisho, hasa kuanzia mwaka wa 1919 na kuendelea, watumwa waaminifu wa Kristo waliotiwa mafuta ambao wangali duniani wamekuwa wakifanya biashara kwa kutumia talanta za Bwana. Kama wale watumwa wawili wa kwanza, ndugu na dada watiwa-mafuta wametumia kile walicho nacho kufanya yote wawezayo. Hakuna haja ya kukisia-kisia ni nani aliyepewa talanta tano na ni nani aliyepewa mbili. Katika mfano huo, watumwa wote wawili walikuwa na bidii ileile kwa kuwa walipata mara mbili zaidi ya talanta walizopewa na bwana wao. Wakristo wenye tumaini la kuishi duniani wanatimiza sehemu gani? Wanatimiza sehemu muhimu sana! Mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi unatufundisha kwamba wale walio na tumaini la kuishi duniani wana pendeleo la kuwaunga mkono kwa ushikamanifu ndugu za Yesu watiwa-mafuta katika kazi ya kuhubiri na kufundisha. Katika siku hizi za mwisho zilizo ngumu, vikundi vyote viwili vinashirikiana kwa bidii kama “kundi moja” katika kazi ya kufanya wanafunzi.—Yoh. 10:16.

10. Ni sehemu gani iliyo muhimu sana ya ile ishara ya kuwapo kwa Yesu?

10 Bwana anatarajia wafuasi wake wote wafanye wanafunzi zaidi. Kama ilivyotajwa awali, bila shaka wanafunzi wake waaminifu wa karne ya kwanza waliongeza mali zake. Namna gani katika siku hizi za mwisho wakati ambapo mfano wa talanta unatimizwa? Watumishi waaminifu wenye bidii wa Yesu wamefanya kazi kubwa zaidi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi katika historia. Kwa sababu ya jitihada zao, mamia ya maelfu ya wanafunzi wapya wanajiunga na watangazaji wa Ufalme kila mwaka. Hilo limefanya kazi ya kuhubiri na kufundisha kuwa sehemu muhimu sana ya ile ishara ya kuwapo kwa Yesu katika mamlaka ya Ufalme. Kwa hakika, Bwana wao anafurahi sana!

Kristo amewakabidhi watumishi wake kazi muhimu sana ya kuhubiri (Tazama fungu la 10)

BWANA ATAKUJA LINI KUFANYA HESABU?

11. Tunajuaje kwamba Yesu atakuja kufanya hesabu wakati wa dhiki kuu?

11 Yesu atakuja kufanya hesabu na watumwa wake kuelekea mwishoni mwa dhiki kuu inayokuja. Tunajuaje jambo hilo? Katika unabii wake ulioandikwa katika Mathayo sura ya 24 na 25, Yesu alitaja tena na tena kuhusu kuja kwake. Akiirejelea hukumu wakati wa ile dhiki kuu, alisema kwamba watu ‘watamwona Mwana wa binadamu akija juu ya mawingu ya mbinguni.’ Aliwahimiza wafuasi wake wanaoishi katika siku za mwisho waendelee kukesha, kwa kusema hivi: “Hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja” na “Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyofikiria.” (Mt. 24:30, 42, 44) Kwa hiyo, Yesu aliposema kwamba “bwana wa watumwa hao alikuja na kufanya hesabu,” ni wazi kwamba alikuwa akizungumzia wakati atakapokuja kutekeleza hukumu katika mwisho wa mfumo huu. *Mt. 25:19.

12, 13. (a) Bwana anawaambia nini wale watumwa wawili wa kwanza, na kwa nini? (b) Watiwa-mafuta wanatiwa muhuri wa mwisho wakati gani? (Tazama sanduku lenye kichwa “ Kutoa Hesabu Wakati wa Kifo.”) (c) Wale watakaohukumiwa kuwa kondoo watapokea thawabu gani?

12 Kulingana na mfano huo, bwana anapokuja, anawakuta watumwa wawili wa kwanza, yaani, yule aliyepewa talanta tano na yule aliyepewa mbili, wamekuwa waaminifu, na kila mmoja ameongeza mara mbili zaidi ya talanta alizopewa. Bwana anawaambia watumwa wote wawili maneno yaleyale: “Vema, mtumwa mwema na mwaminifu! Ulikuwa mwaminifu juu ya mambo machache. Nitakuweka juu ya mambo mengi.” (Mt. 25:21, 23) Basi tunapaswa kutarajia nini wakati Bwana, yaani, Yesu aliyetukuzwa, anapokuja kuhukumu wakati ujao?

13 Wale wanaofananishwa na watumwa wawili wa kwanza, yaani, wanafunzi wake watiwa-mafuta wenye bidii, watakuwa tayari wametiwa muhuri wa mwisho kabla ya dhiki kuu kuanza. (Ufu. 7:1-3) Kabla ya Har–Magedoni, Yesu atawathawabisha kwa kuwapa uhai wa mbinguni. Wakristo wenye tumaini la kuishi duniani waliowaunga mkono ndugu za Kristo katika kazi ya kuhubiri watakuwa wamehukumiwa kuwa kondoo na watapewa pendeleo la kuishi duniani chini ya utawala wa Ufalme.—Mt. 25:34.

MTUMWA MWOVU NA GOIGOI

14, 15. Je, Yesu alimaanisha kwamba idadi kubwa ya ndugu zake watiwa-mafuta wangekuwa waovu na goigoi? Fafanua.

14 Katika mfano huo, mtumwa wa mwisho aliificha talanta yake kwenye udongo badala ya kuitumia kufanya biashara au hata kuiweka kwa watunza-akiba. Mtumwa huyo alikuwa na mtazamo mbaya, kwa kuwa aliamua kimakusudi kutoitumia talanta yake kumwongezea faida bwana wake. Kwa hiyo, haishangazi kwamba bwana akasema mtumwa huyo ni “mwovu na goigoi.” Bwana aliichukua talanta hiyo na kumpa yule aliyekuwa na talanta kumi. Kisha, mtumwa huyo mwovu akatupwa ‘nje katika giza, na huko ndiko atalia na kusaga meno yake.’—Mt. 25:24-30; Luka 19:22, 23.

15 Kwa kuwa mtumwa mmoja kati ya wale watatu alificha talanta yake, je, Yesu alimaanisha kwamba theluthi moja ya wafuasi wake watiwa-mafuta wangekuwa waovu na goigoi? Hapana. Fikiria muktadha. Katika mfano wa mtumwa mwaminifu na mwenye busara, Yesu alieleza kuhusu mtumwa mwovu anayewapiga watumwa wenzake. Yesu hakuwa akitabiri kwamba kungekuwa na jamii ya mtumwa mwovu. Badala yake, alikuwa akimwonya mtumwa mwaminifu asiwe na tabia kama za mtumwa mwovu. Vivyo hivyo, katika mfano wa mabikira kumi, Yesu hakumaanisha kwamba nusu ya wafuasi wake watiwa-mafuta wangekuwa kama wale mabikira watano wapumbavu. Badala yake, alikuwa akiwaonya ndugu zake wa kiroho kuhusu mambo ambayo yangetokea ikiwa hawangeendelea kukesha na kuwa tayari. * Katika muktadha huo, inaonekana kwamba inafaa kufikia mkataa kuwa katika mfano wa talanta, Yesu hakumaanisha kwamba idadi kubwa ya ndugu zake watiwa-mafuta wangekuwa waovu na goigoi katika siku za mwisho. Badala yake, alikuwa akiwaonya wafuasi wake watiwa-mafuta kwamba wanahitaji kuendelea kuwa na bidii, yaani, “kufanya biashara” kwa kutumia talanta yao, na kuepuka mitazamo na matendo ya mtumwa mwovu.—Mt. 25:16.

16. (a) Tunajifunza nini katika mfano wa talanta? (b) Makala hii imeboreshaje uelewaji wetu kuhusu mfano wa talanta? (Tazama sanduku lenye kichwa “ Kuelewa Mfano wa Talanta.”)

16 Tunajifunza mambo gani mawili katika mfano wa talanta? Kwanza, Bwana, yaani, Kristo, amewakabidhi watumwa wake watiwa-mafuta kazi yenye thamani sana—kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Pili, Kristo anatarajia sote tuwe na bidii katika kazi ya kuhubiri. Tukiwa na bidii, tunaweza kuwa na hakika kwamba Bwana atatuthawabisha kwa sababu ya imani yetu, ushikamanifu wetu, na ikiwa tutaendelea kukesha.—Mt. 25:21, 23, 34.

^ fu. 3 Habari kuhusu mtumwa mwaminifu na mwenye busara imezungumziwa katika Mnara wa Mlinzi, Julai 15, 2013, ukurasa wa 21-22, fungu la 8-10. Mfano wa mabikira umefafanuliwa katika makala iliyotangulia ya gazeti hili. Mfano wa kondoo na mbuzi umefafanuliwa katika Mnara wa Mlinzi, Oktoba 15, 1995, ukurasa wa 23-28, na katika makala inayofuata ya gazeti hili.

^ fu. 5 Katika siku za Yesu, talanta moja ilikuwa sawa na dinari 6,000 hivi. Kwa hiyo, mfanyakazi wa kawaida aliyelipwa dinari moja kwa siku, alihitaji kufanya kazi kwa miaka 20 ili kupata talanta moja tu.

^ fu. 8 Baada ya mitume kufa, Shetani alianzisha uasi-imani ambao ulisitawi kwa karne nyingi. Katika kipindi hicho, kazi ya kufanya wanafunzi wa kweli wa Kristo ilifanywa kwa kiwango kidogo sana. Lakini hali hiyo ingebadilika “wakati wa mavuno,” yaani, siku za mwisho. (Mt. 13:24-30, 36-43) Tazama Mnara wa Mlinzi, Julai 15, 2013, ukurasa wa 9-12.

^ fu. 15 Tazama fungu la 13 katika makala yenye kichwa “Je, ‘Utaendelea Kukesha’?” kwenye gazeti hili.